-
“Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Ingawa Mashahidi wa Yehova walikuwa wameonea shangwe kutambuliwa kisheria katika Kanada kwa miaka mingi, Vita ya Ulimwengu 2 iliandaa kisababu cha wapinzani kusadikisha gavana-jenerali mpya awatangaze Mashahidi kuwa wasio halali. Hilo lilifanywa mnamo Julai 4, 1940. Miaka miwili baadaye, wakati Mashahidi walipopewa fursa ya kujitetea mbele ya halmashauri teule ya Bunge, halmashauri hiyo ilipendekeza kwa dhati kwamba marufuku juu ya Mashahidi wa Yehova na mashirika yao halali iondolewe. Hata hivyo, haikuwa hadi kulipokuwa na mijadala ya mara kwa mara na ya muda mrefu katika Bunge na kazi nyingi ya kupata sahihi za maombi mawili ya taifa lote ikafanywa, ndipo waziri wa sheria, ambaye alikuwa ni Mkatoliki wa Roma, alihisi ameshurutishwa kuondoa marufuku kabisa.
-
-
“Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 697]
Mashahidi Waliopigwa Marufuku Waeleza Msimamo Wao Waziwazi
Tengenezo la Mashahidi wa Yehova lilipigwa marufuku na serikali katika Kanada mwaka 1940. Baada ya hapo kulikuwa na mashtaka zaidi ya 500. Mashahidi wangeweza kutoa utetezi gani? Kwa heshima lakini kwa uthabiti, walitolea Mahakama taarifa inayokaribiana na haya yafuatayo:
‘Sitaomba radhi kwa sababu ya vitabu hivi. Vinafunza njia ya kwenda kwenye uhai wa milele. Ninaviamini kikweli kwamba vinaeleza kusudi la Mungu Mweza Yote la kusimamisha Ufalme wa uadilifu duniani. Kwangu mimi, vimekuwa baraka kubwa sana maishani mwangu. Kwa maoni yangu kuviharibu vitabu hivi na ujumbe wa Mungu uliomo kungekuwa ni kufanya dhambi dhidi ya Mweza Yote, kwa njia ileile ambayo ingekuwa dhambi kuchoma Biblia yenyewe. Kila mtu ni lazima achague kama atajasiria kupoteza kibali cha wanadamu au kupoteza kibali cha Mungu Mweza Yote. Kwangu mimi nimechukua msimamo upande wa Bwana na Ufalme Wake, na ninajitahidi kuheshimu jina la Aliye Juu Zaidi, ambalo ni Yehova, na ikiwa nitaadhibiwa kwa ajili ya hilo, basi wale wanaotoa adhabu hiyo watatwaa daraka mbele za Mungu.’
[Sanduku katika ukurasa wa 698]
Maoni ya Wabunge wa Serikali ya Kanada juu ya Jambo Hilo
Hapa pana taarifa zilizotolewa na baadhi ya washiriki wa Bunge la Kanada katika 1943 walipohimiza waziri wa sheria kuondoa marufuku juu ya Mashahidi wa Yehova na mashirika yao ya kisheria:
“Hakuna ithibati iliyotolewa mbele ya halmashauri na idara ya sheria iliyoonyesha kwamba mashahidi wa Yehova wangepaswa kutangazwa kuwa shirika lisilo halali wakati wowote . . . Ni jambo la kufedhehesha kwa Serikali ya Kanada kwamba watu wapaswa kuhukumiwa kwa ajili ya masadikisho yao ya kidini katika njia ile ambayo watu hawa wanaoonewa wamehukumiwa.” “Kwa maoni yangu ni chuki ya kidini ya wazi kabisa inayodumisha marufuku hiyo.”—Bw. Angus MacInnis.
“Maoni ya wengi wetu yamekuwa kwamba hao ni watu wasio na dhara, wasio na kusudi lolote la kukosea serikali. . . . Kwa nini marufuku haijaondolewa? Haiwezi kuwa kwa sababu ya hofu yoyote kwamba shirika hili ni hatari kwa hali njema ya serikali, au kwamba utendaji walo unapinga jitihada ya vita. Hakujapata kamwe kuwa na ithibati hata iliyo ndogo zaidi kwamba hivyo ndivyo mambo yalivyo.”—Bw. John G. Diefenbaker.
“Inafanya mtu afikiri kama hatua dhidi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa hasa kwa sababu ya mtazamo wao kuelekea Wakatoliki wa Roma, badala ya kwamba wana mtazamo unaopotoa.”—Bw. Victor Quelch.
-