-
Iweni Wenye “Huruma Nyororo”Mnara wa Mlinzi—2007 | Desemba 15
-
-
Hata hivyo, nyakati nyingine si rahisi kuonyesha huruma. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo huko Kolosai: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba . . . Kama waliochaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni upendo mwororo wenye huruma.”—Wakolosai 3:9, 10, 12.
Hivyo, jitihada zinahitajiwa ili kusitawisha mtazamo wa huruma. Mtazamo huo ni sehemu ya “utu mpya” ambao Wakristo wanapaswa kuvaa. Paulo aliyeishi katika ulimwengu wenye ukatili wa Roma ya kale, aliwatia moyo waamini wenzake wafanye mabadiliko makubwa katika utu wao ili wawe wenye kujali na wenye huruma zaidi.
-
-
Iweni Wenye “Huruma Nyororo”Mnara wa Mlinzi—2007 | Desemba 15
-
-
Wakristo wanamwiga Yesu wanapowajali wengine. Yesu hakuwa na shughuli nyingi asiwasaidie wengine katika njia ya kimwili na ya kiroho. Alipotambua kwamba wengine wana uhitaji, aliwahurumia na kuwasaidia.
Fikiria jinsi Yesu alivyofanya alipouona umati wa watu waliokuwa wamepuuzwa kiroho: “Alipouona umati akawasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Msomi mmoja wa Biblia anasema kwamba neno linalotafsiriwa hapo kuwa “akawasikitikia” linamaanisha “hisia ya ndani kabisa inayomchochea mtu.” Kwa kweli, inasemekana kuwa neno hilo ndilo neno lenye nguvu zaidi la Kigiriki la kuonyesha hisia za huruma.
Vivyo hivyo, Wakristo wenye huruma hawakawii kuwasaidia wengine kimwili na kiroho. Mtume Petro aliandika hivi: “Ninyi nyote iweni na akili zinazopatana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo.” (1 Petro 3:8) Kwa mfano, familia moja ya Kikristo iliyo maskini ilipolazimika kuhamia eneo lingine kwa sababu za kiafya, waamini wenzao katika eneo hilo waliwaruhusu waishi katika nyumba fulani bila kulipa kodi ya nyumba kwa miezi sita. Mume alisema hivi: “Kila siku walikuja kutujulia hali, na maneno yao yenye kutia moyo yalitustarehesha.”
Wakristo wa kweli wanahangaikia mahitaji ya wageni pia. Kwa shangwe wanatumia wakati, nguvu, na mali zao ili kuwatumikia watu wasiowafahamu. Wafanyakazi wa kujitolea waliotajwa katika habari iliyotangulia ambao waliwasaidia watu wasiowafahamu ni Mashahidi wa Yehova.
Mazingira yenye huruma na fadhili zenye upendo yameenea katika kutaniko lote la Kikristo. Wakichochewa na upendo, washiriki wa kutaniko hilo wanapata nguvu za kutumikia. Huenda mayatima na wajane katika kutaniko wakahitaji uwahangaikie na kuwajali kwa sababu ya matatizo mbalimbali ya kibinafsi. Je, unaweza kuwasaidia watu kama hao wapambane na umaskini, ukosefu wa matibabu yanayofaa, ukosefu wa makao, na matatizo mengine ya kibinafsi?
Wafikirie wenzi fulani wa ndoa huko Ugiriki. Mume alipopatwa na ugonjwa wa kiharusi, alipelekwa katika hospitali iliyokuwa mamia ya kilomita kutoka kwao na mke wake alienda pamoja naye. Wenzi hao wangepata mapato yao madogo ikiwa tu shamba lao la machungwa lingevunwa. Lakini kwa kuwa walikuwa hospitalini, ni nani angefanya kazi hiyo? Kutaniko la kwao lilichukua hatua. Washiriki wa kutaniko hilo walivuna na kuuza machungwa hayo, na hivyo kuwaandalia mapato mume na mke huyo na kuwawezesha kuwa na amani ya akili.
Huruma inaweza kuonyeshwa kwa njia nyingi. Kwa mfano, Wakristo wenye huruma wanatambua kwamba nyakati nyingine baadhi ya wale wanaoteseka wanahitaji hasa kutembelewa na kuonyeshwa fadhili na watu watakaowasikiliza kwa huruma, watakaowajali, na kuwafariji kupitia Maandiko.—Waroma 12:15.
Furahia Mazingira Yenye Huruma
Kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote limethibitika kuwa makao ya amani na faraja ambamo huruma na fadhili zinaonyeshwa. Wakristo wa kweli wanatambua kwamba huruma inawavutia watu, lakini ukatili unachukiza. Hivyo, wanapojaribu kumwiga Baba yao wa mbinguni, wanajitahidi kuonyesha “huruma nyororo” katika njia zinazofaa.
Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha kwa uchangamfu katika jamii yao ya Kikristo ili ufurahie mazingira yenye huruma na upendo ambamo watu wanawajali wengine. Wana hakika kwamba utavutiwa na kupendezwa na mazingira hayo.—Waroma 15:7.
-