Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Estonia
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • WAHUBIRI WA KWANZA

      Makolpota walisafiri na kuhubiri maeneo makubwa kwa baiskeli na walilala popote walipopata mahali pa kulala—iwe ni katika nyumba za mashambani au juu ya marundo ya nyasi. Watu walikuwa maskini, lakini walipenda kusikiliza ujumbe wa Ufalme. Kwa sababu hiyo, wahubiri hao wa wakati wote walihubiri kwa furaha kati ya saa 150 mpaka 200 kwa mwezi. Mmoja wao alihubiri muda wa saa 239 mwezi fulani! Walikuwa watumishi wenye bidii, wajasiri, na wavumilivu. Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa dada mmoja alipoenda kuhubiri kwa mara ya kwanza:

      “Je, unajua kuendesha baiskeli?” dada fulani mwenye bidii kutoka Finland akamuuliza.

      “Ndiyo, ninajua,” dada huyo mpya akamjibu.

      “Basi, twende Sarema,” akasema yule dada kutoka Finland kwa shauku, akirejelea kisiwa kikubwa zaidi cha Estonia, umbali wa kilomita 200 hivi.

      Walipofika kwenye kijiji cha kwanza huko Sarema, yule dada kutoka Finland alipendekeza hivi: “Utaanzia hapa nami nitaanzia upande ule mwingine. Jioni, tukutane katikati ya kijiji.” Yule dada mpya hakuwa amewahi kuhubiri. Lakini alipobisha mlango wa kwanza, alihisi kwamba Yehova alikuwa anamsaidia na upesi akapata ujasiri na kuendelea kuhubiri kwa furaha.

      Hellin Aaltonen (baadaye aliitwa Grönlund) alikutana na watu wa kisiwa cha Vormsi na kugundua kwamba walizungumza lugha asiyoijua.

      “Je, mnazungumza Kiestonia?” akawauliza.

      “Hapana, tunazungumza Kiswedi,” wakasema.

      “Je, mna vitabu vya kusoma vya Kiswedi?” Hellin akawauliza.

      “Hatujawahi kupata vitabu vya Kiswedi kwa mamia ya miaka,” wakajibu kwa kutia chumvi.

      Alipotambua kwamba watu wa Vormsi walihitaji vitabu vya Kiswedi, Hellin aliamua kutembelea tena kisiwa hicho akiwa na Fanny Hietala, ambaye alizungumza Kiswedi.

      “Tulichukua vitabu vyote vya Kiswedi vilivyokuwa kwenye ofisi na kwenda huko kwa mashua,” asema Hellin. “Kwa siku tatu, tuliwahubiria watu katika kisiwa chote na kuwaachia karibu vitabu vyote tulivyobeba. Miaka mingi baadaye, nilisikia kuhusu ndugu fulani kutoka Sweden aliyejifunza kweli kutoka katika vitabu alivyopata kisiwani Vormsi!” Mara nyingi wahubiri wa Ufalme waliona ukweli wa Mhubiri 11:6: “Asubuhi panda mbegu zako na mpaka jioni usiache mkono wako upumzike; kwa maana hujui ni wapi hii itafanikiwa.”

      MATATIZO AMBAYO MAKOLPOTA WALIKABILI

      Kazi ya makolpota haikuwa rahisi. Wakati wa baridi kali, waliteleza juu ya theluji au kutembea kwa miguu umbali wa kilomita 20 hadi 40 kwa siku. Kulikuwa na baridi kali na haikuwa rahisi kupata mahali pazuri pa kulala. Wangeweza tu kubeba chakula na vitu vingine vya lazima, kwa kuwa walibeba pia masanduku ya vitabu. Barabara zilikuwa hazipitiki kukiwa na mvua kubwa. Mara nyingi makolpota hao walilazimika kulala nje. Ili kuendelea na utumishi huo mgumu, walihitaji kuwa na nguvu za kutosha. Hata hivyo, wahubiri hao wenye kujitoa walihisi namna gani kuhusu utumishi wao?

      “Sikukosa chochote muhimu,” asema Vilho Eloranta, ndugu mwenye bidii kutoka Finland aliyekuwa mhubiri wa wakati wote katika maeneo ya mbali kwa miezi mingi. “Mara nyingi, niliwapa watu vitabu, nao wakanipa chakula na mahali pa kulala. Sikuhitaji sana pesa. Jioni ilipofika, ningeanza kuomba mahali pa kulala. Ni wenye nyumba wachache waliokataa, hasa kama ingekuwa usiku au kama hakungekuwa na nyumba nyingine karibu.”

      Vilho anaongeza kusema: “Nilihangaikia sana kuwapelekea watu ujumbe wa Ufalme hivi kwamba hata kukaa katika nyumba za hali ya chini hakukupunguza uradhi na shangwe niliyopata kutokana na kuhubiri.”

      Ndugu na dada hao wenye bidii waliweka msingi kwa ajili ya ongezeko lililotokea miaka ya baadaye kwa kuwaachia watu vitabu vingi. Mnamo 1929, jumla ya vitabu na vijitabu 53,704 viligawanywa na wahubiri wachache.

      “Estonia ilikuwa na makolpota wapatao 30,” asema Adolf Kose, “na walihubiri nchi nzima kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu.”

      Matokeo ya kazi ya wahubiri hao wenye bidii bado yanaonekana. Kwa mfano, mapema miaka ya 1990, Mashahidi wa Yehova walikutana na Ruth, mwanamke mzee. Ujumbe wao haukuwa mpya kwake. Alikumbuka kwamba zaidi ya miaka 60 iliyokuwa imepita, alimsikiliza Mwanafunzi wa Biblia Mjerumani ambaye alimtembelea jirani yake mara kadhaa. Sasa, ingawa alikuwa kiziwi na mzee, Ruth aliitambua kweli, akakubali funzo la Biblia, na kubatizwa—miaka 70 hivi baada ya kuhubiriwa mara ya kwanza!

  • Estonia
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 170]

      Mapainia wa kwanza kutoka Finland, Jenny Felt na Irja Mäkelä

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki