-
Umalizio MzuriFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 39
Umalizio Mzuri
LABDA umefanya utafiti sana na kupanga hotuba yako vizuri. Pia huenda umetayarisha utangulizi unaoamsha upendezi. Lakini bado kuna jambo linalobaki, umalizio mzuri. Umalizio mzuri ni muhimu sana. Jambo unalosema mwisho ndilo hukumbukwa zaidi. Ikiwa umalizio wako ni dhaifu, hata mambo uliyosema awali yanaweza kukosa maana.
Ebu fikiria mifano ifuatayo: Yoshua alipokaribia kufa, aliwatolea wanaume wazee wa taifa la Israeli hotuba isiyoweza kusahaulika. Baada ya kusimulia jinsi Yehova alivyoshughulika na Israeli tangu wakati wa Abrahamu, je, Yoshua alirudia kutaja tu kwa ufupi mambo makuu? La. Badala yake, aliwahimiza hivi kwa hisia sana: “Mcheni BWANA, mkamtumikie kwa unyofu wa moyo na kwa kweli.” Ebu soma umalizio wake katika Yoshua 24:14, 15.
Katika Matendo 2:14-36, mtume Petro alitoa hotuba nyingine muhimu mbele ya umati uliokuwa Yerusalemu kwenye Sherehe ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kwanza alieleza kwamba umati ulikuwa ukishuhudia utimizo wa unabii wa Yoeli kuhusu kumwagwa kwa roho ya Mungu. Kisha akaonyesha jinsi tukio hilo linavyohusiana na unabii mbalimbali wa Zaburi unaohusu Mesiya uliotabiri ufufuo wa Yesu Kristo na jinsi alivyokwezwa hadi kwenye mkono wa kulia wa Mungu. Kisha akimalizia, Petro akataja wazi jambo ambalo kila mmoja wa wasikilizaji wake anapaswa kufikiria. Akasema: “Kwa hiyo acha nyumba yote ya Israeli ijue kwa hakika kwamba Mungu alimfanya Bwana na pia Kristo, Yesu huyu ambaye nyinyi mlimtundika mtini.” Wale waliokuwapo wakauliza: “Wanaume, akina ndugu, tufanye nini?” Petro akajibu: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo.” (Mdo. 2:37, 38) Siku hiyo, watu wapatao 3,000 miongoni mwa wasikilizaji waliguswa moyo sana na mambo hayo wakakubali kweli kuhusu Yesu Kristo.
Kumbuka Mambo Haya. Umalizio ulingane na kichwa kikuu cha hotuba. Umalizio unapaswa kuungana vizuri na mambo makuu ambayo umezungumzia. Ingawa unaweza kutaja baadhi ya maneno makuu ya kichwa kikuu, ni juu yako kuamua kama utarudia kutaja kichwa kikuu chenyewe.
Kwa kawaida, kusudi la kutoa hotuba ni kuwachochea watu wachukue hatua kutokana na habari unayowatolea. Mojawapo ya makusudi makuu ya umalizio ni kuwaonyesha jambo la kufanya. Unapochagua kichwa kikuu na mambo makuu, je, unafikiria kwa makini umuhimu wa habari hiyo kwa wasikilizaji na kusudi lako la kuitoa? Ikiwa ndivyo, unajua hatua ambayo unataka wachukue. Sasa unahitaji kuwaeleza hatua hiyo na labda jinsi ya kuichukua.
Mbali na kuwaonyesha wasikilizaji jambo la kufanya, umalizio unapaswa kuwachochea. Umalizio unapaswa kutaja sababu nzuri za kuchukua hatua fulani na faida za kufanya hivyo. Ukifikiria kwa makini sentensi ya mwisho na kuipanga vizuri, hotuba yote itawachochea wasikilizaji sana.
Kumbuka kwamba unamalizia hotuba. Maneno yako yaonyeshe hivyo. Pia zungumza kwa mwendo unaofaa. Usizungumze mbiombio na kumaliza hotuba kwa ghafula. Na pia usimalizie kwa sauti yenye kufifia. Unapaswa kutumia kiasi kinachofaa cha sauti lakini usiseme kwa sauti kubwa kupita kiasi. Sentensi chache za mwisho zionyeshe unamalizia. Ziseme kwa bidii na kwa usadikisho. Unapotayarisha kutoa hotuba, usikose kufanya mazoezi ya umalizio.
Umalizio uwe mrefu kadiri gani? Umalizio hautegemei muda fulani hususa. Usijikokote unapomalizia. Muda unaofaa wa umalizio unaweza kutegemea matokeo yake kwa wasikilizaji. Sikuzote, umalizio rahisi na wenye kutia moyo hufaa. Umalizio mrefu kidogo wenye mfano mfupi pia unaweza kuwa bora ukipangwa vizuri. Ebu linganisha umalizio mfupi wa kitabu chote cha Mhubiri katika Mhubiri 12:13, 14, na umalizio wa hotuba fupi kidogo ya Mahubiri ya Mlimani uliorekodiwa katika Mathayo 7:24-27.
-