Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kinachowachochea Watu Washerehekee Krismasi
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 1
    • Kinachowachochea Watu Washerehekee Krismasi

      “Ni rahisi kunaswa na pilikapilika za majira ya Krismasi. Desturi za sikukuu zinafuatwa tu ili kutimiza wajibu, wakati unaotumiwa pamoja na familia na marafiki unaweza kuwa mfupi kwa sababu ya ratiba zenye shughuli nyingi. Wakati fulani tunakosa shangwe tunayopaswa kuwa nayo kwa sababu ya mikazo tunayopitia.”​—BRAD HENRY, GAVANA WA ZAMANI WA OKLAHOMA [MAREKANI], DESEMBA 23, 2008.

      MAJIRA ya Krismasi yanapokaribia, nyimbo, sinema, na vipindi vya televisheni huchochea hisia za shangwe na furaha​—mambo yanayowafanya watu washerehekee Krismasi. Unafikiri ni jambo gani hasa linalopaswa kuwachochea watu? Je, huenda ni

      • Kumkumbuka Yesu Kristo?

      • Kushiriki furaha ya kutoa?

      • Kuwasaidia watu wenye uhitaji?

      • Kutumia wakati pamoja na familia?

      • Kudumisha amani?

      Kama alivyosema Gavana Henry, aliyenukuliwa upande wa kushoto, wengi wanaosherehekea Krismasi wanaona ni vigumu kutimiza mambo hayo wakati wa sikukuu. Mara nyingi, wakati wa Krismasi huwa wenye shughuli nyingi, mikazo mingi, na zaidi ya yote ni wakati wa biashara. Je, inawezekana kupata shangwe na upendo, sifa zinazopaswa kuwa sehemu ya Krismasi?

      Biblia inatutia moyo tumkumbuke Yesu Kristo, tuwe wakarimu katika kutoa, tuwasaidie wenye uhitaji, na tutumie wakati pamoja na familia zetu. Pia, inatufundisha jinsi ya kufanya amani. Kwa hiyo, badala ya kuzungumzia kwa nini watu fulani hawasherehekei Krismasi,a mfululizo huu utachunguza maswali yafuatayo:

      • Kwa nini watu fulani wanahisi kwamba wanapaswa kusheherekea Krismasi?

      • Kwa nini ni vigumu kutimiza mambo wanayotazamia wakati wa Krismasi?

      • Ni kanuni gani za Biblia ambazo zimewasaidia mamilioni ya watu kupata jambo bora kuliko Krismasi?

      a Ili kujua sababu za Kimaandiko zinazowafanya watu fulani wasisherehekee Krismasi, ona makala “Wasomaji Wetu Wanauliza​—Kwa Nini Watu Fulani Hawasherehekei Krismasi?”

  • Kumkumbuka Yesu Kristo
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 1
    • Kumkumbuka Yesu Kristo

      “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.”​—LUKA 22:19.

      Kwa nini watu fulani husherehekea Krismasi?

      Kuhusiana na Krismasi, watu fulani wanasema kwamba “imekusudiwa kumkumbuka Yesu.” Wanasherehekea Krismasi ili kukumbuka siku ya kuzaliwa kwake.

      Kwa nini ni vigumu kufanya hivyo?

      Miziki na desturi nyingi za Krismasi hazihusiani na Yesu Kristo. Mamilioni ya watu wanaosherehekea Krismasi hawamwamini; baadhi yao hata hawaamini kwamba aliwahi kuwapo. Katika ulimwengu wa kibiashara, Krismasi imekuwa sikukuu ya kutangaza biashara badala ya siku ya kumkumbuka Yesu.

      Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kutusaidia?

      “Mwana wa binadamu alikuja . . . kutoa nafsi yake iwe fidia badala ya wengi.” (Marko 10:45) Yesu alisema maneno yaliyonukuliwa mwanzoni mwa makala hii, si katika siku yake ya kuzaliwa bali usiku uliotangulia kifo chake. Jioni hiyo, alianzisha sherehe ndogo ya kukumbuka kifo chake. Hata hivyo, kwa nini Yesu alitaka wafuasi wake wakumbuke kifo chake badala ya kuzaliwa kwake? Kwa sababu dhabihu ya fidia ya Yesu inawapa wanadamu watiifu fursa ya kupata uzima wa milele. Biblia inasema: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Hivyo, kila mwaka, kwenye ukumbusho wa kifo chake, wafuasi wa Yesu humkumbuka Yesu Kristo, si kama mtoto mchanga bali kama “mwokozi wa ulimwengu.”​—Yohana 4:42.

      “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Ili kumheshimu na kumkumbuka Yesu, unapaswa kuchunguza mfano alioweka akiwa mwanamume mkamilifu na mwenye akili. Pia, tafakari jinsi Yesu alivyoonyesha huruma, subira, na ujasiri wa kufanya yale yaliyofaa na utafute fursa za kumwiga Yesu katika maisha yako.

      “Ufalme wa ulimwengu umekuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atatawala akiwa mfalme milele na milele.” (Ufunuo 11:15) Unapomkumbuka Yesu Kristo, fikiria kile anachofanya sasa. Yesu anatawala akiwa Mfalme mbinguni. Neno la Mungu lilitabiri hivi kumhusu Yesu: “Atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.” (Isaya 11:4) Sifa hizo zote zenye kuvutia si za mtoto mchanga, bali ni za Mtawala mwenye nguvu.

  • Furaha ya Kutoa
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 1
    • Furaha ya Kutoa

      “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​—MATENDO 20:35.

      Kwa nini watu fulani husherehekea Krismasi?

      Kama Yesu alivyosema, kutoa humfanya mtoaji na mpokeaji kuwa na furaha. Ili kupata furaha hiyo, wengi wameona kutoa zawadi kuwa jambo muhimu zaidi linalopaswa kufanywa wakati wa Krismasi. Kwa mfano, mwaka uliopita wenye matatizo ya kiuchumi, uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba huko Ireland kila familia ilitazamia kutumia karibu dola 660 za Marekani ili kununua zawadi za Krismasi.

      Kwa nini ni vigumu kufanya hivyo?

      Watu wengi wanahisi kwamba zawadi za Krismasi huleta mkazo badala ya furaha. Jinsi gani? Wanunuzi wengi hulazimika kununua zawadi ambazo hawana uwezo wa kuzinunua. Na kwa kuwa kila mtu ananunua zawadi wakati uleule, misongamano ya watu na foleni ndefu huwachosha watu wengi.

      Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kutusaidia?

      Yesu alisema: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu.”a (Luka 6:38) Hakuweka wakati maalumu katika mwaka ambao watu wangetazamiwa kutoa zawadi. Yesu aliwahimiza wafuasi wake wawe na zoea la kutoa zawadi mara kwa mara.

      “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Kitabu kimoja kinachotoa maelezo kuhusu Biblia kinasema kuwa ushauri huo wa Paulo unamaanisha kwamba “mtu asifanye jambo lolote kwa ‘kulazimishwa,’ yaani, asihisi analazimishwa kutoa.” Kuwa “mtoaji mchangamfu” kunaondoa hisia za kulazimishwa kumpa mtu hususa kitu hususa kwa wakati hususa​—kama ilivyo na zawadi za Krismasi.

      “Ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika zaidi kulingana na kile ambacho mtu anacho, si kulingana na kile ambacho mtu hana.” (2 Wakorintho 8:12) Mungu hataki Wakristo wajiingize katika madeni ili kulipia zawadi za bei ghali. Badala yake, mtu anapotoa ‘kulingana na kile alicho nacho,’ zawadi zake zinakuwa nzuri na ‘zinazokubalika zaidi.’ Ni jambo zuri kama nini, ikilinganishwa na ujumbe wa matangazo ya kibiashara ya wakati wa Krismasi yanayosema “nunua sasa, lipa baadaye!”

      a Tafsiri fulani za Biblia zinatumia neno: “Toa.” Katika Kigiriki cha awali, kitenzi hicho huonyesha tendo linaloendelea. Ili kutoa maana kamili ya maneno ambayo Yesu alitumia, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inasema “muwe na mazoea ya kuwapa watu.”

  • Kuwasaidia Watu Wenye Uhitaji
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 1
    • Kuwasaidia Watu Wenye Uhitaji

      “Mwenye jicho la ukarimu atabarikiwa, kwa maana amempa mtu wa hali ya chini chakula chake.”​—METHALI 22:9.

      Kwa nini watu fulani husherehekea Krismasi?

      Kwa kuwa Yesu aliwasaidia maskini, wagonjwa, na wenye kuteseka, watu fulani wanataka kumwiga. Wanahisi kwamba wakati bora wa kufanya hivyo ni Krismasi, ambapo mashirika ya kutoa misaada hujitahidi sana kukusanya michango.

      Kwa nini ni vigumu kufanya hivyo?

      Wakati wa Krismasi, watu wengi huhangaikia sana kununua vitu, tafrija, na kuwatembelea marafiki na watu wa ukoo. Mambo hayo huwamalizia wakati, nguvu, pesa za kuwapa maskini na wenye uhitaji, pia za kuchangia mashirika yanayotoa misaada.

      Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kutusaidia?

      “Usiwanyime watu mema wanayostahili, mkono wako ukiwa na uwezo wa kuyafanya.” (Methali 3:27) Maskini,wenye njaa, na wanaoteseka hawapatwi na matatizo wakati wa Krismasi tu. Ikiwa unatambua kwamba mtu fulani anahitaji msaada na ‘mkono wako una uwezo’ wa kumsaidia, kwa nini usubiri mpaka wakati wa Krismasi ili umsaidie? Utabarikiwa kwa kuwa na matendo ya fadhili na huruma.

      “Kila siku ya kwanza ya juma acheni kila mmoja wenu kwenye nyumba yake mwenyewe aweke kando kitu fulani katika akiba kulingana na anavyofanikiwa.” (1 Wakorintho 16:2) Mtume Paulo alitoa shauri hilo kwa Wakristo wa mapema waliotaka kuwasaidia maskini. Je, unaweza ‘kuweka kando’ au kutenga kiasi fulani cha pesa ili uwape kwa ukawaida watu au shirika linalotoa misaada yake kwa hekima? Kwa kufanya hivyo, utakuwa na hakika kwamba unawajali watu wenye uhitaji huku ukitoa kulingana na uwezo wako.

      “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.” (Waebrania 13:16) Ona kwamba licha ya “kushiriki vitu pamoja na wengine” ni lazima pia tukumbuke “kutenda mema” au kuwasaidia wengine. Kwa mfano, wazazi wenye hekima huwazoeza watoto wao kuwasaidia wazee-wazee kufanya kazi za nyumbani za kila siku; kuwatia moyo wagonjwa kwa kuwapa kadi, kuwatembelea, au kuwapigia simu; na kupendezwa kibinafsi na watoto wengine walio maskini au wanaoteseka kutokana na ulemavu. Matokeo ni kwamba watoto wanajifunza kuwa wenye fadhili na ukarimu wakati wote.

      Wazazi wenye hekima huwazoeza watoto wao kuwasaidia wazee wazee, wagonjwa na watu wenye uhitaji. Matokeo ni kwamba watoto wanajifunza kuwa wenye fadhili na ukarimu wakati wote

  • Umoja Katika Familia
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 1
    • Umoja Katika Familia

      “Tazama! Jinsi ilivyo vyema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!”​—ZABURI 133:1.

      Kwa nini watu fulani husherehekea Krismasi?

      Kwa kuwa Waisraeli walikuwa wazao wa mwanamume mmoja, Yakobo, au Israeli, walikuwa “ndugu,” yaani, washiriki wa familia moja. Walipokusanyika Yerusalemu kwa ajili ya sherehe, lilikuwa jambo ‘jema’ na lenye ‘kupendeza.’ Kama Waisraeli, familia nyingi leo hutafuta fursa za kukutana pamoja na kufurahia wakati wa Krismasi wenye ‘kupendeza’ na ‘mwema.’

      Kwa nini ni vigumu kufanya hivyo?

      Kitabu Encyclopedia of Christmas and New Year’s Celebrations kinasema: “Matatizo madogo-madogo ambayo familia imeyakabili katika kipindi chote cha mwaka, hubadilika na kuwa matatizo makubwa pindi tu familia hizo zinapokusanyika ili kusheherekea Krismasi.”

      Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kutusaidia?

      ‘Endeleeni kuwalipa wazazi na wazazi wa wazazi wenu.’ (1 Timotheo 5:4) Kwa kadiri uwezavyo, panga kuwatembelea watu wa familia yako kwa ukawaida. Ikiwa wanaishi mbali, bado unaweza kuwasiliana nao mara kwa mara. Unaweza kuwaandikia barua, kuwapigia simu, kuwatumia barua-pepe, au kuwatumia ujumbe kupitia Intaneti. Kuwasiliana kwa ukawaida hupunguza hali ya kutoelewana.

      “Mmesongwa mkakosa nafasi katika upendo mwororo. . . . Panukeni.” (2 Wakorintho 6:12, 13) Watoto huwaogopa watu wa ukoo wanaowaona mara moja tu kwa mwaka. Watoto fulani huhisi kwamba hawapatani na babu na nyanya zao au watu wa mbali wa ukoo. Kwa hiyo, watie moyo watoto wako ‘wapanuke’ katika upendo wao kwa kuwahusisha watu wa ukoo ambao ni wazee-wazee.a Watoto wanaotumia muda wao kikawaida na wazee-wazee husitawisha hisia-mwenzi na uthamini kwa watu waliowazidi umri.

      “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!” (Methali 15:23) Unawezaje kuzuia hali ya kutoelewana au matatizo yanayoharibu uhusiano wa familia? Njia moja ni kuchagua “wakati unaofaa” wa kuzungumzia matatizo. Ikiwa mnawasiliana mara kwa mara, itakuwa rahisi kumkaribia kibinafsi mshiriki wa familia ili kusuluhisha tatizo lolote na kufurahia wakati ‘mwema’ na wenye ‘kupendeza’ mnapokuwa pamoja.

      a Ona makala “Kwa Nini Niwajue Vizuri Babu Na Nyanya?” na “Ninawezaje Kusitawisha Uhusiano wa Karibu Pamoja na Babu na Nyanya?” katika matoleo ya gazeti Amkeni! ya Aprili 22 na Mei 22, 2001, yaliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

  • “Amani Kati ya Watu wa Nia Njema”
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 1
    • “Amani Kati ya Watu wa Nia Njema”

      “Utukufu katika vilele vilivyo juu kwa Mungu, na juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.”​—LUKA 2:14.

      Kwa nini watu fulani husherehekea Krismasi?

      Kila mwaka, papa na viongozi wengine wa kidini huhubiri ujumbe wa amani, wakitumaini kwamba majira ya Krismasi yatatimiza tangazo hili la malaika: “Juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.” Wengine hupanga safari za kidini ili kwenda mahali fulani patakatifu na kusheherekea.

      Kwa nini ni vigumu kufanya hivyo?

      Mara nyingi, amani wakati wa Krismasi huwa ni ya muda mfupi tu. Kwa mfano, Desemba 1914, wakati bara Ulaya lilipokuwa katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, wanajeshi wa Uingereza na wa Ujerumani walitoka kwenye mahandaki yao na kusheherekea Krismasi pamoja. Walikula, wakanywa, na kuvuta sigara pamoja. Pia, walicheza mpira wa miguu. Hata hivyo, amani hiyo haikudumu kwa muda mrefu. Katika barua iliyotoka vitani, mwanajeshi wa Uingereza alisimulia kwamba mwanajeshi wa Ujerumani alimwambia: “Leo tuna amani. Kesho utaipigania nchi yako; na mimi nitaipigania nchi yangu.”

      Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kutusaidia?

      “Kuna mtoto ambaye amezaliwa kwetu . . . Naye ataitwa jina . . . Mkuu wa Amani. Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.” (Isaya 9:6, 7) Je, hutiwi moyo na unabii huo kumhusu Yesu Kristo? Yesu hakuzaliwa duniani ili kuleta amani ya siku moja kila mwaka. Akiwa Mtawala aliye mbinguni, ataleta amani ya kweli ambayo itadumu milele.

      “Kupitia kwangu [Yesu] mpate kuwa na amani. Ulimwenguni mna dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Hata leo, Yesu anawasaidia wafuasi wake kuwa na amani. Ni kweli kwamba Wakristo wana dhiki. Hata hivyo, kwa msaada wa Biblia, wanaelewa ni kwa nini watu wanateseka na jinsi Yesu atakavyoleta amani yenye kudumu. Kwa hiyo, wanafurahia kuwa na amani ya akili.

      Kwa kutii maneno ya Yesu, Mashahidi wa Yehova​—kutoka kila taifa, rangi, jamii, au lugha—​wanafurahia amani hiyo. Jionee mwenyewe kwa kuhudhuria mikutano kwenye Jumba lao la Ufalme. Kama watu wengine wengi, huenda utakubali kwamba amani hiyo ni bora kuliko amani yoyote inayotokana na Krismasi.

      Mashahidi wa Yehova wameunganishwa kwa sababu ya amani licha ya rangi au lugha yao. Jionee mwenyewe kwa kuhudhuria mikutano kwenye Jumba lao la Ufalme

  • Wamepata Jambo Bora Kuliko Krismasi
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 1
    • Wamepata Jambo Bora Kuliko Krismasi

      MAMILIONI ya Wakristo wamechagua kutosherehekea Krismasi. Wanahisije kuhusu uamuzi wao? Je, wanahisi kwamba wanakosa kitu fulani? Je, watoto wao wanahisi wamenyimwa nafasi ya kusherehekea? Hebu ona vile Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanavyosema kuhusu jambo hilo.

      Ningeenda tu wakati wa Krismasi au Pasaka. Lakini hata wakati huo, kwa kweli sikumfikiria Yesu Kristo. Sasa sisherehekei Krismasi, bali ninahudhuria mikutano ya Kikristo mara mbili kwa juma na hata kuwafundisha wengine kile ambacho Biblia inasema kumhusu Yesu!”​—EVE, AUSTRALIA.

      Furaha ya kutoa: “Mimi husisimuka ninapopokea zawadi bila kutazamia. Ninafurahia zawadi kama hizo! Pia, napenda kutengeneza kadi na kuwachorea wengine picha, kwa kuwa jambo hilo huwafanya wafurahi, nami pia hufurahi.”​—REUBEN, IRELAND KASKAZINI.

      Kuwasaidia wenye uhitaji: “Tunafurahia kuwapikia wagonjwa chakula. Wakati fulani tunawapelekea maua, keki, au zawadi ndogo ili kuwachangamsha. Tunafurahia kufanya hivyo, kwa sababu tunaweza kuwatembelea watu hao wakati wowote katika mwaka.”​—EMILY, AUSTRALIA.

      Umoja katika familia: “Familia yetu inapokusanyika, watoto wetu wanapata fursa ya kuwajua wajomba, shangazi, babu, nyanya, na binamu zao katika hali yenye kustarehesha. Kwa kuwa hatufanyi hivyo katika tarehe hususa ya mwaka, hatuhisi mkazo, na watu wa familia yetu wanajua kwamba tunawatembelea kwa sababu tunawapenda.”​—WENDY, VISIWA VYA CAYMAN.

      Amani: “Wakati wa Krismasi, inaonekana kuna shughuli nyingi sana hivi kwamba ni watu wachache wanaofikiria kuhusu amani. Nimejifunza ahadi za Biblia kuhusu wanadamu, na ninajihisi huru. Sasa ninajua kwamba watoto wangu watafurahia wakati ujao wenye furaha.”​—SANDRA, HISPANIA.

  • Kwa nini watu fulani hawasherehekei Krismasi?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 1
    • Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

      Kwa nini watu fulani hawasherehekei Krismasi?

      Ulimwenguni pote, karibu watu bilioni mbili husherehekea Krismasi kila Desemba 25, na watu wapatao milioni 200 husherehekea siku ya kuzaliwa kwa Yesu Januari 7. Hata hivyo, pia kuna mamilioni ya watu ambao wameamua kutosherehekea Krismasi kabisa. Kwa nini?

      Sababu moja ni kwamba huenda ni washiriki wa dini ambayo si sehemu ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kwa mfano, wanaweza kuwa Wayahudi, Wahindu, au Washinto. Wengine kama vile, watu wanaoamini hakuna Mungu, wanaoamini kwamba mambo yake hayawezi kujulikana, wanaopinga mambo ya kidini, au wale wanaoshikilia imani zao bila kujihusisha na dini yoyote, huona hadithi ya Krismasi kuwa hekaya.

      Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba idadi fulani ya watu wanaomwamini Yesu wanapinga tamaduni za majira ya Krismasi. Kwa nini? Wanatoa sababu nne hivi.

      Kwanza, hawaamini kwamba Yesu alizaliwa Desemba au Januari. Biblia haitaji tarehe hususa. Inasema hivi: “Katika nchi hiyo kulikuwako pia wachungaji wakiishi nje, wakichunga makundi yao usiku. Na kwa ghafula malaika wa Yehova akasimama kando yao, na . . . akawaambia: ‘. . . Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu.’”​—Luka 2:8-11.

      Hoja zenye kuaminika zinaonyesha kwamba Yesu alizaliwa karibu mwanzoni mwa mwezi wa Oktoba wakati wachungaji walikuwa wakiishi nje wakichunga makundi yao usiku. Katika miezi ya Desemba na Januari, maeneo ya mashambani yanayozunguka Bethlehemu huwa ni majira ya baridi kali sana. Hivyo, ili kuwalinda wanyama wao kutokana na baridi usiku, waliwapeleka kwenye mazizi yaliyoezekwa.

      Sababu ya pili: Tukio pekee ambalo Yesu aliwaagiza kihususa wafuasi wake wakumbuke ni kifo chake, wala si kuzaliwa kwake, na huo ungefanywa kama mlo wa ushirika usio na mambo mengi. (Luka 22:19, 20) Pia, ona kwamba Injili za Marko na Yohana hazitaji kuhusu kuzaliwa kwa Yesu.

      Tukio pekee ambalo Yesu aliwaagiza kihususa wafuasi wake wakumbuke ni kifo chake, wala si kuzaliwa kwake

      Sababu ya tatu: Hakuna uthibitisho wa kihistoria unaoonyesha kwamba Wakristo wa mapema walisherehekea kuzaliwa kwa Kristo. Hata hivyo, walikumbuka kifo chake. (1 Wakorintho 11:23-26) Lakini miaka 300 baada ya kuzaliwa kwa Yesu, dini zinazodai kuwa za Kikristo zilianza rasmi kuadhimisha Krismasi Desemba 25. Jambo la kuvutia ni kwamba katikati mwa karne ya 17, bunge la Uingereza lilipitisha sheria ya kupiga marufuku sherehe za Krismasi. Nchini Marekani, Mahakama Kuu ya Massachusetts ilichukua hatua kama hiyo. Kwa nini? Kitabu The Battle for Christmas, kinasema: “Hakuna sababu yoyote ya kibiblia au kihistoria inayothibitisha kwamba Yesu alizaliwa Desemba 25.” Kinaendelea kusema Wapuriti waliona “Krismasi kuwa sherehe ya kipagani ambayo watu fulani walijaribu kuifanya iwe ya Kikristo.”

      Hilo linatusaidia kupata sababu ya nne: Chanzo kisichofaa cha sherehe hiyo. Krismasi ilitokana na ibada ya kipagani huko Roma ambayo ilikuwa na mchanganyiko wa sherehe za kuheshimu mungu wa kilimo Saratenina na mungu jua Sol Invictus, au Mithra. Wataalamu wa kuchunguza asili ya binadamu Christian Rätsch na Claudia Müller-Ebeling, ambao pia walishiriki katika kuandika kitabu Pagan Christmas, waliandika hivi: “Kama tu desturi na imani nyingi za kabla ya Ukristo, sherehe ya kale ya kukumbuka kurudi kwa jua ilibadilishwa na kuwa sherehe ya kukumbuka kuzaliwa kwa Kristo.”

      Unapofikiria mambo yaliyotajwa katika makala hii, je, umeona ni kwa nini Wakristo wa kweli hawasherehekei Krismasi?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki