-
Acheni Tukirihi Lililo OvuMnara wa Mlinzi—1997 | Januari 1
-
-
Kwa mtu aliyekuwa mwenye kuwasumbua watoto kingono kabla ya kubatizwa, huenda kukawa na tokeo jingine. Ajifunzapo kweli, yeye anatubu na kugeuka, haleti dhambi hiyo katili ndani ya kutaniko. Baadaye huenda akafanya maendeleo mazuri, akashinda kabisa misukumo yake mibaya, na hata kuwa mwenye mbetuko wa ‘kufikilia’ wadhifa wenye madaraka kutanikoni. Lakini namna gani, ikiwa anahitaji bado kukabili sifa mbaya katika jumuiya ya kuwa mwenye kuwasumbua watoto kingono hapo zamani? Je, angekuwa “asiyelaumika, . . . [mwenye] ushuhuda bora kutoka kwa watu walio nje, . . . [asiye na] shtaka”? (1 Timotheo 3:1-7, 10; Tito 1:7) La, asingekuwa hivyo. Kwa sababu hiyo, yeye asingekuwa na sifa za kustahili kuwa na mapendeleo ya kutaniko.
-
-
Acheni Tukirihi Lililo OvuMnara wa Mlinzi—1997 | Januari 1
-
-
Namna Gani Mwenye Kuwasumbua Watoto Kingono?
Namna gani ikiwa Mkristo mtu mzima aliyebatizwa amsumbua mtoto kingono? Je, huyo mtenda-dhambi ni mwovu sana hivi kwamba Yehova hatamsamehe kamwe? Si lazima iwe hivyo. Yesu alisema kwamba ‘ukufuru dhidi ya roho takatifu’ ulikuwa hausameheki. Na Paulo alisema kwamba hakuna tena dhabihu yoyote kwa mtu anayezoea dhambi kwa kusudi ijapokuwa anaijua kweli. (Luka 12:10; Waebrania 10:26, 27) Lakini hakuna kokote ambako Biblia husema kwamba Mkristo mtu mzima amtendaye mtoto vibaya kingono—iwe ni kwa ngono ya maharimu au vingine—hawezi kusamehewa. Kwa kweli, dhambi zake zaweza kuoshwa ziwe safi akitubu kwa moyo mweupe kutoka moyoni na kugeuza mwenendo wake. Hata hivyo, huenda bado akalazimika kung’ang’ana na misukumo mibaya ya kimwili aliyositawisha. (Waefeso 1:7) Na huenda kukawa na matokeo ambayo hawezi kuepuka.
Kwa kutegemea sheria ya nchi anamoishi, ni yamkini kwamba huyo mwenye kusumbua kingono atalazimika kufungwa gerezani kwa muda fulani au kukabili adhabu nyingine kutoka kwa Serikali. Kutaniko halitamkinga dhidi ya hayo. Juu ya hayo, mtu huyo amefunua udhaifu mzito ambao ni lazima ufikiriwe kutoka wakati huo. Ikiwa aonekana kuwa mwenye kutubu, atatiwa moyo kufanya maendeleo ya kiroho, kushiriki katika utumishi wa shambani, hata kuwa na sehemu katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na katika sehemu zisizo za kufundisha katika Mkutano wa Utumishi. Ingawa hivyo, hilo halimaanishi kwamba atakuwa na sifa za kustahili kutumikia katika wadhifa wenye madaraka kutanikoni. Ni zipi sababu za Kimaandiko kwa jambo hilo?
Kwanza, lazima mzee awe “mwenye kujidhibiti.” (Tito 1:8) Ni kweli, hakuna yeyote wetu aliye mwenye kujidhibiti kikamilifu. (Waroma 7:21-25) Lakini Mkristo mtu mzima aliyejiweka wakfu atumbukiaye katika dhambi ya kumtenda mtoto vibaya kingono afunua udhaifu wa kimwili usio wa kiasili. Mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba yaelekea mtu mzima wa jinsi hiyo atasumbua watoto wengine kingono. Ni kweli, si kila mtu mwenye kusumbua mtoto kingono arudiaye dhambi hiyo, lakini wengi hufanya hivyo. Na kutaniko haliwezi kuchunguza mioyo ili kuona ni nani atakayewasumbua na nani hatawasumbua watoto kingono tena. (Yeremia 17:9) Kwa sababu hiyo, shauri la Paulo kwa Timotheo lahusika kwa mkazo katika kisa cha watu wazima waliobatizwa ambao wamewasumbua watoto kingono: “Usiweke kamwe mikono yako haraka-haraka juu ya mtu yeyote; wala usiwe mshiriki katika dhambi za wengine.” (1 Timotheo 5:22) Ili kuwakinga watoto wetu, mtu ajulikanaye kuwa alikuwa mwenye kuwasumbua watoto kingono hana sifa za kustahili kuwa na wadhifa wenye madaraka kutanikoni. Isitoshe, hawezi kuwa painia wala kutumika katika utumishi mwingine wa pekee, wa wakati wote.—Linganisha ile kanuni kwenye Kutoka 21:28, 29.
Huenda wengine wakauliza, ‘Je, wengine hawakufanya dhambi za namna nyinginezo na kuonekana kama wametubu, kisha wakarudia dhambi yao baadaye?’ Ndiyo, hilo limetukia, lakini kuna mambo mengine ya kufikiria. Kwa kielelezo, mtu akimtongoza mtu mzima mwingine, huyo mtu mzima apaswa kuweza kukinza utongozi wake. Ni rahisi zaidi kuwadanganya, kuwatatanisha, au kuwatisha watoto. Biblia husema juu ya ukosefu wa hekima wa watoto. (Mithali 22:15; 1 Wakorintho 13:11) Yesu alitumia watoto kuwa kielelezo cha unyenyekevu wenye weupe wa moyo. (Mathayo 18:4; Luka 18:16, 17) Weupe wa moyo wa watoto hutia ndani kuwa bila uzoefu wowote. Watoto walio wengi ni wanyoofu, wenye hamu ya kupendeza, na hivyo rahisi kutendwa vibaya na mtu mzima mwenye kutunga hila wanayemjua na kuwa na itibari katika yeye. Kwa hiyo, kutaniko lina daraka mbele ya Yehova la kuwakinga watoto walo.
Watoto waliozoezwa vema hujifunza kutii na kuwaheshimu wazazi wao, wazee, na watu wazima wengine. (Waefeso 6:1, 2; 1 Timotheo 5:1, 2; Waebrania 13:7) Ungekuwa upotovu wa kushtua ikiwa mmoja wa watu hao wenye mamlaka angetumia vibaya itibari yenye moyo mweupe ya mtoto huyo ili kumtongoza au kumlazimisha anyenyekee matendo ya kingono. Mara nyingi wale ambao wamesumbuliwa kingono katika njia hiyo hung’ang’ana kwa miaka mingi ili kushinda vurugu ya kihisia-moyo inayotokea. Kwa sababu hiyo, mtu huyo mwenye kuwasumbua watoto kingono atapatwa na nidhamu kali na vizuizi vikali vya kutaniko. Jambo la kuhangaikia si wadhifa wake akiwa mwenye mamlaka, bali ni utakato usio na waa wa kutaniko.—1 Wakorintho 5:6; 2 Petro 3:14.
Mwenye kuwasumbua watoto kingono akitubu kwa moyo mweupe, yeye atatambua hekima ya kutumia kanuni za Biblia. Akijifunza kikweli kukirihi lililo ovu, atachukia sana lile alilofanya na kung’ang’ana ili aepuke kuirudia dhambi yake. (Mithali 8:13; Waroma 12:9) Zaidi, kwa hakika atamshukuru Yehova kwa ukubwa wa upendo Wake, ambao kwa sababu yao mtenda-dhambi mwenye kutubu, kama vile yeye, aweza bado kumwabudu Mungu wetu mtakatifu na kutumaini kuwa miongoni mwa ‘wanyoofu’ watakaokaa duniani milele.—Mithali 2:21.
-