-
Makanisa Yanapatwa na Nini?Amkeni!—2007 | Februari
-
-
Ulaya Yapuuza Makanisa
Kwa zaidi ya miaka 1,600, nchi nyingi za Ulaya zimetawaliwa na serikali zilizodai kuwa za Kikristo. Je, dini huko Ulaya zinazidi kusitawi katika karne hii ya 21? Katika mwaka wa 2002, mwanasosholojia Steve Bruce, alisema hivi kuhusu Uingereza katika kitabu chake God is Dead—Secularization in the West: “Katika karne ya 19 karibu ndoa zote zilifungiwa kanisani.” Lakini kufikia mwaka wa 1971, ni asilimia 60 za ndoa zilizofungiwa kanisani na kufikia mwaka wa 2000, zilikuwa asilimia 31 tu.
Akizungumzia mwelekeo huo, mwandishi mmoja wa mambo ya kidini wa gazeti la London la Daily Telegraph aliandika hivi: “Makanisa yote makubwa kuanzia Kanisa la Anglikana, Katoliki, Methodisti, na makanisa ya United Reformed, yamekuwa na upungufu mkubwa sana wa waumini kwa muda mrefu.” Aliendelea kusema hivi: “Makanisa ya Uingereza yatakuwa yakikaribia kutoweka kufikia mwaka wa 2040 na asilimia mbili tu ya watu ndio watakaokuwa wakihudhuria ibada ya Jumapili.” Kumekuwa na ripoti kama hizo pia kuhusu dini huko Uholanzi.
“Katika miaka ya hivi karibuni, inaonekana kwamba nchi yetu imeaanza kufuatia sana mambo ya kimwili,” ikasema ripoti moja ya Ofisi ya Uholanzi ya Kupanga Masuala ya Kijamii na Kitamaduni. “Inatazamiwa kwamba kufikia mwaka wa 2020, asilimia 72 ya watu nchini humu hawatakuwa wakijihusisha kwa njia yoyote na mambo ya kidini.” Gazeti moja la Ujerumani linasema hivi: “Wajerumani wengi wanageukia uchawi na mizungu ili kupata kitulizo walichokuwa wakipata makanisani, kazini, na katika familia. . . . Makanisa mengi nchini Ujerumani yanalazimika kufungwa kwa kukosa waumini.”
Wale wanaoenda kanisani huko Ulaya hawaendi huko ili kujua yale ambayo Mungu anataka wafanye. Ripoti moja kutoka Italia ilisema: “Waitaliano huchagua dini ambayo inapatana na mapendezi yao.” Mwanasosholojia mmoja huko alisema hivi: “Tunakubali kutoka kwa papa yale ambayo yanatupendeza.” Mambo kama hayo yanaweza kusemwa kuhusu Wakatoliki huko Hispania, ambako watu wameacha kuwa na bidii ya mambo ya dini na badala yake wanafuatilia vitu vya kimwili ambavyo mtu anaweza kuvipata sasa.
Mielekeo hiyo inatofautiana sana na Ukristo ambao Kristo na wafuasi wake walifundisha na kufuata. Yesu hakufundisha kwamba dini ni kama meza yenye vyakula mbalimbali ambapo mtu anaweza kuchagua kile anachopenda na kuacha kile ambacho hapendi. Alisema hivi: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kunifuata sikuzote.” Yesu alifundisha kwamba maisha ya Kikristo yanahusisha kujidhabihu na kujitahidi.—Luka 9:23.
-
-
Makanisa Yanapatwa na Nini?Amkeni!—2007 | Februari
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]
“WATU WANACHAGUA-CHAGUA DINI KAMA BIDHAA”
Mkurugenzi wa Kituo cha Ufundi cha Kitaifa cha Kanisa Katoliki huko Ufaransa, alinukuliwa akisema hivi: “Tunaona watu wakichagua-chagua dini kama bidhaa kwenye maduka makubwa. Watu wanakuwa waumini wa kanisa fulani kwa muda, kisha wakiona haliwafai wanahamia lingine.” Profesa Grace Davie wa Chuo Kikuu cha Exeter huko Uingereza alisema hivi katika uchunguzi aliofanya kuhusu dini huko Ulaya: “Watu wanachagua na kuchanganya mafundisho kutoka dini mbalimbali. Dini imekuwa kama bidhaa nyingine ambazo watu huchagua wanachotaka kwa kutegemea mtindo wao wa maisha na mapendezi.”
-