-
Masihi AfikaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 16
Masihi Afika
Yehova amtambulisha Yesu wa Nazareti kuwa Masihi aliyeahidiwa
JE, Yehova angewasaidia watu wake kumtambua Masihi? Ndiyo. Fikiria aliyofanya. Karne nne baada ya Maandiko ya Kiebrania kumalizika, katika jiji linaloitwa Nazareti, eneo la kaskazini la Galilaya, mwanamke kijana anayeitwa Maria alitembelewa na mgeni asiye wa kawaida. Malaika anayeitwa Gabrieli alimtokea na kumwambia kwamba ijapokuwa yeye ni bikira, Mungu angetumia nguvu zake za utendaji, roho takatifu, kumfanya azae mwana. Mwana huyo ndiye Mfalme aliyeahidiwa zamani, yule ambaye angetawala milele! Mtoto huyo angekuwa Mwana wa Mungu mwenyewe. Mungu angeuhamisha uhai wake kutoka mbinguni na kuutia katika tumbo la uzazi la Maria.
Maria alikubali kwa unyenyekevu mgawo huo wa pekee. Mchumba wake, seremala anayeitwa Yosefu, alimwoa baada ya Mungu kumtuma malaika amhakikishie chanzo cha uja-uzito wa Maria. Hata hivyo, unabii uliosema kwamba Masihi angezaliwa Bethlehemu ungetimizwa jinsi gani? (Mika 5:2) Jiji hilo dogo lilikuwa umbali wa kilomita 140 hivi kutoka Nazareti!
Mtawala Mroma aliagiza watu wahesabiwe. Watu walipaswa kujiandikisha katika miji ya nyumbani kwao. Inaonekana kwamba Bethlehemu kulikuwa nyumbani kwa Yosefu na Maria, kwa hiyo Yosefu na mke wake wakasafiri hadi huko. (Luka 2:3) Maria alizalia zizini, na kumlaza mtoto wake katika hori. Kisha Mungu akatuma malaika wengi wakawaambie wachungaji waliokuwa mlimani kwamba mtoto ambaye amezaliwa ndiye Masihi, au Kristo, aliyeahidiwa.
Baadaye, wengine pia walishuhudia kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. Nabii Isaya alitabiri kwamba mtu fulani angetokea na kutayarisha njia kwa ajili ya kazi muhimu ya Masihi. (Isaya 40:3) Mtu huyo ni Yohana Mbatizaji. Alipomwona Yesu, alipaaza sauti: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!” Baadhi ya wanafunzi wa Yohana wakamfuata Yesu mara moja. Mmoja wao akasema: “Tumempata Masihi.”—Yohana 1:29, 36, 41.
Kulikuwa na ushuhuda zaidi. Yohana alipombatiza Yesu, Yehova mwenyewe alisema kutoka mbinguni. Akitumia roho takatifu, alimweka rasmi Yesu kuwa Masihi na kusema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:16, 17) Masihi aliyeahidiwa akawa amefika!
Hilo lililotokea wakati gani? Mwaka wa 29 W.K., wakati ambapo ile miaka 483 iliyotabiriwa na Danieli ilipokamilika. Ndiyo, utimizo huo ni mojawapo ya ushuhuda wenye kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi, au Kristo. Hata hivyo, alitangaza ujumbe gani alipokuwa duniani?
—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 1 hadi 3; Marko, sura ya 1; Luka, sura ya 2; Yohana, sura ya 1.
-
-
Yesu Afundisha Kuhusu Ufalme wa MunguBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 17
Yesu Afundisha Kuhusu Ufalme wa Mungu
Yesu awafundisha wanafunzi wake mambo mengi, hata hivyo akazia jambo moja kuu—Ufalme wa Mungu
KWA nini Yesu alikuja duniani? Yeye mwenyewe alisema: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Fikiria mambo manne ambayo Yesu alifundisha kuhusu Ufalme, jambo kuu katika mahubiri yake.
1. Yesu aliteuliwa kuwa Mfalme. Yesu alisema waziwazi kwamba yeye ndiye Masihi aliyeahidiwa. (Yohana 4:25, 26) Pia, alionyesha kwamba ndiye Mfalme ambaye nabii Danieli aliona katika maono. Yesu aliwaambia mitume wake kwamba siku moja ataketi juu ya ‘kiti cha ufalme chenye utukufu’ na kwamba wao pia wataketi juu ya viti vya ufalme. (Mathayo 19:28) Alikiita kikundi hicho cha watawala “kundi dogo,” naye alisema kwamba ana “kondoo wengine,” ambao si sehemu ya kikundi hicho.—Luka 12:32; Yohana 10:16.
2. Ufalme wa Mungu utaleta haki ya kweli. Yesu alionyesha kwamba Ufalme utaondolea mbali ukosefu mkubwa zaidi wa haki kwa kulitakasa, au kulifanya kuwa takatifu, jina la Yehova Mungu na kuliondolea masuto yote ambayo Shetani amelimbikiza juu ya jina hilo tangu uasi wa Edeni. (Mathayo 6:9, 10) Pia, Yesu alionyesha kila siku kwamba hana ubaguzi, kwa kuwahubiria wanaume kwa wanawake, matajiri kwa maskini. Ijapokuwa alipaswa kuwafundisha Waisraeli hasa, alikuwa tayari kuwasaidia Wasamaria na Watu wa Mataifa au wasio Wayahudi. Tofauti na viongozi wa dini wa siku zake, hakuonyesha upendeleo hata kidogo.
3. Ufalme wa Mungu si sehemu ya ulimwengu huu. Yesu aliishi wakati ambapo kulikuwa na misukosuko mingi. Nchi ya kwao ilikuwa ikitawaliwa na serikali ya nchi nyingine. Hata hivyo, watu walipojaribu kumhusisha katika masuala ya kisiasa ya siku zake, alijiondoa. (Yohana 6:14, 15) Alimwambia mwanasiasa mmoja: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Nao wafuasi wake, aliwaambia: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Hakuwaruhusu kutumia silaha za vita, hata kwa kusudi la kumlinda yeye mwenyewe.—Mathayo 26:51, 52.
“Akaanza kusafiri . . . kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.”—Luka 8:1
4. Kristo atatawala kwa upendo. Yesu aliahidi kwamba atawaburudisha watu, na kuwapumzisha mizigo yao. (Mathayo 11:28-30) Ndivyo alivyofanya. Alitoa mashauri yenye upendo na yenye kutumika kuhusu kukabiliana na mahangaiko ya maisha, kuboresha mahusiano, kuepuka kufuatia vitu vya kimwili, na kupata furaha. (Mathayo, sura ya 5-7) Kwa sababu alionyesha upendo watu wa tabaka zote walipenda kuwa pamoja naye. Hata watu wa hali ya chini walimiminika kwake, wakiwa na hakika kwamba atawatendea kwa fadhili na heshima. Kwa kweli Yesu atakuwa Mtawala asiye na kifani!
Kuna njia nyingine yenye matokeo sana ambayo Yesu alitumia kuwafundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu. Alifanya miujiza mingi. Kwa nini? Tutaona.
-
-
Yesu Afanya MiujizaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 18
Yesu Afanya Miujiza
Yesu, kupitia miujiza aliyofanya, alionyesha jinsi atakavyotumia nguvu zake akiwa Mfalme
MUNGU alimwezesha Yesu kufanya mambo ambayo wanadamu wengine hawangeweza kufanya. Yesu alifanya miujiza mingi—mara nyingi mbele ya watazamaji wengi. Miujiza hiyo ilionyesha kwamba Yesu ana nguvu kuliko adui zake na pia kuliko vizuizi vingine ambavyo wanadamu wasio wakamilifu hawangeweza kamwe kushinda kwa mafanikio. Fikiria mifano kadhaa.
Njaa. Muujiza wa kwanza wa Yesu ulikuwa kubadili maji yawe divai. Katika pindi nyingine mbili, alilisha maelfu ya watu kwa mikate na samaki wachache. Pindi zote hizo kulikuwa na chakula cha kumtosha kila mtu na hata kubaki.
Ugonjwa. Yesu aliwaponya watu “kila namna ya ugonjwa na kila namna ya udhaifu.” (Mathayo 4:23) Aliwaponya vipofu, viziwi, wenye ukoma, wenye kifafa, vilema, viwete, na wasiojiweza. Hakuna ugonjwa uliomshinda.
Dhoruba kali. Yesu na wanafunzi wake walipokuwa wakisafiri katika Bahari ya Galilaya, dhoruba kali ilizuka. Wanafunzi waliogopa sana. Yesu aliitazama dhoruba hiyo na kusema: “Nyamaza, utulie!” Nayo dhoruba hiyo ikatulia. (Marko 4:37-39) Pindi nyingine, alitembea juu ya maji kulipokuwa na dhoruba yenye kuogopesha.—Mathayo 14:24-33.
Roho waovu. Roho waovu wana nguvu kuliko wanadamu. Watu wengi wameshindwa kujitoa katika mtego wa adui hao hatari wa Mungu. Hata hivyo, tena na tena, Yesu alipowaamuru watoke watu, roho hao hawangeweza tena kuendelea kuwasumbua. Hakuwaogopa. Badala yake, walitambua mamlaka yake nao walimwogopa.
Kifo. Kifo ni adui ambaye hakuna mwanadamu anaweza kumshinda. Ndiyo sababu kinaitwa “adui wa mwisho.” (1 Wakorintho 15:26) Hata hivyo, Yesu aliwafufua wafu. Alimfufua kijana wa mjane na binti ya wazazi waliokuwa na huzuni. Katika kisa cha pekee, Yesu alimfufua rafiki yake mpendwa, Lazaro, mbele ya umati wa waombolezaji, ijapokuwa alikuwa mfu kwa karibu siku nne! Hata adui za Yesu walikiri kwamba alifanya muujiza huo.—Yohana 11:38-48; 12:9-11.
Kwa kuwa wote waliosaidiwa na Yesu hatimaye walikufa, kwa nini alifanya miujiza yote hiyo? Miujiza ya Yesu ilitimiza mambo mazuri yenye kudumu. Ilithibitisha kwamba unabii wote wenye kupendeza kuhusu utawala wa Mfalme wa Kimasihi una msingi. Hakuna haja ya kuwa na shaka kwamba Mfalme aliyewekwa na Mungu hawezi kuondolea mbali njaa, magonjwa, hali hatari ya hewa, roho waovu, au kifo chenyewe. Tayari amethibitisha kwamba Mungu amemkabidhi nguvu za kufanya hivyo.
-
-
Yesu Atabiri Matukio ya Wakati Ujao Yatakayoikumba Dunia NzimaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 19
Yesu Atabiri Matukio ya Wakati Ujao Yatakayoikumba Dunia Nzima
Yesu ataja mambo yatakayotia alama kuwapo kwake katika mamlaka ya kifalme na ya umalizio wa mfumo wa mambo
KATIKA Mlima wa Mizeituni, ambapo jiji la Yerusalemu na hekalu lake lilikuwa likionekana vizuri, mitume wanne wa Yesu walimuuliza faraghani kuhusu mambo fulani aliyokuwa amezungumzia. Yesu alikuwa ametoka kusema kwamba hekalu lililo Yerusalemu litaharibiwa. Na mapema, alikuwa amewaambia kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 13:40, 49) Sasa mitume wakamuuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—Mathayo 24:3.
Akiwajibu, Yesu aliwaambia mambo ambayo yangetokea kabla ya Yerusalemu kuharibiwa. Lakini maneno yake yalikuwa na utimizo zaidi. Unabii wake ungetimizwa kwa kiwango kikubwa zaidi ulimwenguni pote. Yesu alitabiri matukio na hali za ulimwengu ambazo zingekuwa ishara. Ishara hiyo ingewaonyesha walio duniani kwamba kuwapo kwa Yesu akiwa Mfalme mbinguni kumeanza. Yaani, ishara hiyo ingeonyesha kwamba Yehova Mungu amemfanya Yesu kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi ulioahidiwa zamani za kale. Ishara hiyo ingemaanisha kwamba karibuni Ufalme huo utaondolea mbali uovu na kuwaletea wanadamu amani. Mambo ambayo Yesu alitabiri yangetia alama siku za mwisho za mfumo huu wa kale wa mambo—mifumo ya dini, siasa, na kijamii iliyopo leo—na kuashiria mwanzo wa mfumo mpya.
Akieleza mambo ambayo yangetokea duniani wakati wa kuwapo kwake akiwa Mfalme mbinguni, Yesu alisema kwamba kungekuwa na vita kati ya mataifa, upungufu wa chakula, matetemeko makuu ya ardhi, na magonjwa yenye kuenea. Uvunjaji wa sheria ungeongezeka. Wanafunzi wa kweli wa Yesu wangehubiri habari njema za Ufalme wa Mungu katika dunia yote. Yote hayo yangeishia katika “dhiki kuu” ambayo haijapata kutokea tena.—Mathayo 24:21.
Wafuasi wa Yesu wangejua jinsi gani kwamba dhiki hiyo iko karibu? Yesu aliwaambia: “Jifunzeni jambo hili kutokana na mtini.” (Mathayo 24:32) Majani ya mtini yanapotokea kwenye matawi ni ishara ya kwamba msimu wa kiangazi unakaribia. Vivyo hivyo, kutokea kwa ishara zote hizo alizotabiri Yesu katika kipindi kimoja cha wakati kungekuwa ishara ya kwamba mwisho uko karibu. Hakuna yeyote ila Baba aliyejua siku na saa barabara ambayo dhiki kuu ingeanza. Kwa hiyo, Yesu aliwahimiza hivi wanafunzi wake: “Endeleeni kukesha, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni gani.”—Marko 13:33.
—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 24 na 25; Marko, sura ya 13; Luka, sura ya 21.
-
-
Yesu Kristo AuawaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 20
Yesu Kristo Auawa
Yesu aanzisha maadhimisho mapya; asalitiwa na kutundikwa mtini
BAADA ya Yesu kuhubiri na kufundisha kwa miaka mitatu na nusu, alijua kwamba anakaribia mwisho wa maisha yake duniani. Viongozi wa dini Wayahudi walikuwa wakipanga njama ya kumuua, lakini wakawaogopa watu walioamini kwamba yeye ni nabii. Wakati huohuo, Shetani alimshawishi mmoja wa mitume 12 wa Yesu—Yuda Iskariote—akawa msaliti. Viongozi wa dini walimpa Yuda vipande 30 vya fedha ili amsaliti Yesu.
Usiku wake wa mwisho, Yesu aliwakusanya mitume wake kuadhimisha Pasaka. Baada ya Yuda kuondoka, Yesu alianzisha maadhimisho mapya, Mlo wa Jioni wa Bwana. Akachukua mkate, akashukuru, akawapa wale mitume 11 waliobaki. Akasema: “Huu unamaanisha mwili wangu ambao utatolewa kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” Alifanya vivyo hivyo kuhusiana na kikombe na kusema: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu.”—Luka 22:19, 20.
Yesu alikuwa na mengi ya kuwaambia mitume wake usiku huo. Aliwapa amri mpya—kwamba wapendane bila ubinafsi. Aliwaambia: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) Aliwahimiza wasiruhusu mioyo yao itaabike kwa sababu ya mambo yenye kuhuzunisha yaliyokuwa karibu kutokea. Yesu alisali sana kwa ajili yao. Wakaimba nyimbo za sifa na kuondoka.
Wakiwa katika bustani ya Gethsemane, Yesu akapiga magoti na kumimina moyo wake katika sala. Punde si punde askari-jeshi wenye silaha, makuhani, na watu wengine wakaja kumkamata. Yuda akakaribia na kumtambulisha Yesu kwao kwa kumbusu. Askari-jeshi hao walipomkamata Yesu, mitume wakatoroka.
Yesu akiwa mbele ya mahakama kuu ya Wayahudi, alijitambulisha kuwa Mwana wa Mungu. Mahakama hiyo ilimhukumu kuwa na hatia ya kukufuru na anastahili kifo. Baada ya hapo Yesu akapelekwa kwa Gavana Mroma, Pontio Pilato. Ingawa hakumpata Yesu kuwa na hatia, alimkabidhi Yesu kwa umati uliotaka auawe.
Kisha Yesu akapelekwa Golgotha, ambapo askari-jeshi Waroma walimtundika mtini. Kimuujiza, giza likaingia katikati ya mchana. Baadaye, alasiri hiyohiyo, Yesu akafa na kukawa na tetemeko kubwa la nchi. Mwili wake ukalazwa katika kaburi lililokuwa limechongwa katika mwamba. Siku iliyofuata, makuhani wakalifunika kaburi na kuweka mlinzi katika mwingilio wake. Je, Yesu angeendelea kuwa kaburini? Hapana. Muujiza mkubwa kuliko yote ulikuwa karibu kutokea.
—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 26 na 27; Marko sura, ya 14 na 15; Luka, sura ya 22 na 23; Yohana, sura ya 12 hadi 19.
-
-
Yesu Yuko Hai!Biblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 21
Yesu Yuko Hai!
Yesu awatokea wafuasi wake ili kuwapa maagizo na kuwatia moyo
SIKU ya tatu baada ya kifo cha Yesu, wanawake fulani waliokuwa wanafunzi wake waligundua kwamba jiwe lililokuwa kwenye mwingilio wa kaburi limeondolewa. Isitoshe, kaburi lilikuwa tupu!
Malaika wawili wakatokea. Mmoja wao akasema: “Mnamtafuta Yesu Mnazareti. . . . Alifufuliwa.” (Marko 16:6) Bila kukawia, wanawake hao wakakimbia kwenda kuwaambia mitume. Wakiwa njiani, wakakutana na Yesu. Akawaambia: “Msiogope! Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu, ili wapate kwenda zao Galilaya; na huko wataniona.”—Mathayo 28:10.
Baadaye siku hiyo, wanafunzi wawili walikuwa wakitembea kutoka Yerusalemu kuelekea kijiji cha Emau. Mtu wasiyemjua alijiunga nao na kuwauliza wanazungumzia nini. Mtu huyo alikuwa Yesu aliyefufuliwa, aliyewatokea katika umbo ambalo hawakutambua mwanzoni. Wakiwa na nyuso zenye huzuni wakamjibu kwamba wanaongea kuhusu Yesu. Kisha mtu huyo akaanza kuwaeleza mambo kuhusu Masihi katika Maandiko yote. Kwa kweli, Yesu alikuwa ametimiza mambo yote yaliyotabiriwa kuhusu Masihi.a Wanafunzi hao walipotambua kwamba ni Yesu aliyefufuliwa akiwa na mwili wa roho, akatoweka.
Wanafunzi hao wawili wakarudi Yerusalemu mara moja. Wakawakuta mitume wamekusanyika katika chumba kilichokuwa kimefungwa. Walipokuwa wakisimulia mambo waliyokuwa wamejionea, Yesu akatokea. Wafuasi wake walioduwaa hawakuamini macho yao! Yesu akawauliza: “Kwa nini shaka zinatokea mioyoni mwenu?” Kisha akawaambia: “Imeandikwa kwamba Kristo angeteseka na kufufuliwa kutoka kati ya wafu siku ya tatu.”—Luka 24:38, 46.
Kwa siku 40 baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea wanafunzi wake katika pindi tofauti-tofauti. Katika pindi moja, aliwatokea wanafunzi zaidi ya 500! Pengine katika pindi hiyo ndiyo alipowapa mgawo huu mzito: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 28:19, 20.
Alipokutana kwa mara ya mwisho pamoja na mitume wake 11 waliokuwa waaminifu, Yesu aliwaahidi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Kisha Yesu akapanda juu na mawingu yakamfunika.
—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 28; Marko, sura ya 16; Luka, sura ya 24; Yohana, sura ya 20 na 21; 1 Wakorintho 15:5, 6.
a Unabii mbalimbali wa Kimasihi ambao Yesu alitimiza unazungumziwa katika broshua hii Sehemu ya 14, Sehemu ya 15 na Sehemu ya 16 pia nyongeza yenye kichwa “Yesu Kristo—Masihi Aliyeahidiwa” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
-
-
Mitume Wahubiri kwa UjasiriBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 22
Mitume Wahubiri kwa Ujasiri
Kutaniko la Kikristo laongezeka licha ya mateso
SIKU kumi baada ya Yesu kurudi mbinguni, wanafunzi wake 120 hivi walikusanyika katika nyumba fulani jijini Yerusalemu wakati wa Sikukuu ya Kiyahudi ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K. Ghafula, katika nyumba hiyo kukawa na kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma. Wanafunzi wakaanza kuzungumza lugha ambazo hawakuwa wanazijua. Iliwezekanaje? Mungu alikuwa amewapa wanafunzi roho takatifu.
Nje, kulikuwa na umati kwa sababu watu walikuwa wametoka sehemu mbalimbali ili kusherehekea sikukuu hiyo. Walishangaa kuwasikia wanafunzi wa Yesu wakizungumza kwa ufasaha lugha zao wenyewe. Akieleza yaliyotokea, Petro alirejelea unabii wa Yoeli kwamba Mungu ‘angemimina’ roho yake, ambayo ingewawezesha wenye kuipokea kufanya miujiza. (Yoeli 2:28, 29) Uthibitisho huo wenye nguvu wa roho takatifu ulionyesha wazi kwamba badiliko kubwa limetokea: Mungu ameacha kushughulika na taifa la Israeli na kuanza kushughulika na kutaniko jipya la Kikristo lililokuwa limeanzishwa. Sasa, wote waliotaka kumtumikia Mungu walipaswa kuwa wafuasi wa Kristo.
Wakati huohuo upinzani uliongezeka, nao adui wakawatupa wanafunzi gerezani. Hata hivyo, wakati wa usiku, malaika wa Yehova alifungua milango ya gereza na kuwaambia wanafunzi waendelee kuhubiri. Ilipofika asubuhi wakaendelea kuhubiri. Wakaingia hekaluni na kuanza kufundisha habari njema kumhusu Yesu. Wapinzani wao wa kidini walikuwa na hasira nao wakawaagiza waache kuhubiri. Mitume wakajibu kwa ujasiri: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:28, 29.
Mateso yakaongezeka. Wayahudi fulani walimshtaki mwanafunzi Stefano wakidai kwamba amekufuru, nao wakamuua kwa kumpiga kwa mawe. Kijana, anayeitwa Sauli wa Tarso, alikuwa akitazama na kukubaliana na mauaji hayo. Kisha akaenda Damasko kumkamata mfuasi yeyote wa Kristo. Sauli akiwa njiani, nuru kutoka mbinguni ilimulika kumzunguka na akasikia sauti: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?” Akiwa amepofushwa na nuru hiyo, Sauli akauliza: “Wewe ni nani?” Sauti hiyo ikasema: “Mimi ni Yesu.”—Matendo 9:3-5.
Siku tatu baadaye, Yesu alimtuma mwanafunzi anayeitwa Anania ili kumponya Sauli. Sauli akabatizwa na kuanza kuhubiri kwa ujasiri kumhusu Yesu. Baadaye, Sauli akaitwa mtume Paulo naye akawa Mkristo mwenye bidii wa kutaniko la Kikristo.
Wanafunzi wa Yesu walikuwa wakiwatangazia habari njema za Ufalme wa Mungu Wayahudi na Wasamaria pekee. Sasa malaika amtokea Kornelio, ofisa-jeshi Mroma, anayemwogopa Mungu na kumwambia awatume watu wakamwite mtume Petro. Akiwa pamoja na wengine, Petro akamhubiria Kornelio na watu wa nyumbani mwake. Petro alipokuwa akizungumza, roho takatifu ikaja juu ya waamini hao kutoka kwa Mataifa, naye akaagiza wabatizwe katika jina la Yesu. Tangu wakati huo na kuendelea, watu wa mataifa yote wangeweza kupata uzima wa milele. Kutaniko lilikuwa tayari kuhubiri habari njema kwa mapana na marefu.
—Inatoka kwenye Matendo 1:1–11:21.
-
-
Habari Njema YaeneaBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 23
Habari Njema Yaenea
Paulo asafiri nchi kavu na baharini akihubiri
BAADA ya kuwa Mkristo, Paulo alitangaza kwa bidii habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. Mtu huyo aliyekuwa mpinzani alikumbana na upinzani mkali mara nyingi. Mtume huyo mwenye bidii alisafiri sehemu mbalimbali akihubiri habari njema ya Ufalme ambao utatimiza kusudi la awali la Mungu kwa wanadamu.
Katika safari yake ya kwanza ya kuhubiri huko Listra, Paulo alimponya mwanamume aliyekuwa kilema tangu kuzaliwa. Umati ulianza kupaaza sauti kwamba Paulo na Barnaba, msafiri mwenzake ni miungu. Wanaume hao wawili walijaribu sana kuwazuia watu wasiwatolee dhabihu. Hata hivyo, baadaye umati huohuo ulichochewa na adui za Paulo, ukampiga kwa mawe na kumwacha akiwa mahututi. Paulo hakufa na baadaye alirudi katika jiji hilohilo kuwaimarisha wanafunzi kwa maneno ya kutia moyo.
Wakristo fulani Wayahudi walidai kwamba waamini wasio Wayahudi wanapaswa kutimiza matakwa fulani ya Sheria ya Musa. Paulo alikwenda Yerusalemu kwa mitume na wanaume wazee ili kuwasilisha tatizo hilo. Baada ya kuyachunguza Maandiko kwa makini na kwa mwongozo wa roho takatifu ya Mungu, wanaume hao waliyaandikia makutaniko na kuyashauri yajiepushe na ibada ya sanamu, kula damu na nyama zenye damu, na kuepuka uasherati. Amri hizo zilikuwa za “lazima,” hata hivyo, haikumaanisha kwamba walipaswa kufuata Sheria ya Musa.—Mdo. 15:28, 29.
Katika safari yake ya pili ya kuhubiri, Paulo alienda Beroya, eneo ambalo leo liko Ugiriki. Wayahudi waliokuwa wakiishi huko walilipokea neno kwa hamu, wakiyachunguza Maandiko kila siku ili kuyathibitisha mafundisho yake. Kwa mara nyingine tena, upinzani ukamfanya aondoke na kwenda Athene. Akiwa mbele ya Waathene wenye elimu, Paulo alitoa hotuba yenye kuchochea kwelikweli. Leo tunaweza kumwiga Paulo kwa kusema kwa busara, utambuzi, na ufasaha tunapohubiri.
Baada ya safari yake ya tatu ya kuhubiri, Paulo alienda Yerusalemu. Alipoenda hekaluni, Wayahudi fulani walizusha ghasia, wakitaka kumuua. Askari-jeshi Waroma wakaingilia kati na kumhoji Paulo. Kwa kuwa alikuwa raia wa Roma, baadaye alijitetea mbele ya Feliksi, gavana Mroma. Wayahudi hawakuwa na uthibitisho wowote kuhusu mashtaka yao dhidi ya Paulo. Ili kumzuia Festo, aliyekuwa pia gavana Mroma, asimtie mikononi mwa Wayahudi, Paulo alisema: “Ninakata rufani kwa Kaisari!” Festo akajibu: “Utaenda kwa Kaisari.”—Mdo. 25:11, 12
Kisha Paulo akasafirishwa kwa meli hadi Italia ili akahukumiwe. Baada ya meli yao kuvunjika, alilazimika kukaa katika kisiwa cha Malta wakati wa majira ya baridi kali. Mwishowe alipofika Roma, alikaa katika nyumba ya kukodi kwa miaka miwili. Hata ingawa alikuwa akilindwa na askari, mtume huyo mwenye bidii aliendelea kuwahubiria wote waliomtembelea kuhusu Ufalme wa Mungu.
—Inatoka kwenye Matendo 11:22–28:31.
-
-
Paulo Ayaandikia MakutanikoBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 24
Paulo Ayaandikia Makutaniko
Barua za Paulo zaliimarisha kutaniko la Kikristo
KUTANIKO changa la Kikristo lilikuwa na kazi kubwa mbele yake. Lingetimiza sehemu muhimu katika kusudi la Yehova. Hata hivyo, baada ya muda usio mrefu Wakristo hao wa karne ya kwanza walishambuliwa. Je, wangedumisha utimilifu wao kwa Mungu wajapokabili mateso na hali nyingine zenye kuhatarisha uaminifu wao kutoka nje na ndani ya kutaniko? Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yana barua 21 zenye kutia moyo na zenye shauri lililohitajiwa.
Barua 14, Waroma mpaka Waebrania, ziliandikwa na mtume Paulo. Barua hizo zina majina ya wale walioandikiwa—iwe ni mtu binafsi au kutaniko fulani. Fikiria baadhi ya mambo ambayo Paulo anazungumzia katika barua zake.
Mashauri kuhusu maadili na mwenendo. Waasherati, wazinzi, na wanaotenda dhambi nyingine nzito “hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Wagalatia 5:19-21; 1 Wakorintho 6:9-11) Waabudu wa Mungu kutoka mataifa yote wanapaswa kuwa na umoja. (Waroma 2:11; Waefeso 4:1-6) Wanapaswa kuwasaidia kwa hiari waamini wenzao walio na uhitaji. (2 Wakorintho 9:7) Paulo anasema: “Salini bila kuacha.” Kwa kweli, waabudu wanatiwa moyo kummiminia Yehova mioyo yao katika sala. (1 Wathesalonike 5:17; 2 Wathesalonike 3:1; Wafilipi 4:6, 7) Ili sala zinazotolewa zisikiwe na Mungu, lazima zitolewe kwa imani.—Waebrania 11:6.
Ni nini kinachoweza kusaidia familia ziwe na furaha? Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Wake wanapaswa kuwaheshimu sana waume zao. Watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao, kwa kuwa hilo linampendeza Mungu. Wazazi wanapaswa kuwaongoza na kuwafundisha watoto wao kwa upendo, wakitumia kanuni za Mungu.—Waefeso 5:22–6:4; Wakolosai 3:18-21.
Wakristo wasaidiwa kuelewa kusudi la Mungu. Sheria ya Musa ilikusudiwa hasa kuwalinda na kuwaongoza Waisraeli mpaka wakati ambapo Kristo angefika. (Wagalatia 3:24) Hata hivyo, Wakristo hawahitaji kushika Sheria hiyo ili ibada yao kwa Mungu ikubaliwe. Alipokuwa akiwaandikia Waebrania, Wakristo waliokuwa na asili ya Kiyahudi, Paulo alieleza maana ya Sheria na jinsi kusudi la Mungu linavyotimizwa katika Kristo. Paulo alieleza kwamba sehemu mbalimbali za Sheria hiyo zilikuwa za kinabii. Kwa mfano, dhabihu ya Yesu ilikusudiwa kuleta msamaha wa dhambi, nayo iliwakilishwa na dhabihu za wanyama. (Waebrania 10:1-4) Kupitia kifo cha Yesu, Mungu alifuta agano la Sheria, kwa kuwa halikuwa na kazi tena.—Wakolosai 2:13-17; Waebrania 8:13.
Maagizo kuhusu utaratibu wa kutaniko. Wanaume wanaotaka kufikia mapendeleo kutanikoni wanapaswa kuwa na mwenendo mzuri na kutimiza sifa za kiroho. (1 Timotheo 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Waabudu wa Yehova Mungu wanapaswa kukusanyika kwa ukawaida pamoja na waamini wenzao ili kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Mikutano ya ibada inapaswa kuwa yenye kujenga na kuelimisha.—1 Wakorintho 14:26, 31.
Kufikia wakati ambapo alimwandikia Timotheo barua ya pili, Paulo alikuwa amerudi Roma; alikuwa gerezani akisubiri hukumu. Ni watu wachache tu waliojasiria kumtembelea. Paulo alijua kwamba ana wakati mfupi. Alisema: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.” (2 Timotheo 4:7) Yaelekea kwamba muda mfupi baadaye, Paulo aliuawa kwa sababu ya imani yake. Hata hivyo, barua za mtume huyo zina mwongozo ambao waabudu wa kweli wa Mungu wanafuata mpaka leo.
—Inatoka kwenye Waroma; 1 Wakorintho; 2 Wakorintho; Wagalatia; Waefeso; Wafilipi; Wakolosai; 1 Wathesalonike; 2 Wathesalonike; 1 Timotheo; 2 Timotheo; Tito; Filemoni; Waebrania.
-
-
Mashauri Kuhusu Imani, Mwenendo, na UpendoBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 25
Mashauri Kuhusu Imani, Mwenendo, na Upendo
Yakobo, Petro, Yohana, na Yuda, waandika barua za kuwatia moyo waamini wenzao
YAKOBO na Yuda walikuwa ndugu wa kambo wa Yesu. Petro na Yohana walikuwa mitume wa Yesu. Wanaume hao wanne waliandika jumla ya barua saba katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kila moja ya barua hizo ina jina la mwandikaji. Mashauri yaliyoongozwa na roho yaliyo katika barua hizo yalikusudiwa kuwasaidia Wakristo kudumisha utimilifu kwa Yehova na kuendelea kuutazamia Ufalme wake.
Wakristo wanapaswa kuwa na imani. Haitoshi tu kudai kwamba mtu ana imani. Imani ya kweli huambatana na matendo. Yakobo aliandika: “Imani bila matendo imekufa.” (Yakobo 2:26) Mtu anapotenda kwa imani akiwa katika majaribu, anasitawisha sifa ya uvumilivu. Ili kufanikiwa, Mkristo anahitaji kumwomba Mungu ampe hekima, akiwa na imani kwamba Mungu atampa. Uvumilivu humfanya mtu akubaliwe na Mungu. (Yakobo 1:2-6, 12) Mwabudu wa Mungu akidumisha utimilifu kwa imani, Yehova Mungu atajibu sala yake. Yakobo asema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.
Mkristo anapaswa kuwa na imani yenye nguvu inayoweza kumsaidia kushinda vishawishi na kuepuka upotovu wa maadili. Kwa sababu ya upotovu wa maadili uliokuwa umeenea, Yuda aliwahimiza waamini wenzake ‘wafanye pigano kali kwa ajili ya imani.’—Yuda 3.
Dumisha mwenendo safi. Yehova hutaka waabudu wake wawe watakatifu au safi katika kila njia. Petro aandika: “Ninyi wenyewe pia iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Muwe watakatifu, kwa sababu mimi [Yehova] ni mtakatifu.’” (1 Petro 1:15, 16) Wakristo wamewekewa mfano wa kuiga. Petro asema: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Ijapokuwa huenda Wakristo wakateseka kwa sababu wanaishi kulingana na viwango vya Mungu, wanadumisha “dhamiri njema.” (1 Petro 3:16, 17) Petro anawahimiza Wakristo wawe na mwenendo na matendo matakatifu ya ujitoaji-kimungu huku wakiingojea siku ya hukumu ya Mungu na dunia mpya iliyoahidiwa ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:11-13.
“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8
Wakristo wanapaswa kuwa na upendo. Yohana aliandika: “Mungu ni upendo.” Mtume huyo anasema kwamba Mungu alionyesha upendo wake mkuu kwa kumtuma Yesu awe ‘dhabihu kwa ajili ya dhambi zetu.’ Kwa hiyo basi, Wakristo wanapaswa kufanya nini? Yohana anajibu: “Wapendwa, ikiwa Mungu alitupenda hivi, basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu wa kupendana.” (1 Yohana 4:8-11) Njia moja ya kuonyesha upendo kama huo ni kwa kuwaonyesha ukarimu waamini wenzetu.—3 Yohana 5-8.
Hata hivyo, waabudu wa Yehova wanaweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanampenda? Yohana anajibu: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3; 2 Yohana 6) Wale wanaomtii Mungu kwa njia hiyo wanahakikishiwa kwamba Mungu ataendelea kuwapenda huku ‘wakitazamia uzima wa milele.’—Yuda 21.
—Inatoka kwenye Yakobo; 1 Petro; 2 Petro; 1 Yohana; 2 Yohana; 3 Yohana; Yuda.
-
-
Paradiso Yarudishwa!Biblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 26
Paradiso Yarudishwa!
Kupitia Ufalme wa Kristo, Yehova alitakasa jina Lake, atetea enzi Yake kuu, na kuondolea mbali uovu
KITABU cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, kinawapa wanadamu wote tumaini. Kitabu hicho kilichoandikwa na mtume Yohana, kina maono mbalimbali ambayo upeo wake ni kutimizwa kwa kusudi la Yehova.
Katika maono ya kwanza, Yesu aliyefufuliwa anapongeza na kurekebisha makutaniko kadhaa. Katika maono yanayofuata tunaona kiti cha Ufalme cha Mungu, ambapo viumbe wa roho wanamsifu.
Huku kusudi la Mungu likizidi kutimizwa, Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, apokea kitabu cha kukunjwa chenye mihuri saba. Anapofungua mihuri ya kwanza minne, wapanda-farasi wa mfano watokea. Mpanda-farasi wa kwanza ni Yesu akiwa juu ya farasi mweupe naye amevishwa taji la kifalme. Kisha wapanda-farasi juu ya farasi wenye rangi mbalimbali, wanaowakilisha vita, njaa, na tauni, mambo ambayo yanatendeka katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Muhuri wa saba unapofunguliwa, tarumbeta saba za mfano zinapulizwa zikiashiria kutangazwa kwa hukumu za Mungu. Kisha yafuata mapigo saba ya mfano, yanayowakilisha hasira ya Mungu.
Ufalme wa Mungu, unaofananishwa na mwana wa kiume aliyetoka kuzaliwa, wasimamishwa mbinguni. Vita vyatokea mbinguni, Shetani na malaika wake waovu watupwa duniani. Sauti kubwa inasema: “Ole wa dunia.” Ibilisi ana hasira kali, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.—Ufunuo 12:12.
Yohana amwona mwana-kondoo, Yesu, pamoja na wale 144,000 ambao wamechaguliwa kati ya wanadamu, ‘watakaotawala wakiwa wafalme pamoja’ na Yesu. Hivyo, kitabu cha Ufunuo kinafunua kwamba sehemu ya pili ya ule uzao inafanyizwa na jumla ya watu 144,000.—Ufunuo 14:1; 20:6.
Watawala wa dunia wanakusanyika pamoja kwa ajili ya Har–Magedoni, “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” Wanapigana vita na yule anayeketi juu ya farasi mweupe—Yesu, anayeyaongoza majeshi ya mbinguni. Watawala wote wa ulimwengu huu wanaharibiwa. Shetani anafungwa, naye Yesu na wale 144,000 wanatawala juu ya dunia kwa “miaka elfu.” Mwishoni mwa ile miaka elfu, Shetani aharibiwa.—Ufunuo 16:14; 20:4.
Utawala huo wa Kristo na watawala wenzake utawatimizia nini wanadamu watiifu? Yohana anaandika: “[Yehova] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Kisha, dunia inakuwa paradiso!
Hivyo, kitabu cha Ufunuo kinakamilisha ujumbe wa Biblia. Ufalme wa Kimasihi, utalitakasa jina la Yehova na kuitetea enzi yake kuu milele!
—Inatoka kwenye Kitabu cha Ufunuo.
-
-
Mfululizo wa MatukioBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
mnamo 2 K.W.K. Kuzaliwa kwa Yesu
29 W.K. Yesu abatizwa Yesu aanza kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu
31 W.K. Yesu achagua mitume 12; Mahubiri ya Mlimani
32 W.K. Yesu amfufua Lazaro
Nisani 14, 33 W.K. Yesu atundikwa (Sehemu ya mwezi wa 3 na sehemu ya mwezi wa 4 katika kalenda ya leo)
Nisani 16, 33 W.K. Yesu afufuliwa
Sivani 6, 33 W.K. Pentekoste; roho takatifu yamiminwa (Sehemu ya mwezi wa 5 na sehemu ya mwezi wa 6 katika kalenda ya leo)
36 W.K. Kornelio awa Mkristo
mnamo 47-48 W.K. Safari ya kwanza ya Paulo ya kuhubiri
mnamo 49-52 W.K. Safari ya pili ya Paulo ya kuhubiri
mnamo 52-56 W.K. Safari ya tatu ya Paulo ya kuhubiri
mnamo 60-61 W.K. Paulo aandika barua akiwa gerezani Roma
kabla ya 62 W.K. Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, aandika barua yake
66 W.K. Wayahudi waasi dhidi ya Roma
70 W.K. Waroma waharibu Yerusalemu pamoja na hekalu lake
mnamo 96 W.K. Yohana aandika Ufunuo
mnamo 100 W.K. Kifo cha Yohana, mtume wa mwisho
-