Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yehova Apaswa Kuwa Tumaini Letu
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Agosti 15
    • Yehova Apaswa Kuwa Tumaini Letu

      “BWANA atakuwa tumaini lako.”—MITHALI 3:26.

      1. Ingawa wengi hudai kumtumaini Mungu, ni nini kidokezacho kwamba hawafanyi hivyo sikuzote?

      MWITO “Twamtumaini Mungu,” huonekana kwenye fedha za Marekani. Lakini je, wale wote wanaotumia fedha hizo katika nchi hiyo au kwengineko, humtumaini Mungu kwa kweli? Au wao hutumaini zaidi fedha zenyewe? Kutumaini hivyo fedha za nchi hiyo au za nchi nyingine yoyote, hakuwezi kulinganishwa na kumtumaini Mungu wa upendo aliye mweza yote, ambaye hatumii kamwe nguvu zake vibaya, na ambaye kwa vyovyote hana pupa. Kwa kweli, yeye hulaumu pupa waziwazi.—Waefeso 5:5.

      2. Wakristo wa kweli wana mtazamo gani kuhusu nguvu za mali?

      2 Wakristo wa kweli humtumaini Mungu, bali si mali na “nguvu [zake] za udanganyifu.” (Mathayo 13:22) Wao hutambua kwamba fedha zina nguvu ndogo sana za kuendeleza furaha na kuhifadhi uhai. Lakini hali haiko hivyo kuhusiana na nguvu za Mungu Mweza Yote. (Sefania 1:18) Kwa hiyo, ni lenye hekima kama nini onyo hili la upole: “Acheni namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa fedha, huku nyinyi mkiridhika na vitu vilivyopo. Kwa maana yeye amesema: ‘Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.’”!—Waebrania 13:5.

      3. Muktadha wa Kumbukumbu la Torati 31:6 hufafanuaje nukuu la Paulo la mstari huo?

      3 Alipowaandikia Wakristo Waebrania maneno hayo yaliyo juu, mtume Paulo alinukuu maagizo ambayo Musa aliwapa Waisraeli muda mfupi kabla ya kifo chake: “Iweni hodari na moyo wa ushujaa, msiogope wala msiwahofu; kwa maana BWANA, Mungu wako, yeye ndiye anayekwenda pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha.” (Kumbukumbu la Torati 31:6) Muktadha waonyesha kwamba Musa alikuwa akiwatia moyo wawe na tumaini kwamba Yehova angeweza kuwaandalia mengi zaidi ya mahitaji yao ya kimwili. Jinsi gani hivyo?

      4. Mungu aliwathibitishiaje Waisraeli kwamba angeweza kutumainika?

      4 Katika miaka 40 ambayo Waisraeli walilazimika kuzunguka-zunguka nyikani, Mungu aliwaandalia kwa uaminifu mahitaji ya lazima ya maisha. (Kumbukumbu la Torati 2:7; 29:5) Pia aliwaandalia uongozi. Alifanya hivyo kwa kuwaongoza Waisraeli kwa wingu wakati wa mchana na kwa moto wakati wa usiku hadi “nchi ijaayo maziwa na asali.” (Kutoka 3:8; 40:36-38) Wakati ulipofika wa kuingia hasa katika Bara Lililoahidiwa, Yehova alimchagua Yoshua awe mwandamizi wa Musa. Wakaaji wa hiyo nchi wangeweza kutarajiwa kutokeza upinzani. Lakini Yehova alikuwa ametembea pamoja na watu wake kwa miongo mingi, kwa hiyo hawakuhitaji kuhofu jambo lolote. Waisraeli walikuwa na kila sababu ya kumjua Yehova kuwa Mungu ambaye angeweza kutumainika!

      5. Hali ya Wakristo leo ikoje sawa na ile ya Waisraeli kabla ya kuingia katika Bara Lililoahidiwa?

      5 Wakristo leo wamekuwa wakisafiri kupitia nyika ya ulimwengu mwovu wa sasa wakielekea kwenye ulimwengu mpya wa Mungu. Baadhi yao wamekuwa wakitembea kwa muda wa zaidi ya miaka 40. Sasa wanasimama ukingoni mwa ulimwengu mpya wa Mungu. Hata hivyo, maadui wangali wanawazuia, wakinuia kutowapa nafasi wowote waingie katika lile litakalokuwa kama Bara Lililoahidiwa, ambalo ni lenye utukufu kuliko lile la kale lililojaa maziwa na asali. Kwa hiyo maneno haya ya Musa yaliyorudiwa na Paulo yafaa kama nini kwa Wakristo leo: “Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote”! Wale wote ambao huendelea kuwa wenye nguvu na ujasiri, wakijaa imani na kumtumaini Yehova, wana uhakika wa kupata thawabu.

      Tumaini Litegemealo Ujuzi na Urafiki

      6, 7. (a) Tumaini la Abrahamu katika Yehova lilijaribiwa na nini? (b) Huenda Abrahamu alihisije alipokuwa akisafiri kwenda mahali ambapo angemtoa Isaka dhabihu?

      6 Wakati fulani, Abrahamu baba wa zamani wa Waisraeli aliagizwa amdhabihu Isaka mwana wake akiwa toleo la kuteketezwa. (Mwanzo 22:2) Ni nini kilichomwezesha baba huyo mwenye upendo amtumaini Yehova kwa uthabiti hivyo hivi kwamba alikuwa tayari kutii mara moja? Andiko la Waebrania 11:17-19 lajibu: “Kwa imani Abrahamu, alipojaribiwa, ni kana kwamba alimtoa Isaka, na huyo mtu aliyekuwa amezipokea ahadi kwa mteremo akajaribu kutoa mwana wake mzaliwa-pekee, ijapokuwa alikuwa ameambiwa: ‘Itakayoitwa “mbegu yako” itakuwa kupitia Isaka.’ Lakini alihesabu kwamba Mungu alikuwa aweza kumfufua hata kutoka kwa wafu; na kutoka huko alimpokea pia katika njia ya kielezi.”

      7 Kumbuka kwamba iliwachukua Abrahamu na Isaka muda wa siku tatu kufika mahali ambapo dhabihu ingetolewa. (Mwanzo 22:4) Abrahamu alikuwa na wakati mwingi wa kulifikiria tena jambo alilokuwa ametakiwa afanye. Je, twaweza kuwazia jinsi alivyohisi? Kuzaliwa kwa Isaka kulikuwa chanzo kisichotarajiwa cha furaha. Kuzaliwa huko kulikothibitisha kuingilia kati kwa Mungu, kulizidisha uhusiano ambao Abrahamu na mke wake Sara, ambaye hapo kwanza alikuwa tasa, walikuwa nao pamoja na Mungu. Bila shaka baada ya kuzaliwa huko waliishi wakitarajia yale ambayo baadaye yangempata Isaka na wazao wake. Je, matarajio yao yalikuwa yamefikia kikomo kama ionekanavyo kuwa, kwa sababu ya yale ambayo Mungu alitaka sasa yafanywe?

      8. Ni jinsi gani tumaini la Abrahamu katika Mungu lilikuwa zaidi ya kuamini tu kwamba Yeye angeweza kumfufua Isaka?

      8 Bado, tumaini la Abrahamu lilitegemea kule kujuana kibinafsi kwa marafiki wa karibu. Akiwa “rafiki wa Yehova,” Abrahamu “aliweka imani katika Yehova, na ilihesabiwa kwake kuwa uadilifu.” (Yakobo 2:23) Tumaini la Abrahamu katika Yehova lilikuwa zaidi ya kuamini tu kwamba Mungu angeweza kumfufua Isaka. Abrahamu alikuwa amesadiki hivyohivyo kwamba, lile Yehova alilokuwa akitaka afanye lilifaa, hata ingawa Abrahamu hakujua mambo yote. Hakuwa na sababu ya kushuku kwamba Yehova alikuwa na haki ya kumtaka afanye hivyo. Kisha, tumaini la Abrahamu likaimarishwa malaika wa Yehova alipoingilia kati kuzuia kuuawa hasa kwa Isaka akiwa dhabihu.—Mwanzo 22:9-14.

      9, 10. (a) Abrahamu alikuwa ameonyesha tumaini katika Yehova wakati gani wa mapema? (b) Twaweza kujifunza somo gani kutokana na Abrahamu?

      9 Yapata miaka 25 mapema, Abrahamu alionyesha tumaini la aina hiyohiyo katika uadilifu wa Yehova. Akiwa ameonywa kwamba Sodoma na Gomora yangeharibiwa, alihangaikia kiasili hali njema ya watu waadilifu wowote waliokuwa wakiishi huko, kutia ndani Loti, mpwa wake wa kiume. Abrahamu alimsihi Mungu kwa kusema: “Hasha usifanye hivyo, ukamwue mwenye haki pamoja na mwovu, mwenye haki awe kama mwovu. Hasha; Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?”—Mwanzo 18:25.

      10 Mzee wa ukoo Abrahamu alisadiki kwamba Yehova hafanyi kamwe jambo lolote lisilo la uadilifu. Baadaye mtunga-zaburi aliimba: “BWANA ni mwenye haki [“uadilifu,” NW] katika njia zake zote, na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.” (Zaburi 145:17) Yafaa tujiulize hivi: ‘Je, mimi hukubali yale Yehova aruhusuyo yanipate bila kushuku uadilifu wake? Je, mimi nasadiki kwamba yoyote yale aruhusuyo yanipate yataninufaisha na kunufaisha wengine?’ Ikiwa twaweza kujibu ndiyo, tumejifunza somo muhimu kutokana na Abrahamu.

      Kuonyesha Tumaini Katika Wale Ambao Yehova Amechagua

      11, 12. (a) Watumishi wa Mungu wamelazimika kuwa na tumaini la namna gani? (b) Huenda nyakati nyingine sisi tukawa na tatizo gani?

      11 Wale ambao humwona Yehova kuwa tumaini lao huonyesha tumaini pia katika wanaume ambao Yehova amechagua kutumia katika kutimiza makusudi yake. Kwa Waisraeli, hilo lilimaanisha kuonyesha tumaini katika Musa na baadaye Yoshua, mwandamizi wake. Kwa Wakristo wa mapema, hilo lilimaanisha kuonyesha tumaini katika mitume na wanaume wazee wa kutaniko la Yerusalemu. Kwetu leo, hilo lamaanisha kumtumaini “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” aliyewekwa rasmi kutupa ‘chakula chetu cha kiroho kwa wakati ufaao,’ na pia wale kutoka miongoni mwake ambao hufanyiza Baraza Linaloongoza.—Mathayo 24:45.

      12 Kwa kweli, kuwatumaini wale wanaoongoza kutaniko la Kikristo hutunufaisha sisi wenyewe. Twaambiwa hivi: “Iweni watiifu kwa wale ambao wanaongoza miongoni mwenu na kuwa wenye kunyenyekea, kwa maana wao wanafuliza kulinda juu ya nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wapate kufanya hili kwa shangwe na si kwa kutweta, kwa maana hili lingekuwa lenye hasara kwenu.”—Waebrania 13:17.

      Epuka Kuchambua Wale Ambao Yehova Amechagua

      13. Tuna sababu gani ya kuwatumaini wale waliowekwa rasmi kuongoza?

      13 Biblia hutusaidia kuwa na usawaziko katika kuwatumaini wale wanaoongoza watu wa Yehova. Huenda tukajiuliza hivi: ‘Je, Musa alifanya makosa yoyote? Je, sikuzote mitume walionyesha mtazamo kama wa Kristo ambao Yesu aliwataka wawe nao?’ Majibu ni wazi. Yehova amechagua kuwatumia wanaume waaminifu-washikamanifu, wenye kujitolea ili kuwaongoza watu wake, hata ingawa wanaume hao si wakamilifu. Kulingana na hayo, ingawa leo wazee si wakamilifu, bado yatupasa tuwatambue kuwa “[wamewekwa rasmi na] roho takatifu [wawe] waangalizi, kulichunga kutaniko la Mungu.” Wao wastahili kuungwa mkono nasi na kuonyeshwa staha.—Matendo 20:28.

      14. Ni nini kifaacho kuangaliwa kuhusu kuchaguliwa kwa Musa na Yehova kuwa kiongozi badala ya Aroni au Miriamu?

      14 Umri wa Aroni ulipita wa Musa kwa miaka mitatu, lakini wote wawili walikuwa na umri mdogo kuliko dada yao Miriamu. (Kutoka 2:3, 4; 7:7) Na kwa kuwa Aroni alisema kwa ufasaha zaidi kuliko Musa, alichaguliwa rasmi atumikie akiwa msemaji wa ndugu yake. (Kutoka 6:29–7:2) Hata hivyo, Yehova hakumchagua Miriamu aliyekuwa na umri mkubwa zaidi, wala Aroni mwenye kusema kwa ufasaha zaidi ili kuwaongoza Waisraeli. Alimchagua Musa kwa kutambua kabisa mambo yote ya hakika na mahitaji ya wakati huo. Walipokosa kwa muda fulani ufahamu huo wenye kina uliokuwa wazi, Aroni na Miriamu walilalamika hivi: “Je! ni kweli BWANA amenena na Musa tu? hakunena na sisi pia?” Miriamu, ambaye yaelekea ndiye aliyekuwa mchochezi mkuu, aliadhibiwa kwa kuwa na mtazamo huo usio na staha kumwelekea yule aliyechaguliwa na Yehova, ambaye Miriamu na Aroni wangepaswa kumtambua kuwa “mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.”—Hesabu 12:1-3, 9-15.

      15, 16. Kalebu alithibitishaje kwamba alimtumaini Yehova?

      15 Wakati ambapo wapelelezi 12 walitumwa wakapeleleze Bara Lililoahidiwa, 10 walirudisha ripoti isiyofaa. Waliwatia Waisraeli hofu mioyoni mwao kwa kusema juu ya “watu warefu mno” wa Kanaani. Jambo hilo nalo, liliwafanya Waisraeli ‘wamnung’unikie Musa na Aroni.’ Lakini si wapelelezi wote waliokosa kuonyesha tumaini katika Musa na Yehova. Tunasoma hivi: “Kalebu akawatuliza watu mbele ya Musa, akasema, Na tupande mara, tukaitamalaki; maana twaweza kushinda bila shaka.” (Hesabu 13:2, 25–33; 14:2) Msimamo imara wa Kalebu ulionyeshwa pia na Yoshua, mpelelezi mwenzake. Wote wawili walionyesha kwamba walikuwa wamemfanya Yehova kuwa tumaini lao waliposema hivi: “Ikiwa BWANA anatufurahia, atatuingiza katika nchi hii atupe iwe yetu, nayo ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali. Lakini . . . msiwaogope wale wenyeji wa nchi . . . BWANA yu pamoja nasi; msiwaogope.” (Hesabu 14:6-9) Tumaini hilo katika Yehova lilithawabishwa. Kuhusu kizazi cha watu wazima waliokuwa hai wakati huo, ni Kalebu, Yoshua, na Walawi kadhaa tu waliopata pendeleo la kuingia katika Bara Lililoahidiwa.

      16 Miaka kadhaa baadaye, Kalebu alisema hivi: “Ila mimi nilimfuata BWANA, Mungu wangu, kwa utimilifu. . . . Sasa basi, angalia, yeye BWANA ameniweka hai, kama alivyosema, miaka hii arobaini na mitano, tangu wakati huo BWANA alipomwambia Musa neno hilo, wakati Israeli waliokuwa wakienenda barani; na sasa tazama, hivi leo nimepata miaka themanini na mitano umri wangu. Hata sasa mimi nina nguvu zangu hivi leo kama nilivyokuwa siku hiyo Musa aliyonituma; kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, na nguvu zangu ndivyo zilivyo sasa.” (Yoshua 14:6-11) Ona mtazamo ufaao wa Kalebu, uaminifu wake, na uwezo wake mbalimbali wa kimwili. Hata hivyo, Yehova hakuwa amemchagua Kalebu awe mwandamizi wa Musa. Alimtolea Yoshua pendeleo hilo. Twaweza kuwa na tumaini kwamba Yehova alikuwa na sababu za kumchagua, naye alikuwa chaguo bora kabisa.

      17. Ni nini ambacho huenda kilimfanya Petro aonekane kuwa asiyestahili daraka?

      17 Mtume Petro alimkana Bwana-Mkubwa wake mara tatu. Alikuwa pia amechukua mambo mikononi mwake kwa haraka-haraka na kumkata sikio mtumwa wa kuhani wa cheo cha juu. (Mathayo 26:47-55, 69-75; Yohana 18:10, 11) Huenda watu fulani wakasema kwamba Petro alikuwa mtu mwenye hofu, asiye na usawaziko, ambaye hakustahili kupata mapendeleo ya pekee. Hata hivyo, ni nani aliyekuwa amepewa funguo za Ufalme, akiwa na pendeleo la kuviwezesha vikundi vitatu kupata wito wa mbinguni? Alikuwa Petro.—Matendo 2:1-41; 8:14-17; 10:1-48.

      18. Twataka kuepuka kosa gani ambalo limetajwa na Yuda?

      18 Vielelezo hivyo, vyaonyesha kwamba twapaswa kuwa waangalifu dhidi ya kuhukumu watu kwa kutegemea jinsi wanavyoonekana. Tukimtumaini Yehova, hatutashuku wale ambao amewachagua. Ingawa kutaniko lake la kidunia limefanyizwa na wanadamu wasio wakamilifu, ambao hawadai kuwa watu wasioweza kukosea, anawatumia katika njia kubwa sana. Yuda aliyekuwa ndugu-nusu wa Yesu, aliwaonya Wakristo wa karne ya kwanza dhidi ya watu “[walio]puuza ubwana na kusema kwa maneno yenye kuudhi juu ya watukufu.” (Yuda 8-10) Na tusiwe kamwe kama wao.

      19. Kwa nini hatuna sababu ya kuchambua wale ambao Yehova amechagua?

      19 Yaonekana kwamba kwa ajili ya madaraka fulani, Yehova huwachagua watu walio na sifa mahususi zihitajiwazo ili kuwaongoza watu wake katika njia ambayo awataka watembee katika wakati fulani maalumu. Yatupasa tujitahidi kutambua jambo hilo la hakika, wala si kuchambua watu ambao Mungu amechagua, bali kwa unyenyekevu turidhike kutumikia mahali ambapo Yehova ameweka kila mmoja wetu. Hivyo twaonyesha kwamba tumemfanya Yehova kuwa tumaini letu.—Waefeso 4:11-16; Wafilipi 2:3.

      Kutumaini Uadilifu wa Yehova

      20, 21. Twaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Mungu alivyoshughulika na Musa?

      20 Ikiwa nyakati nyingine tuna mwelekeo wa kujitumaini kupita kiasi na kumtumaini Yehova kidogo tu, acheni tujifunze kutokana na Musa. Alipokuwa na umri wa miaka 40, aliondoka kwenda kuwaweka Waisraeli huru kutoka katika utekwa wa Wamisri. Alikuwa na nia nzuri katika jitihada zake, lakini hazikuwakomboa Israeli mara moja, wala hazikuboresha hali yake mwenyewe. Kwa kweli, alilazimika kukimbia. Ilikuwa baada tu ya kupata mazoezi magumu ya miaka 40 katika nchi ya kigeni, ndipo alipostahili kuteuliwa kufanya yale aliyokuwa ametaka kufanya mapema kidogo. Wakati huo angetumaini kupata utegemezo wa Yehova kwa sababu sasa mambo yalikuwa yakifanywa jinsi Yehova alivyotaka katika wakati uliofaana na ratiba Yake ya wakati.—Kutoka 2:11–3:10.

      21 Kila mmoja wetu aweza kujiuliza hivi: ‘Je, nyakati nyingine mimi humtangulia Yehova na wazee alioweka rasmi kutanikoni, nikijaribu kuharakisha mambo au kuyafanya jinsi nitakavyo? Badala ya kuhisi nimepuuzwa kuhusiana na mapendeleo ya utumishi, je, mimi hukubali kwa utayari kipindi cha kuzoezwa kinachoendelea?’ Kimsingi, je, tumejifunza somo muhimu kutokana na Musa?

      22. Musa alihisije juu ya Yehova licha ya kupoteza pendeleo kubwa?

      22 Isitoshe, twaweza kujifunza somo jingine kutokana na Musa. Andiko la Hesabu 20:7-13 latuambia juu ya kosa alilofanya, lililofanya apoteze pendeleo lake. Alipoteza pendeleo la kuwaongoza Waisraeli hadi Bara Lililoahidiwa. Je, wakati huo alisema kwamba uamuzi wa Yehova haukuwa wa haki? Je, alijitenga, akinuna kwa sababu Mungu alikuwa akimtendea isivyo haki? Je, Musa aliacha kutumaini uadilifu wa Yehova? Twaweza kupata majibu katika maneno ambayo Musa mwenyewe aliwaambia Waisraeli muda mfupi kabla ya kifo chake. Kumhusu Yehova, Musa alisema: “Kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu. Yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Bila shaka Musa aliendelea kuweka tumaini lake katika Yehova hadi kifo. Namna gani sisi? Je, sisi mmoja-mmoja tunachukua hatua ya kuimarisha tumaini letu katika Yehova na uadilifu wake? Twaweza kufanyaje hivyo? Acheni tuone.

  • Kuliimarisha Tumaini Letu Katika Uadilifu wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Agosti 15
    • Kuliimarisha Tumaini Letu Katika Uadilifu wa Mungu

      ‘Ili tumaini lako uliweke kwa BWANA, leo nimekujulisha wewe haya.’ —MITHALI 22:19.

      1, 2. (a) Kwa nini Mashahidi wa Yehova huonyesha tumaini katika Yehova? (Mithali 22:19) (b) Ni nini kionyeshacho kwamba watu fulani wanahitaji kuimarisha tumaini lao katika Yehova?

      WAKRISTO wa kweli wamebarikiwa kuwa na ujuzi sahihi juu ya Yehova na juu ya makusudi yake. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huwaandalia kwa upendo ‘chakula chao kwa wakati ufaao.’ (Mathayo 24:45) Ujuzi ambao wao hupata huwaandalia msingi thabiti ambao juu yake tumaini katika Mungu hutegemezwa. Hivyo, wakiwa kikundi, Mashahidi wa Yehova huonyesha tumaini lisilo na kifani katika Yehova na uadilifu wake.

      2 Hata hivyo, yaonekana kwamba, wakiwa watu mmoja-mmoja, huenda Mashahidi fulani wakahitaji kuimarisha tumaini kama hilo. Pindi kwa pindi Sosaiti hupokea barua ambazo hushuku maelezo yatolewayo katika vichapo vyake. Huenda shaka hizo zikatokana na marekebisho katika uelewevu, au zikahusu mambo yanayoathiri mwenye kuuliza, hasa kihisia-moyo.—Linganisha Yohana 6:60, 61.

      3. Watumishi waaminifu wa Yehova waweza kupatwa na nini, na kwa nini?

      3 Hata watumishi wa kweli wa Yehova hupata kujua ukweli wa Mhubiri 9:11: “Nikarudi, na kuona chini ya jua, ya kwamba si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” NW] huwapata wote.” Hayo yaweza kuthibitikaje kuwa kweli katika maana iliyo kubwa, au ya kiroho? Huenda tukawa tuliwajua Wakristo waliokuwa wepesi sana juu ya kutumia shauri la Biblia, wenye uwezo wa kuitetea kweli, wenye hekima katika kutumia kanuni za Biblia, na wenye bidii katika kufuatia ujuzi sahihi. Hata hivyo, kwa sababu ya ‘wakati na tukio lisilotazamiwa,’ huenda wengine wakajiona kuwa hawawezi kufanya mengi kwa sababu ya aksidenti au uzee. Huenda wakashuku uwezekano wa kuigia katika ulimwengu mpya wa Mungu bila hata kufa.

      4, 5. Kwa nini Wakristo hawana sababu ya kukosa tumaini katika uadilifu wa Yehova?

      4 Mkristo anapofiwa na mwenzi wake wa ndoa, huzuni na hisia za kumpoteza ni kali. Huenda wakawa walimtumikia Yehova pamoja wakiwa wenzi, kwa miaka au hata miongo mingi. Mwenzi aliyebaki hai ajua kwamba kifo huvunja kifungo cha ndoa.a (1 Wakorintho 7:39) Sasa ili kukinga tumaini lake lisidhoofike, ni lazima adhibiti hisia-moyo zake.—Linganisha Marko 16:8.

      5 Ni jambo la hekima kama nini kukiona kifo cha mwenzi, mzazi, mtoto, au Mkristo aliye rafiki wa karibu kuwa fursa ya kuonyesha tumaini katika uadilifu wa Yehova! Hata sisi binafsi tunapofiwa, twaweza kuwa na tumaini kwamba Yehova ni mwadilifu. Twaweza kuwa na tumaini kwamba kila mtu apataye uhai wa milele—iwe ni kwa kubaki hai au kupitia ufufuo—atafurahi. Kumhusu Mungu, mtunga-zaburi asema hivi: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake. BWANA ni mwenye haki [“mwadilifu,” NW] katika njia zake zote, na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote. BWANA yu karibu na wote wamwitao, wote wamwitao kwa uaminifu. Atawafanyia wamchao matakwa yao, naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.”—Zaburi 145:16-19.

      Tukihisi Kuwa Tuliteseka Isivyo Lazima

      6, 7. (a) Kwa nini sasa Mashahidi fulani ambao waliteseka wakati uliopita wana uelewevu tofauti? (b) Kwa nini hatupaswi kumwona Yehova kuwa asiye mwadilifu kwa kuruhusu kuteseka huko wakati uliopita?

      6 Wakati uliopita, Mashahidi fulani wameteseka kwa kukataa kushiriki katika utendaji fulani ambao dhamiri yao sasa yaweza kuwaruhusu kushiriki. Kwa kielelezo, huenda waliteseka kwa sababu ya uchaguzi waliofanya miaka mingi iliyopita kuhusiana na aina fulani ya utumishi wa kiraia. Huenda sasa ndugu akahisi kwamba angeweza kwa kudhamiria kufanya utumishi kama huo bila kukiuka kutokuwamo kwake kwa Kikristo kwa habari ya mfumo wa mambo wa sasa.

      7 Je, Yehova alikosa uadilifu kwa kumruhusu ateseke kwa sababu ya kukataa kufanya jambo ambalo sasa aweza kufanya bila madhara? Wengi ambao wamepatwa na jambo hilo hawangefikiri hivyo. Badala yake, wao hufurahi kwamba walipata fursa ya kuonyesha hadharani na waziwazi kwamba waliazimia kuwa imara kuhusu suala la enzi kuu ya ulimwengu. (Linganisha Ayubu 27:5.) Ni sababu gani ambayo ingeweza kufanya yeyote ajute kuwa alifuata dhamiri yake katika kuchukua msimamo imara kwa ajili ya Yehova? Kwa kuziunga mkono kanuni za Kikristo kwa uaminifu-mshikamanifu kama walivyozielewa au kwa kuitikia midukuo ya dhamiri ya mtu, walithibitika kuwa wenye kustahili urafiki wa Yehova. Bila shaka, ni hekima kuepuka mwendo ambao ungesumbua dhamiri ya mtu au ambao ungeelekea kufanya wengine wakwazike. Kuhusiana na hilo twaweza kufikiria kielelezo ambacho mtume Paulo aliweka.—1 Wakorintho 8:12, 13; 10:31-33.

      8. Kwa nini Wakristo Wayahudi walioshika Sheria hapo zamani, hawana sababu ya kushuku uadilifu wa Yehova?

      8 Ili wampendeze Yehova, Wayahudi walihitajika kutii zile Amri Kumi na pia sheria nyingi mbalimbali za ziada zipatazo 600. Baadaye, chini ya mpango wa Kikristo, kutii sheria hizo zikiwa hivyo hakukutakiwa tena ili kumtumikia Yehova, hata kwa Wayahudi wa kimwili. Sheria ambazo haikuwa lazima zifuatwe zilihusu tohara, kushika Sabato, kutoa dhabihu za wanyama, na kushika sheria zilizozuia ulaji wa vyakula fulani. (1 Wakorintho 7:19; 10:25; Wakolosai 2:16, 17; Waebrania 10:1, 11-14) Wayahudi—kutia ndani wale mitume—waliopata kuwa Wakristo waliwekwa huru na wajibu wa kushika sheria ambazo walihitajika kuzitii walipokuwa chini ya agano la Sheria. Je, walilalamika kwamba mipango ya Mungu ilikosa uadilifu hapo zamani kwa kuwataka wafanye mambo ambayo hayakuwa ya lazima tena? La, walifurahia uelewevu uliopanuka wa makusudi ya Yehova.—Matendo 16:4, 5.

      9. Ni jambo gani limekuwa kweli kuhusu Mashahidi fulani, lakini kwa nini hawana sababu ya kujuta?

      9 Nyakati za kisasa kumekuwa na Mashahidi waliokuwa na maoni makali sana kuhusu yale ambayo wangefanya au yale wasingeweza kufanya. Kwa sababu hiyo waliteseka zaidi ya wengine. Baadaye, ujuzi ulioongezeka uliwasaidia kuona mambo kwa njia iliyopanuka. Lakini hawana sababu ya kujuta kwa kutenda kupatana na dhamiri yao hapo awali, hata wakati ambapo hilo labda liliwaletea mateso zaidi. Ni jambo linalostahili pongezi kwamba, walionyesha utayari wao wa kuteseka kwa kuwa waaminifu kwa Yehova, ili “[wafanye] mambo yote kwa ajili ya habari njema.” Yehova hubariki aina hiyo ya ujitoaji kimungu. (1 Wakorintho 9:23; Waebrania 6:10) Mtume Petro aliandika hivi kwa ufahamu wenye kina: “Ikiwa, mnapotenda mema na kuteseka, mwalivumilia, hili ni jambo lenye kukubalika kwa Mungu.”—1 Petro 2:20.

      Kujifunza Kutokana na Yona

      10, 11. Yona alionyeshaje ukosefu wa tumaini katika Yehova (a) alipopewa mgawo wa kwenda Ninewi? (b) Mungu alipokosa kuwaharibu Waninewi?

      10 Alipoagizwa aende Ninewi, Yona alikosa kuthamini tumaini ambalo Yehova alikuwa akiweka kwake. Baada ya kupatwa na jambo lenye kuogofya ambalo yeye mwenyewe alilitokeza kwa kutokuwa tayari kutii, Yona alirudiwa na fahamu, akatambua kosa lake, akakubali mgawo wake wa kwenda nchi ya kigeni, na kuwaonya Waninewi juu ya uharibifu uliokuwa ukikaribia. Kisha jambo lisilotarajiwa likatokea: Kwa sababu ya mtazamo wa toba wa Waninewi, Yehova aliamua kutowaharibu.—Yona 1:1–3:10.

      11 Yona aliitikiaje? Kwa kuchukizwa, Yona alimlalamikia Mungu katika sala. Kiini cha lalamiko lake kilikuwa: ‘Niliwazia kwamba mambo yangekuwa hivyo. Hiyo ndiyo sababu sikutaka kuja Ninewi pale mwanzoni. Sasa baada ya yote yaliyonipata, kutia ndani hofu kuu na kutwezwa kwa kumezwa na samaki mkubwa, na baada ya kufanya kazi ngumu ya kuwaonya Waninewi juu ya kukaribia kwa uharibifu, haya ndiyo matokeo! Kazi yangu na mateso yangu yote yalikuwa ya bure! Afadhali ningekuwa mfu!’—Yona 4:1-3.

      12. Twaweza kujifunza nini kutokana na lililompata Yona?

      12 Je, Yona alikuwa na sababu halali ya kulalamika? Je, Yehova alikosa uadilifu kwa kuwaonyesha rehema wakosaji wenye kutubu? Kwa kweli, Yona angepaswa kufurahi; watu makumi ya maelfu wangeepushwa na kifo! (Yona 4:11) Lakini mtazamo wake wa kulalamika usiokuwa na staha, ulionyesha kwamba hakuwa akitumaini uadilifu wa Yehova. Alikuwa akijifikiria kupita kiasi na kufikiria wengine kidogo tu. Acheni tujifunze kutokana na Yona kwa kutotanguliza hisia zetu binafsi. Acheni tusadiki kwamba kumtii Yehova, kwa kufuata mwongozo utolewao kupitia tengenezo lake na kukubali maamuzi yake, ndilo jambo lifaalo kufanya. Twasadiki kwamba “itakuwa heri kwao wamchao Mungu.”—Mhubiri 8:12.

      Sasa Ndio Wakati wa Kuimarisha Tumaini Letu!

      13. Sote twaweza kuimarishaje tumaini letu katika Yehova?

      13 Kuimarisha tumaini letu katika Yehova ndio mwendo wa hekima. (Mithali 3:5-8) Bila shaka, twapaswa kufanya mengi zaidi ya kusali kwa Yehova ili atusaidie tuwe na tumaini zaidi. Tumaini hukua likitegemezwa juu ya ujuzi sahihi, kwa hiyo, twapaswa kufanya funzo la Biblia la kibinafsi, kusoma Biblia na pia fasihi inayofafanua Biblia, kuwa kawaida yetu ya kila siku. Ni muhimu kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na vilevile kutayarisha vizuri na kushiriki kadiri iwezekanavyo. Kuzoea kushiriki kweli za Biblia na wengine, tukishinda vipingamizi kwa busara, pia huongeza kina cha tumaini letu katika Yehova na Neno lake. Hivyo tunajihusisha naye zaidi kila siku.

      14. Kwa nini karibuni watu wa Mungu watahitajika kuonyesha tumaini lao katika Yehova zaidi ya wakati mwingine wowote?

      14 Wakati ujao ulio karibu, wakati wa dhiki kubwa zaidi ambayo haijawahi kukumba jamii ya kibinadamu utafyatuka ghafula. (Mathayo 24:21) Ufyatukapo, watumishi wa Mungu watahitaji kuonyesha tumaini katika uadilifu wa Yehova na mwongozo utolewao na tengenezo lake zaidi ya wakati mwingine wowote. Kisha kwa njia ya ufananisho, watatii kwa tumaini amri hii ya Mungu: “Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako, ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita.” (Isaya 26:20) Tayari wameingia katika mazingira yenye ulinzi ya makutaniko zaidi ya 85,000 katika nchi 232. Lolote ambalo huenda likatiwa ndani ya amri “ingia wewe ndani ya vyumba vyako,” twaweza kutumaini kwamba Yehova atatusaidia kulitimiza.

      15. Tumaini limekaziwaje katika mwaka wa 1998, na kwa nini hilo lafaa?

      15 Ni lazima tuimarishe tumaini letu sasa. Tukikosa kuwatumaini ndugu zetu Wakristo, tengenezo la Yehova na, zaidi ya yote, Yehova mwenyewe, kuokoka hakutawezekana. Kwa hiyo ni jambo lifaalo kama nini kwamba, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wamekumbushwa tena na tena na maneno ya andiko lao la mwaka wa 1998 kwamba, “kila mtu aitiaye jina la Yehova ataokolewa”! (Waroma 10:13) Kuhusu hilo yatupasa tuendelee kuwa na tumaini. Tukigundua hata kiwango kidogo cha ukosefu wa uhakika katika tumaini hilo, twapaswa kujitahidi kuurekebisha sasa, naam, leo.

      Hukumu ya Yehova Itakuwa Yenye Uadilifu

      16. Tumaini laweza kupatwa na nini ikiwa halikuzwi, na twaweza kuzuiaje isitukie hivyo?

      16 Kwenye Waebrania 3:14, Wakristo watiwa-mafuta wameonywa hivi: “Sisi kwa kweli twawa washiriki wa Kristo ikiwa tu twaushikilia sana uhakika tuliokuwa nao mwanzoni kwa imara hadi mwisho.” Kimsingi, maneno hayo pia hutumika kuwahusu Wakristo wenye tumaini la kidunia. Lile tumaini la kwanza laweza kumomonyoka lisipokuzwa. Ni muhimu kama nini kuendelea kufuatia ujuzi sahihi, hivyo tukiimarisha msingi ambao juu yake tumaini letu limetegemezwa!

      17. Kuhusu kuokoka, kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu ataamua mambo kwa usahihi?

      17 Karibuni mataifa yote yatachunguzwa na Kristo ili aweze “[ku]tenganisha watu mmoja na mwenzake, kama vile mchungaji atenganishavyo kondoo na mbuzi.” (Mathayo 25:31-33) Tunaweza kutumaini kwamba Kristo atakuwa mwenye uadilifu katika kuamua anayestahili kuokoka. Yehova amempa hekima, ufahamu wenye kina, na sifa nyinginezo za lazima ‘ili aihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa.’ (Matendo 17:30, 31) Acheni usadikisho wetu uwe kama ule wa Abrahamu, aliyesema hivi: “Hasha usifanye hivyo [Yehova], ukamwue mwenye haki pamoja na mwovu, mwenye haki awe kama mwovu. Hasha; Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?”—Mwanzo 18:25.

      18. Kwa nini hatupaswi kuhangaikia kupita kiasi yale ambayo huenda tusijue wakati wa sasa?

      18 Tukitumaini kabisa uadilifu wa Yehova, hatupaswi kuwa na wasiwasi juu ya kujibiwa maswali kama: ‘Watoto watahukumiwaje? Huenda ikawa kwamba habari njema haitakuwa imefikia idadi kubwa ya watu Har–Magedoni ifikapo? Namna gani wale wenye ugonjwa wa akili? Namna gani . . . . ?’ Ni kweli kwamba huenda wakati wa sasa tusijue jinsi ambavyo Yehova atatatua masuala hayo. Hata hivyo, atafanya hivyo katika njia ya uadilifu na rehema. Hatupaswi kamwe kushuku hilo. Kwa kweli, huenda tukashangaa na kufurahi kuona akiyatatua masuala hayo katika njia ambayo hata hatukuifikiria kamwe.—Linganisha Ayubu 42:3; Zaburi 78:11-16; 136:4-9; Mathayo 15:31; Luka 2:47.

      19, 20. (a) Kwa nini si vibaya kuuliza maswali yenye kupatana na akili? (b) Yehova atatoa lini majibu yahitajiwayo?

      19 Tengenezo la Yehova halivunji moyo kuuliza maswali yafaayo ya moyo mweupe, kama ambavyo wapinzani fulani hudai kimakosa. (1 Petro 1:10-12) Hata hivyo, Biblia hutushauri tuepuke maswali ya kipumbavu, yenye kudadisi. (Tito 3:9) Kuuliza maswali yenye kupatana na akili na kutafuta majibu ya Kimaandiko katika Neno la Mungu na vichapo vya Kikristo, kwaweza kuongeza ujuzi wetu sahihi na hivyo kuliimarisha tumaini letu katika Yehova. Tengenezo hufuata kielelezo cha Yesu. Alijiepusha na kutoa maelezo juu ya maswali ambayo wakati ufaao wa kuyajibu haukuwa umefika. Alieleza hivi: “Bado nina mambo mengi ya kuwaambia nyinyi, lakini hamwezi kuyahimili wakati wa sasa.” (Yohana 16:12) Pia alikiri kwamba kuna mambo fulani ambayo yeye mwenyewe hakuyajua wakati huo.—Mathayo 24:36.

      20 Yehova bado ana mengi ya kufunua. Ni jambo la hekima kama nini kumngojea, tukitumaini kwamba Mungu atafunua makusudi yake wakati ufaao. Twaweza kutumaini kwamba mara wakati wa Yehova ufaao ufikapo, tutafurahi kupata ufahamu wenye kina wa ziada juu ya njia zake. Naam, tutathawabishwa, mradi tu tunadhihirisha tumaini kamili katika Yehova na tengenezo analotumia. Andiko la Mithali 14:26 latuhakikishia hivi: “Kumcha BWANA ni tumaini imara; watoto wake watakuwa na kimbilio.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki