Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tafuta Mashauri Mazuri
    Amkeni!—2007 | Agosti
    • Hatua ya 1

      Tafuta Mashauri Mazuri

      Kwa nini hatua hii ni muhimu? Mara ya kwanza wazazi wanapombeba mtoto wao mchanga, huenda wakawa na hisia mbalimbali. “Nilikuwa na shangwe na niliduwaa,” anasema Brett, baba anayeishi Uingereza. “Lakini pia nilihisi kuwa nina jukumu kubwa sana ambalo sikuona ikiwa ninaweza kulitimiza.” Monica, mama anayeishi Argentina, anasema: “Nilikuwa na wasiwasi kwamba sitaweza kumtimizia binti yangu mahitaji yake. Nilijiuliza, ‘Je, nitaweza kumlea afikie kuwa mtu mzima mwenye kutegemeka?’”

      Je, unaweza kuelewa shangwe na wasiwasi wa wazazi hao? Kwa kweli, kati ya kazi ambazo mtu anaweza kufanya, kumlea mtoto ni kazi inayochosha na kutamausha lakini inayoridhisha na kuthawabisha. Baba mmoja alisema, “mtu huwa mtoto mara moja tu maishani hivyo una nafasi moja tu ya kumlea.” Kwa kuwa sehemu kubwa ya afya na furaha ya watoto hutegemea hasa uvutano wa wazazi, huenda ukataka sana kupata mashauri yanayotegemeka ya jinsi unavyoweza kuwa mzazi bora.

      Tatizo: Inaonekana kwamba kila mtu ana mashauri ya jinsi ya kulea watoto. Zamani wazazi walipopata mtoto wao wa kwanza walifuata hasa mfano wa wazazi wao au mafundisho yao ya kidini. Lakini katika nchi kadhaa, familia zinazorota na dini haziwavutii tena watu. Kwa sababu hiyo, wazazi wengi hutafuta mashauri kutoka kwa wataalamu wa kulea watoto. Mambo fulani ambayo wataalamu hao husema yanategemea kanuni zinazofaa. Kwa upande mwingine, mashauri ya wataalamu kama hao yanaweza kupingana na baada ya muda yanaweza kuonwa kuwa yamepitwa na wakati.

      Suluhisho: Tafuta mashauri ya Yule anayejua vizuri zaidi jinsi ya kuwalea watoto—Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu. (Matendo 17:26-28) Neno lake, Biblia, lina mashauri ya moja kwa moja na mifano halisi ambayo inaweza kukusaidia kuwa mzazi bora. Anaahidi hivi, “Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.”—Zaburi 32:8.

      Mungu anawapa wazazi mashauri gani ambayo yanaweza kuwasaidia kulea watoto wenye furaha?

      [Blabu katika ukurasa wa 3]

      “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.”—Methali 3:5

  • Onyesha Upendo Nyumbani
    Amkeni!—2007 | Agosti
    • Hatua ya 2

      Onyesha Upendo Nyumbani

      Kwa nini hatua hii ni muhimu? Watoto wanahitaji upendo na wanapoukosa, hawakui vizuri. Katika miaka ya 1950, M. F. Ashley Montagu, mtaalamu wa tabia na tamaduni za wanadamu aliandika hivi: “Mwanadamu anahitaji hasa upendo ili akue vizuri; upendo ndio chanzo cha afya nzuri hasa katika miaka sita ya kwanza.” Watafiti wa kisasa wanakubaliana na maneno ya Montagu aliposema kwamba “watoto huathiriwa sana wasipoonyeshwa upendo wa kutosha.”

      Tatizo: Kuishi katika ulimwengu huu usio na upendo na wenye ubinafsi hufanya hali ya familia iwe ngumu. (2 Timotheo 3:1-5) Huenda wenzi wa ndoa wakaona kwamba mikazo ya kihisia na kifedha inayotokana na kuwalea watoto huongeza matatizo katika ndoa. Kwa mfano, wenzi wa ndoa ambao tayari wana shida ya kuwasiliana huongeza matatizo hayo wanapotofautiana kuhusu jinsi wanavyopaswa kuwatia nidhamu na kuwapa watoto wao zawadi.

      Suluhisho: Panga muda wa kuwa pamoja na familia. Pia, wenzi wa ndoa wanahitaji kupanga wakati wao wa kuwa pamoja. (Amosi 3:3) Tumieni vizuri wakati mnaopata watoto wanapolala. Msiruhusu televisheni ichukue wakati huo muhimu. Endeleeni kuonyeshana upendo katika ndoa yenu. (Methali 25:11; Wimbo wa Sulemani 4:7-10) Badala ya “kutafuta makosa” wakati wote, tafuta njia za kumpongeza mwenzi wako kila siku.—Zaburi 103:9, 10; Methali 31:28.

      Waambie watoto wako kwamba unawapenda. Yehova Mungu aliwawekea wazazi kielelezo kizuri kwa kumwonyesha Mwana wake, Yesu, upendo waziwazi. (Mathayo 3:17; 17:5) Fleck, baba anayeishi Austria, anasema: “Nimegundua kwamba watoto ni kama maua fulani. Kama vile mimea hiyo midogo hugeuka kuelekea jua ili kupata mwangaza na joto, watoto huwategemea wazazi wao ili wapate upendo na kuhakikishiwa kwamba wao ni washiriki wa familia wenye thamani.”

      Uwe umeoa au kuolewa au wewe ni mzazi asiye na mwenzi, ukisaidia familia yako kupendana na kumpenda Mungu, maisha ya familia yako yatakuwa bora.

      Lakini, Neno la Mungu linasema nini kuhusu wazazi kutumia mamlaka yao?

      [Blabu katika ukurasa wa 4]

      “Upendo . . . ni kifungo kikamilifu cha muungano.” —Wakolosai 3:14

  • Tumia Mamlaka Yako
    Amkeni!—2007 | Agosti
    • Hatua ya 3

      Tumia Mamlaka Yako

      Kwa nini hatua hii ni muhimu? Uchunguzi unaonyesha kwamba “watoto wanaolelewa na wazazi wanaotumia mamlaka yao ifaavyo, yaani wazazi wenye upendo lakini wanaoweka mipaka imara, hufanya vema shuleni, wana uhusiano mzuri na watu wengine, wanajiheshimu, na wana furaha kuliko watoto ambao wazazi wao huwaendekeza au ni wakali kupita kiasi,” linasema gazeti Parents.

      Tatizo: Kuanzia utoto hadi ujanani, watoto watapinga mamlaka yako. “Watoto hutambua haraka ikiwa wazazi wanaogopa kutumia mamlaka yao na ni wakati gani wazazi watakubali chochote wanachoombwa,” anaandika John Rosemond, mwandishi wa kitabu Parent Power! “Kuhusu suala la ‘ni nani mwenye mamlaka,’ ikiwa wazazi hawatatumia mamlaka yao, basi watoto watawatawala,” anasema mwandishi huyo.

      Suluhisho: Usihofu kwamba ukitumia mamlaka watoto wako watakuchukia au utawavunja moyo. Yehova Mungu, Mwanzilishi wa familia, hakukusudia watoto wawe na mamlaka ya kuamua jinsi familia itakavyoongozwa. Badala ya hivyo, yeye amewapa wazazi mamlaka na anawaamuru watoto hivi: “Watiini wazazi wenu.”—Waefeso 3:14, 15; 6:1-4.

      Unaweza kutumia mamlaka yako bila kuwakandamiza watoto. Kwa njia gani? Kwa kumwiga Yehova. Ingawa ana uwezo wa kuwalazimisha watoto wake wa kibinadamu wafanye mapenzi yake, yeye hutumia sifa zetu nzuri kutuchochea kufanya hivyo. “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto,” linasema Neno lake. (Isaya 48:18) Yehova anataka tumtii, si kwa sababu tunamwogopa isivyofaa, lakini kwa sababu tunampenda. (1 Yohana 5:3) Yeye hatazamii tufanye mengi kuliko uwezo wetu na anajua tutafaidika tukiishi kupatana na viwango vyake vya maadili.—Zaburi 19:7-11.

      Utapataje ujasiri wa kutumia mamlaka yako kwa usawaziko ukiwa mzazi? Kwanza, unapaswa kuamini kwamba Mungu anakutazamia utumie mamlaka yako. Pili, unapaswa kusadiki kwamba kuishi kupatana na viwango vya Mungu vya maadili kutakufaidi wewe na watoto wako pia.—Waroma 12:2.

      Ni mambo gani hususa unayopaswa kufanya ili kutumia mamlaka yako?

      [Blabu katika ukurasa wa 5]

      “Watie nidhamu watoto wako, . . . nao wataufurahisha moyo wako.”—Methali 29:17, New Revised Standard Version

  • Weka Sheria Zilizo Wazi na Utekeleze Adhabu Haraka
    Amkeni!—2007 | Agosti
    • Hatua ya 4

      Weka Sheria Zilizo Wazi na Utekeleze Adhabu Haraka

      Kwa nini hatua hii ni muhimu? Ronald Simons, mwanasosholojia katika Chuo Kikuu cha Georgia, anasema: “Ukweli wa mambo ni kwamba maisha ya watoto huwa mazuri wanapowekewa sheria zilizo wazi na kuadhibiwa kila mara wanapozivunja. Wazazi wasipofanya hivyo, watoto hujifikiria tu, huwa wenye ubinafsi, na wanakosa furaha, na hivyo wanafanya kila mtu akose furaha pia.” Neno la Mungu linasema hivi waziwazi: “Ikiwa unawapenda watoto wako, utawarekebisha.”—Methali 13:24, New Century Version.

      Tatizo: Kuweka sheria zinazofaa kuhusu jinsi watoto wako wanavyopaswa kujiendesha na kutekeleza adhabu sheria hizo zinapovunjwa huchukua wakati, jitihada, na uvumilivu. Na watoto huwa na mwelekeo wa kutaka kuvunja sheria hizo. Mike na Sonia, ambao wana watoto wawili, wanasema hivi kuhusu tatizo hilo: “Watoto ni watu wadogo wenye akili na tamaa zao wenyewe na mwelekeo wa kiasili wa kufanya dhambi.” Wazazi hao wanawapenda sana binti zao. Lakini wanakiri hivi, “Nyakati nyingine, watoto wanaweza kuwa na vichwa vigumu na wenye ubinafsi.”

      Suluhisho: Iga jinsi Yehova alivyoshughulika na taifa la Israeli. Njia moja ambayo Yehova aliwaonyesha watu wake upendo ilikuwa kwa kutaja waziwazi sheria ambazo alitaka wafuate. (Kutoka 20:2-17) Alionyesha wazi madhara ya kutotii sheria hizo.—Kutoka 22:1-9.

      Hivyo, kwa nini usiandike orodha ya sheria unazotaka watoto wako watii. Wazazi fulani wanapendekeza orodha ya sheria chache tu, kama tano hivi. Ni rahisi kuhakikisha kwamba orodha ya sheria chache inafuatwa na ni rahisi vilevile kuzikumbuka. Kando ya sheria hizo, andika adhabu. Hakikisha kwamba adhabu haipiti kiasi na kwamba uko tayari kuitekeleza. Pitieni sheria hizo mara kwa mara ili nyote, kutia ndani Baba na Mama, mjue mnachopaswa kufanya.

      Sheria zinapovunjwa, tekeleza adhabu haraka, na ufanye hivyo kwa utulivu, uthabiti, na kila mara kosa linapofanywa. Kumbuka: Usitoe adhabu ukiwa umekasirika; tulia kwanza. (Methali 29:22) Hata hivyo, usiiahirishe. Usijadiliane kuhusu adhabu utakayotoa. Ukiahirisha, mtoto wako atafikiri kwamba hahitaji kuchukua sheria hizo kwa uzito. Hilo linapatana na maneno haya ya Biblia: “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya.”—Mhubiri 8:11.

      Ni katika njia gani nyingine unaweza kutumia mamlaka kuwasaidia watoto wako?

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.”—Mathayo 5:37

  • Panga Ratiba na Kuifuata
    Amkeni!—2007 | Agosti
    • Hatua ya 5

      Panga Ratiba na Kuifuata

      Kwa nini hatua hii ni muhimu? Watu wengi wazima hufuata ratiba. Watu wengi hufanya kazi, huabudu, na kuburudika wakati fulani hususa. Wazazi watakuwa wakiwanyima watoto wao jambo fulani wasipowafundisha kupanga wakati wao na kufuata ratiba. Kwa upande mwingine, “uchunguzi unaonyesha kwamba kuwa na sheria na kufuata ratiba kunamfanya mtoto ahisi salama na kumfunza kujidhibiti na kujitegemea,” anasema Dakt. Laurence Steinberg, profesa wa saikolojia.

      Tatizo: Maisha yana pilikapilika nyingi. Wazazi wengi wanafanya kazi kwa saa nyingi, hivyo kwa kawaida hawana wakati mwingi wa kuwa na watoto wao. Kupanga na kudumisha ratiba kunahitaji kujidhabihu na jitihada nyingi hasa mwanzoni mtoto anapokataa kufuata ratiba.

      Suluhisho: Tumia kanuni ya shauri hili la Biblia: “Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.” (1 Wakorintho 14:40) Kwa mfano, watoto wakiwa bado wachanga, wazazi wengi wanaweka saa hususa za kwenda kulala. Hata hivyo, watoto wanapaswa kufurahia kipindi hicho. Tatiana anayeishi Ugiriki na ambaye ana binti wawili, anasema: “Watoto wakiingia kitandani, mimi huwapapasa-papasa na kuwaambia kile ambacho nilifanya walipokuwa shuleni. Kisha ninawauliza ikiwa wangependa kuniambia mambo ambayo wao wamefanya siku hiyo. Wanatulia. Mara nyingi wao huniambia yaliyo moyoni mwao.”

      Kostas, mume wa Tatiana, huwasomea wasichana wao hadithi. Anasema: “Wao hutaja mambo fulani kuhusu hadithi hiyo na mara nyingi wao huanza kuzungumzia mahangaiko yao. Nikiwalazimisha wanieleze mahangaiko yao, hawataniambia.” Bila shaka, watoto wanapozidi kukua itakubidi ubadilishe saa zao za kulala. Lakini ukidumisha utaratibu huo, inaelekea watoto wako wataendelea kutumia wakati huo kukueleza mahangaiko yao.

      Isitoshe, familia zinapaswa kuwa na zoea la kula angalau mlo mmoja kwa siku pamoja. Ili kudumisha utaratibu huo, huenda mkahitaji kubadili wakati wa kula. Charles ambaye ana binti wawili anasema: “Nyakati nyingine mimi hurudi nyumbani nikiwa nimechelewa. Ingawa nyakati nyingine mke wangu huwapa watoto chakula chepesi ili kutuliza njaa, kila mtu husubiri hadi tule pamoja tukiwa familia. Sisi huzungumzia utendaji wa siku hiyo, tunapitia Andiko moja, tunazungumzia matatizo, na kucheka pamoja. Lazima nikiri kwamba utaratibu huo umechangia sana kuwa na familia yenye furaha.”

      Ili ufanikiwe katika hatua hii, usiruhusu kufuatia vitu vya kimwili kuvuruge ratiba ya familia yako. Fuata shauri hili la Biblia: ‘Hakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.’—Wafilipi 1:10.

      Ni jambo gani lingine ambalo wazazi wanaweza kufanya ili kuboresha mawasiliano pamoja na watoto wao?

      [Blabu katika ukurasa wa 7]

      “Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.”—1 Wakorintho 14:40

  • Tambua Hisia za Mtoto Wako
    Amkeni!—2007 | Agosti
    • Hatua ya 6

      Tambua Hisia za Mtoto Wako

      Kwa nini hatua hii ni muhimu? Watoto wanataka na wanahitaji watu muhimu zaidi maishani mwao, yaani, wazazi wao wajue wanavyohisi. Ikiwa wazazi wana zoea la kuwapuuza watoto wanapowaeleza hisia zao, huenda watoto wakasita kuwaeleza hisia zao na hata wakaanza kutilia shaka uwezo wao wa kuhisi na kufikiri.

      Tatizo: Huenda watoto wakatilia chumvi wanapoeleza fikira na hisia zao. Ni kweli kwamba baadhi ya mambo ambayo watoto wanasema humshtua mzazi. Kwa mfano, mtoto aliyekata tamaa anaweza kusema, “Maisha yangu yamenichosha.”a Mzazi akisikia hilo anaweza kusema, “Hujui unalosema!” Huenda wazazi wakaogopa kwamba kutambua hisia hizo zisizofaa za mtoto kunamaanisha kuwa unakubaliana nazo.

      Suluhisho: Fuata shauri la Biblia la kuwa “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.” (Yakobo 1:19) Kumbuka kwamba Yehova Mungu alitambua hisia zisizofaa za watumishi wake wengi waaminifu na akaruhusu ziandikwe katika Biblia. (Mwanzo 27:46; Zaburi 73:12, 13) Kwa mfano, Ayubu alipokuwa akipatwa na majaribu makali, alisema anataka kufa.—Ayubu 14:13.

      Ni wazi kwamba mawazo na hisia fulani za Ayubu zilihitaji kurekebishwa. Lakini badala ya kupuuza hisia za Ayubu au kumnyamazisha, Yehova alimtendea Ayubu kwa heshima kwa kumruhusu kwa subira aumimine moyo wake. Baadaye tu ndipo Yehova alipomsahihisha kwa fadhili. Baba mmoja Mkristo alisema hivi, “Kwa kuwa Yehova ananiruhusu nimmiminie moyo wangu katika sala, nafikiri inafaa pia niwaruhusu watoto wangu wanimiminie hisia zao zinazofaa na zisizofaa.”

      Ukihisi kwamba unataka kumwambia mtoto wako “Sidhani kama unajua unachosema,” kumbuka sheria hii maarufu ya Yesu: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.” (Luka 6:31) Kwa mfano, wazia kwamba umenyanyaswa au kutamaushwa kazini kwa sababu labda ulifanya kosa fulani. Unamweleza rafiki yako wa karibu hisia zako na kumwambia kwamba huwezi kuendelea na kazi hiyo. Ungependa rafiki yako afanye nini? Je, ungetaka akuambie kwamba haumaanishi unachosema na kwamba umejiletea tatizo hilo mwenyewe? Au je, ungependa rafiki yako akuambie: “Lazima iwe ilikuwa vigumu kushughulika na hali hiyo. Inaonekana leo umeshinda vibaya”?

      Watoto na vilevile watu wazima wanaweza kukubali mashauri ikiwa wanahisi kwamba yule anayeyatoa anawaelewa vizuri na anaelewa matatizo wanayokabili. “Moyo wa mtu mwenye hekima hukifanya kinywa chake kionyeshe ufahamu, na kwenye midomo yake huongeza ushawishi,” lasema Neno la Mungu.—Methali 16:23.

      Unaweza kuhakikishaje kwamba shauri lolote unalotoa linachukuliwa kwa uzito?

      [Maelezo ya Chini]

      a Usiwapuuze watoto wako wanapozungumza kuhusu kujiua.

      [Blabu katika ukurasa wa 8]

      ‘Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu kwake.’—Methali 18:13

  • Fundisha kwa Kuweka Kielelezo
    Amkeni!—2007 | Agosti
    • Hatua ya 7

      Fundisha kwa Kuweka Kielelezo

      Kwa nini hatua hii ni muhimu? Matendo hufundisha. Mara nyingi maneno hueleza tu jambo. Kwa mfano, wazazi wanaweza kuwaambia watoto wao wawe na heshima na waseme ukweli. Hata hivyo, ikiwa wazazi haohao hufokeana au huwafokea watoto wao na kusema uongo ili kuhepa majukumu wasiyotaka kutekeleza, wanawafundisha watoto wao kwamba watu wazima wanapaswa kutenda hivyo. Kuwaiga wazazi ni “mojawapo ya njia bora ambazo watoto hujifunza,” anasema mwandishi Dakt. Sal Severe.

      Tatizo: Wazazi si wakamilifu. “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu,” akaandika mtume Paulo. (Waroma 3:23) Kuhusu kudhibiti maneno yetu, mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Ulimi, hakuna hata mmoja wa wanadamu anayeweza kuufuga.” (Yakobo 3:8) Isitoshe ni jambo la kawaida kwa watoto kuwaudhi sana wazazi. “Nilishangazwa na jinsi watoto wangu walivyonifanya nikasirike sana,” anasema Larry, baba ya watoto wawili ambaye kwa kawaida huwa mtulivu na hujidhibiti.

      Suluhisho: Jitahidini kuwa vielelezo bora, si wazazi wakamilifu. Na mtumie makosa mnayofanya mara kwa mara kuwafundisha watoto wenu. “Ikiwa ningewakasirikia watoto wangu au ikiwa ningefanya uamuzi mbaya ambao ungewaathiri,” anasema Chris baba ya watoto wawili, “ningekubali kosa langu na kuomba msamaha. Hilo liliwafundisha watoto wangu kwamba wazazi pia hufanya makosa na kwamba sisi sote tunapaswa kujitahidi kuboresha mwenendo wetu.” Kostas, aliyetajwa awali anasema: “Nimegundua kwamba ninapoomba msamaha kwa sababu ya kukasirika, binti zangu wanajifunza kuomba msamaha wao wanapokosea.”

      Yehova Mungu anasema: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Mtu aliye na mamlaka anaposema jambo moja na kufanya kinyume, hilo huwakasirisha watoto kama, au hata zaidi ya, linavyowakasirisha watu wazima. Kwa hiyo, mbona usijiulize maswali haya kila siku: Ikiwa nisingesema chochote siku nzima, watoto wangu wangejifunza nini kutokana na matendo yangu? Je, hayo ndiyo mambo ninayojaribu kuwafundisha kwa maneno?

      [Blabu katika ukurasa wa 9]

      “Je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe?”—Waroma 2:21

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Mzazi anapoomba msamaha, mtoto anajifunza kufanya vivyo hivyo

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki