Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb09 kur. 43-64
  • Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote
  • 2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb09 kur. 43-64

Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote

AFRIKA

IDADI YA NCHI 57

IDADI YA WATU 848,582,269

IDADI YA WAHUBIRI 1,122,493

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 2,202,217

Rwanda

Alipokuwa akirudi nyumbani kutoka shuleni, msichana fulani mwenye umri wa miaka tisa alipata pesa nyingi ndani ya mfuko mmoja uliokuwa barabarani. Watu wa familia yao waliokuwa wakijifunza Biblia na Mashahidi, waliamua kutenda kupatana na mambo waliyojifunza katika Biblia. Hivyo, walimtafuta mwenye pesa hizo na kumrudishia. Mtu aliyepoteza pesa hizo alimwuliza hivi msichana aliyeziokota, “Ikiwa ningekupa pesa kwa sababu ya unyoofu wako, ungenunua nini?”

“Ningenunua Biblia,” msichana huyo akasema.

Mtu huyo alisema hivi kwa mshangao, “Nilifikiri ungenunua viatu au nguo kwa sababu ninaona zile ulizo nazo zimezeeka sana.” Lakini msichana huyo alisisitiza kwamba angependelea kununua Biblia. Mtu huyo alitaka kujua ni kwa nini watu wa familia hiyo hawakutumia pesa hizo. Baada ya kuambiwa kwamba walikuwa wakijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, mtu huyo alinunua Biblia mbili, moja kwa ajili ya familia yake na nyingine kwa ajili ya msichana huyo. Pia aliwaomba Mashahidi watembelee familia yake na kujifunza Biblia pamoja nao. Familia zote mbili zinafanya maendeleo ya kiroho.

Jamhuri ya Afrika ya Kati

Theodora alikuwa mwenye haya nyingi sana, lakini kwa msaada wa Yehova akaishinda. Ingawa alilelewa katika familia ya Kikristo, hakuhudhuria mikutano mara nyingi katika Jumba la Ufalme kwa sababu ya haya. Alipoanza kuhudhuria, aliketi peke yake, bila kuzungumza na mtu yeyote na aliondoka mara moja baada ya wimbo na sala ya mwisho. Muda si muda, aliacha kuondoka mara moja, lakini ni mara chache sana aliponyoosha mkono wake ili kumsalimu yeyote aliyetaka kumsalimia. Baada ya muda, alianza kutoa maelezo mikutanoni na akaanza kuwafikia wengine na kuwasalimu. Haikuwa rahisi kwake alipoanza kuhubiri. Wasichana majirani walipomdhihaki, Theodora alitaka kuacha kuhubiri, lakini alisali kwa Yehova akimwomba ampe nguvu. Sasa amebatizwa, anafanya upainia msaidizi, na anatoa maelezo mazuri kutanikoni. Anajifunza Biblia na watu wanne, kutia ndani jirani mmoja aliyekuwa akimdhihaki.

Madagaska

Mwangalizi fulani wa mzunguko na mke wake walikuwa wakisafiri kuelekea kutaniko moja la mashambani. Wakiwa njiani, walikutana na wezi wa ng’ombe waliokuwa wamebeba mashoka na mikuki. Baada ya kusali kimya-kimya ili apate ujasiri, mke wa mwangalizi huyo wa mzunguko aliwatolea trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani. Alisema: “Leo tunaishi kwa woga. Hata hivyo, karibuni Mungu ataharibu waovu na kuleta ulimwengu mpya wenye amani.” Mmoja wa watu hao alisikiliza kwa makini na kukubali trakti hiyo.

Kwenye kusanyiko mwaka mmoja baadaye, mtu fulani alimfikia mke wa mwangalizi huyo na kumwuliza kama anamkumbuka. Alimwambia kwamba alikuwa mmoja wa wale wezi wa ng’ombe aliokutana nao kwenye barabara yenye matope, na ni yeye aliyekubali trakti. Kisha akamweleza hivi: “Tulikuwa tumetoka kushambulia eneo fulani tulipokutana nanyi. Mambo uliyosema yalinifanya nifikiri. Niliwaza hivi: ‘Hatuwaogopi polisi wala askari kwa sababu tunaweza kuwatoroka. Lakini ninaweza kumtoroka Mungu jinsi gani ikiwa atawaharibu waovu?’ Kwa hiyo, niliamua kuwatafuta Mashahidi. Niliporudi nyumbani, nilimtembelea jirani aliyekuwa akijifunza Biblia na painia wa pekee. Nilikubali kujifunza Biblia naye, na sasa nitabatizwa kwenye kusanyiko hili.”

Msumbiji

Mnamo 1992, Madalena alihusika katika aksidenti iliyomlemaza alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi. Baada ya aksidenti hiyo, haikuwa rahisi kutoka nyumbani. Miaka mitatu baadaye, Mashahidi walizungumza na baba yake nje ya nyumba yao. Baba yake alikuwa kiongozi wa kikundi fulani cha dini ya kienyeji kilichokutana nyuma ya nyumba yake. Madalena aliyekuwa akisikiliza mazungumzo hayo, aliwasikia ndugu hao wakiuliza habari zake, ndipo akawaalika ndani ya nyumba. Aliguswa moyo sana alipotambua walimjali kikweli! Alikubali kujifunza Biblia na akapendezwa sana na mambo aliyojifunza. Walipoona bidii yake, Mashahidi walimsaidia kwa njia mbalimbali, na hata kumsaidia kufika kwenye mikutano. Kwa sababu ya msaada huo, Madalena alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa mwaka wa 2002.

Wazazi wa Madalena walivutiwa sana na jinsi Mashahidi walivyomtunza binti yao. Mama yake alianza kuhudhuria mikutano na akaacha dini ya mume wake. Mwanzoni, babake Madalena alisema hataiacha dini yake, lakini baada ya muda yeye pia akaanza kuhudhuria mikutano. Watu wa dini yake walimshinikiza aache kwenda mikutanoni kwa sababu alikuwa kiongozi wao. Hata hivyo, alisimama imara na kuteketeza vitu vyake vya kidini. Yeye na mke wake walibatizwa mwaka wa 2007. Familia nzima inafanya maendeleo ya kiroho.

Zimbabwe

Decibel, ambaye ana umri wa miaka tisa, anawahubiria wanafunzi wenzake na walimu. Siku moja aliona kwamba mwalimu wake hakuwa na furaha, kwa hiyo akamwuliza ikiwa kuna kitu kilichomfanya akose furaha. Mwalimu huyo alimwambia kwamba dadake alikuwa amefiwa na mtoto. Decibel alimwahidi kwamba angemletea kitu ambacho kingemfariji. Wazazi wake walimpa broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, naye akampelekea mwalimu siku iliyofuata. Mwalimu huyo alisoma mafungu kadhaa katika broshua hiyo na akalia kwa shangwe. Baadaye, aliwaandikia wazazi wa Decibel ujumbe akiwashukuru kwa jinsi walivyomfundisha binti yao na kwa faraja ambayo Decibel alimpa wakati wa huzuni.

Ghana

Abigail, aliyeishi kusini mwa Ghana pamoja na babu na nyanya yake ambao ni Wapresbiteri, alikuwa ameambiwa kwamba Mashahidi wa Yehova ni manabii wa uongo. Alipojua kwamba wazazi wake, walioishi katika eneo lingine, walikuwa wakijifunza na Mashahidi, aliingiwa na wasiwasi na akawaandikia barua akiwashawishi waache kujifunza. Kwa kuwa wazazi wake hawakuacha kujifunza, alisafiri mwendo wa zaidi ya kilomita 1,000 ili kuzungumza nao. Abigail alishtuka kujifunza kutoka katika Biblia yake kwamba waovu hawatateswa kwenye moto wa mateso. Alianza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme pamoja na wazazi wake, na akawa mhubiri ambaye hajabatizwa. Abigail alibatizwa kwenye kusanyiko la mzunguko lililofanywa hivi majuzi.

AMERIKA

IDADI YA NCHI 55

IDADI YA WATU 898,130,531

IDADI YA WAHUBIRI 3,449,038

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 3,548,101

Dominika

Katika kisiwa hiki wanawake wengi wanafua nguo zao kandokando ya mito na kuzianika kwenye mawe makubwa. Mwanamke mmoja aliona kitabu fulani kikielea juu ya maji karibu na mahali alipokuwa akifulia nguo. Alipokiangalia alitambua kuwa kitabu hicho kilikuwa kama kile alichojifunza na Mashahidi wa Yehova kila juma. Alikiweka juu ya jiwe ili kikauke, na akaendelea kufua.

Baadaye siku hiyo, alipokusanya nguo zake zilizokauka, alisahau kitabu hicho. Hata hivyo, wavuvi fulani waliokuwa wakitoka baharini waliona kitabu hicho chenye rangi ya dhahabu, na mmoja wao akakichukua. Alivutiwa na kichwa chake Biblia Inafundisha Nini Hasa? na akaanza kukisoma. Baadaye, dada wawili mapainia walikutana na mvuvi huyo walipowatembelea watu katika kijiji chake. Aliwaeleza kwamba ni watu 144,000 tu watakaoenda mbinguni na kwamba Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mwaka wa 1914. Pia alisema kwamba karibuni dunia itafanywa kuwa paradiso. Walipomuuliza jinsi alivyopata kuyajua mambo hayo, aliwaeleza jinsi alivyopata kitabu Biblia Inafundisha, na kuongeza kwamba anakisoma kila siku. Aliwaonyesha kitabu hicho, ambacho sasa kilikuwa kimekauka lakini kimefura.

Mmoja wa mapainia hao alitambua kwamba kitabu hicho ni kile mwanafunzi wake wa Biblia alikuwa amekiokota mtoni. Mvuvi huyo alianza kujifunza Biblia. Yeye huwa anangoja kwa hamu kujifunza kila juma na anafanya maendeleo.

Bolivia

Kuhubiri katika eneo la Amazoni huko Bolivia ni kazi ngumu lakini yenye kuridhisha. Kikundi cha ndugu na dada kumi ambao ni mapainia, walijazana kwenye mashua yenye injini. Walibeba mahema, vyombo vya kupikia, na masanduku mengi ya vichapo vya Biblia. Walisafiri umbali wa kilomita 800 hivi kwenye Mto Beni kutoka Rurrenabaque hadi Riberalta. Walitembelea vijiji zaidi ya 70 na kuwaachia watu vitabu zaidi ya 800 na pia broshua na trakti. Waliwaonyesha watu 700 hivi waliopendezwa jinsi ya kujifunza Biblia na wakarudi kujifunza na watu zaidi ya 200 kati yao. Mara nyingi Mashahidi walipokuwa wakiondoka katika vijiji hivyo, watu waliwaambia, “Mnaweza kukaa na kujifunza nasi kwa muda mrefu kidogo?” Katika mji fulani mdogo, mtu mmoja alitaka sana Mashahidi waendelee kujifunza naye na alivunjika moyo walipokuwa wakiondoka. Alisema: “Mmeukata mti. Sasa mnahitaji kuuchonga na kuupiga msasa.”

Kanada

Kwa miaka mingi Normand amefanya kazi katika kiwanda cha kusafisha chuma jijini Montreal. Wakati wa mapumziko, alisoma kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku kwa ukawaida kwenye chumba cha kulia chakula. Wafanyakazi wenzake walimwona akikisoma, na baadhi yao wakakubali kuzungumzia andiko la kila siku pamoja naye. Wakati wa mazungumzo hayo mafupi, Normand alijitahidi hasa kuonyesha jinsi andiko hilo lingetumiwa katika familia na mahusiano mbalimbali. Mmoja wa wasimamizi wa kiwanda hicho pia alikuja kusikiliza mazungumzo hayo na baadaye akamwita Normand ofisini mwake kumpongeza. Alisema kwamba mazungumzo hayo yangekuwa na matokeo mazuri katika maisha ya wafanyakazi na yangechangia kuwapo kwa mahusiano bora.

Idadi ya watu walioshiriki mazungumzo hayo ilipoongezeka kufikia watu zaidi ya 30, wasimamizi wa kiwanda walimwomba Normand apange kuwe na vikundi vidogo vya mazungumzo katika sehemu mbalimbali za kiwanda hicho. Anasema hivi: “Kwa sasa ninazungumzia andiko la siku na vikundi vitatu kila siku, nao wafanyakazi wenzangu wanayaita mazungumzo hayo vikumbusho vya kila siku. Wanayafurahia sana hivi kwamba wakati ambapo sipo, mmoja wao anaongoza mazungumzo hayo. Kisha ninaporudi, wananiuliza maswali kuhusu mambo ambayo hawakuelewa.” Normand amewasaidia wafanyakazi wenzake watafakari andiko la Biblia kila siku kwa miaka mitano sasa. Kwa sababu hiyo, watu zaidi ya 40 kati ya wafanyakazi na familia zao wamekubali kweli.

Barbados

Dada Barker, mwenye umri wa miaka 89, alitaka kuanzisha funzo la Biblia. Kwa sababu ya udhaifu fulani wa kimwili, hawezi kwenda nyumba kwa nyumba, hivyo alijaribu kuhubiri kupitia simu bila matokeo yoyote. Baada ya kutiwa moyo na sehemu fulani ya mkutano kuhusu sala, alianza kumwomba Yehova amsaidie kuanzisha funzo la Biblia. Siku chache baadaye, alichukua Biblia yake na magazeti na akaamua kumhubiria mtu yeyote ambaye angepita mbele ya nyumba yake, ingawa nyumba hiyo haiko kwenye mtaa wenye shughuli nyingi. Alimwonyesha magazeti mtu fulani ambaye alikuwa akielekea nyumbani kutoka kazini. Juma moja baadaye, alipokuwa mbele ya nyumba yake, alimwona mtu huyo tena. Kwa sababu alipendezwa na magazeti aliyokuwa amempa, dada huyo alimwonyesha kitabu Biblia Inafundisha na kumweleza kuhusu mpango wa kujifunza Biblia. Alifurahi sana mtu huyo alipokubali kujifunza. Walijifunza mara ya kwanza mwishoni mwa Machi (Mwezi wa 3) 2008. Baadaye, aligundua kwamba mtu huyo aliishi karibu na nyumbani kwake. Majuma machache baadaye, alianza kuhudhuria mikutano. Dada huyo alisema, “Ninajua kwamba Yehova anajibu sala, lakini sikudhani atanijibu haraka hivyo!”

Chile

Wakati dada mmoja ambaye ni painia huko Santiago aliposhuka kwenye teksi katika sehemu fulani ya mji wao, aliacha faili yenye magazeti kwenye kiti cha nyuma bila kujua. Faili hiyo ilikuwa na magazeti kadhaa pamoja na nakala yake ya Huduma Yetu ya Ufalme, iliyokuwa na jina lake. Kwa sababu hiyo, siku mbili baadaye dereva wa teksi hiyo alisaidiwa na Mashahidi wengine waliokuwa wanahubiri katika eneo hilo kumpata dada huyo. Alipomrudishia painia huyo faili yake ya magazeti, haikuwa na gazeti lolote ila tu ile Huduma ya Ufalme. Magazeti yote yalikuwa yamechukuliwa. Aliomba msamaha na kumweleza kwamba baadhi ya wateja wake waliyaangalia magazeti hayo na kuomba kuyachukua. Hivyo, kwa siku moja magazeti yote yalijipeana yenyewe!

Nikaragua

Ernesto aliyekuwa kapteni wa kikosi maalumu cha jeshi, alikuwa akiishi katika mji mdogo karibu na Pwani ya Karibea. Jairo, painia wa pekee aliyekuja kuhubiri hapo kutoka sehemu nyingine ya nchi, alikutana na Ernesto alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba na akamweleza kuhusu mpango wa kujifunza Biblia nyumbani. Ingawa askari huyo alikataa, Jairo aliendelea kumtia moyo ajifunze, na mwishowe akakubali. Wakati wa mazungumzo yao, Jairo alisema kwamba babake alikuwa kamanda wa kikosi cha wanaharakati waliokuwa wakipigana na vikosi vya serikali katika eneo la karibu na kwamba alikufa vitani. Ernesto aliendelea kujifunza na akaanza kufanya maendeleo. Wakati huo wote kuna jambo fulani alilomficha mwalimu wake, lakini mwishowe ikambidi amwambie. Akiwa mwenye huzuni nyingi, Ernesto alimweleza kwamba yeye alikuwa kiongozi wa kikosi kilichomkamata baba ya Jairo akiwa hai na yeye binafsi ndiye aliyesababisha kifo chake. Jairo alishtuka, lakini alijua Ernesto alisema ukweli kwa sababu mambo yenye kutisha aliyoeleza yalilingana na yale aliyokuwa ameelezwa na askari waliokuwa na babake. Ernesto alifikiri kwamba urafiki wao ungeishia hapo. Lakini badala ya kumchukia mwanafunzi wake, Jairo aliendelea kujifunza naye. Ernesto alifanya maendeleo na kubatizwa pamoja na mke wake. Yeye na Jairo bado ni marafiki.

Venezuela

Ndugu kutoka mji wa Machiques walikuwa wakihubiri katika eneo lisilohubiriwa mara nyingi upande wa magharibi wa nchi hiyo, karibu na mpaka wa Kolombia. Kila mtu alisikiliza! Kiongozi wa jamii ya Yukpa aliruhusu ndugu waadhimishe Ukumbusho kwa mara ya kwanza katika eneo hilo. Majirani na pia shule fulani iliyo karibu iliwapa viti, na watu zaidi ya 200 wakahudhuria. Baada ya mkutano, kiongozi huyo alisema hivi kwa heshima kwa niaba ya jamii hiyo: “Tungependa kuwashukuru Mashahidi wa Yehova. Tunatumaini hii haitakuwa mara yenu ya mwisho kuja hapa. Mnatufundisha kweli, na mnakaribishwa kwa moyo mkunjufu!” Sasa watu zaidi ya 50 wanajifunza Biblia kila juma.

ASIA NA MASHARIKI YA KATI

IDADI YA NCHI 47

IDADI YA WATU 4,026,656,360

IDADI YA WAHUBIRI 618,088

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 538,957

Taiwan

Dada mmoja anaandika: “Nilifurahi kukutana na ndugu yangu wa kambo, ambaye sikuwa nimewahi kuonana naye kwa sababu yeye na familia yake wanaishi eneo la mbali na si rahisi kufika huko. Baba yangu na watu wengine wa familia yetu walifurahi kusikia kwamba ndugu yangu wa kambo na familia yake walikuwa wakifanya jitihada kubwa za kututembelea. Kwa kuwa wanaishi katika eneo ambako hakuna Mashahidi, nilitumaini kwamba wangekubali habari njema. Nilifurahi sana mke na binti yake walipopendezwa na Biblia! Hata hivyo, ningeweza kuwasaidia jinsi gani wajifunze mengi zaidi kuhusu makusudi ya Yehova wakati ambapo wangerudi kwao? Niligundua kwamba walikuwa na kompyuta na wangeweza kutumia Intaneti. Mimi na mume wangu tulinunua kompyuta yenye kamera inayowezesha mtu kuona yule anayezungumza naye. Baada ya kurudi kwao, tuliendelea kujifunza Biblia kupitia kompyuta. Nilishangaa kwamba njia hii ya kuongoza funzo inafaa sana. Tunaweza kuona jinsi wanavyoitikia wanaposoma Biblia yao wenyewe na kitabu tunachojifunza. Jambo hilo linanisaidia kujua ninachohitaji kufanya ili niwasaidie. Tunafurahi kwamba tunaweza kutumia tekinolojia hii ambayo inatuwezesha kuwafundisha kweli watu wa ukoo ambao hatungeweza kuwahubiria kwa njia nyingine.”

Nepal

Purnamaya mwenye umri wa miaka 16 anaishi kwenye mji mdogo huko Nepal. Mjomba wake alimhubiria na akaanza kujifunza. Sasa, yeye anahudhuria mikutano mara moja kwa juma bila kukosa, ingawa anahitaji kusafiri kwa basi muda wa saa mbili na nusu ili kufika kutanikoni. Si rahisi kwake kufanya hivyo. Wazazi wake wana ukoma, kwa hiyo wao ni maskini sana. Asubuhi na mapema, Purnamaya anavunja mawe kutengeneza kokoto ili kuitegemeza familia yao kifedha, mbali na kufanya kazi za nyumbani kama kupika na kufua nguo. Isitoshe, yeye anaenda shuleni. Ili kufika kwenye mikutano, Purnamaya analipa nauli inayolingana na mshahara ambao mfanyakazi analipwa kwa siku moja. Nyakati nyingine, wazazi wake wanamtia moyo aende katika kanisa lililo karibu. Lakini Purnamaya anajua kwamba anaweza kujifunza kumhusu Yehova katika Jumba la Ufalme tu, kwa hiyo anajitahidi kuhudhuria mikutano. Hivi karibuni, ilimbidi auze saa yake aliyopewa na nyanyake kama zawadi. Yeye anatoa maelezo mazuri mikutanoni na pia anawaeleza watu katika mji wao mambo anayojifunza. Anawatia moyo watu wote wanaomjua.

Malasia

Wakati wa utawala wa kikoloni wa Uingereza, maelfu ya vibarua waliletwa Malasia kufanya kazi kwenye mashamba ya miti ya mpira. Walijengewa vijiji katika mashamba hayo, na vijiji vingi bado vipo. Vingi kati ya vijiji hivyo havifikiki kwa urahisi na hata havionyeshwi kwenye ramani. Ndugu katika kutaniko moja walipata kijiji fulani katika shamba la miti ya mpira walipokuwa wakihubiri katika eneo ambalo halijagawiwa yeyote. Vijana wawili wenye umri wa karibu miaka 20, ambao tayari walikuwa wamechukua magazeti, walipendezwa sana na kazi ya kuhubiri ya ndugu hao. Vijana hao walijitolea kuwaonyesha vijiji vingine. Tofauti na ndugu hao, wao walijua eneo hilo vizuri sana. Walipanda pikipiki zao na kuongoza gari za ndugu hao. Walipita kwenye mashamba wakifuata vijia na barabara zenye matope, na nyakati nyingine iliwachukua muda wa dakika 45 hivi kutoka kijiji kimoja hadi kingine. Waliwaongoza ndugu hao kwenye mashamba ambayo hayakuwa yamewahi kutembelewa na Mashahidi. Ndugu hao walipokuwa wakihubiri, vijana hao waliwahimiza wanavijiji wachukue magazeti na kuhakikisha kwamba wameyasoma. Kwa ujumla, waliwapeleka ndugu hao kwenye vijiji vitatu vilivyokuwa mbali. Msaada wa vijana hao wasio na ubinafsi uliwawezesha ndugu kuwahubiria watu ambao hawakuwa wamewahi kusikia habari njema. Katika siku mbili walizokuwa huko, yaani, Jumamosi na Jumapili (Siku ya Yenga), wahubiri 50 kutoka kutaniko hilo waliachia watu magazeti zaidi ya 5,000.

ULAYA

IDADI YA NCHI 47

IDADI YA WATU 733,775,190

IDADI YA WAHUBIRI 1,542,507

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 789,219

Urusi

Tatyana ana kansa ya ubongo. Baada ya kufanyiwa upasuaji miaka kadhaa iliyopita, aliwekwa kwenye wodi ya wagonjwa wasio na tumaini la kupona. Kasisi wa Kanisa Othodoksi alitembelea wodi hiyo ili wagonjwa waungame dhambi zao kabla ya kufa. Tatyana aliona kwamba mwanamke mmoja katika wodi hiyo alijikakamua kumpa kasisi huyo pesa. Baada ya kasisi kuondoka, Tatyana alimwuliza mwanamke huyo ikiwa alijihisi vizuri zaidi. “Hapana,” mwanamke huyo alijibu akiwa amekata tamaa, “sikuelewa chochote alichosema.” Tatyana alimhubiria habari njema kuhusu tumaini la ufufuo. Mwanamke huyo alimshukuru Tatyana na kumwambia, “Sasa ninahisi vizuri!” Msimamizi wa hospitali hiyo alisikia kilichotukia na kumwambia kasisi huyo asirudi tena. Badala yake, Tatyana aliwekwa kwenye wodi nyingine ili azungumze na wagonjwa wengine. Pia, msimamizi huyo aliuliza mahali ambapo Mashahidi wa Yehova wanafanyia mikutano yao. Kabla ya kulazwa hospitalini, Tatyana alikuwa amemwomba Yehova ampe nguvu za kuendelea kuhubiri. Ana hakika kwamba Yehova alijibu sala yake. Mwezi huo aliripoti zaidi ya saa 100! Ingawa tangu wakati huo afya yake imezorota na hawezi kutoka nyumbani, bado anatembelewa na watu aliowahubiria alipokuwa akienda hospitalini mara kwa mara.

Georgia

Dada wawili ambao ni mapainia wa pekee wa muda, walitumwa kuhubiri katika eneo ambalo halikuwa na Mashahidi wa Yehova. Walipokuwa wakikagua eneo lao jipya, walipotea. Walichoka na kuhisi baridi kwa sababu ya kutembea kwenye theluji iliyofika kwenye magoti wakitafuta njia ya kurudi nyumbani. Mwishowe, waliona nyayo karibu na nyumba fulani na wakapaaza sauti kuita wenye nyumba. Mwanamke anayeitwa Khatuna alitoka kwenye lango na mara moja akawakaribisha ndani ya nyumba iliyokuwa na joto, jambo walilothamini sana. Baada ya kuhakikisha kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova, Khatuna aliwaeleza kwamba wakati dada hao walipokuwa wakitangatanga kwenye theluji wakiwa wamepotea njia, yeye na familia yake walikuwa wakimwomba Mungu awaonyeshe kweli. Dakika chache baadaye, mapainia hao wawili walifika kwenye nyumba yao. Khatuna alisema kwamba ana hakika hilo lilikuwa jibu kwa sala yao! Leo, watu wanne katika familia hiyo wanajifunza Biblia na wawili kati yao—Khatuna na mama-mkwe wake—ni wahubiri ambao hawajabatizwa.

Uingereza

Reston, ambaye hakuwa amewahi kuanzisha funzo la Biblia kwa njia ya moja kwa moja, aliamua kujaribu njia hiyo. Kabla ya kubisha mlango wa kwanza, alisali kifupi, akimwomba Yehova amsaidie awe na maoni yanayofaa. Kisha akamweleza mwenye nyumba anayeitwa Andy mpango wa kujifunza Biblia. Andy alikubali mara moja kujifunza. Reston aliamua kumletea kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? baadaye siku hiyo. Alipokuwa akirudi huko kwa basi, Reston aligundua kwamba dereva wa basi hilo ni mtu aliyempelekea Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa ukawaida. Kwa sababu alikuwa ametiwa moyo na jinsi Andy alivyoitikia asubuhi, aliamua kumwonyesha dereva mpango wetu wa kujifunza Biblia na watu bila malipo punde tu basi litakapofika mwisho wa safari.

Wakati huohuo, abiria fulani mzee alitambua kwamba Reston ni Shahidi na akamwomba amtembelee rafiki yake mgonjwa ili amwombee. Reston alisema angefurahi kuzungumza naye na kumfariji kupitia Maandiko. Alitumia ile nakala aliyokuwa nayo ya kitabu Biblia Inafundisha, kumwonyesha abiria huyo jinsi funzo la Biblia linavyoweza kumsaidia. Mwanamke huyo alisema angependa funzo kama hilo. Kijana aliyekuwa ameketi upande ule mwingine alisikiliza mazungumzo yao. Alivutiwa na picha katika kitabu hicho. Hivyo kwa furaha Reston akaamua kumpa. Basi lilipofika mwisho wa safari, Reston alimweleza yule dereva kuhusu mpango wa kujifunza Biblia nyumbani bila malipo. Alishangaa dereva huyo alipokubali kwa shauku na kusema kwamba alikuwa na maswali mengi ya Biblia. Mara moja, Reston alienda kwa ndugu aliyeishi karibu ili kupata nakala nyingine ya kitabu Biblia Inafundisha na mwishowe akafika nyumbani kwa Andy jioni. Andy alichukua kitabu hicho kwa furaha. Alianza kujifunza Biblia na punde si punde akaanza kuishi kupatana na mambo aliyojifunza. Andy na yule dereva wa basi wanahudhuria mikutano, na Reston anaongoza mafunzo ya Biblia 15 ambayo aliyaanzisha kwa njia ya moja kwa moja. Sasa anahakikisha kwamba ana nakala kadhaa za kitabu Biblia Inafundisha anapohubiri.

François na Monica pamoja na watoto wao wawili, walienda kwenye gari lao baada ya kuhubiri asubuhi. Hata hivyo, Shaé, binti yao mwenye umri wa miaka miwili na nusu hakutaka kuingia kwenye gari kabla ya kumpa mtu trakti yake ya mwisho. Wakati huo, gari fulani lilisimama upande ule mwingine wa barabara, na wanawake wawili wakashuka. Shaé alimpa mmoja wao trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani, na Monica akamweleza trakti hiyo inazungumzia nini. Mwanamke huyo anayeitwa Sierra, alipendezwa na akamwalika Monica nyumbani kwake kujifunza Biblia pamoja na dada zake wenye umri wa chini ya miaka 20. Walipojifunza mara ya kwanza, Sierra aliuliza kama wana wake wawili wanaweza kujifunza Biblia. Baadaye, mwana wa dada ya Sierra alianza kujifunza pia. Mwishowe, hata Sierra alikubali kujifunza. Kisha mume wake akaanza kujifunza pia. Halafu mama ya Sierra, na vilevile watu wengine katika familia na marafiki, wakataka kujifunza Biblia. Azimio la Shaé la kupeana trakti yake ya mwisho lilifanya watu 11 waanze kujifunza Biblia. Wanne kati ya wanafunzi hao wanahudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida.

Italia

Jennifer yuko katika Kutaniko la Milan la Kirusi. Alikuwa amezungumza kwa simu mara kadhaa na mwanamke Mukrainia anayeitwa Valentina, lakini hakuwa amekutana naye. Siku moja walipanga kukutana kwenye kituo cha gari-moshi la chini ya ardhi. Ili Jennifer aweze kumtambua, Valentina alimwambia kwamba atavaa koti jekundu. Jennifer alifika kwenye kituo na kumwona mwanamke aliyevaa koti jekundu ambaye alikuwa akimtafuta mtu fulani. Jennifer alimkaribia na kusema, “Jambo, je, wewe ni Valentina?” Mwanamke huyo alisema yeye ni Valentina, hivyo Jennifer akamwambia, “Mimi ni Jennifer.” Lakini mwanamke huyo hakumjibu. Akiwa amechanganyikiwa kidogo, Jennifer alimwuliza, “Ulikuwa unaningoja, sivyo?”

“Hapana,” mwanamke huyo akajibu. Kumbe mwanamke huyo alikuwa Mukrainia, aliitwa Valentina, na alikuwa amevaa koti jekundu; lakini alikuwa akimngoja mtu mwingine! Jennifer alicheka na kumweleza kisa chote. Pia, alitaka kumweleza jambo fulani katika Biblia alilokuwa ametayarisha kwa ajili ya yule Valentina mwingine. Valentina alikubali na akasikiliza kwa makini. Baadaye alimwonyesha Jennifer karatasi aliyokuwa ameandika sura yote ya Zaburi 91 kwa mkono, na kumweleza kwamba aliipenda Biblia. Jennifer alianza kujifunza Biblia na Valentina huyu. Namna gani yule Valentina mwingine? Baadaye Jennifer alikutana naye, na yeye pia akaanza kujifunza Biblia.

Rumania

Ndugu fulani alimtembelea mtu aliyejuana naye na kuzungumza naye na mke wake kuhusu mambo fulani katika Biblia. Walitaka hasa kusikia Biblia inafundisha nini kuhusu uhusiano kati ya mume na mke, lakini ilikuwa vigumu kwao kupata wakati wa kuzungumzia Biblia. Mtu huyo na mke wake walithamini kuwa na afya nzuri, kwa hiyo mume alikuwa akikimbia kilomita nane kila siku. Baada ya kujaribu mara kadhaa kuendeleza mazungumzo hayo ya Biblia, ndugu huyo aliamua kumwuliza mtu huyo kama wanaweza kukimbia pamoja. Mtu huyo alikubali kwa furaha. Hata hivyo, ndugu huyo hakuwa amefanya mazoezi yoyote, na punde si punde alitambua kwamba kuhubiri na kukimbia wakati uleule kunachosha! Ndugu huyo alisema, “Nilihubiri nikiwa nimevaa nguo za michezo na bila Biblia, nikinukuu maandiko niliyokumbuka.” Baada ya kukimbia mara kadhaa, mume na mke huyo walipendezwa zaidi, nao wakaanza kujifunza Biblia nyumbani kwa ukawaida. Sasa mtu huyo ni mhubiri ambaye hajabatizwa. Anahubiri kwa bidii na amejiandikisha kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi pamoja na mwana na binti yake.

OCEANIA

IDADI YA NCHI 30

IDADI YA WATU 37,545,115

IDADI YA WAHUBIRI 97,329

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 55,266

Australia

Ndugu fulani painia anaandika: “Daktari mmoja anayeitwa Pam aliomba nimtembelee kwa ukawaida ili kumpelekea magazeti ya karibuni. Ana shughuli nyingi sana, na nilimpata nyumbani mara moja tu katika muda wa miezi sita, kwa hiyo, nilikuwa nikiacha magazeti na barua fupi ya kirafiki chini ya mlango wake. Baada ya kujaribu kwa miezi saba kukutana na Pam, niliacha magazeti chini ya mlango wake pamoja na mwaliko wa kuhudhuria kusanyiko la wilaya lililokuwa linakaribia. Pia nilimwachia namba yangu ya simu lakini hakunipigia. Mwezi wa Novemba, baada ya kusanyiko, nilimtembelea tena na nikapata barua fupi kwenye mlango wake.

“Pam aliandika kwamba alifurahia sana kusoma magazeti hayo, na alikuwa akiwapa wafanyakazi wenzake. Wao nao waliwapa wagonjwa wao hospitalini. Alinieleza jinsi alivyofurahia ‘mkutano.’ Alikuwa amesoma ule mwaliko na akaomba ruhusa ya siku tatu ili ahudhurie. Alinieleza kwamba alitoa nakala za mwaliko huo na kuziweka kwenye visanduku vya kuwekea barua vya wafanyakazi wenzake. Aliambatanisha nakala hizo na barua fupi ya kuwaomba wampigie simu kama wangependa kuhudhuria. Kufikia mwisho wa juma hilo, wafanyakazi wenzake 16 ambao ni madaktari, pia waliomba ruhusa ya siku tatu ili wahudhurie. Watu hao wote 17 wenye kupendezwa walihudhuria kusanyiko hilo kwa siku tatu kwa sababu ya mwaliko mmoja ulioachwa chini ya mlango! Sasa Pam anajifunza Biblia kwa ukawaida akitumia kitabu Biblia Inafundisha na amepanga kuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja na wote waliohudhuria kusanyiko.”

Ndugu mwingine anasema: “Nilipokuwa nikipita karibu na nyumba ambayo Mashahidi walikuwa wameambiwa wasihubiri, nilimwona mwanamume na mwanamke nje ya nyumba hiyo wakilia kwa huzuni. Singeweza kuwapita kwa kuwa ilionekana wazi kwamba walihitaji msaada fulani, kwa hiyo niliwakaribia na kuwauliza kama ningeweza kuwasaidia. Mume na mke huyo walinialika ndani ya nyumba yao na kuanza kunieleza matatizo yao. Hawakuwa wamemwona binti yao kwa miaka mitatu. Mke huyo alihitaji kufanyiwa upasuaji kwa sababu ya kansa, na hakuwa na hakika kama angepona. Alikuwa na wasiwasi kwamba huenda asimwone binti yake tena. Siku kadhaa kabla, walikuwa wamemwomba kasisi wa kanisa lao awasaidie, lakini hakuchukulia jambo hilo kwa uzito na hakufanya lolote. Niliwaonyesha Maandiko kadhaa yanayosema kwamba Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo.

“Baada ya saa moja hivi, mlango ulibishwa. Mwanzoni nilifikiri ni kasisi wa kanisa lao. Lakini mlango ulipofunguliwa tuliona mwanamke aliyevalia vizuri. Kumbe alikuwa ni binti yao aliyekuwa amepotea kwa muda mrefu! Hali hiyo ilikuwa yenye kugusa hisia sana, hivyo nikapendekeza kwamba ingefaa niondoke. Lakini, nilishangaa binti huyo aliposema hataki niende kwa sababu alitaka kuwaambia wazazi wake jambo fulani. Aliwaeleza kwamba alikuwa amejiingiza katika ulevi na utumiaji wa dawa za kulevya na alikuwa akiharibu maisha yake, lakini funzo la Biblia lilimfanya arudi nyumbani kuwaona. Alikuwa amebatizwa hivi karibuni na kuwa Shahidi wa Yehova.”

Siku kadhaa baadaye, kasisi yule aliwatembelea, nao wakamwambia kwamba binti yao alikuwa amerudi kwa sababu amekuwa Shahidi wa Yehova. Aliondoka kwenye nyumba hiyo bila kusema chochote. Alipokuwa akiondoka, baba ya binti huyo alimwita na kumwambia achukue barua iliyokuwa mezani ambayo yeye na mkewe waliandika wakitaka majina yao yaondolewe kwenye orodha ya kanisa hilo.

Papua New Guinea

Kikundi cha ndugu na dada 23 walienda kuhubiri kwenye eneo lisilohubiriwa mara nyingi. Walisafiri kwa miguu, lakini haikuwa rahisi kwa sababu walihitaji kupanda milima na kuvuka mito. Katika kijiji kimoja dada fulani alikutana na kasisi wa Kanisa la Anglikana ambaye alifurahi kusikia ufafanuzi wa andiko la Danieli 2:44. Alimwambia dada huyo, “Huku sisi ni kama kondoo waliopotea.” Alichukua magazeti na broshua na akaomba apewe Biblia.

Siku tatu baadaye, katika kijiji kingine, dada wawili walizungumza na wanawake wawili vijana ambao walifurahia kusikiliza ujumbe wa Ufalme. Baba yao alipotoka shambani alasiri hiyo, walimwambia mambo waliyojifunza katika Biblia. Baba yao alisema kwamba angependa kusikiliza ujumbe huo mzuri yeye mwenyewe. Alipanga kuonana na ndugu na dada wote kwenye nyumba walimokuwa wakiishi. Kwa kuwa mtu huyo alikuwa kiongozi wa kijiji hicho, alipanga chakula kipikwe na kupelekewa ndugu hao. Baadaye jioni aliwasili akiwa amebeba taa yake, huku akiandamana na wanakijiji wengine. Walisema, “Tulishangaa kuwaona, kwa sababu hii ni mara ya kwanza kwa Mashahidi wa Yehova kuja kijijini mwetu.” Walionyeshwa kwamba andiko la Mathayo 24:14 ndilo lililowafanya wawatembelee. Walielezwa kuhusu baraka za Ufalme na wakaachiwa vichapo.

Siku ya tano ya safari yao, ndugu hao walifika kwenye kijiji kimoja saa saba hivi alasiri. Wanakijiji walifikiri ndugu hao watalala hapo, hivyo wakaanza kuwatayarishia kibanda kisicho na kuta. Hata hivyo, ndugu waliwaeleza kwamba walitaka kuzungumza na kila mtu, kisha waondoke siku hiyohiyo. Waliwahubiria watu wote, kutia ndani kiongozi wao, ambaye alichukua vichapo na kuwapa ndugu nazi, ndizi, na papai.

Fiji

Katika eneo fulani la mashambani, mapainia wanasafiri kwa miguu wanapohubiri, na njia wanazopitia zina vumbi au matope. Nagamma na binti yake, Reshma, ambao ni mapainia wa kawaida, walimwalika Ushla ambaye ni dada kipofu, aandamane nao na kufanya upainia kwa mwezi mmoja. Walitembea kwa kilomita nyingi kila siku wakiwa wamemshika mikono. Familia moja iliyokuwa imeketi nje ya nyumba yao siku moja yenye joto, walitazama dada hao watatu wakijaribu kuepuka kuingia kwenye vidimbwi vidogo kwenye barabara yenye matope. Kisha wakamwona yule dada kipofu akiingia kwenye kidimbwi na kujirushia matope kwenye mguu. Dada hao wengine walisimama na kumpangusa. Akitaka sana kujua yaliyokuwa yakiendelea, baba wa familia hiyo aliwaita dada hao. Alisema: “Kila siku tunawaona nyinyi watatu mkitembea. Mnaenda wapi?” Walimweleza kwamba walikuwa wakienda kuongoza funzo la Biblia. Mtu huyo aliwaambia kwamba ikiwa ujumbe wao ni muhimu sana hivi kwamba wanaenda mbali hivyo ili kuwafundisha watu, angependa kuusikia pia! Familia hiyo ilianza kujifunza.

Guam

Liza, mwanamke kutoka Filipino, aliishi na kufanya kazi za nyumbani katika kisiwa cha Tinian. Mara nyingi Mashahidi wa Yehova walipotembelea nyumba hiyo, aliwaomba Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ingawa alisema kwamba alipenda magazeti hayo, alikuwa akiyatumia kuwashia moto.

Mapema katika mwaka wa 2007, Liza alipoteza kazi yake, na kwa kuwa hakuwa na mahali pa kuishi, alilala ufuoni. Siku moja alitembea karibu na Jumba la Ufalme, ambako dada wawili walikuwa wameketi nje chini ya kivuli. Walimwalika Liza ale maembe, na walikuwa na mazungumzo ya kirafiki. Siku iliyofuata alipopita nje ya Jumba la Ufalme, dada hao walizungumza naye tena, na katika mazungumzo hayo alisema, “Ninatumaini siku moja nitaweza kuja kwenye kanisa lenu.” Ingawa dada hao waliaibika kidogo kwamba hawakuwa wamemwalika tayari, walimtia moyo ahudhurie mkutano jioni hiyo. Alikubali mwaliko wao, akitumaini kwamba Mashahidi wangemsaidia kupata kazi.

Wakati wa mkutano Liza alipendezwa na unyoofu wa ndugu na dada na jinsi walivyowahangaikia watu. Hilo lilimfanya Liza alie, kwa kuwa alikumbuka kwamba sababu iliyomfanya aje mkutanoni ni ya ubinafsi. Pia alikumbuka magazeti yote aliyoteketeza. Kwa sababu aliguswa moyo na upendo alioonyeshwa na ndugu na dada, tangu wakati huo hakukosa mkutano wowote na alijifunza Biblia kwa ukawaida. Alipata kazi, akawa mhubiri ambaye hajabatizwa, na akabatizwa Februari 2008.

[Picha katika ukurasa wa 45]

Madalena

[Picha katika ukurasa wa 48]

Ndugu na dada wakifurahia Funzo la “Mnara wa Mlinzi” katika mashua

[Picha katika ukurasa wa 50]

Dada Barker akingoja kwa subira kuwahubiria wapita-njia

[Picha katika ukurasa wa 53]

Purnamaya akitengeneza kokoto ili kuitegemeza familia yao

[Picha katika ukurasa wa 54]

Kumhubiria mwanamke Mhindi katika shamba la mipira

[Picha katika ukurasa wa 57]

Reston akijifunza na Andy

[Picha katika ukurasa wa 58]

Shaé

[Picha katika ukurasa wa 63]

Nagamma na Reshma wakimsaidia Ushla

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki