-
Mpende Mungu AnayekupendaMnara wa Mlinzi—2006 | Desemba 1
-
-
Mpende Mungu Anayekupenda
“Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.”—MATHAYO 22:37.
1, 2. Inaelekea ni nini kilichowachochea watu waulize swali kuhusu amri iliyo kuu?
INAELEKEA swali lililoulizwa lilisababisha ubishi mkali kati ya Mafarisayo wa siku za Yesu. Kati ya sheria zaidi ya 600 ambazo zilifanyiza Sheria ya Musa, ni sheria gani iliyokuwa muhimu zaidi? Je, ilikuwa sheria iliyohusu dhabihu? Kwa kweli, dhabihu zilitolewa ili kupata msamaha wa dhambi na kumshukuru Mungu. Au je, sheria iliyokuwa muhimu zaidi ilikuwa sheria ya kutahiriwa? Sheria hiyo pia ilikuwa muhimu kwa sababu kutahiriwa kulikuwa ni ishara ya agano ambalo Yehova alifanya pamoja na Abrahamu.—Mwanzo 17:9-13.
2 Kwa upande mwingine, inaelekea watu wasiopenda mabadiliko walidai kwamba lingekuwa kosa kuinua sheria moja juu ya nyingine kwa kuwa kila sheria ambayo Mungu alitoa ilikuwa muhimu, hata ingawa sheria nyingine hazikuonekana kuwa muhimu sana. Mafarisayo waliamua kumuuliza Yesu swali hilo la ubishi. Huenda angesema jambo fulani ambalo lingeharibu sifa yake. Mmoja wao alimfikia Yesu na kumuuliza: “Amri iliyo kuu katika ile Sheria ni gani?”—Mathayo 22:34-36.
3. Yesu alisema ni amri gani iliyo kuu zaidi?
3 Jibu ambalo Yesu alitoa ni la maana sana kwetu leo. Katika jibu lake, alizungumzia kwa ufupi jambo ambalo daima lilikuwa muhimu zaidi katika ibada ya kweli wakati huo na hata leo. Akitaja maneno ya Kumbukumbu la Torati 6:5, Yesu alisema: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza.” Ingawa Farisayo huyo aliuliza kuhusu amri moja tu, Yesu alimtajia amri nyingine. Akitaja maneno ya Mambo ya Walawi 19:18, Yesu alisema hivi: “Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’” Kisha, Yesu akaonyesha kwamba amri hizo mbili ndizo zilizokuwa muhimu zaidi katika ibada safi. Ili kuwazuia wasimwambie ataje zile sheria nyingine kulingana na umuhimu wake, Yesu alimalizia hivi: “Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.” (Mathayo 22:37-40)
-
-
Mpende Mungu AnayekupendaMnara wa Mlinzi—2006 | Desemba 1
-
-
Umuhimu wa Upendo
4, 5. (a) Kwa nini Farisayo hakushangazwa na maneno ya Yesu? (b) Ni nini kilicho na thamani zaidi kwa Mungu kuliko dhabihu na matoleo?
4 Inaonekana kwamba yule Farisayo aliyemuuliza Yesu swali hakushtuka wala kushangazwa na jibu alilopewa. Alijua kwamba kumpenda Mungu ni jambo muhimu katika ibada ya kweli, ingawa wengi hawakuonyesha upendo huo. Katika masinagogi, kulikuwa na desturi ya kurudia-rudia kwa sauti sala ya Shema, au ungamo la imani, ambalo lilitia ndani maneno ya Kumbukumbu la Torati 6:4-9, andiko ambalo Yesu alizungumzia. Kulingana na simulizi la Marko, Farisayo huyo alimwambia Yesu hivi: “Mwalimu, umesema vema kupatana na kweli, ‘Yeye ni Mmoja, na hakuna mwingine ila Yeye’; na jambo hili la mtu kumpenda yeye kwa moyo wote na kwa uelewaji wote na kwa nguvu zote na mtu kumpenda jirani kama yeye mwenyewe ni bora zaidi kuliko matoleo yote mazima ya kuteketezwa na dhabihu zote.”—Marko 12:32, 33.
-