Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Niliweka Kiolezo kwa Ajili Yenu”
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Agosti 15
    • “Niliweka Kiolezo kwa Ajili Yenu”

      “Mwapaswa kuwa walimu kwa kufikiria wakati.”—WAEBRANIA 5:12.

      1. Kwa nini maneno ya andiko la Waebrania 5:12 yanaweza kumtia wasiwasi Mkristo kwa kadiri fulani?

      UNAPOSOMA maneno hayo ya andiko la msingi yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu, je, yanakutia wasiwasi kwa kadiri fulani? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayetiwa wasiwasi na maneno hayo. Tukiwa wafuasi wa Kristo tunajua kwamba ni lazima tuwe walimu. (Mathayo 28:19, 20) Tunajua kwamba tunaishi nyakati zinazofanya iwe muhimu kufundisha kwa ustadi iwezekanavyo. Na tunajua kwamba kufundisha kwetu kunaweza kumaanisha kifo au uhai kwa wale tunaofundisha! (1 Timotheo 4:16) Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kujiuliza: ‘Je, ninafundisha jinsi ninavyopaswa kufundisha? Ninawezaje kuboresha ufundishaji wangu?’

      2, 3. (a) Mwalimu mmoja alielezaje msingi wa ufundishaji bora? (b) Yesu alituwekea kiolezo gani kuhusu ufundishaji?

      2 Wasiwasi huo usituvunje moyo. Huenda tukaona ni vigumu kuboresha ufundishaji wetu iwapo tunafikiri kwamba tunahitaji kuwa na ustadi fulani maalumu. Hata hivyo, mbali na ustadi, kuna jambo jingine muhimu linalotusaidia kuwa wafundishaji bora. Ona jinsi mwalimu mmoja mwenye uzoefu alivyoandika katika kitabu chake kuhusu ufundishaji: ‘Si lazima uwe na ustadi maalumu, njia, au utaratibu fulani ili uweze kufundisha vizuri. Ufundishaji hutegemea sana upendo.’ Bila shaka, mwalimu huyo alitoa maoni ya mwalimu wa kawaida wa shule. Hata hivyo, maoni yake yanafaa katika ufundishaji wetu tukiwa Wakristo. Jinsi gani?

      3 Kielelezo chetu cha mwalimu bora ni Yesu Kristo, naye aliwaambia hivi wafuasi wake: “Niliweka kiolezo kwa ajili yenu.” (Yohana 13:15) Katika andiko hilo, Yesu alikuwa akizungumzia kielelezo chake cha unyenyekevu, lakini hapana shaka kwamba kiolezo ambacho alituwekea kinatia ndani kazi yake muhimu zaidi akiwa mwanadamu duniani—ile ya kufundisha watu habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Luka 4:43) Kwa hiyo, kama ungechagua neno moja tu linalofafanua kazi ya Yesu ya kuhubiri, inaelekea ungechagua neno “upendo,” sivyo? (Wakolosai 1:15; 1 Yohana 4:8) Yesu alimpenda Yehova, Baba yake wa mbinguni, kuliko kitu kingine chochote. (Yohana 14:31) Hata hivyo, akiwa mwalimu, Yesu alionyesha upendo kwa njia nyingine mbili. Alipenda kweli alizofundisha, na aliwapenda watu aliofundisha. Hebu tuchunguze kwa makini zaidi mambo haya mawili kuhusiana na kiolezo alichotuwekea.

      Upendo wa Muda Mrefu wa Kweli za Mungu

      4. Yesu alisitawishaje upendo kwa mafundisho ya Yehova?

      4 Ubora wa ufundishaji unategemea sana mtazamo wa mwalimu kuelekea somo analofundisha. Akiwa mwenye ubaridi, yaelekea wanafunzi wake watatambua jambo hilo nao pia watakuwa wenye ubaridi. Yesu hakuwa mwenye ubaridi kuelekea kweli zenye thamani alizofundisha kuhusu Yehova na Ufalme Wake. Yesu alipenda sana kufundisha juu ya Yehova na Ufalme Wake. Alisitawisha upendo huo alipokuwa mwanafunzi. Mwana mzaliwa-pekee alikuwa mwanafunzi mwenye bidii kwa muda mrefu alioishi kabla ya kuzaliwa akiwa mwanadamu. Andiko la Isaya 50:4, 5 linatumia maneno haya yanayofaa: “Bwana MUNGU amenipa ulimi wa hao wafundishwao, nipate kujua jinsi ya kumtegemeza kwa maneno yeye aliyechoka, huniamsha asubuhi baada ya asubuhi; huniamsha, sikio langu lipate kusikia kama watu wafundishwao. Bwana MUNGU amenizibua sikio langu, wala sikuwa mkaidi, wala sikurudi nyuma.”

      5, 6. (a) Yaonekana Yesu alipatwa na jambo gani wakati wa ubatizo wake, nalo lilikuwa na matokeo gani kwake? (b) Yesu na Shetani walitumiaje Neno la Mungu kwa njia tofauti?

      5 Alipokuwa akikua akiwa mwanadamu hapa duniani, Yesu aliendelea kupenda hekima itokayo kwa Mungu. (Luka 2:52) Kisha alipokuwa akibatizwa, alipatwa na jambo la pekee. Andiko la Luka 3:21 linasema: “Mbingu ilifunguliwa.” Yaonekana wakati huo Yesu aliweza kukumbuka maisha yake kabla ya kuwa mwanadamu. Baadaye, alienda nyikani na kufunga kwa siku 40. Ni lazima awe alifurahi sana kutafakari juu ya pindi nyingi alizofundishwa na Yehova huko mbinguni. Hata hivyo, baada ya muda mfupi upendo wake kwa kweli za Mungu ulijaribiwa.

      6 Yesu alipokuwa amechoka na mwenye njaa, Shetani alitaka kumjaribu. Wana hawa wawili wa Mungu wana sifa zinazotofautiana kama nini! Wote wawili walinukuu Maandiko ya Kiebrania—lakini wakiwa na mitazamo tofauti kabisa. Shetani alipotosha Neno la Mungu, na kwa ubinafsi akalitumia bila heshima. Kwa kweli, mwasi huyo alizidharau kweli kutoka kwa Mungu. Kwa upande mwingine, Yesu alinukuu Maandiko kwa njia iliyoonyesha kwamba aliyapenda, na alitumia Neno la Mungu kwa uangalifu katika kila jibu. Yesu alikuwako muda mrefu kabla ya kuandikwa kwa maneno hayo yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu, hata hivyo, aliyaheshimu sana. Aliyaona kuwa kweli zenye thamani kutoka kwa Baba yake wa mbinguni! Alimwambia Shetani kwamba maneno hayo ya Yehova ni muhimu kuliko chakula. (Mathayo 4:1-11) Naam, Yesu alipenda kweli zote alizofundishwa na Yehova. Hata hivyo, alionyeshaje upendo huo akiwa mwalimu?

      Alipenda Kweli Alizofundisha

      7. Kwa nini Yesu aliepuka kubuni mafundisho yake mwenyewe?

      7 Ni wazi kwamba Yesu alipenda kweli alizofundisha. La sivyo, angeweza kubuni kwa urahisi mafundisho yake mwenyewe. Alikuwa na ujuzi na hekima nyingi. (Wakolosai 2:3) Hata hivyo, mara nyingi aliwakumbusha wasikilizaji wake kwamba mambo yote aliyofundisha yalitoka kwa Baba yake wa mbinguni, wala hayakutoka kwake. (Yohana 7:16; 8:28; 12:49; 14:10) Alipenda sana kweli kutoka kwa Mungu hivi kwamba hangeweza kufundisha mawazo yake mwenyewe.

      8. Yesu aliwekaje kiolezo cha kutegemea Neno la Mungu alipoanza kuhubiri?

      8 Yesu aliweka kiolezo mara alipoanza kuhubiri hadharani. Ona jinsi alivyowajulisha watu wa Mungu kwamba yeye ndiye Mesiya aliyeahidiwa. Je, alijitokeza tu mbele ya umati, akajitangaza kuwa Kristo, kisha akafanya miujiza fulani yenye kustaajabisha ili kuthibitisha jambo hilo? La. Alienda kwenye sinagogi, ambako kwa kawaida watu wa Mungu walisoma Maandiko. Huko alisoma kwa sauti kubwa unabii wa Isaya 61:1, 2 na kueleza kwamba kweli hizo za kiunabii zilimhusu yeye. (Luka 4:16-22) Miujiza yake mingi ilisaidia kuthibitisha kwamba Yehova alimwunga mkono. Hata hivyo, sikuzote alitegemea Neno la Mungu katika mafundisho yake.

      9. Yesu alionyeshaje upendo mwaminifu-mshikamanifu kwa Neno la Mungu aliposhughulika na Mafarisayo?

      9 Yesu alipopingwa na maadui wa kidini, hakujaribu kushindana nao kiakili, ingawa angeweza kufanya hivyo na kuwashinda kwa urahisi. Badala yake, aliacha Neno la Mungu liwathibitishe kuwa waongo. Kwa mfano, je, unakumbuka wakati Mafarisayo walipowashutumu wafuasi wa Yesu kuwa wamevunja sheria ya Sabato kwa sababu walikwanyua masuke machache ya nafaka na kuyala walipokuwa wakipita katika shamba fulani? Yesu aliwajibu: “Je, hamjasoma alilofanya Daudi wakati yeye na wale watu waliokuwa pamoja naye walipoona njaa?” (Mathayo 12:1-5) Yawezekana kwamba watu hao waliojiona kuwa waadilifu walisoma masimulizi hayo yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yanayopatikana katika andiko la 1 Samweli 21:1-6. Ikiwa waliyasoma, basi hawakuelewa somo muhimu linalofundishwa na masimulizi hayo. Lakini Yesu hakuyasoma tu masimulizi hayo, bali aliyatafakari na kufuata kanuni alizojifunza kutokana nayo. Alipenda kanuni ambazo Yehova alifundisha kupitia masimulizi hayo. Kwa hiyo aliyatumia na vilevile akatumia kielelezo fulani katika Sheria ya Musa kuonyesha kwamba Sheria ilikuwa na usawaziko. Vivyo hivyo, upendo mwaminifu-mshikamanifu wa Yesu ulimchochea kulitetea Neno la Mungu dhidi ya viongozi wa kidini ambao walijaribu kulipotosha kwa faida yao wenyewe au kufanya lisieleweke kwa sababu ya mapokeo ya wanadamu.

      10. Yesu alitimizaje unabii kuhusu ubora wa ufundishaji wake?

      10 Kwa kuwa Yesu alipenda kweli aliyofundisha, yeye hangeweza kamwe kufunza watu waikariri tu, wala kuwafunza kwa njia yenye kuchosha, au bila kufikiri. Unabii ulioongozwa kwa roho ya Mungu ulidokeza kwamba Mesiya angezungumza akiwa na ‘neema midomoni mwake’ na kutumia “maneno mazuri.” (Zaburi 45:2; Mwanzo 49:21) Yesu alitimiza unabii huo kwa kufanya ujumbe wake uwe wenye kuvutia na wenye kueleweka, naye alitumia “maneno yenye uvutio mwingi” alipofundisha kweli alizozipenda sana. (Luka 4:22) Yaelekea Yesu alikuwa mwenye shauku, nayo macho yake yaling’aa kwa shauku kwa kuwa alipendezwa na kweli alizofundisha. Ilipendeza kama nini kumsikiliza, naye alituwekea kiolezo bora kama nini cha kufuata tunapozungumza na wengine kuhusu yale ambayo tumejifunza!

      11. Kwa nini uwezo wa Yesu akiwa mwalimu haukumfanya ajitutumue kwa kiburi?

      11 Je, Yesu alijitutumua kwa kiburi kwa sababu alikuwa na ujuzi mwingi wa kweli inayotoka kwa Mungu na kwamba angeweza kutumia maneno yenye kuvutia? Mara nyingi walimu wa kibinadamu hufanya hivyo. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yesu alikuwa na hekima ya kimungu. Mtu akiwa na hekima hiyo hawezi kujigamba, kwa kuwa “hekima hukaa na wanyenyekevu.” (Mithali 11:2) Kuna jambo jingine lililomfanya Yesu asiwe mwenye kiburi au mwenye kujigamba.

      Yesu Aliwapenda Watu Aliofundisha

      12. Yesu alionyeshaje kwamba hakutaka kuwaogopesha wafuasi wake?

      12 Kupitia mafundisho yake, sikuzote Yesu alidhihirisha kwamba aliwapenda watu sana. Tofauti na wanadamu wenye kiburi, Yesu hakufundisha kwa njia yenye kuogopesha watu. (Mhubiri 8:9) Baada ya kuona muujiza mmoja wa Yesu, Petro alishtuka sana, akaanguka kwenye magoti ya Yesu. Lakini Yesu hakutaka wafuasi wake wawe na woga usiofaa kumwelekea hivyo akasema hivi kwa fadhili, “Koma kuogopa,” kisha akamweleza Petro kuhusu kazi yenye kufurahisha ya kufanya wanafunzi ambayo Petro mwenyewe angeshiriki. (Luka 5:8-10) Yesu hakutaka wanafunzi wake wachochewe kwa sababu walimwogopa mwalimu wao, bali alitaka wachochewe na kweli zenye thamani kumhusu Mungu.

      13, 14. Yesu aliwaonyesha watu hisia-mwenzi katika njia zipi?

      13 Yesu pia alidhihirisha upendo wake kwa watu aliofundisha kwa kuwaonyesha hisia-mwenzi. “Alipouona umati alihisi sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu ulikuwa umechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Aliwahurumia kwa sababu ya hali yao yenye kusikitisha naye alichochewa kuwasaidia.

      14 Ona jinsi alivyoonyesha hisia-mwenzi pindi nyingine. Mwanamke fulani mwenye mtiririko wa damu alipona kimuujiza alipomkaribia Yesu akiwa katikati ya umati na kugusa upindo wa vazi lake. Yesu alihisi kwamba nguvu fulani zimemtoka, lakini hakuona yule aliyeponywa na hivyo akasisitiza kumwona mwanamke huyo. Kwa nini? Yesu hakutaka kumwona ili amshutumu kwa kuvunja Sheria au amri za waandishi na Mafarisayo, jambo ambalo huenda lilimtia wasiwasi mwanamke huyo. Badala yake, alimwambia hivi: “Binti, imani yako imekufanya upone. Nenda kwa amani, na uwe katika afya njema kutokana na ugonjwa wako wa kutia kihoro.” (Marko 5:25-34) Ona jinsi maneno hayo yalivyojaa hisia-mwenzi. Hakusema tu, “Pona,” bali alisema: “Uwe katika afya njema kutokana na ugonjwa wako wa kutia kihoro.” Hapa Marko anatumia neno ambalo kihalisi linaweza kumaanisha “kupiga mjeledi,” namna ya kuchapa kwa kiboko ambayo mara nyingi hutumiwa kumtesa mtu. Hivyo, Yesu alikiri kwamba ugonjwa wa mwanamke huyo ulimletea mateso, labda maumivu ya kimwili na ya kihisia-moyo. Alimhurumia sana.

      15, 16. Ni mambo gani yaliyotokea wakati wa huduma ya Yesu yanayoonyesha kwamba alizingatia sifa nzuri za watu?

      15 Yesu pia aliwaonyesha watu upendo kwa kuzingatia sifa zao nzuri. Ona yaliyotukia alipokutana na Nathanaeli, ambaye baadaye alipata kuwa mtume wake. “Yesu akamwona Nathanaeli akija kumwelekea na kusema kumhusu yeye: ‘Ona, Mwisraeli kwa uhakika, ambaye katika yeye hamna udanganyi.’” Yesu alikuwa amechunguza moyo wa Nathanaeli kimuujiza, na hivyo kujua mambo mengi kumhusu. Bila shaka, Nathanaeli hakuwa mkamilifu. Yeye alikuwa na udhaifu kama sisi sote. Hata aliposikia juu ya Yesu, alisema hivi waziwazi: “Je, kitu chochote kilicho chema chaweza kuja kutoka Nazareti?” (Yohana 1:45-51) Hata hivyo, ingawa kuna mambo mengi ambayo Yesu angeweza kusema kumhusu Nathanaeli, yeye aliamua kuzingatia sifa moja nzuri, unyofu wake.

      16 Vivyo hivyo, wakati afisa mmoja wa jeshi—labda Mroma au mtu asiye Myahudi—alipomkaribia Yesu na kumwomba amponye mtumwa wake mgonjwa, Yesu alijua kwamba askari huyo alikuwa na udhaifu mbalimbali. Nyakati hizo, yaelekea afisa wa jeshi kama huyo angekuwa ametenda vitendo vikatili sana, ameua watu, na kushiriki ibada isiyo ya kweli. Hata hivyo, Yesu alikazia jambo jingine zuri—imani yake yenye kutokeza. (Mathayo 8:5-13) Baadaye, Yesu alipozungumza na mtenda-maovu aliyekuwa akining’inia kwenye mti wa mateso kando yake, yeye hakumshutumu mtu huyo kwa matendo yake ya uhalifu, bali alimtia moyo kwa kumpa tumaini la wakati ujao. (Luka 23:43) Yesu alijua kwamba maoni yasiyofaa na kuwashutumu wengine kungewavunja moyo tu. Yaelekea juhudi zake za kuzingatia sifa nzuri za wengine ziliwachochea wengi wafanye maendeleo.

      Utayari wa Kutumikia Watu

      17, 18. Yesu alionyeshaje utayari wa kuwatumikia wengine alipokubali mgawo wa kuja duniani?

      17 Utayari wa Yesu wa kuwatumikia watu aliofundisha ni uthibitisho mwingine mkubwa kwamba aliwapenda. Hata kabla ya kuja duniani, Mwana wa Mungu aliwapenda wanadamu. (Mithali 8:30, 31) Akiwa “Neno” au msemaji wa Yehova, huenda aliwasiliana mara nyingi sana na wanadamu. (Yohana 1:1) Hata hivyo, ili aweze kuwafundisha wanadamu kwa njia ya moja kwa moja, Yesu “alijifanya mwenyewe kuwa mtupu na kuchukua umbo la mtumwa” na kuacha cheo chake cha juu huko mbinguni. (Wafilipi 2:7; 2 Wakorintho 8:9) Alipokuwa duniani, Yesu hakungoja ahudumiwe. Badala yake alisema: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Yesu alitimiza maneno hayo kikamili.

      18 Yesu alitimiza mahitaji ya watu aliofundisha na alikuwa tayari kuwatumikia. Alisafiri kwa miguu kotekote katika Bara Lililoahidiwa, akitembea mwendo mrefu sana ili kuwafikia na kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo. Yeye alikuwa tofauti na Mafarisayo na waandishi wenye kiburi kwa kuwa alikuwa mnyenyekevu na watu walijihisi huru kumfikia. Watu wa aina zote—waheshimiwa, askari, wanasheria, wanawake, watoto, maskini, wagonjwa, na hata waliokuwa wamekataliwa na jamii—walimfikia bila kusitasita wala kuogopa. Ingawa alikuwa mkamilifu, Yesu alihisi njaa na uchovu. Lakini alitanguliza mahitaji ya wengine hata alipokuwa amechoka, alipohitaji kupumzika, au alipohitaji kuwa na wakati mtulivu wa kusali.—Marko 1:35-39.

      19. Yesu aliwawekeaje wanafunzi wake kiolezo cha kutendeana kwa unyenyekevu, subira, na fadhili?

      19 Yesu pia alikuwa tayari kuwatumikia wanafunzi wake. Alifanya hivyo kwa kuwafundisha kwa fadhili na kwa subira. Yeye hakukata tamaa, wala kukasirika, wala kuwashutumu wanafunzi wake waliposhindwa kuelewa mambo fulani muhimu. Aliendelea kutafuta njia za kuwasaidia kuelewa. Kwa mfano, hebu fikiria jinsi wanafunzi hao walivyozozana mara kwa mara kuhusu ni nani kati yao aliye mkubwa. Hadi usiku wa kuamkia kifo chake, Yesu aliendelea kutafuta njia za kuwafundisha kutendeana kwa unyenyekevu. Kuhusu unyenyekevu, sawa na mambo mengine, Yesu angeweza kusema hivi kwa kufaa: “Mimi niliweka kiolezo kwa ajili yenu.”—Yohana 13:5-15; Mathayo 20:25; Marko 9:34-37.

      20. Ni njia gani ya kufundisha iliyomtofautisha Yesu na Mafarisayo, na kwa nini njia hiyo ilikuwa na matokeo?

      20 Ona kwamba badala ya kuwaeleza wanafunzi wake kiolezo hicho ni nini, Yesu ‘aliwawekea kiolezo.’ Aliwafundisha kwa kielelezo. Hakuzungumza nao kama watu wa hali ya chini, kana kwamba alijiona kuwa mtu bora au mtu wa maana sana asiweze kufanya mambo aliyowafundisha. Hivyo ndivyo Mafarisayo walivyofanya. Yesu alisema hivi kuwahusu: “Wao husema lakini hawafanyi.” (Mathayo 23:3) Kwa unyenyekevu, Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake maana hasa ya mafundisho yake kwa kuishi kupatana nayo. Kwa hiyo alipowatia moyo wafuasi wake waishi maisha sahili bila kufuatia vitu vya kimwili, walielewa mara moja alichomaanisha. Wangeweza kuona kwamba maneno yake yafuatayo yalikuwa ya kweli: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:20) Yesu aliwatumikia wanafunzi wake kwa kuwawekea kiolezo kwa unyenyekevu.

      21. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

      21 Hapana shaka kwamba Yesu ndiye Mwalimu Mkuu zaidi aliyepata kuishi! Watu wote wenye mioyo minyofu waliomwona na kumsikiliza waliona wazi kwamba Yesu anapenda mambo aliyofundisha na watu aliowafundisha. Leo, sisi pia tunaweza kuona upendo huo tunapojifunza kiolezo alichoweka. Hivyo basi, tunawezaje kufuata kielelezo kikamilifu cha Kristo? Makala inayofuata itajibu swali hilo.

  • ‘Nifuateni kwa Kuendelea’
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Agosti 15
    • ‘Nifuateni kwa Kuendelea’

      “Kwenye mwendo huu mliitwa, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia kigezo ili nyinyi mfuate hatua zake kwa ukaribu.”—1 PETRO 2:21.

      1, 2. Kwa nini kielelezo kikamilifu cha Yesu si cha juu sana tusiweze kukiiga?

      YESU KRISTO ndiye Mwalimu mkuu zaidi aliyepata kuishi. Zaidi ya hilo, alikuwa mkamilifu na hakutenda dhambi muda wote alioishi duniani akiwa mwanadamu. (1 Petro 2:22) Ingawa hivyo, je, hiyo inamaanisha kwamba kielelezo cha Yesu akiwa mwalimu ni cha juu sana hivi kwamba sisi wanadamu wasio wakamilifu hatuwezi kukiiga? La, hasha.

      2 Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, upendo ndio uliokuwa msingi wa ufundishaji wa Yesu. Na sote tunaweza kusitawisha sifa hiyo ya upendo. Mara nyingi Neno la Mungu hututia moyo tusitawishe na kuboresha upendo wetu kwa wengine. (Wafilipi 1:9; Wakolosai 3:14) Yehova hatazamii viumbe wake wafanye zaidi ya yale wanayoweza. Naam, kwa kuwa “Mungu ni upendo” na ametuumba kwa mfano wake, tunaweza kusema kwamba alituumba ili tuonyeshe upendo. (1 Yohana 4:8; Mwanzo 1:27) Kwa hiyo, tunaposoma maneno ya Petro kwenye andiko letu la msingi, tunaweza kujibu kwa uhakika kwamba tunaweza kufuata hatua za Kristo kwa ukaribu. Hata tunaweza kutii amri hii ya Yesu: ‘Nifuateni kwa kuendelea.’ (Luka 9:23) Hebu tuone jinsi tunavyoweza kuiga upendo ambao Kristo alionyesha, kwanza kuelekea kweli alizofundisha, kisha kuelekea watu aliofundisha.

      Kusitawisha Upendo kwa Kweli Tunazojifunza

      3. Kwa nini ni vigumu kwa watu wengine kujifunza, lakini tunapata himizo gani kwenye andiko la Mithali 2:1-5?

      3 Ili kupenda kweli tunazowafunza wengine, ni lazima sisi wenyewe tupende kujifunza kweli hizo. Katika ulimwengu wa leo, mara nyingi si rahisi kusitawisha upendo kama huo. Kutokuwa na elimu ya kutosha, na mazoea mabaya ya kujifunza yaliyositawishwa ujanani hufanya wengi wachukie kabisa kujifunza. Hata hivyo, ni muhimu tujifunze kutoka kwa Yehova. Andiko la Mithali 2:1-5 linasema: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia [“kuendelea kuutafuta,” NW] kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu [“ujuzi juu ya Mungu,” NW].”

      4. Inamaanisha nini ‘kuuelekeza’ moyo, na ni mtazamo gani utakaotusaidia kufanya hivyo?

      4 Ona kwamba katika mstari wa 1 hadi wa 4, tumesihiwa tena na tena tujitahidi ‘kukubali,’ ‘kuweka akiba,’ na pia ‘kuendelea kutafuta.’ Ni nini basi kitakachotuchochea kufanya mambo hayo yote? Ona maneno ‘elekeza moyo wako upate ufahamu.’ Kitabu kimoja kinachofafanua andiko hilo kinasema kwamba katika himizo hilo “hatuombwi tu tusikilize; bali tunatakiwa kuwa na mtazamo fulani: hamu ya kusikiliza yale tunayojifunza.” Ni nini kinachoweza kutufanya tusikilize na tuwe na hamu ya kujifunza yale ambayo Yehova hutufundisha? Ni mtazamo wetu. Tunahitaji kuona “ujuzi juu ya Mungu” kuwa kama “fedha” na kama “hazina iliyositirika.”

      5, 6. (a) Ni nini kinachoweza kutokea baada ya muda, na tunawezaje kuzuia jambo hilo lisitokee? (b) Kwa nini tuendelee kuongeza hazina za ujuzi ambazo tumepata katika Biblia?

      5 Si vigumu kusitawisha mtazamo kama huo. Kwa mfano, yaelekea “ujuzi juu ya Mungu” ambao umejifunza unatia ndani ile kweli ya kwamba Yehova anakusudia wanadamu waaminifu waishi milele katika dunia Paradiso. (Zaburi 37:28, 29) Ulipojifunza kweli mara ya kwanza, inaelekea uliiona kuwa hazina ya kweli, ujuzi uliojaza tumaini na furaha katika akili na moyo wako. Namna gani leo? Baada ya muda fulani kupita, je, uthamini kwa hazina yako umefifia? Basi, jaribu kufanya mambo haya mawili. Kwanza, jaribu kuwa na uthamini tena, yaani, ujikumbushe mara kwa mara ni kwa nini unathamini kila mojawapo ya kweli ambazo Yehova amekufundisha, hata zile ulizojifunza miaka mingi iliyopita.

      6 Pili, endelea kuongeza hazina yako. Kwani, ikiwa bila kutazamia ungechimba na kupata jiwe lenye thamani kubwa, je, ungeliweka mfukoni tu na kwenda zako ukiwa umeridhika? Au ungeendelea kuchimba kuona kama unaweza kupata mawe zaidi yenye thamani? Neno la Mungu limejaa kweli zilizo kama fedha au mawe yenye thamani kubwa. Hata uwe umejifunza kweli nyingi kiasi gani, bado unaweza kujifunza zaidi. (Waroma 11:33) Unapojifunza kweli fulani mpya, jiulize: ‘Ni nini kinachoifanya iwe hazina? Je, kweli hiyo inanisaidia kuwa na ufahamu zaidi kuhusu utu wa Yehova au makusudi yake? Je, inatoa mwongozo unaoweza kunisaidia kufuata hatua za Yesu?’ Kutafakari juu ya maswali hayo kutakusaidia usitawishe upendo kwa kweli ambazo Yehova amekufundisha.

      Kupenda Kweli Tunazojifunza

      7, 8. Ni katika njia zipi tunaweza kuwaonyesha wengine kwamba tunapenda kweli tunazojifunza katika Biblia? Toa mfano.

      7 Tunapofunza wengine, tunawezaje kuonyesha kwamba tunapenda kweli ambazo tumejifunza katika Neno la Mungu? Kwa kufuata kielelezo cha Yesu, tunaitegemea sana Biblia tunapohubiri na kufundisha. Katika nyakati za karibuni, watu wa Mungu ulimwenguni pote wametiwa moyo waitumie Biblia zaidi wanapohubiri. Unapofuata dokezo hilo, tafuta njia za kumwonyesha mwenye nyumba kwamba hata wewe unathamini Maandiko unayomweleza.—Mathayo 13:52.

      8 Kwa mfano, muda mfupi baada ya lile shambulio la magaidi huko New York City, dada mmoja Mkristo aliwasomea andiko la Zaburi 46:1, 11 watu aliokutana nao alipokuwa akihubiri. Kwanza aliwauliza jinsi wanavyokabiliana na hali baada ya msiba huo. Alisikiliza majibu yao kwa makini, akawashukuru, kisha akasema: “Je, ninaweza kuwasomea andiko ambalo limenifariji kwelikweli wakati huu mgumu?” Ni watu wachache sana waliokataa, naye aliweza kuanzisha mazungumzo mengi mazuri. Anapozungumza na vijana, mara nyingi dada huyo husema hivi: “Nimekuwa nikifundisha Biblia kwa miaka 50 sasa, na unajua nini? Sijawahi kupata tatizo hata moja ambalo kitabu hiki hakiwezi kunisaidia kulitatua.” Kwa kuwa wanyofu na wenye shauku, tunawaonyesha watu kwamba tunathamini yale ambayo tumejifunza katika Neno la Mungu.—Zaburi 119:97, 105.

      9, 10. Kwa nini ni muhimu kutumia Biblia tunapojibu maswali kuhusu imani yetu?

      9 Watu wanapotuuliza maswali kuhusu imani yetu, tunakuwa na nafasi nzuri ya kuwaonyesha kwamba tunalipenda Neno la Mungu. Kwa kufuata kielelezo cha Yesu, sisi hatuwajibu kwa kutumia maoni yetu. (Mithali 3:5, 6) Badala yake, sisi hutumia Biblia. Je, unaogopa kwamba huenda mtu fulani akakuuliza swali ambalo hutaweza kujibu? Ona hatua mbili unazoweza kuchukua.

      10 Jitayarishe kwa kadiri uwezavyo. Mtume Petro aliandika: “Mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwenu sababu ya tumaini lililo katika nyinyi, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.” (1 Petro 3:15) Je, uko tayari kutetea imani yako? Kwa mfano, ikiwa mtu anataka kujua ni kwa nini hufuati desturi au zoea fulani lisilopatana na Maandiko, usiridhike kusema tu, “Dini yangu hainiruhusu kufanya hivyo.” Huenda jibu kama hilo likadokeza kwamba wewe hutegemea watu wengine wakufanyie maamuzi, na hivyo lazima uwe unashirikiana na madhehebu fulani. Ingefaa kusema, “Neno la Mungu, Biblia, hukataza jambo hilo” au, “Jambo hilo linamchukiza Mungu wangu.” Kisha eleza kwa busara ni kwa nini unasema hivyo.—Waroma 12:1.

      11. Ni kifaa gani cha kufanyia utafiti kinachoweza kukusaidia kuwa tayari kujibu maswali kuhusu kweli za Neno la Mungu?

      11 Ikiwa unaona hujajitayarisha, kwa nini usisome kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko?a Chagua habari ambazo yaelekea watu watakuwa na maswali kuzihusu, na uweke akilini Maandiko fulani. Weka kitabu chako cha Kutoa Sababu na Biblia yako mahali unapoweza kuvipata kwa urahisi. Usisite kuvitumia na pia kumweleza anayeuliza swali kwamba una kifaa cha kufanyia utafiti ambacho ungependa kutumia ili kupata majibu ya Biblia kwa maswali yake.

      12. Tunaweza kuitikiaje ikiwa hatujui jibu la swali fulani la Biblia?

      12 Jaribu kuepuka kuwa na wasiwasi kupita kiasi. Mwanadamu asiye mkamilifu hawezi kujua jibu la kila swali analoulizwa. Kwa hiyo, ukiulizwa swali la Biblia usilojua jibu lake, unaweza kusema hivi: “Asante sana kwa swali lako zuri. Kusema kweli, sijui jibu lake, lakini nina hakika kwamba Biblia inajibu swali hilo. Mimi hupenda kufanya utafiti wa mambo yanayohusiana na Biblia, hivyo nitachunguza swali lako kisha nirudi kukujibu.” Huenda njia hiyo iliyo wazi na ya unyenyekevu ikafanya iwezekane kuwa na mazungumzo zaidi.—Mithali 11:2.

      Kuwapenda Watu Tunaofundisha

      13. Kwa nini tunapaswa kudumisha maoni yanayofaa kuelekea wale tunaohubiria?

      13 Yesu aliwapenda watu aliofundisha. Tunaweza kumwigaje katika jambo hilo? Tusiwe na mtazamo wa kutowajali watu wanaotuzunguka. Ni kweli kwamba, “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote” inakaribia sana, na watu wengi sana wataharibiwa. (Ufunuo 16:14; Yeremia 25:33) Hata hivyo, hatujui ni nani atakayeokoka na ni nani atakayeharibiwa. Hukumu hiyo ni ya wakati ujao, nayo itatekelezwa na yule ambaye Yehova ameweka rasmi, Yesu Kristo. Hadi hukumu hiyo itekelezwe, sisi tunaona kwamba mtu yeyote yule anaweza kuwa mtumishi wa Yehova.—Mathayo 19:24-26; 25:31-33; Matendo 17:31.

      14. (a) Tunaweza kujichunguzaje kuona kama tuna hisia-mwenzi kuelekea watu? (b) Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba tuna hisia-mwenzi na tunapendezwa na wengine?

      14 Kama Yesu basi, tunataka kuwaonyesha watu hisia-mwenzi. Huenda tukajiuliza: ‘Je, mimi huhurumia watu ambao wamedanganywa kwa hila na wanadini, wanasiasa, na wafanyabiashara? Ikiwa wanaonekana kuwa na ubaridi kuelekea ujumbe tunaowapelekea, je, mimi hujitahidi kuelewa ni kwa nini wanahisi hivyo? Je, ninatambua kwamba mimi, au wengine ambao sasa wanamtumikia Yehova kwa uaminifu, walihisi vivyo hivyo wakati fulani? Je, mimi hubadili utangulizi wangu ninapohubiri ili ufaane na hali? Au mimi hupuuza watu hao na kuwaona kuwa hawawezi kubadilika? (Ufunuo 12:9) Watu wakiona kwamba kwa kweli tuna hisia-mwenzi, inaelekea sana kwamba watasikiliza ujumbe wetu. (1 Petro 3:8) Hisia-mwenzi zinaweza kutuchochea tupendezwe zaidi na watu tunaokutana nao tunapohubiri. Tunaweza kuandika maswali na mahangaiko yao. Tunaporudi, tunaweza kuwaeleza kwamba tulifikiria mambo waliyosema tulipowatembelea wakati uliopita. Na ikiwa wakati huo wana jambo fulani linalohitaji kushughulikiwa haraka, tunaweza kuwasaidia.

      15. Kwa nini tuzingatie sifa nzuri za watu, na tunawezaje kufanya hivyo?

      15 Kama Yesu, sisi huzingatia sifa nzuri za watu. Labda mwanamke fulani asiye na mume anajitahidi sana kulea watoto wake. Mwanamume fulani anajitahidi sana kuitunza familia yake. Mtu fulani mzee anapendezwa na mambo ya kiroho. Je, tunaona sifa hizo katika watu tunaokutana nao, na je, tunawapongeza? Kwa kufanya hivyo, tunatilia mkazo mambo ambayo sote tunakubaliana, na huenda jambo hilo likatuwezesha kutoa ushahidi juu ya Ufalme.—Matendo 26:2, 3.

      Unyenyekevu Ni Muhimu Katika Kuonyesha Upendo

      16. Kwa nini ni muhimu kuwa wapole na wenye staha kuelekea wale tunaohubiria?

      16 Ikiwa tunawapenda watu tunaofundisha, tutachochewa kutii onyo hili la Biblia lenye hekima: “Ujuzi hututumuka, lakini upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Yesu alikuwa na ujuzi mwingi sana, lakini hakuwa na kiburi. Kwa hiyo unapowaeleza wengine kuhusu imani yako, usiwe mwenye mabishano au kujionyesha kwamba unajua sana. Lengo letu ni kufikia mioyo ya watu na kuwavutia kwenye kweli ambazo tunazipenda sana. (Wakolosai 4:6) Kumbuka, wakati Petro alipowashauri Wakristo wawe tayari kujitetea, alitukumbusha pia kwamba tunapaswa kufanya hivyo “kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.” (1 Petro 3:15) Tukiwa wapole na wenye staha, inaelekea sana kwamba tutavuta watu kwa Mungu tunayemtumikia.

      17, 18. (a) Tutatendaje kuelekea watu wenye mitazamo ya kuchambua kustahili kwetu kuwa wahubiri? (b) Kwa nini kujua lugha za kale zilizotumiwa kuandika Biblia si muhimu kwa wanafunzi wa Biblia?

      17 Hakuna haja ya kuonyesha watu kwamba tuna ujuzi au elimu nyingi. Usivunjwe moyo na watu fulani katika eneo lenu ambao watakataa kusikiliza yeyote asiye na digrii ya chuo kikuu au jina fulani la cheo. Yesu hakujali malalamiko ya watu waliosema kwamba hakuwa ameenda kwenye shule za hali ya juu za kirabi zilizokuweko wakati huo; wala hakufuata maoni yasiyofaa ya wengi kwa kujionyesha kwamba alikuwa na ujuzi mwingi.—Yohana 7:15.

      18 Sifa ya unyenyekevu na upendo ni muhimu zaidi kwa wahubiri Wakristo kuliko elimu yoyote ya kilimwengu. Mwalimu Mkuu, Yehova, hutuwezesha kuwa na sifa za kustahili kuhubiri. (2 Wakorintho 3:5, 6) Na hata makasisi wa dini zinazojiita eti za Kikristo wasemeje, sisi hatuhitaji kujifunza lugha za kale zilizotumiwa kuandika Biblia ili tustahili kuwa walimu wa Neno la Mungu. Yehova alitumia roho yake ili Biblia iandikwe katika lugha rahisi na yenye kueleweka kusudi karibu kila mtu aweze kufahamu kweli za Biblia zenye thamani. Kweli hizo hazibadiliki hata kidogo hata zinapotafsiriwa katika mamia ya lugha nyingine. Kwa hiyo kujua lugha hizo za kale si muhimu ingawa mara kwa mara ujuzi huo hutusaidia. Zaidi ya hayo, kuwa na kiburi kwa kujua lugha fulani kunaweza kufanya mtu akose sifa fulani muhimu kwa Wakristo wa kweli—kuwa mwenye kufundishika.—1 Timotheo 6:4.

      19. Ni katika maana gani kazi yetu ya Kikristo ya kuhubiri ni utumishi?

      19 Bila shaka, tunahitaji kuwa wanyenyekevu tunapofanya kazi yetu ya Kikristo ya kuhubiri. Mara nyingi sisi hukabili upinzani, ubaridi, na hata mnyanyaso. (Yohana 15:20) Hata hivyo, kwa kuendelea kuhubiri kwa uaminifu, tunafanya utumishi muhimu. Tukiendelea kutumikia wengine kwa unyenyekevu katika kazi hii, tutakuwa tukiiga upendo ambao Yesu Kristo alionyesha watu. Hebu fikiria: Kama tungelazimika kuhubiria watu elfu moja wenye ubaridi ili kupata mtu mmoja tu mwenye mfano wa kondoo, je, hiyo isingekuwa jitihada inayofaa? Bila shaka! Kwa hiyo kwa kuendelea kufanya kazi hiyo bila kuacha, tunawatumikia kwa uaminifu watu wenye mfano wa kondoo ambao hatujawafikia bado. Bila shaka Yehova na Yesu watahakikisha kwamba wengi wa watu hao wenye thamani watapatikana na kusaidiwa kabla ya mwisho kufika.—Hagai 2:7.

      20. Tunaweza kufundisha kwa kielelezo chetu kupitia njia zipi?

      20 Kufundisha kwa kielelezo chetu wenyewe ni njia nyingine inayoonyesha tu tayari kuwatumikia wengine. Kwa mfano, tunataka kuwafundisha watu kwamba kumtumikia Yehova, “Mungu mwenye furaha,” ndiyo njia bora na yenye kuridhisha zaidi maishani. (1 Timotheo 1:11) Wanapotazama mwenendo wetu na jinsi tunavyoshughulika na majirani, wanashule, na wafanyakazi wenzetu, je, wanaweza kuona kwamba tuna furaha na tumeridhika? Vivyo hivyo, sisi hufunza wanafunzi wa Biblia kwamba katika kutaniko la Kikristo, wanaweza kupata upendo ambao hauwezi kupatikana katika ulimwengu usiojali na mkatili. Je, wanafunzi wanaweza kuona kwamba tunapenda kila mtu katika kutaniko na tunajitahidi kudumisha amani na kila mmoja?—1 Petro 4:8.

      21, 22. (a) Kujichunguza kuhusiana na kazi yetu ya kuhubiri kunaweza kutusaidia kutumia fursa gani? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala za toleo linalofuata la Mnara wa Mlinzi?

      21 Huenda nyakati nyingine utayari wetu wa kuhubiri ukatuchochea tujichunguze upya. Wengi huona kwamba wanaweza kuongeza muda wanaotumia katika mahubiri kwa kuanza utumishi wa wakati wote au kwa kuhamia sehemu zenye uhitaji mkubwa zaidi. Wengine wameamua kujifunza lugha ya kigeni ili kuhubiria jamii ya wahamiaji wanaozidi kuongezeka katika maeneo yao. Ikiwa unaweza kutumia fursa kama hizo, basi zifikirie kwa makini na kwa sala. Maisha ya kutumikia huleta furaha nyingi, uradhi, na amani ya akili.—Mhubiri 5:12.

      22 Na tujitahidi tuwezavyo kumwiga Yesu Kristo kwa kusitawisha upendo kuelekea kweli tunazofundisha na kwa watu tunaofundisha. Kusitawisha na kuonyesha upendo katika njia hizo mbili kutatusaidia kuweka msingi mzuri wa kuwa walimu walio kama Kristo. Hata hivyo, tunaweza kujengaje juu ya msingi huo? Toleo linalofuata la Mnara wa Mlinzi litakuwa na mfululizo wa makala zitakazozungumzia njia fulani hususa ambazo Yesu alitumia kufundisha.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki