-
“Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Ni Nani kwa Kweli Aliyeyachochea?
Je, yote hayo kwa kweli yalichochewa na makasisi? John Lord O’Brian alikana hilo. Lakini mambo ya hakika yalijulikana vema na wale walioishi wakati huo. Katika Machi 22, 1919, gazeti lililochapwa katika Girard, Kansas liitwalo Appeal to Reason, liliteta hivi: “Wafuasi wa Pasta Russell, Wakifuatiwa na Ukorofi wa Makasisi wa ‘Orthodoksi,’ Walihukumiwa na Kufungwa Bila Dhamana, Ingawa Walifanya Kila Jitihada Iliyowezekana ili Kushikamana na Masharti ya Sheria ya Ujasusi. . . . Tunajulisha kwamba, hata iwe au isiwe kwamba Sheria ya Ujasusi ilikuwa ya kikatiba kikweli au inayofaa kiadili, wafuasi hao wa Pasta Russell walihukumiwa isivyo haki chini ya masharti yayo. Uchunguzi wa akili iliyofunguka wa ithibati utamsadikisha yeyote upesi kwamba watu hao si kwamba tu hawakuwa na kusudi la kukiuka sheria, bali pia hawakuikiuka.”
Miaka mingi baadaye, katika kitabu Preachers Present Arms, Dakt. Ray Abrams alionelea hivi: “Ni jambo lenye kutokeza kwamba makasisi wengi walishiriki sehemu ya uchochezi katika kujaribu kuwaondolea mbali Warusselli [kama vile Wanafunzi wa Biblia walivyoitwa kwa dharau]. Mizozo ya kidini na chuki za muda mrefu, ambazo hazikushughulikiwa kwa vyovyote mahakamani katika wakati wa amani, sasa zilifika mahakamani chini ya uvutano wa harara ya wakati wa vita.” Yeye pia alisema: “Uchanganuzi wa kesi yote huongoza kwenye mkataa kwamba hapo awali makanisa na makasisi walichochea harakati ya kuwafutilia mbali Warusselli.”—Kur. 183-185.
Hata hivyo, mwisho wa vita haukuleta mwisho wa mnyanyaso wa Wanafunzi wa Biblia. Kipindi kipya cha mnyanyaso ndicho kilichoanza.
Mapadri Wawachochea Polisi
Vita ikiwa imekwisha, masuala mengine yalichochewa na makasisi ili kukomesha utendaji wa Wanafunzi wa Biblia, ikiwa ingewezekana. Katika Bavaria ya Katoliki na sehemu nyingine za Ujerumani, wengi walikamatwa katika miaka ya 1920 chini ya sheria za uchuuzi. Lakini wakati kesi hizo zilipokuja kwenye mahakama za rufani, mara nyingi mahakimu waliwaunga mkono Wanafunzi wa Biblia. Hatimaye, baada ya mahakama kugharikishwa kwa maelfu ya kesi kama hizo, Wizara ya Mambo ya Ndani ilitoa agizo katika 1930 kwa maofisa wote wa polisi ikiwaagiza waache kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Wanafunzi wa Biblia chini ya sheria za uchuuzi. Hivyo, kwa muda mfupi, msongo kutoka kwa chanzo hicho ulikoma, na Mashahidi wa Yehova wakaendelea na utendaji wao kwa kiwango kisicho cha kawaida katika shamba la Ujerumani.
Makasisi pia walikuwa na uvutano wenye nguvu katika Rumania wakati wa miaka hiyo. Walifanikiwa kufanya sheria zichapishwe zilizopiga marufuku fasihi na utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Lakini mapadri waliogopa kwamba huenda watu bado wakasoma fasihi ambazo tayari walikuwa nazo na hivyo wangejifunza juu ya mafundisho yasiyo ya Kimaandiko na madai ya uwongo ya kanisa. Ili kuzuia hilo, mapadri hasa walienda pamoja na polisi nyumba hadi nyumba wakitafuta fasihi zozote ambazo zilikuwa zimegawanywa na Mashahidi wa Yehova. Hata wangeuliza watoto wadogo wasiotambua kitu kama wazazi wao walikuwa wamekubali fasihi hizo. Ikiwa yoyote ilipatikana, watu walitishwa kupigwa na kufungwa ikiwa wangekubali kupata zaidi. Katika baadhi ya vijiji padri alikuwa pia ndiye meya na hakimu, na mtu yeyote aliyekosa kufanya yale ambayo padri alisema, hakupata haki yoyote.
Rekodi ambayo baadhi ya maofisa Waamerika waliweka katika kufanya mapenzi ya makasisi wakati wa kipindi hicho si nzuri pia. Kufuatia ziara ya Askofu wa Katoliki O’Hara katika La Grange, Georgia, kwa kielelezo, meya na wakili wa jiji walikamata baadhi ya Mashahidi wa Yehova katika 1936. Wakati wa kufungwa kwao, walilazimishwa kulala kando ya rundo la mbolea wakilalia magodoro yaliyomwagiwa mkojo wa ng’ombe, wakapewa chakula chenye mabuu, na kulazimishwa kujenga barabara na wafungwa wengineo.
Katika Poland pia, makasisi Wakatoliki walitumia kila njia ambayo wangeweza kubuni ili kuzuia kazi ya Mashahidi wa Yehova. Waliwachochea watu wafanye jeuri, wakachoma fasihi za Mashahidi wa Yehova waziwazi, wakawashutumu kuwa Wakomunisti, na kuwapeleka mahakamani kwa mashtaka kwamba fasihi zao zilikuwa zenye “kukufuru.” Hata hivyo, si maofisa wote waliotaka kufuata matakwa yao. Kwa kielelezo, wakili mkuu wa mahakama ya rufani wa Posen (Poznan), alikataa kumshtaki mmoja wa Mashahidi wa Yehova ambaye makasisi walikuwa wamemshutumu kwa shtaka kwamba alikuwa amerejezea makasisi Wakatoliki kuwa “tengenezo la Shetani.” Wakili mkuu mwenyewe alitaja kwamba roho ya kukosa maadili ambayo imeenea kotekote katika Jumuiya ya Wakristo kutoka kwa mahakama ya kipapa ya Aleksanda 6 (1492-1503 W.K.) ilikuwa kwa kweli ni roho ya tengenezo la kishetani. Na wakati makasisi walipomshtaki mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwa kukufuru Mungu kwa sababu ya kugawanya fasihi za Watch Tower, wakili mkuu wa mahakama ya rufani katika Thorn (Toruń) aliamuru aachiliwe, akisema: ‘Mashahidi wa Yehova wana msimamo uleule kama Wakristo wa kwanza. Wakisingiziwa na kunyanyaswa, wanategemeza maadili ya juu zaidi katika ulimwengu mpotovu unaoangamia.’
Jumba la kuhifadhia hati za serikali la Kanada lilifunua kwamba ilikuwa ni kupatana na barua kutoka kwa makao makuu ya Kadinali Mkatoliki Villeneuve, wa Quebec, kwa waziri wa sheria, Ernest Lapointe, kwamba Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku katika Kanada mwaka 1940. Baadaye maofisa wengine wa serikali waliomba maelezo kamili ya sababu ya hatua hiyo, lakini majibu ya Lapointe hayakuridhisha hata kidogo wengi wa washiriki wa Bunge la Kanada.
Katika upande ule mwingine wa dunia, kulikuwa hila hizohizo za makasisi. Jumba la kuhifadhia hati za serikali la Australia lina barua kutoka kwa askofu mkuu wa Katoliki ya Roma wa Sydney kwa Mkuu wa Sheria W. M. Hughes ikihimiza kwamba Mashahidi wa Yehova watangazwe kuwa wasio halali. Barua hiyo iliandikwa Agosti 20, 1940, miezi mitano tu kabla ya marufuku kuwekwa. Baada ya kupitia tena msingi wa marufuku hiyo, Bw. Justice Williams wa Mahakama Kuu ya Australia alisema baadaye kwamba ilikuwa na “tokeo la kufanya utetezi wa kanuni na mafundisho ya dini ya Kikristo kuwa usio halali na kila mkutano wa kanisa unaofanywa na waamini katika kuzaliwa kwa Kristo kuwa kusanyiko lisilo halali.” Juni 14, 1943, Mahakama iliamua kwamba marufuku haikupatana na sheria za Australia.
Katika Uswisi gazeti la Katoliki lilitaka wenye mamlaka watwae fasihi za Mashahidi ambazo kanisa liliona kuwa zenye kuudhi. Walitisha kwamba ikiwa hilo halingefanywa, wao wenyewe wangechukua hatua bila kutumia njia halali. Katika sehemu nyingi za ulimwengu, hivyo ndivyo walivyofanya hasa!
Viongozi wa Kidini Waamua Kutumia Jeuri
Makasisi Wakatoliki katika Ufaransa walihisi kwamba bado walikuwa na uvutano wenye nguvu juu ya watu, na waliazimia kutoruhusu jambo lolote liingilie umiliki huo. Wakati wa mwaka 1924-1925, Wanafunzi wa Biblia katika nchi nyingi walikuwa wakigawanya trakti Ecclesiastics Indicted (Makasisi Washtakiwa). Katika 1925, J. F. Rutherford alipaswa ahutubu katika Paris juu ya kichwa “Hila za Makasisi Zafunuliwa.” Kuhusu yale yaliyotukia kwenye mkutano huo, mmoja aliyekuwapo alisema: “Jumba lilikuwa limejaa. Ndugu Rutherford alitokea kwenye jukwaa, na kulikuwa na makofi ya uchangamfu. Alianza kusema, wakati ghafula mapadri na washiriki wa Aksio ya Katoliki kama 50, waliojihami kwa vijiti, walipoingia upesi ndani ya jumba wakiimba La Marseillaise [wimbo wa taifa wa Ufaransa]. Walitupa trakti kutoka juu ya ngazi. Padri mmoja alipanda jukwaani. Vijana wawili walimtupa chini. Mara tatu, Ndugu Rutherford aliondoka jukwaani na kurudi tena. Hatimaye, aliondoka kabisa. . . . Meza zilizoonyesha fasihi zetu zilipinduliwa na vitabu vyetu vikatupwa huku na huku. Kulikuwa na mvurugo kabisa!” Lakini visa kama hivyo vilitukia tena na tena.
Akitoa ushahidi katika Ireland, Jack Corr, alighadhibikiwa na makasisi Wakatoliki mara kwa mara. Katika pindi moja, wafanyaghasia, wakichochewa na padri wa parishi, walimtoa kitandani usiku wa manane na kisha kuchoma fasihi zake zote katikati mwa mji. Mjini Roscrea katika Wilaya ya Tipperary, Victor Gurd na Jim Corby waliwasili mahali pao pa kulala na kupata kwamba wapinzani walikuwa wameiba fasihi zao, wakazimwagia petroli, na kuzichoma. Kuzunguka moto huo walikuwa polisi wa mahali hapo, makasisi, na watoto wa eneo hilo, wakiimba “Imani ya Baba Zetu.”
Kabla ya Mashahidi wa Yehova kukutana katika Madison Square Garden jijini New York mwaka 1939, matisho yalitolewa na wafuasi wa padri Mkatoliki Charles Coughlin kwamba kusanyiko hilo lingevunjwa. Polisi walijulishwa. Mnamo Juni 25, Ndugu Rutherford alisema kwa watu 18,000 au zaidi waliokuwa katika jumba hilo, kutia na wasikilizaji wengi wa kimataifa kwa njia ya redio, juu ya kichwa “Serikali na Amani.” Baada ya hotuba hiyo kuanza, Wakatoliki wa Roma na Wanazi 200 au zaidi, wakiongozwa na mapadri kadhaa Wakatoliki, walisongamana kwenye roshani. Baada ya kutolewa kwa ishara fulani, walianza kuvuma kwa sauti, wakipiga kelele kusema “Heil Hitler!” na “Viva Franco!” Walitumia kila aina ya lugha chafu na vitisho na kuwapiga wakaribishaji wengi waliochukua hatua kuzima mchafuko huo. Magenge hayo hayakufanikiwa kuvunja mkutano huo. Ndugu Rutherford aliendelea kusema kwa nguvu na bila kuogopa. Kwenye kilele cha mvurugo huo, alijulisha hivi: “Angalieni leo Wanazi na Wakatoliki ambao wangependa kuvunja mkutano huu, lakini kwa neema ya Mungu hawawezi kufanya hivyo.” Wasikilizaji waliunga mkono hilo kwa makofi mazito ya kurudiarudia. Mchafuko huo ulinaswa na vinasasauti katika pindi hiyo, na umesikiwa na watu katika sehemu nyingi za ulimwengu.
Hata hivyo, mahali ilipowezekana, kama katika siku za Baraza la Kuwahukumu Wazushi wa Kidini, makasisi wa Katoliki ya Roma walitumia Serikali ili kukandamiza wowote waliojaribu kutilia shaka mafundisho na mazoea ya kanisa.
Kutendwa Kikatili Katika Kambi za Mateso
Adolf Hitler alikuwa rafiki mkubwa wa makasisi. Wakati wa 1933, mwaka uleule ambao mwafaka kati ya Vatikani na Nazi ya Ujerumani ulitiwa sahihi, Hitler alianzisha kampeni ya kuwaangamiza Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani. Kufikia 1935 waliharimishwa katika taifa lote. Lakini ni nani aliyeanzisha hayo?
Padri mmoja Mkatoliki, akiandika katika Der Deutsche Weg (gazeti la Kijerumani lililochapwa katika Lodz, Poland), alisema katika toleo lalo la Mei 29, 1938 hivi: “Sasa kuna nchi moja duniani ambako wale waitwao eti . . . Wanafunzi wa Biblia [Mashahidi wa Yehova] wameharimishwa. Hiyo ni Ujerumani! . . . Wakati Adolf Hitler alipochukua mamlaka, na Episkopati (Baraza la Maaskofu) ya Wakatoliki wa Ujerumani ikarudia ombi lao, Hitler alisema: ‘Hawa waitwao eti Wanafunzi wa Biblia Wenye Bidii [Mashahidi wa Yehova] ni wazusha-fujo; . . . Mimi ninawaona kuwa watu bandia; Mimi sivumilii kwamba Wakatoliki Wajerumani watashushiwa heshima kwa njia hiyo na huyu Mwamerika Jaji Rutherford; Ninaharimisha [Mashahidi wa Yehova] katika Ujerumani.’”—Italiki ni zetu.
Je, ilikuwa tu ni Baraza la Maaskofu Wakatoliki wa Ujerumani waliotaka hatua hizo zichukuliwe? Kama ilivyoripotiwa katika Oschatzer Gemeinnützige, la Aprili 21, 1933, katika hotuba ya redio Aprili 20, mhudumu Mluther Otto alihutubu kuhusu “ushirikiano wa karibu zaidi” kwa upande wa Kanisa la Luther la Ujerumani la Jimbo la Saxony pamoja na viongozi wa kisiasa wa taifa, na kisha yeye akajulisha hivi: “Matokeo ya kwanza ya ushirikiano huo tayari yaweza kuonwa katika kupigwa marufuku leo kwa International Association of Earnest Bible Students [Mashahidi wa Yehova] na madhehebu yalo katika Saxony.”
-
-
“Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 655]
Makasisi Waonyesha Hisia Zao
Maitikio ya magazeti ya kidini baada ya kuhukumiwa kwa J. F. Rutherford na washiriki wake mwaka 1918 yanastahili kuangaliwa:
◆ “The Christian Register”: “Kile ambacho Serikali hapa inashambulia moja kwa moja kwa njia ya kufisha ni ile dhana kwamba mawazo ya kidini, hata yawe ya kichaa na yenye kudhuru jinsi gani, yanaweza kuenezwa bila hofu ya kuadhibiwa. Dhana hiyo ni uwongo wa kale, na kufikia sasa hatujakuwa waangalifu sana kulihusu. . . . Hukumu hiyo inaonekana kuwa ndiyo mwisho wa Urusselli.”
◆ “The Western Recorder,” kichapo cha Baptisti, kilisema: “Haishangazi kwamba kiongozi wa kidhehebu hicho chenye ukaidi amefungiwa katika mojawapo ya vituo vya watu wakaidi. . . . Tatizo lenye kutatanisha kwelikweli kuhusiana na jambo hilo ni ikiwa washtakiwa wangepaswa wapelekwe kwenye makao ya wenye kichaa au kwenye gereza.”
◆ “The Fortnightly Review” lilielekeza fikira kwenye maelezo katika gazeti la New York “Evening Post,” ambalo lilisema: “Tunatumaini kwamba walimu wa dini kila mahali wataona maoni ya hakimu huyu kwamba kufunza dini yoyote isipokuwa ile ambayo inapatana kabisa na sheria zilizowekwa ni hatia kubwa ambayo inafanywa kuwa kubwa zaidi, ikiwa wewe ukiwa mhudumu wa gospeli, ungali mnyoofu.”
◆ “The Continent” kwa kuwashushia heshima liliwaonyesha washtakiwa kuwa “wafuasi wa ‘Pasta’ Russell aliyekufa” na likapotoa imani zao kwa kusema kwamba waliunga mkono “kwamba watu wote wanapaswa wasipelekwe kupigana na kaiser wa Ujerumani isipokuwa wale wenye dhambi.” Lilidai kwamba kulingana na wakili mkuu katika Washington, “muda fulani uliopita serikali ya Italia ililalamikia Marekani kwamba Rutherford na washiriki wake . . . walikuwa wameeneza kiasi fulani cha propaganda ya kupinga vita katika majeshi ya Italia.”
◆ Juma moja baadaye, “The Christian Century” lilichapa sehemu kubwa ya habari iliyo juu neno kwa neno, ikionyesha kwamba walikubaliana nayo kabisa.
◆ Gazeti la Katoliki “Truth” liliripoti kifupi ile hukumu waliyopewa na kisha likaeleza hisi za wahariri walo, likisema: “Fasihi za shirika hilo zimejaa mashambulizi makali sana juu ya Kanisa Katoliki na upadri walo.” Ili kujaribu kuweka kibandiko cha “uasi” juu ya yeyote ambaye huenda akapinga hadharani maoni ya Kanisa Katoliki, liliongezea hivi: “Inazidi kuwa wazi kwamba roho ya kutovumilia inafungamanishwa kwa ukaribu na ile ya uasi.”
◆ Dakt. Ray Abrams, katika kitabu chake “Preachers Present Arms,” alionelea hivi: “Wakati habari za hukumu ya vifungo hivyo vya miaka ishirini zilipofikia wahariri wa magazeti ya kidini, karibu kila kimoja cha vichapo hivyo, kikubwa na kidogo, kilishangilia tukio hilo. Mimi nimeshindwa kupata maneno yoyote ya masikitiko katika yoyote ya majarida ya kidini yanayokubaliwa.”
-