Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mzazi Mmoja, Matatizo Mengi
    Amkeni!—2002 | Oktoba 8
    • Magumu Ambayo Wazazi Waliotalikiwa Hukabili

      Wazazi wasio na wenzi wa ndoa hutambua kwamba mahitaji ya kila mtoto ni tofauti nayo hubadilika daima. Wazazi ambao wametalikiwa hukabili magumu yasiyo ya kawaida wanapojitahidi kuwapa watoto wao mwongozo wa kiroho.

      Kwa mfano, baadhi ya wazazi walio Mashahidi wa Yehova ambao wametalikiwa hawakupewa haki ya kulea watoto wao. Wao wamejitahidi kupanga watoto wao wawatembelee wakati wanapoweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo pamoja. Hivyo, mtoto anaweza kushirikiana na ndugu na dada katika kutaniko la Kikristo kwa ukawaida, jambo ambalo huwanufaisha sana watoto wa wazazi waliotalikiana.

      Itawabidi wazazi waliotalikiana wasio na nafasi nyingi za kuwa pamoja na watoto wao watafute njia nyingine za kuwaonyesha kwamba wanawapenda. Ili kufaulu, ni lazima mzazi atambue na kuhangaikia hisia za moyoni za mtoto zinazobadilika-badilika. Jambo hilo ni muhimu hasa mtoto anapofikia umri wa kubalehe na anapoanza kupendezwa zaidi na ushirika wa watu wengine na marafiki.

      Mzazi ambaye amefaulu kulea mtoto wake huelewa uwezo, utu, na mawazo yake. (Mwanzo 33:13) Mzazi huyo huwa na uhusiano wa karibu na mtoto wake, nao huongea na kushirikiana kwa upendo. Wanaweza kuongea bila kizuizi chochote. Mtoto hushiriki katika shughuli za mzazi, na mzazi hushiriki katika shughuli za mtoto.

      Kuelewana Ni Muhimu

      Baada ya talaka, watoto wanahitaji kushirikiana na wazazi wote wawili. Vipi ikiwa wazazi wana imani tofauti, mmoja ni Shahidi wa Yehova, na yule mwingine si Shahidi? Kuzungumza mambo waziwazi na kwa ukawaida husaidia kuzuia mgongano. ‘Mwe na sifa ya kuwa wenye kukubali sababu,’ mtume Paulo aliandika. (Wafilipi 4:5, Phillips) Watoto wanapaswa kufundishwa kwamba wazazi wote wawili wana haki ya kufuata dini yao.

      Huenda mzazi asiye Shahidi akasisitiza mtoto ahudhurie ibada katika kanisa lake. Mzazi ambaye ni Shahidi wa Yehova anaweza kufanya nini katika hali hiyo? Yeye pia anaweza kumfundisha mtoto imani yake. Baadaye, mtoto ataweza kufanya uamuzi wake mwenyewe kuhusu ibada, kama kijana Timotheo, ambaye alifundishwa kanuni za Biblia na mama na nyanya yake. (2 Timotheo 3:14, 15) Mtoto akisumbuka kwa sababu ya kuhudhuria ibada ya dini nyingine, anaweza kufikiria kisa cha Naamani. Biblia inaeleza kwamba mtu huyo, hata baada ya kuwa mwabudu wa kweli, aliendelea kutimiza wajibu wake kwa kuambatana na mfalme aliyeabudu katika nyumba ya Rimoni. Huenda simulizi hilo likamhakikishia mtoto kwamba Yehova anamwelewa na kumpenda ijapokuwa yeye huhudhuria ibada nyingine ambayo hajazoea.—2 Wafalme 5:17-19.

      Mzazi mzuri anajua jinsi ya kuongoza fikira za mtoto au watoto na kuelewa hisia zao. (Kumbukumbu la Torati 6:7) Ni kweli kwamba wazazi wasiooa au kuolewa huenda wakaaibikia maisha yao ya awali. Hata hivyo, ni lazima wazazi hao wakumbuke kwamba watoto wana wazazi wawili. Watoto wanataka kuwajua wazazi wote wawili, na wanahitaji kujua kwamba wazazi wanawapenda. Na wanahitaji pia kujua kwamba kuzaliwa kwao hakukuwa tukio baya lisilotazamiwa. Kwa kusema kwa heshima juu ya yule mzazi mwingine na kujibu maswali yake kwa njia ambayo mtoto wa umri wake anaweza kuelewa, au anahitaji kujua, mzazi anaweza kumliwaza mtoto kwa upendo.

      Wazazi wanapaswa kukumbuka kwamba maoni ya mtoto kuhusu upendo, mamlaka, na nguvu hutegemea uhusiano wake pamoja na mzazi wake. Kwa kutumia mamlaka na nguvu kwa njia ya upendo mzazi Mkristo anaweza kumsaidia sana mtoto kumpenda Yehova na kuheshimu utaratibu uliopo katika kutaniko.—Mwanzo 18:19.

  • Mzazi Mmoja, Matatizo Mengi
    Amkeni!—2002 | Oktoba 8
    • Jambo hilo halimaanishi kwamba wazazi wasio na wenzi wa ndoa wanataka watoto wao wajiamulie mambo kana kwamba wao ni watu wazima wasiohitaji mwongozo wowote kutoka kwa mzazi. Si jambo la hekima kumwacha mtoto mdogo peke yake au bila mtu wa kumtunza.

      Wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa hufikiri kwa makosa kwamba inawabidi kuwa marafiki tu wa watoto wao. Ijapokuwa uhusiano wa karibu ni wa lazima, wazazi hao wanapaswa kukumbuka kwamba watoto wanahitaji mzazi na mtoto hana ukomavu wa kutosha ili awe rafiki au msiri wa mzazi. Watoto wako wanataka utende kama mzazi.

  • Msaada kwa Mzazi Asiye na Mwenzi wa Ndoa
    Amkeni!—2002 | Oktoba 8
    • Msaada kwa Mzazi Asiye na Mwenzi wa Ndoa

      “Watoto wangu wanaporudi nyumbani na kunikumbatia na kuniambia kwamba wananipenda ndipo ninapofurahi sana kuwa na watoto.”—DORIS, MAMA ASIYE NA MUME, MWENYE WATOTO WAWILI.

      WAZAZI wasio na wenzi wa ndoa wanaweza kutiwa moyo wanaposoma maneno haya katika Biblia: “Watoto ni baraka na zawadi kutoka kwa BWANA.” (Zaburi 127:3, Contemporary English Version) Mungu huwapenda watoto wanaolelewa na mzazi mmoja kama anavyowapenda watoto wengine. Muumba wetu anataka familia za mzazi mmoja zifaulu. Biblia inasema hivi kumhusu: “Huwategemeza yatima na mjane.” (Zaburi 146:9) Wazazi wasio na wenzi wa ndoa wanaweza kuwa na hakika kwamba Mungu yu tayari kuwasaidia.

      Mtoto ana haki ya kulelewa katika familia yenye upendo na amani ili aweze kukomaa kimwili, kihisia, na kiroho. Ni daraka na pendeleo la kila mzazi kutumiwa na Mungu kumzoeza mtoto.

      Wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa wameona kwamba ni muhimu kutoa sala za moyoni, kufuata kanuni za Biblia bila kigeugeu, na kumtumaini Yehova kabisa. Jambo hilo linalingana na himizo linalopatikana katika Zaburi 55:22: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza.”

      Mara kwa mara, nyanya na babu, wazee wa kutaniko, na wazazi katika kutaniko la Kikristo, ambao wamefaulu kulea watoto, huenda wakaweza kusaidia familia yenye mzazi mmoja kushinda magumu. Ni kweli kwamba watu wa ukoo na waabudu wenzi wanaweza kuwasaidia sana wazazi wasio na wenzi wa ndoa, lakini Mungu amempa mzazi daraka la kumlea mtoto.a

      Jambo la kufurahisha ni kwamba wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa wamefaulu kushinda magumu na kulea watoto wenye kutegemeka, wenye mwenendo mzuri, na wenye kumcha Mungu. Mwandishi wa Amkeni! aliwahoji baadhi yao. Mambo kadhaa ambayo wazazi hao walitaja yameorodheshwa hapa chini.

      • Kupanga kazi za nyumbani vizuri. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu hujitahidi kupanga kazi za nyumbani na shughuli mbalimbali vizuri. Kupanga mambo vizuri na kufanya mambo kwa utaratibu ni muhimu sana. Biblia inasema hivi: “Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu.”—Mithali 21:5.

      • Kuwajibika kutunza familia. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu wanaona familia zao kuwa muhimu sana. Wao hutanguliza mahitaji ya watoto wao wala si mahitaji yao wenyewe.—1 Timotheo 5:8.

      • Kuwa na kiasi ni muhimu. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu hawapuuzi matatizo wala hawayatii chumvi; wao hutafuta suluhisho. Wao hutambua magumu na kuyashughulikia bila kujihurumia wala kuhisi uchungu.

      • Mawasiliano mazuri. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu hujitahidi kuwa na mawasiliano mazuri. Wao huwatia moyo watoto waeleze waziwazi mawazo na hisia zao bila kuficha. Baba mmoja asiye na mke anasema hivi kuwahusu watoto wake: “Ninaongea nao kila ninapopata nafasi. Tunafurahia kuwa pamoja tunapotayarisha chakula cha jioni. Ndipo wanaponieleza mambo yaliyomo mioyoni mwao.”

      • Kujitunza. Ijapokuwa wana shughuli nyingi mno, wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu, hutambua kwamba ni lazima wajitunze wenyewe pia kiroho, kihisia, na kiafya. Ethel, mama aliyetalikiwa mwenye watoto wawili, alieleza hivi: “Ninajaribu kuweka kando wakati kwa ajili yangu mwenyewe. Kwa mfano, wakati rafiki yangu mmoja anapowafundisha watoto kucheza ala fulani ya muziki, ninapata saa moja ya kupumzika. Wakati huo mimi huketi chini bila kuwasha televisheni.”

      • Maoni yanayofaa. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu wana maoni yanayofaa kuhusu daraka lao na juu ya maisha kwa ujumla. Wao huona kwamba katika hali ngumu kunaweza kuwa na faida fulani. Mama mmoja asiye na mume anasema hivi: “Mimi nimegundua kwamba kulea watoto wangu nikiwa peke yangu kunaweza kufurahisha pia.”

      Wale Waliofaulu

      Je, kanuni zilizotajwa juu, zinafanya kazi? Naam, kama tunavyoweza kuona kutokana na masimulizi mengi kuwahusu wazazi ambao wamefaulu kulea watoto wao wakiwa peke yao. Gloria, mama aliyetalikiwa, ambaye alitajwa katika makala ya kwanza, anafanya kazi ya kuajiriwa huko Uingereza na alilea wana wawili na binti mmoja akiwa peke yake. Wote watatu wakawa wahudumu Wakristo wa wakati wote, ambao hutumia maisha yao kufundisha Biblia. Alipoulizwa jinsi alivyofaulu, Gloria alieleza hivi: “Jambo gumu hasa lilikuwa kuongoza funzo la Biblia lenye kupendeza kwa ukawaida. Nilitaka watoto wawe wenye furaha, wawe na amani akilini, waridhike, na kulindwa na mitego. Nilipata kazi ya usiku. Nilitaka kuwa pamoja na watoto kila nilipoweza. Kabla ya kwenda kazini, tulitoa sala pamoja, kisha nikawalaza. Nilipokuwa kazini mama yangu mdogo alilinda nyumba.

      Gloria aliwasaidiaje watoto wake kutanguliza mambo muhimu maishani? Aongeza: “Lengo langu kuu lilikuwa kutanguliza mambo ya kiroho. Hatukuwa na fedha nyingi, na sikuficha jambo hilo kwa watoto. Kila jambo ambalo niliwaomba wafanye, nilikuwa tayari kulifanya mwenyewe pia, na wote walikuwa tayari kusaidia.” Akikumbuka jinsi alivyodumisha uhusiano mzuri pamoja na watoto wake, Gloria anasema hivi: “Nilifaulu kwa sababu tulifanya mambo pamoja. Hakuna aliyejitenga katika chumba chake. Tulipika pamoja, na tulisafisha na kupamba nyumba pamoja. Tulifanya kila kitu kwa kiasi. Sikuzote nilihakikisha kwamba tulipata nafasi ya kujiburudisha pia.”

      Carolyn, mama asiye na mume mwenye mwana mdogo anayeitwa Joseph, anafurahia kuona maendeleo yake. Nini kinachomsaidia kufaulu? “Sisi husoma Biblia kabla ya kulala,” anasema, “baadaye mimi humwuliza maswali kuhusu yale aliyojifunza. Isitoshe, sisi huchunguza mafungu fulani katika vichapo vya Biblia na kuona jinsi tunavyoweza kutumia mambo hayo katika maisha yetu. Jambo hilo humsaidia Joseph anapokabili matatizo, kama vile kuchokozwa shuleni.” Carolyn anakubali kwamba maisha yake si rahisi, lakini hajihisi mpweke. Anasema hivi: “Nahitaji kujikakamua, lakini nahisi kwamba Yehova amenisaidia sana. Mimi hutiwa moyo pia katika kutaniko la Kikristo.”

      Masimulizi ya maelfu ya mama wasio na waume kama vile Gloria na Carolyn, yanaonyesha kwamba kanuni za Biblia zinategemeka. Tangu zamani kanuni hizo zimewasaidia wazazi kulea watoto wenye sifa nzuri na wenye nguvu kiroho. (Mithali 22:6) Inawezekana kufaulu! Mzazi asiye na mwenzi wa ndoa anapatwa na magumu mengi yanayompa fursa za kufanya maendeleo na kuwasaidia wengine. Kumtegemea Mungu kikamili na kutumaini msaada wake ni njia bora ya kushinda magumu yanayowakabili wazazi wasio na wenzi wa ndoa.—Zaburi 121:1-3.

      [Maelezo ya Chini]

      a Habari zaidi kuhusu jinsi familia za mzazi mmoja zinavyoweza kufaulu zinapatikana katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, sura ya 9, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki