-
“Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Furiko la Kimataifa la Hatua za Kisheria
Muda mrefu kabla ya vita ya ulimwengu ya kwanza, makasisi walijitahidi kuzuia kugawanywa kwa fasihi na Wanafunzi wa Biblia katika maeneo yao kwa kuwakaza maofisa wenyeji. Hata hivyo, kufuatia Vita ya Ulimwengu 1, upinzani uliongezeka. Katika nchi moja baada ya nyingine, vizuizi vya kisheria vya kila aina vinavyoweza kuwaziwa viliwekwa mbele ya wale waliokuwa wakijaribu kutii amri ya kiunabii ya Kristo ya kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu kwa kusudi la kutoa ushahidi.—Mt. 24:14.
Wakichochewa na ithibati ya kutimizwa kwa unabii wa Biblia, Wanafunzi wa Biblia waliondoka kwenye mkusanyiko Cedar Point, Ohio, katika 1922, wakiazimia kujulisha ulimwengu kwamba Nyakati za Mataifa zilikuwa zimekwisha na kwamba Bwana alikuwa amechukua uwezo wake mkuu na alikuwa akitawala kutoka mbinguni akiwa Mfalme. Shime ilikuwa ni “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Mwaka uo huo, makasisi katika Ujerumani walichochea polisi wawakamate baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walipokuwa wakigawanya fasihi za Biblia. Hilo halikuwa tukio la peke yalo. Kufikia 1926, kulikuwa na visa kama hivyo 897 vikingojea kuamuliwa katika mahakama za Ujerumani. Uchochezi mwingi sana ulihusika hivi kwamba katika 1926 ilikuwa lazima Watch Tower Society ianzishe idara ya sheria katika ofisi yayo ya tawi katika Magdeburg. Wakati wa 1928, katika Ujerumani pekee kulikuwa na mashtaka 1,660 dhidi ya Wanafunzi wa Biblia, na mkazo ukazidi kuongezeka mwaka baada ya mwaka. Makasisi waliazimia kukomesha kazi ya Wanafunzi wa Biblia, na walishangilia wakati uamuzi wowote wa mahakama ulipoonyesha kwamba walikuwa wakifanikiwa kwa kadiri fulani.
Katika Marekani, Wanafunzi wa Biblia walikamatwa kwa ajili ya kuhubiri nyumba hadi nyumba katika 1928, katika South Amboy, New Jersey. Katika muda wa mwongo mmoja idadi ya kila mwaka ya waliokamatwa kuhusiana na huduma yao katika Marekani ilizidi 500. Wakati wa 1936 idadi hiyo ilipanda sana—hadi 1,149. Ili kuandaa msaada wa kisheria uliohitajika, ikawa lazima kuwa na idara ya sheria kwenye makao makuu ya Sosaiti pia.
Vilevile utendaji mwingi wa kuhubiri nchini Rumania ulikabili upinzani mkali kutoka kwa wenye mamlaka waliokuwa uongozini. Mashahidi wa Yehova waliogawanya fasihi za Biblia walikamatwakamatwa na kupigwa kikatili. Kuanzia 1933 hadi 1939, Mashahidi huko walikabiliwa na mashtaka 530. Hata hivyo, sheria za nchi hiyo zilihakikisha kwamba kuna uhuru, kwa hiyo kukatwa rufani katika Mahakama Kuu ya Rumania kulileta maamuzi mengi mazuri. Wakati polisi walipoanza kung’amua jambo hilo, wao wangetwaa fasihi na kuwatenda vibaya Mashahidi lakini wangejaribu kuepuka kuchukua hatua za kisheria. Baada ya Sosaiti hatimaye kuruhusiwa usajili ikiwa shirika katika Rumania, wapinzani walijitahidi kuzuia kusudi la usajili huo halali kwa kupata agizo la mahakama la kukataza kugawanywa kwa fasihi za Watch Tower. Uamuzi huo ulibatilishwa na mahakama ya juu zaidi, lakini makasisi walimshawishi waziri wa madhehebu achukue hatua ili kukinza uamuzi huo.
Nchini Italia na Hungaria, kama vile nchini Rumania, fasihi za Biblia zilizotumiwa na Mashahidi zilitwaliwa na polisi chini ya serikali zilizokuwa zikitawala wakati huo. Jambo hilohilo lilifanywa katika Japani, Korea, na Gold Coast (sasa inayoitwa Ghana). Mashahidi wa Yehova waliokuwa wametoka ng’ambo waliamriwa waondoke Ufaransa. Kwa miaka mingi hakuna yeyote wa Mashahidi wa Yehova aliyeruhusiwa kuingia katika Muungano wa Sovieti ili kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu.
Huku harara ya utukuzo wa taifa ikikumba ulimwengu wote kuanzia 1933 hadi miaka ya 1940, Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku na serikali katika nchi moja baada ya nyingine. Maelfu ya Mashahidi waliletwa mbele ya mahakama wakati wa kipindi hicho kwa sababu ya kukataa kwao kwa kudhamiria kusalimu bendera na kusisitiza kwao juu ya kutokuwamo kwa Kikristo. Katika 1950 iliripotiwa kwamba wakati wa miaka 15 iliyotangulia, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 10,000 walikuwa wamekamatwa katika Marekani pekee.
Wakati zaidi ya Mashahidi 400 walipoletwa mbele ya mahakama ya Ugiriki katika muda mfupi mwaka 1946, huo haukuwa mwanzo wa kushtakiwa kwao huko. Kulikuwa kumeendelea kwa miaka mingi. Zaidi ya vifungo, faini kubwa zilitozwa, zikifilisisha akina ndugu kifedha. Lakini kama walivyoona hali yao, walisema: “Bwana alifungua njia ili kazi ya kutoa ushahidi ifikie maofisa wa Ugiriki, waliosikia kuhusu kusimamishwa kwa ufalme wa uadilifu; pia mahakimu katika mahakama walikuwa na fursa ileile.” Mashahidi wa Yehova waliliona jambo hilo waziwazi katika ile njia ambayo Yesu alisema wafuasi wake wapaswa kuliona.—Luka 21:12, 13.
Vita Iliyoonekana Kuwa Haiwezekani Kushinda
Wakati wa miaka ya 1940 na 1950, mkoa wa Quebec wa Kanada ulikuwa uwanja wa vita kihalisi. Kukamatwa kwa ajili ya kuhubiri habari njema kulikuwa kumekuwa kukiendelea huko tangu 1924. Kufikia kipupwe cha 1931, Mashahidi fulani mmoja-mmoja walikuwa wakichukuliwa na polisi kila siku, nyakati nyingine mara mbili kwa siku. Gharama za kisheria za Mashahidi katika Kanada zikawa kubwa. Kisha, mapema katika 1947, jumla ya idadi ya kesi zilizohusisha Mashahidi zilizokuwa zikisubiri mahakamani katika Mkoa wa Quebec zikaongezeka kufikia 1,300; na bado, kulikuwa na kikundi kidogo tu cha Mashahidi wa Yehova huko.
Hicho kilikuwa kipindi ambacho Kanisa la Katoliki ya Roma lilikuwa na uvutano mwingi ambao kila mwanasiasa na kila hakimu katika mkoa huo asingepuuza. Katika Quebec makasisi kwa kawaida walionwa kwa heshima kuu, na watu wengine walitii kwa utayari maneno ya padri mwenyeji. Kama vile kitabu State and Salvation (1989) kilivyoeleza hali hiyo: “Kadinali wa Quebec alikuwa na kiti kikuu Bungeni kando tu ya kile cha mkuu wa serikali. Kwa njia moja au nyingine sehemu kubwa ya Quebec ilikuwa chini ya udhibiti wa moja kwa moja wa kanisa . . . Kwa kweli, lengo la kanisa lilikuwa ni kufanya hali ya kisiasa ya Quebec ipatane na wazo la Katoliki ya Roma ambalo kwalo kweli ni Ukatoliki, kosa ni chochote kisicho cha Ukatoliki, na uhuru ni kutozuiwa kusema na kuishi kulingana na kweli ya Katoliki ya Roma.”
Kusema kibinadamu, magumu yaliyokabili Mashahidi katika Quebec na ulimwenguni pote yalionekana kuwa yasiyoshindika.
-
-
“Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Picha katika ukurasa wa 681]
Maurice Duplessis, waziri mkuu wa Quebec, akipiga magoti hadharani mbele ya Kadinali Villeneuve mwishoni-mwishoni mwa miaka ya 1930 na kuweka pete kwenye kidole chake ukiwa uthibitisho wa uhusiano wa karibu kati ya Kanisa na Serikali. Katika Quebec, mnyanyaso wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa mwingi hasa
-