-
Wakristo Wanapaswa Kufanya Nini Leo?Mnara wa Mlinzi—2012 | Mei 1
-
-
Wakristo Wanapaswa Kufanya Nini Leo?
WAKRISTO wa kweli leo hawashiriki katika siasa. Kwa nini? Kwa sababu wanaiga mfano wa Yesu. Alisema hivi kujihusu: “Mimi si sehemu ya ulimwengu.” Na akasema hivi kuwahusu wafuasi wake: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19; 17:14) Fikiria sababu kadhaa kwa nini Wakristo hawapaswi kujiingiza katika siasa.
1. Wanadamu hawana uwezo kamili. Biblia inasema kwamba wanadamu hawana uwezo wala haki ya kujitawala. Nabii Yeremia aliandika: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.
Kama vile ambavyo wanadamu hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kupaa angani kwa nguvu zao wenyewe, vilevile hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kujitawala wenyewe kwa mafanikio. Akionyesha kwamba serikali hazina uwezo kamili, mwanahistoria David Fromkin alisema hivi: “Serikali hufanyizwa na wanadamu; hivyo basi mara nyingi hazifaulu na wakati wao ujao haujulikani. Zina nguvu kwa kiasi fulani, lakini si kikamili.” (The Question of Government) Ndiyo sababu Biblia inatuonya tusiwategemee wanadamu!—Zaburi 146:3.
2. Roho waovu wanaongoza wanadamu. Shetani alipotaka kumpa Yesu utawala wa dunia, Yesu hakusema kwamba Ibilisi hakuwa na mamlaka ya kumpa falme zote za ulimwengu. Baadaye, hata Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu.” Miaka kadhaa baadaye mtume Paulo alisema kwamba Shetani ni “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (Yohana 14:30; 2 Wakorintho 4:4) Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Tuna kushindana mweleka . . . juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Roho waovu ndio wanaotawala ulimwengu ingawa watu wengi hawafahamu hivyo. Jambo hilo linapaswa kufanya tuwe na maoni gani kuhusu siasa?
Fikiria ulinganisho huu: Kama vile mashua ndogo zinavyoweza kusukumwa na upepo wa baharini, ndivyo mifumo ya kisiasa ya wanadamu inavyoongozwa na nguvu za roho waovu. Na kama vile mabaharia katika mashua hizo wasivyoweza kubadili upepo huo wenye nguvu, ndivyo pia wanasiasa wasivyoweza kubadili nguvu za roho hao waovu. Roho hao waovu wameazimia kuwapotosha wanadamu kabisa na kusababisha ‘ole kwa dunia.’ (Ufunuo 12:12) Kwa hiyo, badiliko la kweli linaweza kuletwa tu na mtu mwenye nguvu kuliko Shetani na mashetani wake. Mtu huyo ni Yehova Mungu.—Zaburi 83:18; Yeremia 10:7, 10.
3. Wakristo wa kweli wanaunga mkono Ufalme wa Mungu peke yake. Yesu na wanafunzi wake walijua kwamba Mungu alikuwa amepanga wakati ambao atasimamisha serikali mbinguni itakayotawala dunia nzima. Biblia inasema serikali hiyo ni Ufalme wa Mungu na inafunua kwamba Yesu Kristo ndiye aliyechaguliwa kuwa Mfalme. (Ufunuo 11:15) Kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu kilikuwa “habari njema ya ufalme wa Mungu,” kwa sababu alijua kwamba Ufalme huo unawahusu wanadamu wote. (Luka 4:43) Pia, aliwafundisha wanafunzi wake kusali: “Ufalme wako na uje.” Kwa nini? Kwa sababu chini ya ufalme huo, bila shaka, mapenzi ya Mungu yatatimia mbinguni na duniani.—Mathayo 6:9, 10.
Hivyo basi, serikali za wanadamu zitapatwa na nini? Biblia inajibu kwamba serikali za “dunia nzima inayokaliwa,” zitaharibiwa. (Ufunuo 16:14; 19:19-21) Ikiwa kwa kweli mtu anaamini kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa serikali zote za wanadamu, basi itakuwa jambo la busara kutounga mkono mifumo ya kisiasa. Zaidi ya hayo, ikiwa mtu ataunga mkono serikali za wanadamu ambazo zitaharibiwa, basi atakuwa akimpinga Mungu.
Kwa sababu Wakristo wa kweli hawashiriki katika siasa, je, hilo linamaanisha kwamba hawataki kabisa kujaribu kusaidia watu wengine wawe na maisha bora? Ona jibu linalotolewa katika makala inayofuata.
-
-
Mafundisho ya Kikristo Yanasaidiaje Jamii?Mnara wa Mlinzi—2012 | Mei 1
-
-
Mafundisho ya Kikristo Yanasaidiaje Jamii?
MAKALA zilizotangulia zimeeleza kwa nini Wakristo wa kweli hawashiriki katika siasa. Hata hivyo, Wakristo wanaweza kuonyeshaje kwamba wanataka kuwasaidia watu katika jamii wawe na maisha bora? Njia moja ni kwa kutii amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Mathayo 28:19, 20.
Kutii amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi’ kunahusiana na kufuata mashauri yake ya kuwa kama chumvi na nuru kwa ulimwengu. (Mathayo 5:13, 14) Mambo hayo yanahusianaje? Na kazi hiyo inaweza kuwasaidiaje watu?
Ujumbe wa Kristo Unaelimisha na Kulinda
Chumvi hutumiwa kuhifadhi vitu visiharibike. Vivyo hivyo, ujumbe ambao Yesu aliwaamuru wafuasi wake wawapelekee watu wa mataifa yote unaweza kuwahifadhi. Watu wanaokubali na kuishi kulingana na mafundisho ya Yesu wanajilinda kutokana na maadili mapotovu ambayo yameenea sana leo. Hilo linawezekanaje? Wanajifunza jinsi ya kuepuka mazoea ambayo yanaweza kuwadhuru kiafya, kwa mfano kuvuta sigara, na wanasitawisha sifa kama vile upendo, amani, ustahimilivu, fadhili, na wema. (Wagalatia 5:22, 23) Sifa kama hizo zinafanya wawe watu wazuri katika jamii. Wakristo wanaoshiriki pamoja na jirani zao ujumbe huo wenye kuhifadhi, wanasaidia sana jamii zao.
Vipi kuhusu mfano wa nuru? Kama vile tu mwezi unavyoangaza nuru kutoka kwenye jua, ndivyo wafuasi wa Kristo wanavyoangaza “nuru” kutoka kwa Yehova Mungu. Wanaangaza nuru hiyo kupitia ujumbe wenye kuelimisha wanaohubiri na pia kupitia matendo yao mazuri.—1 Petro 2:12.
Zaidi ya hayo, Yesu alieleza uhusiano uliopo kati ya kuwa nuru na kuwa mwanafunzi aliposema: “Watu huwasha taa na kuiweka, si chini ya kikapu cha kupimia, bali juu ya kinara cha taa, nayo huangazia watu wote waliomo ndani ya nyumba. Vivyo hivyo acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu.” Taa inayong’aa ambayo imewekwa juu ya kinara inaonekana na watu wote wanaoizunguka. Vilevile, kazi ya kuhubiri na matendo mengine mazuri ambayo Wakristo wa kweli wanatenda yanapaswa kuonekana waziwazi na watu wanaowazunguka. Kwa nini? Yesu alisema kwamba wale wanaoona matendo hayo mazuri watamtukuza Mungu bali si Wakristo.—Mathayo 5:14-16.
Daraka la Wakristo Wote
Yesu aliposema, “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu” na “acheni nuru yenu iangaze,” alikuwa akiwaagiza wanafunzi wake wote. Amri ambayo Yesu alitoa haiwezi kutimizwa na watu wachache waliotawanyika katika dini mbalimbali. Badala yake, waamini wote ni “nuru.” Mashahidi wa Yehova milioni saba hivi ambao wanaishi katika nchi zaidi ya 235, wanaamini kwamba wana jukumu la kuwatembelea jirani zao na kuwaeleza kuhusu ujumbe ambao Kristo anataka wafuasi wake watangaze.
Kichwa kikuu cha ujumbe wa Mashahidi wa Yehova ni nini? Yesu alipotoa amri ya kuhubiri, hakuwaagiza wafuasi wake wahubiri kuhusu mabadiliko ya kijamii au kisiasa, muungano wa Kanisa na Serikali, au sera nyingine za wanadamu. Badala yake, alitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Hivyo, Wakristo wa kweli leo wanatii maagizo ya Yesu kwa kuendelea kuongea na jirani zao kuhusu Ufalme wa Mungu ambao ni serikali pekee iliyo na uwezo wa kukomesha mfumo mwovu wa Shetani na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu.
Unaposoma masimulizi ya Injili, utaona mambo mawili makuu kuhusu huduma ya Yesu ambayo yanaongoza matendo ya Wakristo wa kweli leo. Mambo hayo mawili yanazungumziwa katika makala inayofuata.
-