Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Biblia Inatueleza Mambo Yote Kumhusu Yesu?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
    • Ni Nani Aliyechagua Vitabu Halali vya Biblia?

      Waandikaji fulani wamedai kuwa vitabu halali vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo vilichaguliwa karne kadhaa baadaye na kanisa lililokuwa na mamlaka, chini ya mwongozo wa Maliki Konstantino. Hata hivyo, mambo ya hakika yanaonyesha kwamba jambo hili si kweli.

      Kwa mfano, Oskar Skarsaune, Profesa wa Historia ya Kanisa, anasema hivi: “Hakuna baraza lolote la kanisa wala mtu yeyote binafsi aliyeamua ni maandishi gani yaliyo halali na yasiyo halali katika Agano Jipya . . . Njia iliyotumiwa kuchagua vitabu halali ilikuwa ya wazi na ya busara: Maandishi ya karne ya kwanza W.K. yaliyofikiriwa kuwa yaliandikwa na mitume na waandikaji wengine walioshirikiana nao, yalionwa kuwa yenye kutegemeka. ‘Vitabu vya injili,’ barua, na maandishi mengine ambayo yaliandikwa baadaye, hayakuchaguliwa kuwa sehemu ya maandiko halali . . . Kuchaguliwa kwa vitabu hivyo kulikamilika muda mrefu kabla ya utawala wa Konstantino na kabla ya kuanzishwa kwa kanisa lake lenye mamlaka. Kwa hiyo, kanisa la wafia imani ndilo lililochagua vitabu vya Agano Jipya wala si lile kanisa lenye mamlaka.”

      Ken Berding, ambaye ni mtaalamu wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, anasema hivi kuhusu jinsi vitabu halali vya Biblia vilivyochaguliwa: “Kanisa halikuchagua vitabu ambavyo lilipendelea viwe sehemu ya maandishi halali ya Biblia; ni afadhali kusema kwamba kanisa lilitambua vitabu ambavyo sikuzote Wakristo waliviona kuwa Neno la Mungu lenye kutegemeka.”

      Hata hivyo, je, Wakristo wa karne ya kwanza walichagua vitabu hivyo bila msaada wowote? Biblia inatuambia kwamba kuna kitu fulani muhimu na chenye nguvu kilichowasaidia.

      Biblia inasema kwamba mojawapo ya zawadi za kimuujiza za roho ambazo kutaniko la Kikristo la mapema lilipewa ni “utambuzi wa maneno yaliyoongozwa na roho.” (1 Wakorintho 12:4, 10) Baadhi ya Wakristo hao walipewa uwezo unaopita ule wa wanadamu wa kutofautisha kati ya maneno yaliyoongozwa na roho ya Mungu na yale yasiyoongozwa na roho hiyo. Kwa hiyo, Wakristo leo wanaweza kuwa na hakika kwamba Maandiko yaliyo katika Biblia yameongozwa na roho.

      Hivyo basi, vitabu halali vya Biblia vilichaguliwa mapema kwa mwongozo wa roho takatifu. Mwishoni mwa karne ya pili W.K., waandikaji fulani walitoa maelezo fulani kuhusu uhalali wa vitabu hivyo. Hata hivyo, waandikaji hao, hawakuchagua orodha ya vitabu ambavyo ni halali; walithibitisha tu vitabu ambavyo Mungu alikuwa tayari amevikubali kupitia wawakilishi wake walioongozwa na roho yake.

      Pia, hati za kale zina uthibitisho unaounga mkono orodha ya vitabu halali vya Biblia leo. Kuna hati zaidi ya 5,000 za Maandiko ya Kigiriki katika lugha ya awali, kutia ndani hati fulani za karne ya pili na ya tatu. Ni hati hizi, bali si maandishi ya Apokrifa, zilizoonwa kuwa zenye kutegemeka katika karne za kwanza-kwanza W.K. na hivyo zikanakiliwa na kusambazwa kwa wingi.

      Hata hivyo, uhalali wa vitabu hivyo unathibitishwa na mambo yanayotajwa ndani. Maandishi hayo halali yanapatana na “kielelezo cha maneno yenye afya” tunachopata kotekote katika Biblia. (2 Timotheo 1:13) Yanawahimiza wasomaji wampende, wamwabudu na kumtumikia Yehova, huku yakitoa onyo kuhusu ushirikina, mambo ya mashetani, na kuabudu viumbe. Maandishi hayo ni sahihi kihistoria na yana unabii wa kweli. Pia, yanawatia moyo wasomaji wawapende wanadamu wenzao. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yana mambo yanayoonyesha wazi uhalali wake. Je, tunaweza kusema hivyo kuhusu maandishi ya Apokrifa?

  • Je, Biblia Inatueleza Mambo Yote Kumhusu Yesu?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
    • a Biblia ina vitabu halali 66 ambavyo vinatoa uthibitisho wenye kusadikisha kwamba viliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Vitabu hivyo muhimu sana vinajulikana kama Neno la Mungu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki