Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ninashukuru Kwamba Nimemtumikia Yehova, Hata Chini ya Majaribu
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Januari 15
    • Kisha, Agosti (Mwezi wa 8) 1941, nikapelekwa Ravensbrück—kambi ya mateso ya wanawake iliyojulikana sana kwa uovu, kilomita 80 hivi upande wa kaskazini wa Berlin, Ujerumani.

      “Changamka, Dada”

      Tulipofika, tuliambiwa kwamba tungeenda nyumbani ikiwa tungetia sahihi hati ya kuonyesha kwamba tumekana imani yetu. Lakini bila shaka sikutia sahihi. Badala yake, nililazimika kuwapa vitu nilivyokuwa navyo na nikavua mavazi yangu yote ndani ya bafu, ambamo nilikutana na dada fulani Wakristo kutoka Uholanzi. Katika kambi, tulipewa nguo za kuvaa ambazo zilikuwa na alama ya pembetatu ya zambarau iliyokuwa imeshonwa juu yake, tukapewa pia sahani, kikombe, na kijiko. Usiku wa kwanza, tuliwekwa katika vyumba vya kuweka wafungwa kwa muda. Nikiwa humo, nililia machozi kwa mara ya kwanza tangu nilipokamatwa. Nililia nikijiuliza, “Ni nini kitakachotokea? Nitakaa humu kwa muda gani?” Kwa kweli, wakati huo uhusiano wangu pamoja na Yehova haukuwa na nguvu sana, kwa kuwa nilikuwa nimejua kweli kwa miezi michache tu. Bado nilikuwa na mengi ya kujifunza. Siku iliyofuata tulipokuwa tukiitwa majina, inaonekana kwamba dada mmoja kutoka Uholanzi aliona nilivyohuzunika. Akasema: “Changamka, dada, changamka! Ni nini kinachoweza kutudhuru?”

      Baada ya kuitwa majina, tulipelekwa katika vyumba vingine, ambamo tulikaribishwa na mamia ya akina dada Wakristo kutoka Ujerumani na Uholanzi. Tayari akina dada fulani kutoka Ujerumani walikuwa wameishi katika vyumba hivyo kwa zaidi ya mwaka mmoja. Ushirika wao ulinitia nguvu—kwa kweli, ushirika huo ulinichangamsha. Pia, nilifurahi sana kwa kuwa vyumba ambamo dada zetu walikuwa wakiishi vilikuwa safi kuliko vyumba vingine katika kambi hiyo. Mbali na kuwa safi, vyumba vyetu vilijulikana kuwa mahali ambapo watu hawakuiba, kutukanana, au kupigana. Tofauti na hali mbaya sana tulizokabili katika kambi, vyumba vyetu vilikuwa kama kisiwa safi kilichozungukwa na bahari chafu.

      Maisha ya Kila Siku Katika Kambi

      Maisha kambini yalihusisha kufanya kazi nyingi na kula chakula kidogo sana. Tulikuwa tukiamka saa kumi na moja asubuhi, na muda mfupi baadaye tuliitwa majina. Walinzi walitulazimisha kusimama nje kwa karibu saa moja, iwe kulikuwa na mvua au jua. Saa kumi na moja jioni, baada ya kufanya kazi ngumu kwa siku nzima, tuliitwa tena majina. Kisha tulikula mkate na supu halafu tukalala—tukiwa tumechoka.

      Kila siku isipokuwa Jumapili (Siku ya Yenga), nilifanya kazi katika mashamba, ambako nilivuna ngano kwa upanga wa kufyeka majani, na pia niliondoa takataka kwenye mifereji au mitaro na kusafisha nyumba za nguruwe. Ingawa kazi hiyo ilikuwa ngumu na chafu, niliifanya kila siku kwa sababu bado nilikuwa kijana na nilikuwa na nguvu. Pia, nilijitia nguvu kwa kuimba nyimbo zenye ujumbe wa Biblia nilipokuwa nikifanya kazi. Hata hivyo, kila siku nilitamani kumwona mume wangu na mtoto wangu.

      Tulipewa chakula kidogo sana, lakini sisi dada wote tulijaribu kuweka kando kipande cha mkate kila siku ili tuwe na chakula cha ziada ambacho tungekula Jumapili, wakati ambapo tulipata nafasi ya kuwa pamoja ili kuzungumzia habari za Biblia. Hatukuwa na vichapo vya Biblia, lakini niliwasikiliza kwa makini dada Wajerumani wenye umri mkubwa waliokuwa waaminifu walipokuwa wakizungumzia mambo ya kiroho. Hata tuliadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

      Kutaabika, Kujuta, na Kutiwa Moyo

      Nyakati nyingine, tuliamuriwa kufanya kazi ambayo iliunga mkono moja kwa moja jitihada za kivita za Wanazi. Kwa sababu ya msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote katika vita, dada wote walikataa kufanya kazi hiyo, na nilifuata mfano wao wa ujasiri. Tuliadhibiwa kwa kunyimwa chakula kwa siku nyingi na tulilazimika kusimama kwa saa nyingi wakati wa kuitwa majina. Pindi moja, wakati wa majira ya baridi kali, tulifungiwa kwa siku 40 katika jumba ambalo halikuwa na mfumo wa kupasha joto.

      Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tuliambiwa tena na tena kwamba tungeachiliwa na kuruhusiwa kwenda nyumbani ikiwa tungetia sahihi hati ya kukana imani yetu. Baada ya kuishi Ravensbrück kwa zaidi ya mwaka mmoja, nilivunjika moyo sana. Tamaa ya kumwona mume wangu na binti yangu ikawa yenye nguvu sana hivi kwamba nilienda kwa walinzi, nikawaomba fomu ambayo ilisema kwamba mimi si Mwanafunzi wa Biblia tena, na nikaitia sahihi.

      Akina dada walipotambua jambo nililokuwa nimefanya, wengine wao walianza kuniepuka. Ingawa hivyo, dada wawili Wajerumani wenye umri mkubwa, Hedwig na Gertrud walinitafuta na kunihakikishia tena kwamba wananipenda. Tulipokuwa tukifanya kazi pamoja katika nyumba za nguruwe, walinieleza kwa fadhili kwa nini ni jambo la maana kudumisha utimilifu kwa Yehova na jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunampenda kwa kutolegeza msimamo wetu. Niliguswa moyo sana kwa sababu walinijali na kunionyesha shauku nyororo kama ya mama.a Nilijua kwamba nilikuwa nimekosea, na nilitaka hati ile ifutiliwe mbali. Jioni moja nilimwambia dada fulani kuhusu uamuzi wangu wa kutaka hati ile ifutiliwe mbali. Inaonekana kwamba ofisa mmoja katika kambi ile alisikia mazungumzo yetu kwa kuwa jioni hiyohiyo, mara moja niliwekwa huru kutoka katika ile kambi na kurudishwa Uholanzi kwa gari-moshi. Mmoja wa wasimamizi, ambaye bado ninakumbuka sura yake, aliniambia hivi: “Bado wewe ni Bibelforscher (Mwanafunzi wa Biblia), na utaendelea kuwa hivyo.” Nikamjibu: “Ndiyo, nitaendelea, ikiwa ni mapenzi ya Yehova.” Lakini bado niliendelea kufikiria, ‘Ninaweza kubadilisha jinsi gani hati niliyokuwa nimetia sahihi?’

      Sehemu moja katika hati ile ilisema hivi: “Kupitia hati hii ninatoa uhakikisho kwamba sitashirikiana tena kamwe na shirika la International Bible Students Society.” Nilijua jambo ambalo nilipaswa kufanya! Mnamo Januari (Mwezi wa 1) 1943, mara tu baada ya kufika nyumbani, nilianza tena kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Bila shaka, ikiwa ningeshikwa mara ya pili na askari wa Nazi nikihubiri kuhusu Ufalme wa Mungu, ningeadhibiwa vikali zaidi.

      Ili kumhakikishia zaidi Yehova kwamba nilitamani kutoka moyoni kuwa mtumishi mshikamanifu, mimi na mume wangu tulifanya tena nyumba yetu iwe mahali ambapo wasafirishaji wa vichapo na waangalizi wanaosafiri wangeishi. Nilithamini kama nini kupata nafasi nyingine ya kuthibitisha upendo wangu kwa Yehova na kwa watu wake!

  • Ninashukuru Kwamba Nimemtumikia Yehova, Hata Chini ya Majaribu
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Januari 15
    • Jambo moja kuu katika maisha yangu lilitokea mwaka wa 1995, nilipopata mwaliko wa kuhudhuria mwadhimisho huko Ravensbrück. Nikiwa huko nilikutana na dada ambao tulikuwa pamoja katika kambi hiyo na sikuwa nimewaona kwa miaka zaidi ya 50! Kuwa pamoja nao kulikuwa jambo lenye kugusa moyo sana na lisiloweza kusahaulika na ilikuwa nafasi nzuri ya kutiana moyo kuendelea kutazamia siku ambayo wapendwa wetu waliokufa wataishi tena.

  • Ninashukuru Kwamba Nimemtumikia Yehova, Hata Chini ya Majaribu
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Januari 15
    • [Picha katika ukurasa wa 12]

      Mwaka wa 1995, niliguswa moyo sana nilipokutana tena na marafiki wa zamani. Nimeketi kwenye safu ya mbele, wa pili kutoka kushoto

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki