Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yesu Ana Nguvu Kuliko Roho Waovu
    Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
    • Sura Ya 10

      Yesu Ana Nguvu Kuliko Roho Waovu

      JE, UNAKUMBUKA kilichomfanya malaika mmoja wa Mungu awe Shetani Ibilisi?— Tamaa yake ya kutaka kuabudiwa ilimfanya amwasi Mungu. Je, malaika wengine walimfuata Shetani?— Ndiyo. Biblia inawaita ‘malaika wa Shetani,’ au roho waovu.—Ufunuo 12:9.

      Je, hao malaika wabaya wanamwamini Mungu?— Biblia inasema hivi: ‘Roho waovu wanaamini Mungu yuko.’ (Yakobo 2:19) Lakini wanaogopa wakati huu. Na wanaogopa kwa sababu wanajua kwamba Mungu atawaadhibu kwa sababu ya mabaya ambayo wamefanya. Kwani wamefanya nini?—

      Biblia inasema kwamba malaika hao waliacha makao yao yanayowafaa mbinguni wakaja kuishi duniani kama wanadamu. Walikuja kwa sababu walitaka kufanya ngono pamoja na wanawake warembo duniani. (Mwanzo 6:1, 2; Yuda 6) Ngono ni nini?—

      Ngono ni tendo linalokuwa kati ya mwanamume na mwanamke, wanapokaribiana sana kwa njia ya pekee. Baadaye, mtoto anaweza kukua ndani ya tumbo la mama. Lakini ni makosa kwa malaika kufanya ngono. Mungu anaruhusu tu ngono kati ya mwanamume na mwanamke ambao wameoana. Kwa njia hiyo ikiwa mtoto atazaliwa, mume na mke wanaweza kumtunza.

      Malaika walipovaa miili ya wanadamu na kufanya ngono na wanawake duniani, watoto wao wakawa majitu. Walikuwa wabaya sana na waliwaumiza watu. Kwa sababu hiyo Mungu alileta gharika kubwa sana ili kuharibu majitu hao pamoja na wanadamu wote waovu. Lakini alimwambia Noa ajenge safina, au mashua kubwa sana, ili watu wachache waliofanya mema wapate kuokoka. Mwalimu Mkuu alisema kwamba ni muhimu kukumbuka yaliyotokea wakati wa Gharika.—Mwanzo 6:3, 4, 13, 14; Luka 17:26, 27.

      Unajua ni nini kilichowapata malaika wabaya wakati wa Gharika?— Waliacha miili yao ya wanadamu wakarudi mbinguni. Lakini hawangeendelea kuwa malaika wa Mungu, kwa hiyo wakawa malaika wa Shetani, au roho waovu. Namna gani watoto wao, wale majitu?— Walikufa katika Gharika, pamoja na watu wengine wote ambao hawakumtii Mungu.

      Tangu wakati wa Gharika, Mungu hakuwaruhusu roho waovu wawe kama wanadamu tena. Lakini hata kama hatuwaoni, roho waovu bado wanajaribu kuwashawishi watu wafanye mabaya. Wanasababisha matatizo mengi sasa kuliko wakati mwingine wowote. Hii ni kwa sababu walitupwa hapa duniani kutoka mbinguni.

      Unajua ni kwa nini hatuwezi kuwaona roho waovu?— Ni kwa sababu wana miili ya roho. Lakini tuna uhakika kwamba wako. Biblia inasema kwamba Shetani ‘anapotosha dunia nzima,’ akisaidiwa na roho waovu. —Ufunuo 12:9, 12.

      Je, sisi pia tunaweza kudanganywa na Ibilisi na roho wake waovu?— Ndiyo, inawezekana tusipokuwa waangalifu. Hata hivyo tusiogope. Mwalimu Mkuu alisema: ‘Ibilisi hana uwezo juu yangu.’ Tukiwa karibu sana na Mungu, yeye atatulinda kutokana na Ibilisi na roho wake waovu. —Yohana 14:30.

      Ni muhimu kujua ni mambo gani mabaya ambayo roho waovu watajaribu kutushawishi tufanye. Yafikirie. Roho waovu walifanya mambo gani mabaya walipokuja duniani?— Kabla ya Gharika, walifanya ngono na wanawake, jambo ambalo malaika hawakupaswa kufanya. Leo roho waovu wanafurahi wakati watu wanakosa kutii sheria ya Mungu kuhusu ngono. Hebu nikuulize, Ni nani pekee wanaopaswa kufanya ngono?— Ndiyo, ni wale tu waliooana.

      Leo wavulana na wasichana wadogo wanafanya ngono, lakini ni kosa kufanya hivyo. Biblia inataja ‘kiungo cha uzazi,’ au uume. (Mambo ya Walawi 15:1-3) Sehemu ya uzazi ya mwanamke inaitwa uke. Yehova aliumba sehemu hizi za mwili kwa kusudi la pekee la kufurahiwa na watu waliooana tu. Roho waovu wanafurahi wakati watu wanapofanya mambo ambayo Yehova anakataza. Kwa mfano, roho waovu hufurahi wakati mvulana na msichana wanapocheza na uume au uke wao. Hatutaki kuwafurahisha roho waovu, sivyo?—

      Kuna kitu kingine ambacho roho waovu wanapenda lakini Yehova anachukia. Unajua hicho ni nini?— Ni jeuri. (Zaburi 11:5) Watu wanapokuwa wakatili na kuumiza wengine, hiyo ni jeuri. Kumbuka kwamba hivyo ndivyo wana wa roho waovu, yaani, wale majitu walivyofanya.

      Roho waovu pia wanapenda kuogopesha watu. Wakati mwingine wanajifanya kuwa watu waliokufa. Hata wanaweza kuiga sauti za watu waliokufa. Kwa kufanya hivyo, roho waovu wanafanya watu waamini kwamba wafu wako hai na kwamba wanaweza kuongea na wale walio hai. Ndiyo, roho waovu wanafanya watu wengi waamini mizuka.

      Kwa hiyo tunapaswa kuwa macho tusidanganywe na Shetani na roho waovu. Biblia inatuonya hivi: ‘Shetani na watumishi wake hujaribu kujifanya waonekane kuwa malaika wazuri.’ (2 Wakorintho 11:14, 15) Lakini kwa kweli, roho waovu ni wabaya. Hebu tuone vile wanavyoweza kujaribu kutufanya tuwe kama wao.

      Watu wanajifunzaje kuhusu jeuri na ngono isiyo halali na kuhusu viumbe wenye miili ya roho na mashetani?— Je, si kwa kutazama vipindi fulani katika televisheni, sinema, mashirika mabaya shuleni, rafiki wabaya, na kusoma vitabu vya katuni? Je, kufanya mambo hayo hutuleta karibu na Mungu au karibu na Ibilisi na roho wake waovu? Unaonaje?—

      Unafikiri ni nani anayetaka tusikilize na kutazama mambo mabaya?— Bila shaka ni Shetani na roho wake waovu. Kwa hiyo, mimi na wewe tunahitaji kufanya nini?— Tunahitaji kusoma, kusikiliza, na kutazama mambo mazuri ambayo yatatusaidia kumtumikia Yehova. Je, unaweza kuwazia baadhi ya mambo hayo mazuri ambayo tunaweza kufanya?—

      Tukifanya mambo mazuri, hakuna haja ya kuogopa roho waovu. Yesu ana nguvu kuwashinda na wanamwogopa. Siku moja roho waovu walisema hivi walipomwona Yesu: “Je, umekuja kutuangamiza?” (Marko 1:24) Tutafurahi sana wakati ambapo Yesu atamharibu Shetani na roho wake waovu, sivyo?— Kwa sasa, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu atatulinda dhidi ya roho waovu tukiwa karibu naye na Baba yake wa mbinguni.

      Hebu tusome kuhusu yale tunayohitaji kufanya kwenye 1 Petro 5:8, 9 na Yakobo 4:7, 8.

      [Picha katika ukurasa wa 57]

      Malaika hawa walifanya mambo gani mabaya?

      [Picha katika ukurasa wa 58]

      Kwa nini kuna matatizo mengi duniani sasa kuliko wakati mwingine wowote?

      [Picha katika ukurasa wa 60]

      Ni nini kinachoweza kutokea tukitazama jeuri?

      [Picha katika ukurasa wa 61]

      Inafaa tufanye mambo gani mazuri?

  • Msaada wa Malaika wa Mungu
    Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
    • Sura Ya 11

      Msaada wa Malaika wa Mungu

      WATU wengine husema kwamba wao wanaamini tu kile wanachoweza kuona. Lakini huo ni upumbavu. Kuna vitu vingi vilivyoko ambavyo hatujawahi kuviona kwa macho yetu. Unaweza kutaja kimoja?—

      Namna gani hewa tunayopumua? Je, tunaweza kuihisi?— Nyosha mkono wako, kisha uupulizie hewa. Umesikia chochote?— Ndiyo, lakini huwezi kuiona hewa yenyewe, sivyo?—

      Tayari tumezungumza kuhusu watu wenye miili ya roho, ambao hatuwezi kuwaona. Tulijifunza kwamba wengine ni wazuri na wengine ni wabaya. Hebu taja watu wazuri wenye miili ya roho ambao hatuwezi kuwaona.— Kuna Yehova Mungu, Yesu, na kuna malaika wazuri. Je, kuna malaika wabaya pia? — Biblia inasema wako. Hebu niambie umejifunza nini kuwahusu.—

      Tunajua kwamba malaika wote wazuri na wabaya wana nguvu kutushinda. Mwalimu Mkuu alijua mambo mengi kuhusu malaika. Na hiyo ni kwa sababu yeye alikuwa malaika kabla ya kuzaliwa akiwa mtoto duniani. Aliishi na malaika wengine mbinguni. Alijua mamilioni ya malaika. Je, malaika hao wote wana majina?—

      Tulijifunza kwamba Mungu alizipatia nyota majina. Kwa hiyo tuna hakika kwamba malaika wote wana majina pia. Na tunajua kwamba wanaweza kuongea pamoja kwa sababu Biblia inataja ‘lugha ya malaika.’ (1 Wakorintho 13:1) Unafikiri malaika huongea juu ya nini? Je, wao huongea juu yetu tukiwa duniani?—

      Tunajua kwamba malaika wa Shetani, wale roho waovu, wanajaribu kutufanya tusimtii Yehova. Kwa hiyo ni lazima wazungumze namna wanavyoweza kutufanya tusitii. Wanataka tuwe kama wao ili Yehova asitupende pia. Lakini namna gani malaika waaminifu wa Mungu? Je, unafikiri wao pia huzungumza juu yetu?— Ndiyo. Wao wanataka kutusaidia. Hebu nikuambie namna malaika wengine wa Mungu walivyowasaidia watu waliompenda Yehova na kumtumikia.

      Kwa mfano, kuna mtu aliyeitwa Danieli ambaye aliishi Babiloni. Watu wengi wa Babiloni hawakumpenda Yehova. Watu hata walitunga sheria ya kuadhibu mtu yeyote anayesali kwa Yehova Mungu. Lakini Danieli hakuacha kusali kwa Yehova. Je, unajua walimfanyia Danieli nini?—

      Watu wabaya walimtupa Danieli ndani ya shimo la simba. Danieli alikaa humo ndani peke yake pamoja na simba wenye njaa. Kisha kukatokea nini?— Danieli alisema, ‘Mungu alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.’ Hakuumizwa hata kidogo! Malaika wanaweza kuwafanyia mazuri wale wanaomtumikia Yehova. —Danieli 6:18-22.

      Kisha kuna wakati Petro alikuwa gerezani. Kumbuka kwamba Petro alikuwa rafiki ya Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo. Watu wengine hawakufurahi Petro alipowaambia kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. Basi wakamfunga Petro gerezani. Askari walimlinda Petro ili kuhakikisha kwamba hatoroki. Je, kuna mtu yeyote ambaye angeweza kumsaidia?—

      Petro alikuwa amelala katikati ya askari wawili akiwa amefungwa minyororo mikononi. Lakini Biblia inasema: ‘Tazama! malaika wa Yehova akaja, na nuru ikang’aa katika chumba cha gereza. Akampiga Petro ubavuni, akamwamsha, akisema, “Amka upesi!”’

      Mara tu minyororo ya Petro ikaanguka kutoka mikononi mwake! Na malaika akamwambia: ‘Vaa vazi lako na viatu vyako, unifuate.’ Askari hawangewazuia kwa sababu malaika alikuwa akimsaidia Petro. Halafu wakafika kwenye lango la chuma, na jambo la ajabu likafanyika. Lango likajifungua! Malaika huyo alimweka huru Petro ili aendelee kuhubiri.—Matendo 12:3-11.

      Je, malaika wa Mungu wanaweza kutusaidia pia?— Ndiyo. Je, hiyo inamaanisha kwamba hawatatuacha tuumie hata kidogo?— La, malaika hawawezi kuzuia tusiumie ikiwa tunafanya mambo ya upumbavu. Lakini hata kama hatufanyi mambo ya upumbavu, huenda bado tukaumia. Malaika hawajaambiwa wazuie mabaya yasitupate. Badala yake Mungu amewapa kazi muhimu ya kufanya.

      Biblia inataja malaika ambaye anawaambia watu kila mahali wamwabudu Mungu. (Ufunuo 14:6, 7) Malaika anafanyaje hivyo? Je, anapiga kelele kutoka mbinguni ili kila mtu asikie?— La, badala yake wafuasi wa Yesu duniani wanawaambia wengine kuhusu Mungu, na malaika wanawaongoza katika kazi yao. Malaika wanahakikisha kwamba wale wanaotaka kumjua Mungu kikweli wanapata nafasi ya kusikia. Tunaweza kufanya kazi hiyo ya kuhubiri, na malaika watatusaidia.

      Namna gani ikiwa watu wasiompenda Mungu wanatusumbua? Vipi wakitufunga gerezani? Je, malaika watatuweka huru pia?— Wanaweza. Lakini hawafanyi hivyo kila wakati.

      Paulo, ambaye alikuwa mfuasi wa Yesu, alikuwa gerezani wakati mmoja. Alikuwa anasafiri kwa meli wakati wa upepo mkali. Lakini malaika hawakumsaidia wakati huo kwa sababu kulikuwa na watu ambao walihitaji kusikia habari kumhusu Mungu. Malaika alimwambia: “Usiogope, Paulo. Utasimama mbele ya Kaisari.” Bila shaka, Paulo angepelekwa kwa Kaisari, mtawala wa ulimwengu ili Paulo amhubirie. Kila mara malaika walijua mahali Paulo alikuwa, nao walimsaidia. Watatusaidia pia ikiwa kwa kweli tutamtumikia Mungu. —Matendo 27:23-25.

      Kuna kazi nyingine kubwa ambayo malaika watafanya, nao wataifanya hivi karibuni. Wakati wa Mungu wa kuwaharibu waovu umekaribia sana. Wale wote wasiomwabudu Mungu wa kweli wataharibiwa. Wale wanaosema kwamba hawaamini malaika eti kwa sababu hawawezi kuwaona malaika hao watatambua kwamba wamekosea sana. —2 Wathesalonike 1:6-8.

      Hiyo itamaanisha nini kwetu?— Ikiwa sisi tutakuwa upande wa malaika wa Mungu, watatusaidia. Lakini, je, tuko upande wao?— Ndiyo, iwapo sisi tunamtumikia Yehova. Na ikiwa tunamtumikia Yehova, tutawaambia wengine wamtumikie pia.

      Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu namna malaika wanavyohusika katika maisha ya watu, soma Zaburi 34:7; Mathayo 4:11; 18:10; Luka 22:43; na Matendo 8:26-31.

      [Picha katika ukurasa wa 63]

      Mungu alifanya nini ili kumwokoa Danieli?

      [Picha katika ukurasa wa 64]

      Malaika alimsaidiaje Petro kutoka gerezani?

      [Picha katika ukurasa wa 66]

      Malaika anamwambia Paulo nini?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki