-
Kuhubiri Hadharani na Kutoka Nyumba Hadi NyumbaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Makolpota Wenye Bidii Wachukua Uongozi
Mwito wa kwanza kwa wanaume na wanawake waliojiweka wakfu ambao wangeweza kutumia kiasi kikubwa cha wakati wao katika utumishi huo ulitolewa katika Aprili 1881. Wangewatolea wenye nyumba na wafanya-biashara kitabu kidogo kinachoeleza kweli za Biblia na uandikisho wa Watch Tower. Kusudi lao lilikuwa kuwatafuta wale waliokuwa na njaa ya kiroho na kushiriki elimu pamoja nao. Kwa wakati fulani walijaribu kusema machache tu ili kuchochea kupendezwa, wakiacha katika kila nyumba pakiti yenye fasihi ili mwenye nyumba azichunguze, na kisha kurudi baada ya siku chache. Baadhi ya wenye nyumba walikuwa wakirudisha fasihi hizo; wengine walitaka kuzinunua; mara nyingi kulikuwa fursa za mazungumzo. Kuhusu kusudi lao, Watch Tower lilisema: “Si kuuzwa kwa pakiti, wala kufanya maandikisho, bali ni kuenezwa kwa kweli, kwa kuwafanya watu waisome.”
Idadi ya walioshiriki wakiwa makolpota wa kueneza evanjeli ilikuwa ndogo kwa kadiri fulani. Wakati wa miaka 30 ya kwanza, idadi yao ilikuwa kuanzia wachache hadi 600 hivi. Makolpota hao walikuwa mapainia katika maana halisi, wakifungua eneo jipya. Anna Andersen alikuwa mmoja wa wale waliovumilia katika utumishi huo kwa miongo ya miaka, mara nyingi akisafiri kwa baiskeli, na yeye binafsi alifika karibu kila mji katika Norway akiwa na habari njema. Makolpota wengine walisafiri ng’ambo na walikuwa wa kwanza kupeleka ujumbe kwa nchi kama Finland, Barbados, El Salvador, Guatemala, Honduras, na Burma (sasa Myanmar). Pia kulikuwa na wengine ambao hawakuweza kuhamia sehemu nyingine lakini waliotumikia wakiwa makolpota waeneza-evanjeli katika eneo lao la nyumbani.
Kazi ya makolpota ilikuwa ya kutokeza. Mmoja aliyekuwa akitumikia katika pwani ya magharibi mwa Marekani aliandika katika 1898 kwamba katika miezi 33 iliyotangulia, alikuwa amesafiri kilometa 12,800 kwa farasi na kigari chake, akatoa ushahidi katika majiji 72, akafanya ziara za kurudia 18,000, akaangusha vitabu 4,500, akapata maandikisho 125, akatoa trakti 40,000, na kuona watu 40 wakikubali ujumbe na pia kuanza kuushiriki na wengine. Mume na mke katika Australia pamoja walifaulu kuangusha vitabu 20,000 kwa watu waliopendezwa wakati wa kipindi cha miaka miwili na nusu tu.
Je, maangusho mengi yalikuwa jambo lisilo la kawaida badala ya kuwa tukio la kawaida? Ripoti ya 1909 inaonyesha kwamba makolpota 625 hivi (jumla katika orodha wakati huo) walipokea kutoka kwa Sosaiti vitabu vilivyojalidiwa 626,981 ili waviangushe kwa umma (wastani wa zaidi ya elfu moja kwa kila kolpota), kwa kuongezea kiasi kikubwa cha fasihi za bure. Mara nyingi hawangeweza kubeba vitabu vya kutosha kwenda nyumba hadi nyumba, kwa hiyo wangechukua maagizo na kisha kurudi baadaye kuvileta.
Hata hivyo, wengine walipinga hivi: “Huku si kuhubiri!” Lakini, kwa kweli, kama vile Ndugu Russell alivyoeleza, kulikuwa aina ya mahubiri yenye matokeo zaidi. Badala ya kusikia hotuba moja tu, watu walikuwa wakipokea hotuba nyingi kwa namna ya maandishi na hivyo wangeweza kuzifurahia tena na tena na wangeweza kuhakikisha yaliyomo kwa kutumia Biblia zao wenyewe. Huo ulikuwa uenezaji evanjeli wenye kutambua uhakika wa kwamba elimu kwa ujumla ilikuwa imewawezesha watu kusoma. Kitabu The New Creation kilitaja kwamba: “Jambo la kwamba hao waeneza-evanjeli wanafanya kazi wakitumia njia zinazofaa siku yetu badala ya njia zilizofaa zamani, sio hoja dhidi ya kazi hii kama vile ambavyo wao husafiri kwa nguvu ya mvuke na ya umeme badala ya kwa miguu au kwa ngamia. Kuenezwa kwa evanjeli kunafanywa kupitia kutolewa kwa Kweli . . . , Neno la Mungu.”
-
-
Kuhubiri Hadharani na Kutoka Nyumba Hadi NyumbaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Picha katika ukurasa wa 558]
Waeneza-evanjeli makolpota waligawanya vitabu vilivyoeleza juu ya Biblia
[Picha katika ukurasa wa 559]
Anna Andersen alifikia karibu kila mji katika Norway na fasihi za Biblia
-