-
Msaada Kutoka kwa “Mungu Anayetoa Uvumilivu na Faraja”Mnara wa Mlinzi—2007 | Mei 1
-
-
Msaada Kutoka kwa Marafiki wa Kweli
Wale waliofiwa na mtoto mara nyingi wanahitaji wakati wa kuomboleza na kukabiliana na hisia zao wakiwa peke yao. Hata hivyo, halingekuwa jambo la hekima kwao kujitenga na wengine kwa muda mrefu. Kulingana na Methali 18:1, “mtu anayejitenga” anaweza kuumia. Kwa hiyo, wale wanaoomboleza wanapaswa kuwa waangalifu wasianguke katika mtego wa kujitenga.
Marafiki wanaomwogopa Mungu wanaweza kuwasaidia sana wale wanaotaabika. Andiko la Methali 17:17 linasema hivi: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” Lucy, ambaye pia alitajwa katika habari iliyotangulia, alifarijiwa na marafiki wa kweli baada ya kufiwa na mwana wake. Alisema hivi kuhusu waamini wenzake kutanikoni: “Walitusaidia sana walipotutembelea, hata ingawa nyakati nyingine walisema machache. Rafiki mmoja alinitembelea siku ambazo nilikuwa peke yangu. Alijua kwamba ningekuwa nyumbani nikilia, na mara nyingi alikuja na kulia pamoja nami. Mwingine alinipigia simu kila siku ili kunitia moyo. Wengine walitualika nyumbani kwao kwa ajili ya chakula, na waliendelea kufanya hivyo.”
-
-
Msaada Kutoka kwa “Mungu Anayetoa Uvumilivu na Faraja”Mnara wa Mlinzi—2007 | Mei 1
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
‘Ninataka Kusaidia, lakini Sijui Jinsi ya Kufanya Hivyo’
Ingawa wazazi, ndugu, na dada za mtoto aliyekufa wanahuzunika sana, huenda marafiki wakawa na wasiwasi. Wanataka kuitegemeza familia hiyo lakini wanaogopa kwamba watasema au kufanya jambo litakalowaumiza hata zaidi. Yafuatayo ni mapendekezo fulani kwa ajili ya wale ambao huenda wakasema, ‘Ninataka kusaidia, lakini sijui jinsi ya kufanya hivyo.’
❖ Usiwaepuka watu waliofiwa eti kwa sababu hujui useme au ufanye nini. Utawatia nguvu kwa kuwa tu pamoja nao. Je, unashindwa useme nini? Kuwakumbatia na kusema kwa unyofu “Poleni sana,” kutawafanya watambue kwamba unawajali. Je, unaogopa kwamba ukianza kulia utafanya wahuzunike zaidi? Biblia inasema hivi: “Lieni pamoja na watu wanaolia.” (Waroma 12:15) Machozi yako yanaonyesha kwamba unahuzunika pamoja nao, na hilo linafariji.
❖ Chukua hatua ya kwanza. Je, unaweza kutayarishia familia hiyo chakula kidogo? Je, unaweza kusafisha vyombo walivyotumia? Je, unaweza kwenda kuwafanyia shughuli mbalimbali? Usiseme, “Mnaweza kunijulisha ikiwa mnahitaji chochote.” Hata ukisema maneno hayo kwa unyofu, wazazi wengi waliofiwa wataelewa kwamba huwezi kuwasaidia kwa sababu una shughuli nyingi. Badala yake, uliza “Ninaweza kuwasaidia jinsi gani sasa?” na kisha utimize ombi lao. Lakini epuka kuingia sehemu za faragha nyumbani mwao au kuingilia mambo yao ya kibinafsi.
❖ Epuka kusema, “Ninajua jinsi mnavyohisi.” Kila mwanadamu anakuwa na hisia tofauti kuelekea kifo cha mpendwa wake. Hata ikiwa wewe pia umefiwa na mtoto, hujui kwa uhakika jinsi wanavyohisi.
❖ Muda mrefu utapita kabla ya familia hiyo kurudia hali yake ya kawaida. Endelea kusaidia kadiri unavyoweza. Mwanzoni, watu wengi wanaishughulikia familia iliyofiwa, lakini familia hiyo inahitaji mengi zaidi. Uwe macho kuona mahitaji yao katika majuma na miezi itakayofuata.a
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kuwasaidia wale wanaoomboleza kifo cha mtoto, ona sura “Wengine Waweza Kusaidiaje?” kwenye ukurasa 20-24 wa broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-