-
Faraja Wakati wa MatatizoMnara wa Mlinzi—2002 | Oktoba 1
-
-
Faraja Wakati wa Matatizo
SIKU hizi taarifa za habari hazifariji. Mtu mmoja aliandika: “Matukio ya sasa ni mabaya sana hivi kwamba mara nyingi sisi hushindwa kuamua kama tutatazama habari za jioni au la.” Ulimwengu umejaa vita, vitendo vyenye kutisha, mateso, uhalifu, na magonjwa—maovu ambayo huenda yakatupata karibuni, ikiwa bado hayajatupata.
Biblia ilitabiri kwa usahihi hali hiyo. Akieleza juu ya wakati wetu, Yesu alisema kwamba kungekuwa na vita kubwa-kubwa, magonjwa ya kuambukiza, upungufu wa chakula, na matetemeko ya ardhi. (Luka 21:10, 11) Vivyo hivyo, mtume Paulo aliandika kuhusu “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” wakati ambapo watu wangekuwa wakali, wapenda pesa, na wasiopenda wema. Aliziita nyakati hizo “siku za mwisho.”—2 Timotheo 3:1-5.
Hivyo, zinapozungumzia hali za ulimwengu, taarifa za habari hutaja mambo ambayo kwa njia fulani yanafanana na yale yaliyotabiriwa na Biblia. Lakini ufanani huo unaishia hapo. Biblia hueleza mambo fulani ambayo taarifa hizo hazielezi. Kupitia Neno la Mungu lililoandikwa kwa roho yake, tunaweza kujua ni kwa nini kuna uovu mwingi na pia jinsi wakati ujao utakavyokuwa.
Jinsi Mungu Anavyouona Uovu
Biblia hueleza jinsi Mungu anavyoziona hali zenye kuhuzunisha za sasa. Ingawa alijua kimbele kuhusu matatizo ya sasa, yeye hayakubali wala hanuii kuyavumilia milele. “Mungu ni upendo,” akaandika mtume Yohana. (1 Yohana 4:8) Yehova huwajali sana watu naye huchukia uovu wote. Ni jambo linalofaa kabisa kusali kwa Mungu ili tupate faraja, kwa kuwa yeye ni mwema, mwenye huruma, na ana uwezo na nia ya kuondoa uovu duniani. Mtunga-zaburi aliandika: “[Mfalme wa mbinguni aliyewekwa na Mungu] atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.”—Zaburi 72:12-14.
Je, unawahurumia wale wanaoteseka? Labda unafanya hivyo. Kwa kuwa Yehova alituumba kwa mfano wake, tunaweza kuonyesha sifa ya hisia-mwenzi. (Mwanzo 1:26, 27) Kwa hiyo tunaweza kuwa na hakika kwamba anawajali wanadamu wanaoteseka. Yesu ambaye alimjua Yehova vema kuliko mtu mwingine yeyote, alifundisha kwamba Yehova anapendezwa sana nasi na ana huruma nyororo nyingi.—Mathayo 10:29, 31.
Uumbaji wenyewe unaonyesha kwamba Mungu anawajali wanadamu. Yesu alisema kwamba Mungu “hufanya jua lake lichomoze juu ya watu waovu na wema na kufanya mvua inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:45) Mtume Paulo aliwaambia hivi watu wa jiji la Listra: “[Mungu] hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa nyinyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.”—Matendo 14:17.
Ni Nani Anayesababisha Uovu?
Inafaa kuona kwamba Paulo pia aliwaambia watu wa Listra hivi: “Katika vizazi vilivyopita [Mungu] aliruhusu mataifa yote yaendelee katika njia zayo.” Kwa hiyo, mataifa—au watu wenyewe—husababisha mengi ya matatizo yanayowapata leo. Hatupaswi kumlaumu Mungu.—Matendo 14:16.
Kwa nini Yehova huruhusu mambo mabaya yatokee? Je, atachukua hatua yoyote? Majibu ya maswali hayo yanaweza kupatikana tu katika Neno la Mungu. Hiyo ni kwa sababu majibu yake yanahusiana sana na kiumbe mwingine wa roho na pia suala alilotokeza katika ulimwengu wa roho usioonekana.
-
-
Ujuzi Sahihi Kumhusu Mungu HutufarijiMnara wa Mlinzi—2002 | Oktoba 1
-
-
Ujuzi Sahihi Kumhusu Mungu Hutufariji
WATU wengine hutatanishwa na yale ambayo Biblia husema kuhusu upendo na rehema ya Mungu. Wao huuliza: Ikiwa Mungu anataka kumaliza uovu, anajua jinsi ya kufanya hivyo, na ana uwezo wa kufanya hivyo, kwa nini uovu unaendelea kuongezeka? Ni vigumu kwao kuelewa mambo haya matatu yasiyopatana: (1) Mungu ni mwenye nguvu zote; (2) Mungu ni mwenye upendo na mwema; na (3) maafa yanaendelea kutokea. Wanasababu kwamba kwa kuwa jambo hili la tatu ni la kweli kabisa, basi mojawapo kati ya hayo mawili ya kwanza haliwezi kuwa la kweli. Wanaona kwamba, ama Mungu hawezi kuzuia uovu au hajali.
Siku kadhaa baada ya kuharibiwa kwa majengo ya World Trade Center ya New York, kiongozi mmoja mashuhuri wa kidini huko Marekani alisema: “Nimeulizwa . . . mara nyingi sana maishani mwangu ni kwa nini Mungu huruhusu misiba na kuteseka. Lazima nikiri kwamba sina jibu kamili linaloweza hata kuniridhisha.”
Akitoa maoni yake kuhusu maelezo hayo, profesa mmoja wa theolojia aliandika kwamba aliguswa moyo na “theolojia nzuri” ambayo kiongozi huyo wa dini alihubiri. Profesa huyo pia alikubaliana na maoni ya msomi mmoja aliyeandika: ‘Kama vile tusivyoweza kumwelewa Mungu ndivyo tusivyoweza kuelewa sababu ya kuteseka.’ Lakini, je, ni kweli kwamba hatuwezi kuelewa ni kwa nini Mungu huruhusu uovu?
Chanzo cha Uovu
Tofauti na yale ambayo huenda viongozi wa kidini wakasema, Biblia inaonyesha kwamba tunaweza kuelewa ni kwa nini Mungu huruhusu uovu. Ili kuelewa jambo hilo ni muhimu sana kutambua kwamba Yehova hakuumba ulimwengu mwovu. Aliumba wanadamu wawili wa kwanza wakiwa wakamilifu, bila dhambi. Yehova alitazama kazi yake ya uumbaji na kuona kwamba ilikuwa ‘njema sana.’ (Mwanzo 1:26, 31) Alikusudia Adamu na Hawa waipanue Paradiso ya Edeni duniani pote na kuijaza watu wenye furaha chini ya utawala wake wenye ulinzi na upendo.—Isaya 45:18.
Uovu ulianza na kiumbe wa roho ambaye, ingawa mwanzoni alikuwa mwaminifu kwa Mungu, alisitawisha tamaa ya kuabudiwa. (Yakobo 1:14, 15) Uasi wake ulidhihirika duniani alipowashawishi watu wawili wa kwanza wajiunge naye kumpinga Mungu. Badala ya kutii agizo la Mungu lililokuwa wazi kwamba wasile wala kugusa matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya, Adamu na Hawa walichukua kati ya matunda ya mti huo na kula. (Mwanzo 3:1-6) Kwa kufanya hivyo walikosa kumtii Mungu na pia wakaonyesha kwamba walitaka kuishi bila kumtegemea.
Suala Kuhusu Mema na Mabaya Lilizushwa
Uasi huo uliotokea Edeni ulizusha suala kuhusu yaliyo mema na yaliyo mabaya. Suala hilo lilitokeza upinzani unaohusisha watu wote ulimwenguni. Waasi hao wa kibinadamu walitilia shaka kama Yehova hutawala viumbe wake kwa njia inayofaa. Je, Muumba alikuwa na haki ya kudai utii kamili kutoka kwa wanadamu? Je, maisha ya wanadamu yangekuwa bora zaidi kama wangetenda bila kumtegemea Muumba?
Yehova alishughulika na upinzani huo dhidi ya utawala wake kwa njia inayoonyesha jinsi anavyotumia kwa usawaziko sifa zake za upendo, haki, hekima, na uwezo. Angeweza kutumia uwezo wake kukomesha uasi huo mara moja. Huenda hilo lingeonekana kuwa tendo la haki kwa kuwa Mungu alikuwa na haki ya kufanya hivyo. Lakini kufanya hivyo hakungejibu masuala yaliyozushwa kuhusu mema na mabaya. Kwa upande mwingine, leo huenda wengine wakaona kwamba lingekuwa tendo la upendo kama Mungu angepuuza tu uasi huo. Hata hivyo, kufanya hivyo hakungejibu dai la Shetani kwamba hali ya wanadamu ingekuwa bora zaidi kama wangejitawala. Zaidi ya hayo, je, kufanya hivyo hakungewachochea wengine wamwasi Yehova? Matokeo yangekuwa kuteseka daima.
Kwa kutumia hekima yake, Yehova amewaruhusu wanadamu watende wanavyotaka kwa muda fulani. Ingawa kufanya hivyo kumemaanisha kuruhusu uovu uendelee kwa muda, wanadamu wamepata fursa ya kuonyesha kama wanaweza kujitawala kwa mafanikio bila kumtegemea Mungu, wakiishi kulingana na viwango vyao vya mema na mabaya. Matokeo yamekuwa nini? Kumekuwa na vita, ukosefu wa haki, uonevu, na kuteseka katika maisha yote ya mwanadamu. Kushindwa kwa uasi huo dhidi ya Yehova kutatatua kabisa masuala yaliyotokea Edeni.
Wakati huohuo, Mungu ameonyesha upendo wake kwa kumtoa Mwana wake, Yesu Kristo, ambaye alitoa uhai wake uwe dhabihu ya fidia. Dhabihu hiyo huwaondolea wanadamu hukumu inayoletwa na dhambi na kifo ambacho kilitokana na kutotii kwa Adamu. Fidia hiyo itawawezesha wote wanaoonyesha imani katika Yesu wapate uhai udumuo milele.—Yohana 3:16.
Yehova anatuhakikishia kwa njia yenye kufariji kwamba kuteseka kwa mwanadamu ni kwa muda tu. “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo,” akaandika mtunga-zaburi. “Utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.
Wakati Ujao Wenye Usalama na Furaha
Kutimizwa kwa unabii wa Biblia huonyesha kwamba wakati wa Mungu wa kukomesha magonjwa, huzuni, na kifo umekaribia. Ona mambo mazuri tunayotazamia ambayo Yohana alionyeshwa katika maono. Aliandika hivi: “Nami nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali, na bahari haipo tena. . . . Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja na [wanadamu]. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Yohana aliambiwa hivi ili kukazia kwamba ahadi hizo ni za kutumainika: “Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.”—Ufunuo 21:1-5.
Namna gani mabilioni ya watu wasio na hatia ambao wamekufa tangu uasi huo utokee Edeni? Yehova aliahidi kwamba atawafufua wote wanaolala usingizi wa kifo. Mtume Paulo alisema: “Nina tumaini kuelekea Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Hao wana matazamio ya kuishi katika ulimwengu ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.
Kama vile ambavyo baba mwenye upendo huruhusu mtoto wake afanyiwe upasuaji wenye maumivu ikiwa anajua kwamba utamletea mtoto manufaa ya kudumu, ndivyo Yehova ameruhusu wanadamu duniani wapatwe na uovu kwa muda mfupi. Lakini wale wanaojitahidi kufanya mapenzi ya Mungu watapata baraka za milele. Paulo alieleza: “Viumbe vilitiishwa chini ya ubatili, si kwa mapenzi yavyo vyenyewe bali kupitia yeye aliyevitiisha hivyo, juu ya msingi wa tumaini kwamba viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Waroma 8:20, 21.
Hizi kwa kweli ni habari njema—zilizo tofauti na zile tunazotazama kwenye televisheni au kusoma kwenye magazeti. Hizi ni habari njema sana kutoka kwa “Mungu wa faraja yote,” anayetujali sana.—2 Wakorintho 1:3.
-