-
Paulo Ayaandikia MakutanikoBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 24
Paulo Ayaandikia Makutaniko
Barua za Paulo zaliimarisha kutaniko la Kikristo
KUTANIKO changa la Kikristo lilikuwa na kazi kubwa mbele yake. Lingetimiza sehemu muhimu katika kusudi la Yehova. Hata hivyo, baada ya muda usio mrefu Wakristo hao wa karne ya kwanza walishambuliwa. Je, wangedumisha utimilifu wao kwa Mungu wajapokabili mateso na hali nyingine zenye kuhatarisha uaminifu wao kutoka nje na ndani ya kutaniko? Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yana barua 21 zenye kutia moyo na zenye shauri lililohitajiwa.
Barua 14, Waroma mpaka Waebrania, ziliandikwa na mtume Paulo. Barua hizo zina majina ya wale walioandikiwa—iwe ni mtu binafsi au kutaniko fulani. Fikiria baadhi ya mambo ambayo Paulo anazungumzia katika barua zake.
Mashauri kuhusu maadili na mwenendo. Waasherati, wazinzi, na wanaotenda dhambi nyingine nzito “hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Wagalatia 5:19-21; 1 Wakorintho 6:9-11) Waabudu wa Mungu kutoka mataifa yote wanapaswa kuwa na umoja. (Waroma 2:11; Waefeso 4:1-6) Wanapaswa kuwasaidia kwa hiari waamini wenzao walio na uhitaji. (2 Wakorintho 9:7) Paulo anasema: “Salini bila kuacha.” Kwa kweli, waabudu wanatiwa moyo kummiminia Yehova mioyo yao katika sala. (1 Wathesalonike 5:17; 2 Wathesalonike 3:1; Wafilipi 4:6, 7) Ili sala zinazotolewa zisikiwe na Mungu, lazima zitolewe kwa imani.—Waebrania 11:6.
Ni nini kinachoweza kusaidia familia ziwe na furaha? Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Wake wanapaswa kuwaheshimu sana waume zao. Watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao, kwa kuwa hilo linampendeza Mungu. Wazazi wanapaswa kuwaongoza na kuwafundisha watoto wao kwa upendo, wakitumia kanuni za Mungu.—Waefeso 5:22–6:4; Wakolosai 3:18-21.
Wakristo wasaidiwa kuelewa kusudi la Mungu. Sheria ya Musa ilikusudiwa hasa kuwalinda na kuwaongoza Waisraeli mpaka wakati ambapo Kristo angefika. (Wagalatia 3:24) Hata hivyo, Wakristo hawahitaji kushika Sheria hiyo ili ibada yao kwa Mungu ikubaliwe. Alipokuwa akiwaandikia Waebrania, Wakristo waliokuwa na asili ya Kiyahudi, Paulo alieleza maana ya Sheria na jinsi kusudi la Mungu linavyotimizwa katika Kristo. Paulo alieleza kwamba sehemu mbalimbali za Sheria hiyo zilikuwa za kinabii. Kwa mfano, dhabihu ya Yesu ilikusudiwa kuleta msamaha wa dhambi, nayo iliwakilishwa na dhabihu za wanyama. (Waebrania 10:1-4) Kupitia kifo cha Yesu, Mungu alifuta agano la Sheria, kwa kuwa halikuwa na kazi tena.—Wakolosai 2:13-17; Waebrania 8:13.
Maagizo kuhusu utaratibu wa kutaniko. Wanaume wanaotaka kufikia mapendeleo kutanikoni wanapaswa kuwa na mwenendo mzuri na kutimiza sifa za kiroho. (1 Timotheo 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Waabudu wa Yehova Mungu wanapaswa kukusanyika kwa ukawaida pamoja na waamini wenzao ili kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Mikutano ya ibada inapaswa kuwa yenye kujenga na kuelimisha.—1 Wakorintho 14:26, 31.
Kufikia wakati ambapo alimwandikia Timotheo barua ya pili, Paulo alikuwa amerudi Roma; alikuwa gerezani akisubiri hukumu. Ni watu wachache tu waliojasiria kumtembelea. Paulo alijua kwamba ana wakati mfupi. Alisema: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.” (2 Timotheo 4:7) Yaelekea kwamba muda mfupi baadaye, Paulo aliuawa kwa sababu ya imani yake. Hata hivyo, barua za mtume huyo zina mwongozo ambao waabudu wa kweli wa Mungu wanafuata mpaka leo.
—Inatoka kwenye Waroma; 1 Wakorintho; 2 Wakorintho; Wagalatia; Waefeso; Wafilipi; Wakolosai; 1 Wathesalonike; 2 Wathesalonike; 1 Timotheo; 2 Timotheo; Tito; Filemoni; Waebrania.
-
-
Mashauri Kuhusu Imani, Mwenendo, na UpendoBiblia—Ina Ujumbe Gani?
-
-
Sehemu ya 25
Mashauri Kuhusu Imani, Mwenendo, na Upendo
Yakobo, Petro, Yohana, na Yuda, waandika barua za kuwatia moyo waamini wenzao
YAKOBO na Yuda walikuwa ndugu wa kambo wa Yesu. Petro na Yohana walikuwa mitume wa Yesu. Wanaume hao wanne waliandika jumla ya barua saba katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kila moja ya barua hizo ina jina la mwandikaji. Mashauri yaliyoongozwa na roho yaliyo katika barua hizo yalikusudiwa kuwasaidia Wakristo kudumisha utimilifu kwa Yehova na kuendelea kuutazamia Ufalme wake.
Wakristo wanapaswa kuwa na imani. Haitoshi tu kudai kwamba mtu ana imani. Imani ya kweli huambatana na matendo. Yakobo aliandika: “Imani bila matendo imekufa.” (Yakobo 2:26) Mtu anapotenda kwa imani akiwa katika majaribu, anasitawisha sifa ya uvumilivu. Ili kufanikiwa, Mkristo anahitaji kumwomba Mungu ampe hekima, akiwa na imani kwamba Mungu atampa. Uvumilivu humfanya mtu akubaliwe na Mungu. (Yakobo 1:2-6, 12) Mwabudu wa Mungu akidumisha utimilifu kwa imani, Yehova Mungu atajibu sala yake. Yakobo asema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.
Mkristo anapaswa kuwa na imani yenye nguvu inayoweza kumsaidia kushinda vishawishi na kuepuka upotovu wa maadili. Kwa sababu ya upotovu wa maadili uliokuwa umeenea, Yuda aliwahimiza waamini wenzake ‘wafanye pigano kali kwa ajili ya imani.’—Yuda 3.
Dumisha mwenendo safi. Yehova hutaka waabudu wake wawe watakatifu au safi katika kila njia. Petro aandika: “Ninyi wenyewe pia iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Muwe watakatifu, kwa sababu mimi [Yehova] ni mtakatifu.’” (1 Petro 1:15, 16) Wakristo wamewekewa mfano wa kuiga. Petro asema: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Ijapokuwa huenda Wakristo wakateseka kwa sababu wanaishi kulingana na viwango vya Mungu, wanadumisha “dhamiri njema.” (1 Petro 3:16, 17) Petro anawahimiza Wakristo wawe na mwenendo na matendo matakatifu ya ujitoaji-kimungu huku wakiingojea siku ya hukumu ya Mungu na dunia mpya iliyoahidiwa ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:11-13.
“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8
Wakristo wanapaswa kuwa na upendo. Yohana aliandika: “Mungu ni upendo.” Mtume huyo anasema kwamba Mungu alionyesha upendo wake mkuu kwa kumtuma Yesu awe ‘dhabihu kwa ajili ya dhambi zetu.’ Kwa hiyo basi, Wakristo wanapaswa kufanya nini? Yohana anajibu: “Wapendwa, ikiwa Mungu alitupenda hivi, basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu wa kupendana.” (1 Yohana 4:8-11) Njia moja ya kuonyesha upendo kama huo ni kwa kuwaonyesha ukarimu waamini wenzetu.—3 Yohana 5-8.
Hata hivyo, waabudu wa Yehova wanaweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanampenda? Yohana anajibu: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3; 2 Yohana 6) Wale wanaomtii Mungu kwa njia hiyo wanahakikishiwa kwamba Mungu ataendelea kuwapenda huku ‘wakitazamia uzima wa milele.’—Yuda 21.
—Inatoka kwenye Yakobo; 1 Petro; 2 Petro; 1 Yohana; 2 Yohana; 3 Yohana; Yuda.
-