-
“Hamwijui Ile Siku Wala Saa”Mnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 15
-
-
WATIWA-MAFUTA WATHIBITISHA KWAMBA WAKO TAYARI
11. Baada ya mwaka wa 1914, kwa nini watiwa-mafuta fulani walifikiri kwamba Bwana amekawia?
11 Kumbuka mifano ya Yesu kuhusu wale mabikira na talanta. Ikiwa mabikira au watumwa katika mifano hiyo wangejua wakati ambapo bwana-arusi au bwana mkubwa angekuja, hawangehitaji kuendelea kukesha. Lakini hawakujua, kwa hiyo, walihitaji kuendelea kuwa tayari. Ingawa kwa miongo mingi watiwa-mafuta waliuona mwaka wa 1914 kuwa mwaka wa pekee, hawakuelewa waziwazi ni nini ambacho kingetukia. Mambo yalipokosa kutukia kama walivyotarajia, huenda baadhi yao walidhani kwamba Bwana-arusi amekawia. Baadaye, ndugu mmoja alikumbuka hivi: “Wachache kati yetu walifikiri kwa hakika kwamba tungeenda mbinguni katika juma la kwanza la Oktoba [mwaka wa 1914].”
12. Watiwa-mafuta walionyeshaje kwamba ni waaminifu na wenye busara?
12 Hebu fikiria jinsi ilivyovunja moyo kutarajia mwisho uje lakini haukuja! Isitoshe, akina ndugu walikabiliana na upinzani wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu! Kisha kukawa na kipindi cha kutotenda, kama cha usingizi. Lakini mwaka wa 1919, kulikuwa na mwito wa kuamka! Yesu alikuja katika hekalu la kiroho la Mungu, na wakati wa ukaguzi ulikuwa umefika. Hata hivyo, baadhi ya Wakristo hawakufaulu kupita ukaguzi huo na hivyo wakapoteza pendeleo lao la kuendelea kufanya “biashara” ya Mfalme. (Mt. 25:16) Kama wale mabikira wapumbavu, ni kana kwamba hawakuwa na bidii ya kuongeza mafuta yao ya kiroho. Na kama yule mtumwa goigoi, hawakuwa tayari kujidhabihu kwa ajili ya Ufalme. Hata hivyo, idadi kubwa ya watiwa-mafuta walionyesha ushikamanifu usioyumba-yumba na tamaa kubwa ya kumtumikia Bwana wao hata katika ile miaka migumu ya vita.
-
-
“Hamwijui Ile Siku Wala Saa”Mnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 15
-
-
15, 16. Wenzi fulani wa ndoa walithawabishwaje kwa sababu ya bidii yao katika huduma ya Kikristo, na unaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi kama hayo?
15 Kondoo wengine pia wanajishughulisha sana na kazi ya Bwana, wakiwaunga mkono kikamili ndugu za Kristo. (Mt. 25:40) Wao si kama yule mtumwa mwovu aliye goigoi katika mfano wa Yesu, wako tayari kujidhabihu na kujikakamua kabisa ili kutanguliza masilahi ya Ufalme. Kwa mfano, Jon na Masako walipoalikwa wasaidie kuhubiri eneo la Kichina nchini Kenya, mwanzoni walisitasita. Lakini baada ya kusali na kufikiria hali zao, waliamua kuhamia nchini Kenya.
16 Walithawabishwa sana kwa sababu ya jitihada zao. Walisema hivi: “Huduma hapa inafurahisha sana.” Walianzisha mafunzo saba ya Biblia. Walipata mambo mengine mengi yenye kusisimua katika huduma. Walifikia mkataa huu, “Tunamshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya kuturuhusu kuwa hapa.” Bila shaka, kuna ndugu na dada wengine wengi ambao wameonyesha kupitia maamuzi yao kwamba wameazimia kujitoa kikamili katika utumishi wa Mungu haidhuru mwisho utakuja wakati gani. Wafikirie maelfu ambao wamehitimu katika Shule ya Gileadi na kuanza utumishi wa umishonari. Kwa nini usisome kuhusu utumishi huo wa pekee katika makala yenye kichwa “Tunafanya Yote Tuwezayo! ” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 2001? Unaposoma masimulizi hayo yenye kusisimua kuhusu maisha ya kila siku katika kazi ya umishonari, fikiria njia ambazo unaweza kuongeza utumishi wako na hivyo kumsifu Mungu. Ukifanya hivyo, utapata shangwe zaidi.
-