-
“Hakuna Aliye na Upendo Mkuu Kuliko Huu”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
“Mpendane; Kama Vile Ambavyo Nimewapenda Ninyi”
10, 11. Yesu aliwapa wafuasi wake amri gani mpya, nayo inatia ndani nini, na kwa nini tunapaswa kuitii?
10 Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake wa karibu hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) “Mpendane”—kwa nini hiyo ni “amri mpya”? Tayari Sheria ya Musa ilikuwa imeagiza: “Mpende mwenzako [au, jirani yako] kama wewe mwenyewe.” (Mambo ya Walawi 19:18) Lakini amri hiyo mpya inatutaka tuonyeshe upendo mkubwa hata zaidi, upendo ambao utatuchochea kuutoa uhai wetu wenyewe kwa ajili ya wengine. Yesu mwenyewe alitaja hilo waziwazi aliposema: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda ninyi. Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:12, 13) Ni kana kwamba amri hiyo mpya inasema: “Wapende wengine, si kama unavyojipenda, bali kuliko unavyojipenda.” Bila shaka, Yesu alionyesha upendo huo katika maisha yake na vilevile kwa kuwa tayari kufa.
11 Kwa nini tunapaswa kutii amri hiyo mpya? Kumbuka kwamba Yesu alisema: “Kwa jambo hili [yaani, upendo wa kujidhabihu] wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu.” Ndiyo, upendo wa kujidhabihu unatutambulisha kuwa Wakristo wa kweli. Tunaweza kuufananisha upendo huo na beji ya kujitambulisha. Wajumbe ambao huhudhuria makusanyiko ya kila mwaka ya Mashahidi wa Yehova huvaa beji. Beji hiyo inamtambulisha aliyeivaa, ikionyesha jina na kutaniko lake. Upendo wa kujidhabihu kwa ajili ya wengine ni “beji” inayowatambulisha Wakristo wa kweli. Yaani, upendo tunaoonyeshana unapaswa kuonekana wazi sana hivi kwamba unakuwa ishara, au beji, inayojulisha watazamaji kwamba bila shaka sisi ni wafuasi wa kweli wa Kristo. Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, “beji” yangu ya upendo wa kujidhabihu inaonekana waziwazi maishani mwangu?’
Upendo wa Kujidhabihu Unatia Ndani Nini?
12, 13. (a) Tunapaswa kujidhabihu kiasi gani kuonyesha kwamba tunapendana? (b) Kujidhabihu ni nini?
12 Tukiwa wafuasi wa Yesu tunapaswa kupendana kama vile alivyotupenda. Hilo linamaanisha kuwa tayari kujidhabihu kwa ajili ya waamini wenzetu. Tunapaswa kujidhabihu kiasi gani? Biblia inatuambia: “Kwa hili tumeujua upendo, kwa sababu huyo aliitoa nafsi yake kwa ajili yetu; na sisi tuko chini ya wajibu kuzitoa nafsi zetu kwa ajili ya ndugu zetu.” (1 Yohana 3:16) Kama Yesu, tunapaswa kuwa tayari hata kufa kwa ajili ya ndugu zetu ikihitajika. Wakati wa mateso, afadhali tufe kuliko kuwasaliti ndugu zetu wa kiroho na hivyo kuhatarisha maisha yao. Katika nchi ambazo zimegawanyika kwa sababu ya mizozo ya kikabila au kijamii, tutakuwa tayari kuhatarisha maisha yetu ili kuwalinda ndugu zetu, haidhuru jamii au kabila lao. Mataifa yanapoenda vitani, afadhali tufungwe au hata kufa kuliko kupigana na waamini wenzetu au mtu mwingine yeyote.—Yohana 17:14, 16; 1 Yohana 3:10-12.
13 Kuwa tayari kufa kwa ajili ya ndugu zetu siyo njia pekee ya kuonyesha upendo wa kujidhabihu. Kwa kweli, ni wachache kati yetu ambao huenda wakahitaji kutoa dhabihu kubwa kama hiyo. Hata hivyo, ikiwa tunawapenda ndugu zetu kiasi cha kufa kwa ajili yao, je, hatupaswi kuwa tayari kujidhabihu kwa njia ndogo-ndogo, kujitolea kuwasaidia sasa? Kujidhabihu ni kujinyima mapendezi na starehe kwa faida za wengine. Tunafanya hivyo kwa kutanguliza mahitaji yao na kuwahangaikia hata ikiwa si rahisi. (1 Wakorintho 10:24) Tunaweza kujidhabihu katika njia gani mbalimbali?
Katika Kutaniko na Katika Familia
14. (a) Wazee wanajidhabihu katika njia gani? (b) Una maoni gani kuhusu wazee wa kutaniko lenu ambao wanafanya kazi kwa bidii?
14 Wazee wa kutaniko wanajidhabihu sana ili ‘kulichunga kundi.’ (1 Petro 5:2, 3) Mbali na kutunza familia zao wenyewe, huenda wakahitaji kutumia wakati wao jioni au mwishoni mwa juma ili kushughulikia mambo ya kutaniko, kutia ndani kutayarisha migawo watakayokuwa nayo katika mikutano, kufanya ziara za uchungaji, na kushughulikia visa vya hukumu. Wazee wengi wanajidhabihu hata zaidi, wakifanya kazi kwa bidii katika makusanyiko na kutumikia wakiwa washiriki wa Halmashauri za Uhusiano na Hospitali, Vikundi vya Kuwatembelea Wagonjwa, na Halmashauri za Ujenzi za Mkoa. Ninyi wazee, msisahau kwamba mnaonyesha upendo wa kujidhabihu mnapotumikia kwa hiari mkitumia wakati wenu, nguvu zenu, na mali zenu kulichunga kundi. (2 Wakorintho 12:15) Bidii yenu isiyo na ubinafsi inathaminiwa na Yehova na vilevile kutaniko mnalochunga.—Wafilipi 2:29; Waebrania 6:10.
15. (a) Wake za wazee hujidhabihu kwa njia gani? (b) Una maoni gani kuhusu wake wanaowaunga mkono waume zao kwa kudhabihu wakati ambao wangetumia pamoja nao ili kutaniko lenu lifaidike?
15 Hata hivyo, namna gani wake za wazee? Je, si kweli kwamba dada hao wenye kuwaunga mkono wanajidhabihu pia ili waume zao walitunze kundi? Ni kweli kwamba mke hujidhabihu mume wake anapotumia wakati kwa ajili ya mambo ya kutaniko, wakati ambao angeweza kuutumia pamoja na familia yake. Wafikirie pia wake za waangalizi wanaosafiri na jinsi wanavyojidhabihu ili kusafiri pamoja na waume zao kutoka kutaniko moja kwenda lingine na kutoka mzunguko mmoja kwenda mwingine. Wao huacha makao yao wenyewe na nyakati nyingine wanalazimika kulala katika kitanda tofauti kila juma. Wake wanaotanguliza faida za kutaniko kwa hiari wanastahili pongezi kwa kuonyesha upendo wa kujidhabihu.—Wafilipi 2:3, 4.
16. Wazazi Wakristo hujidhabihu jinsi gani kwa ajili ya watoto wao?
16 Ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha upendo wa kujidhabihu katika familia? Ninyi wazazi mnajidhabihu sana ili kutosheleza mahitaji ya watoto wenu na kuwalea “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Huenda mkalazimika kufanya kazi ngumu zenye kuchosha, tena kwa muda mrefu, ili kuwaandalia watoto chakula na kuhakikisha kwamba wana mavazi na makao mazuri. Huenda hata mkajinyima ili kuhakikisha kwamba mnatosheleza mahitaji ya msingi ya watoto wenu. Pia, ninyi hutia bidii sana kujifunza na watoto wenu, kwenda nao kwenye mikutano ya Kikristo, na kwenda pamoja nao katika huduma ya shambani. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Upendo wenu wa kujidhabihu unamfurahisha Mwanzilishi wa maisha ya familia na kuwawezesha watoto wenu kuwa na tumaini la uzima wa milele.—Methali 22:6; Waefeso 3:14, 15.
17. Waume Wakristo wanaweza kumwiga Yesu jinsi gani kwa kutokuwa na ubinafsi?
17 Ninyi waume, mnaweza kumwiga Yesu jinsi gani kwa kuonyesha upendo wa kujidhabihu? Biblia inajibu: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Waefeso 5:25) Kama tulivyoona, Yesu aliwapenda wafuasi wake sana kiasi cha kufa kwa ajili yao. Mume Mkristo huiga mtazamo usio na ubinafsi alioonyesha Yesu, ambaye “hakujipendeza mwenyewe.” (Waroma 15:3) Mume kama huyo anatanguliza mahitaji na mapendezi ya mke wake kwa hiari. Hasisitizi kwa ushupavu kwamba kila kitu kifanywe anavyotaka, bali yuko tayari kukubali maoni ya mke wake ikiwa hakuna kanuni ya Kimaandiko inayohusika. Mume anayeonyesha upendo wa kujidhabihu hupata kibali cha Yehova, naye anapendwa na kuheshimiwa na mke na watoto wake.
Utafanya Nini?
18. Ni nini kinachotuchochea kutii ile amri mpya ya kupendana?
18 Si rahisi kutii ile amri mpya ya kupendana, hata hivyo, kuna jambo kuu ambalo linatuchochea kufanya hivyo. Paulo aliandika hivi: “Upendo alio nao Kristo hutulazimisha, kwa sababu hili ndilo tumehukumu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote . . . , naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.” (2 Wakorintho 5:14, 15) Kwa kuwa Yesu alikufa kwa ajili yetu, je, hatupaswi kujitahidi kuishi kwa ajili yake? Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwaonyesha wengine upendo wa kujidhabihu kama vile alivyofanya.
19, 20. Ni zawadi gani yenye thamani kubwa ambayo Yehova ametupa, nasi tunaweza kufanya nini kuonyesha kwamba tunaikubali?
19 Yesu hakuwa akitia chumvi wakati ambapo alisema maneno haya: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Kwa kukubali kuitoa nafsi yake kwa ajili yetu, alionyesha kwa njia kuu zaidi upendo wake kwetu. Hata hivyo, kuna mwingine ambaye ametuonyesha upendo mkubwa hata zaidi. Yesu mwenyewe alieleza: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Mungu anatupenda sana hivi kwamba alimtoa Mwana wake awe fidia, na kutukomboa kutoka katika dhambi na kifo. (Waefeso 1:7) Fidia ni zawadi yenye thamani kubwa kutoka kwa Yehova, hata hivyo hatulazimishi tuikubali.
-