-
Jinsi ya Kumfurahisha MunguJifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Sura Ya 40
Jinsi ya Kumfurahisha Mungu
TUNAWEZA kufanya nini kumfurahisha Mungu? Je, tunaweza kumpa chochote?— Yehova anasema: “Kila mnyama wa mwituni ni wangu.” Anasema pia: “Fedha ni yangu, na dhahabu ni yangu.” (Zaburi 24:1; 50:10; Hagai 2:8) Hata hivyo kuna kitu tunachoweza kumpa Mungu. Ni kitu gani?—
Yehova huturuhusu tuchague kama tutamtumikia au la. Hatulazimishi tufanye yale anayotaka. Hebu tujaribu kuelewa ni kwa nini Mungu alituumba na uhuru wa kuchagua kama tutamtumikia au la.
Huenda unajua mashine ambazo hutumiwa kufanya kazi. Mashine hizo hufanya tu yale ambayo wenye kuzitengeneza hutaka zifanye. Kwa hiyo haziwezi kujichagulia jambo la kufanya. Kama Yehova angetaka, angetuumba sisi sote kama mashine. Angetuumba ili tufanye tu yale ambayo anataka. Lakini Mungu hakufanya hivyo. Unajua ni kwa nini?—Ni kweli kwamba vitu vingine vya kuchezea ni kama mashine. Vinapobonyezwa, vinafanya tu yale ambayo aliyevitengeneza alivipangia. Umewahi kuona kitu kama hicho?— Mara nyingi watu huchoka kucheza na kitu ambacho kinaweza kufanya tu yale ambayo mwenye kukitengeneza alikipangia. Mungu hataki tumtii kwa kulazimishwa. Yehova anataka tumtumikie kwa sababu tunampenda na tunataka kumtii.
Unafikiri Baba yetu wa mbinguni anahisije tunapomtii kwa kupenda?— Hebu niambie, tabia yako hufanya wazazi wako wahisije?— Biblia inasema kwamba mwana mwenye hekima ‘humfurahisha babake’ bali mwana mpumbavu “ni huzuni ya mama yake.” (Mithali 10:1) Je, umeona kwamba unawafurahisha baba na mama unapofanya kile ambacho wanakuambia?— Lakini wanahisije unapokosa kuwatii?—
Sasa hebu tumfikirie Baba yetu wa mbinguni, Yehova. Anatuambia namna tunavyoweza kumfurahisha. Tafadhali chukua Biblia yako na ufungue Mithali 27:11. Mungu anazungumza nasi anaposema: “Uwe na hekima, mwanangu [au binti yangu], na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” Je, unajua maana ya kumdhihaki mtu?— Mtu anaweza kukudhihaki kwa kukucheka akisema eti huwezi kufanya jambo ulilosema utafanya. Shetani humdhihakije Yehova?— Hebu tuone.
Kumbuka kwamba tulijifunza katika Sura ya 8 ya kitabu hiki kwamba Shetani hujitanguliza na anataka kila mtu amtii. Shetani husema kwamba watu humwabudu Yehova kwa sababu tu Yehova atawapa uzima wa milele wakimwabudu. Shetani alimpinga Mungu alipowashawishi Adamu na Hawa kumwasi Yehova. Alimwambia Mungu: ‘Watu wanakutumikia tu kwa sababu ya kile unachowapa. Nipe nafasi, nami nitafanya wakuache.’
Ni kweli kwamba maneno hayo hususa hayako katika Biblia. Lakini tunaposoma kuhusu Ayubu, ni wazi kwamba Shetani alimwambia Mungu jambo kama hilo. Lilikuwa jambo muhimu kwa Shetani na kwa Yehova kama Ayubu angekuwa mwaminifu kwa Mungu au la. Na tufungue Biblia zetu kwenye Ayubu sura ya 1 na ya 2 tuone jinsi mambo yalivyokuwa.
Ona kwamba katika Ayubu sura ya 1 Shetani yuko mbinguni malaika wanapoenda mbele za Yehova. Yehova anamwuliza Shetani: “Unatoka wapi?” Shetani anajibu kwamba amekuwa akizunguka-zunguka duniani. Kwa hiyo Yehova anamwuliza: ‘Umemwona Ayubu, kwamba ananitumikia wala hafanyi mabaya?’—Ayubu 1:6-8.
Mara moja Shetani anajitetea. ‘Ayubu anakutumikia tu kwa sababu hana matatizo. Ukiacha kumlinda na kumbariki, atakulaani mbele za uso wako.’ Yehova anamjibu: ‘Haya Shetani, unaweza kumfanyia chochote utakacho, lakini usimwumize Ayubu mwenyewe.—Ayubu 1:9-12.
Shetani anafanya nini?— Anapanga watu wamwibie Ayubu ng’ombe na punda na kuwaua wachungaji wao. Kisha radi inapiga na kuwaua kondoo na wachungaji wao. Baadaye, watu wanakuja na kuiba ngamia na kuwaua wachungaji wao. Hatimaye, Shetani anasababisha upepo mkali unaoiangusha nyumba walimokuwamo watoto kumi wa Ayubu na wote wanakufa. Licha ya hayo yote, Ayubu anaendelea kumtumikia Yehova.—Ayubu 1:13-22.
Yehova anapomwona Shetani tena, Yehova anamwambia kwamba Ayubu bado ni mwaminifu. Shetani anatoa udhuru akisema: ‘Ukiniacha tu niumize mwili wake, atakulaani mbele za uso wako.’ Yehova anamruhusu Shetani amwumize Ayubu lakini anamwonya asimwue.
Shetani anampiga Ayubu kwa ugonjwa, mwili wake wote unakuwa na vidonda. Vidonda hivyo vinanuka sana hivi kwamba hakuna anayetaka kumkaribia. Hata mke wa Ayubu anamwambia: “Mlaani Mungu, ufe!” Watu wanaojifanya kuwa rafiki za Ayubu wanapomtembelea wanamhuzunisha hata zaidi wanapomwambia kwamba ni lazima awe anateseka kwa sababu ya maovu anayotenda. Hata hivyo, Ayubu anaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu kujapokuwa matatizo na maumivu mengi yanayosababishwa na Shetani.—Ayubu 2:1-13; 7:5; 19:13-20.
Unafikiri uaminifu wa Ayubu ulimfanya Yehova ahisije?— Ulimfurahisha Yehova kwa sababu Yehova aliweza kumwambia Shetani: ‘Mwone Ayubu! Ananitumikia kwa sababu anataka.’ Je, utakuwa kama Ayubu, mtu ambaye Yehova anaweza kumtumia kama mfano wa kumthibitisha Shetani kuwa mwongo?— Kwa kweli, ni pendeleo kujibu mashtaka ya Shetani kwamba anaweza kuwafanya watu waache kumtumikia Yehova. Bila shaka Yesu aliliona kuwa pendeleo.
Mwalimu Mkuu hakumruhusu Shetani kamwe amwongoze kufanya mabaya. Wazia jinsi mfano wake ulivyomfurahisha Baba yake! Yehova aliweza kumjibu Shetani hivi kumhusu Yesu: ‘Ona Mwana wangu! Amekuwa mwaminifu kabisa kwangu kwa sababu ananipenda!’ Wazia pia shangwe ya Yesu kwa kufurahisha moyo wa Baba yake. Kwa sababu ya shangwe hiyo, Yesu hata alivumilia kifo kwenye mti wa mateso.—Waebrania 12:2.
Je, unataka kuwa kama Mwalimu wetu Mkuu kwa kumfurahisha Yehova?— Basi endelea kujifunza kuhusu yale Yehova anataka ufanye, na umfurahishe kwa kuyafanya!
Soma mambo ambayo Yesu alifanya ili kumfurahisha Mungu na yale ambayo tunahitaji kufanya pia, kwenye Mithali 23:22-25; Yohana 5:30; 6:38; 8:28; na 2 Yohana 4.
[Picha katika ukurasa wa 207]
Kwa nini Mungu hakutuumba kama mashine hii?
[Picha katika ukurasa wa 208]
Unawezaje kumfurahisha Yehova na wazazi wako?
[Picha katika ukurasa wa 209]
Shetani alimpingaje Yehova baada ya uasi wa Adamu na Hawa?
[Picha katika ukurasa wa 210]
Ayubu alivumilia nini, na kwa nini Mungu alifurahi?
-
-
Watoto Wanaomfurahisha MunguJifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Sura Ya 41
Watoto Wanaomfurahisha Mungu
UNAFIKIRI ni mtoto gani duniani aliyemfurahisha Yehova zaidi?— Ni Mwana wake, Yesu. Tuzungumzie mambo ambayo Yesu alifanya ili kumfurahisha Baba yake wa mbinguni.
Yesu na familia yao waliishi umbali wa safari ya siku tatu hivi kutoka Yerusalemu, kulipokuwa lile hekalu maridadi la Yehova. Yesu aliliita hekalu “nyumba ya Baba yangu.” Yeye na familia yao walienda huko kila mwaka kuhudhuria Pasaka.
Mwaka fulani, Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, familia yao ilianza safari ya kurudi nyumbani baada ya sherehe za Pasaka. Hawakutambua kwamba Yesu hayuko miongoni mwa watu wao wa ukoo na rafiki zao hadi waliposimama mahali ambapo wangelala usiku. Bila kupoteza wakati Maria na Yosefu wakarudi Yerusalemu kumtafuta. Unafikiri Yesu alikuwa wapi?—
Walimpata Yesu hekaluni. Alikuwa akiwasikiliza walimu na kuwauliza maswali. Nao walipomwuliza swali, alijibu. Walishangazwa na majibu yake mazuri. Unaelewa ni kwa nini Mungu alipendezwa na Mwana wake?—
Hatimaye Maria na Yosefu walitulia walipompata Yesu. Lakini Yesu hakuwa na wasiwasi. Alijua kwamba hekaluni ni mahali salama na panapofaa kuwa. Akawauliza: “Je! hamkujua kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?” Alijua kwamba hekalu ni nyumba ya Mungu, naye alipenda kuwa huko.
Baada ya hayo, Maria na Yosefu wakarudi nyumbani Nazareti wakiwa na Yesu mwenye umri wa miaka 12. Unafikiri Yesu aliwatendeaje wazazi wake?— Biblia inasema kwamba aliendelea “kujitiisha kwao.” Unafikiri hiyo inamaanisha nini?— Inamaanisha kwamba aliwatii. Ndiyo, alifanya kile wazazi wake walimwambia afanye, hata kama ilimaanisha kuteka maji kisimani.—Luka 2:41-52.
Basi fikiria hili: Ijapokuwa Yesu alikuwa mkamilifu, aliwatii wazazi wake wasio wakamilifu. Je, hilo lilimfurahisha Mungu?— Bila shaka, kwani Neno la Mungu linawaambia watoto: “Watiini wazazi wenu.” (Waefeso 6:1) Wewe pia utamfurahisha Mungu ukiwatii wazazi wako kama Yesu.
Njia nyingine ya kumfurahisha Mungu ni kwa kuwaambia wengine juu yake. Huenda watu wengine wakasema kwamba haifai vijana kufanya hivyo. Lakini watu walipojaribu kuwanyamazisha wavulana kufanya hivyo, Yesu alisema: ‘Hamkusoma katika Maandiko, “Kutoka katika kinywa cha watoto Mungu atatoa sifa”?’ (Mathayo 21:16) Kwa hiyo sote tunaweza kuwaambia wengine juu ya Yehova na jinsi alivyo Mungu mzuri, iwapo kwa kweli tunataka. Na kama tutafanya hivyo, tutamfurahisha Mungu.
Tunajifunza wapi mambo kumhusu Mungu ili tuwaambie wengine?— Tunapojifunza Biblia nyumbani. Lakini tunajifunza mengi mahali watu wa Mungu wanapokutana ili kujifunza. Lakini tutawajuaje watu wa Mungu?—
Watu hufanya nini katika mikutano yao? Je, kweli wao hufundisha yaliyo katika Biblia? Wao huisoma na kuizungumzia? Hivyo ndivyo tunavyomsikiliza Mungu, sivyo?— Tukiwa kwenye mikutano ya Kikristo tunatazamia kusikia yale ambayo Mungu anasema, sivyo?— Lakini vipi watu wakisema kwamba si lazima uishi kulingana na yale ambayo Biblia inasema? Je, utasema kwamba hao ni watu wa Mungu?—
Tufikirie jambo hili. Biblia inasema kwamba watu wa Mungu wangekuwa “watu kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14) Kwa sababu jina la Mungu ni Yehova, tunaweza kuwauliza watu kama Yehova ndiye Mungu wao. Wakisema la, basi tutajua kwamba wao si watu wake. Watu wa Mungu huwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu pia. Nao wanaonyesha upendo wao kwa Mungu kwa kutii amri zake.—1 Yohana 5:3.
Iwapo unawajua watu wanaofanya mambo yote hayo, jiunge nao ili kumwabudu Mungu. Usikilize kwa makini kwenye mikutano hiyo kisha utoe majibu maswali yanapoulizwa. Ndivyo Yesu alivyofanya alipokuwa katika nyumba ya Mungu. Nawe ukifanya mambo hayo, utamfurahisha Mungu kama vile Yesu alivyomfurahisha.
Unaweza kuwafikiria watoto wengine wanaotajwa katika Biblia ambao walimfurahisha Mungu?— Timotheo ni mfano bora. Baba yake hakuwa mwabudu wa Yehova. Lakini mama yake Eunike, na nyanya yake Loisi walimwamini Yehova. Timotheo aliwasikiliza na akajifunza kumhusu Yehova.
Timotheo alipokuwa mtu mzima, mtume Paulo alitembelea mji wao. Akatambua kwamba Timotheo anataka sana kumtumikia Yehova. Basi akamwalika Timotheo aambatane naye ili afanye zaidi katika utumishi wake kwa Mungu. Kila walikokwenda waliwaambia watu kuhusu Ufalme wa Mungu na kuhusu Yesu.—Matendo 16:1-5; 2 Timotheo 1:5; 3:14, 15.
Lakini, je, ni mifano tu ya wavulana wadogo waliomfurahisha Mungu tunayopata katika Biblia?— La. Mfikirie msichana mdogo Mwisraeli aliyemfurahisha Mungu. Alipokuwa hai, mataifa ya Siria na Israeli yalikuwa maadui. Siku moja Wasiria walipigana na Israeli wakamchukua msichana huyo mateka. Wakampeleka nyumbani kwa jemadari fulani aliyeitwa Naamani. Akawa kijakazi wa mke wa Naamani.
Naamani alikuwa na ugonjwa unaoitwa ukoma. Hakuna daktari aliyeweza kumponya. Lakini msichana huyo mdogo aliamini kwamba nabii fulani, mtumishi wa pekee wa Mungu, angeweza kumsaidia Naamani. Naamani na mke wake hawakuwa kamwe waabudu wa Yehova. Je, msichana huyo awaambie alichojua? Wewe ungalifanya nini?—
Basi, msichana mdogo akasema: ‘Kama tu Naamani angeenda kwa nabii wa Yehova huko Israeli, angeponywa ukoma wake.’ Naamani akamsikiliza msichana huyo, akaenda kwa nabii wa Yehova. Alipofanya alivyoambiwa na nabii, alipona. Hiyo ikamfanya Naamani kuwa mwabudu wa Mungu wa kweli.—2 Wafalme 5:1-15.
Je, ungependa kumsaidia mtu kujifunza kumhusu Yehova na kuhusu yale awezayo kufanya, kama alivyofanya msichana yule mdogo?— Unaweza kumsaidia nani?— Labda mwanzoni hawatakubali kwamba wanahitaji msaada. Lakini unaweza kuwaambia mambo mazuri ambayo Yehova hufanya. Na huenda wakasikiliza. Kwa hakika hilo litamfurahisha Mungu.
Mambo yenye kutia moyo vijana wafurahie zaidi utumishi wa Mungu yanaweza kupatikana katika Zaburi 122:1; 148:12, 13; Mhubiri 12:1; 1 Timotheo 4:12; na Waebrania 10:23-25.
[Picha katika ukurasa wa 213]
Yesu akiwa mtoto alimfurahishaje Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 215]
Timotheo alitaka kufanya nini ijapokuwa baba yake hakuwa mwabudu wa Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 216]
Msichana huyu Mwisraeli alimfurahishaje Mungu?
-