Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mbona Kuna Tatizo la Ukosefu wa Tumaini?
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Agosti 15
    • Mbona Kuna Tatizo la Ukosefu wa Tumaini?

      ‘JE, UNAWEZA kwa kweli kutumaini yeyote siku hizi?’ Huenda ukawa umemsikia mtu fulani aliyevunjika moyo akiuliza swali hilo. Au huenda hata ukawa ulijiuliza swali hilo uliposumbuliwa sana kihisia-moyo na jambo fulani lililokupata maishani mwako.

      Bila shaka, ulimwenguni pote kuna ukosefu wa tumaini katika mashirika na katika watu wengine. Mara nyingi, ukosefu huo wa tumaini ni halali. Je, kuna yeyote kwa kweli awezaye kutarajia wanasiasa watimize ahadi walizotoa kabla ya kuchaguliwa? Uchunguzi wa mwaka wa 1990 wa wanafunzi 1,000 huko Ujerumani ulionyesha kwamba asilimia 16.5 ya wanafunzi walitumaini kwamba wanasiasa wangeweza kutatua matatizo ya ulimwengu, ilhali wanafunzi asimilia 33 walikuwa na shaka kubwa. Wengi walisema kwamba walikosa tumaini katika uwezo wa wanasiasa wa kutatua matatizo na pia katika utayari wao wa kufanya hivyo.

      Gazeti la habari la Stuttgarter Nachrichten lililalamika hivi: “Wanasiasa walio wengi hutanguliza masilahi yao wenyewe, kisha ikiwezekana tu, yale ya waliowapigia kura.” Watu wa nchi nyinginezo hukubaliana na hilo. Gazeti la habari la The European lilisema hivi juu ya nchi moja: “Madharau ya vijana na pia wazee kuelekea wanasiasa, yana msingi mzuri.” Lilisema kwamba ‘kwa kawaida wapiga-kura huviondoa madarakani vyama vya kisiasa.’ Gazeti la habari hilo liliendelea kusema hivi: “Yeyote anayetumia wakati miongoni mwa vijana [huko] hutambua mara moja kukosa kwao tumaini na kuhisi kuwa wametengwa.” Hata hivyo, serikali ya kidemokrasi haiwezi kuwa na mafanikio makubwa ikikosa kutumainiwa na umma. Wakati mmoja, John F. Kennedy, Rais wa zamani wa Marekani alisema hivi: “Kutumainiwa na umma ndio msingi wa serikali yenye matokeo.”

      Kuhusiana na tumaini katika nyanja za kifedha, hali ambazo kwa ghafula hubadilika kuwa mbaya na mipango isiyofanikiwa ya kupata utajiri haraka-haraka, imefanya wengi wasitesite. Masoko ya hisa yalipopanda na kushuka bila kuzuilika katika Oktoba 1997, gazeti la habari fulani lilizungumza kuhusu “ukosefu mwingi wa tumaini ambao nyakati nyingine haupatani na akili,” na pia juu ya “uenezaji wa ukosefu huo wa tumaini.” Lilisema pia kwamba ‘tumaini limefifia sana [katika nchi moja ya Asia] hivi kwamba hali hiyo yatishia kule kuwepo kwa serikali.’ Kifupi, gazeti la habari hilo lilitaarifu jambo hili lililo dhahiri: “Uchumi mbalimbali hutegemea tumaini.”

      Dini pia inashindwa kuchochea watu kuwa na tumaini. Kwa kusikitisha, jarida la kidini la Ujerumani liitwalo Christ in der Gegenwart, laeleza hivi: “Kiwango cha tumaini ambacho watu wa kawaida wanalo katika Kanisa chaendelea kushuka.” Kati ya mwaka wa 1986 na 1992, idadi ya Wajerumani wenye kiwango kikubwa, au angalau kiwango fulani cha tumaini katika kanisa, ilishuka kutoka asilimia 40 hadi asilimia 33. Kwa kweli, katika Ujerumani Mashariki ya zamani, idadi hiyo ilishuka hadi chini ya asilimia 20. Kwa upande mwingine, watu waliokuwa na tumaini ndogo au bila tumaini lolote katika kanisa, waliongezeka kutoka asilimia 56 hadi asilimia 66 katika Ujerumani Magharibi ya zamani, na kuongezeka hadi asimilia 71 katika Ujerumani Mashariki ya zamani.

      Kushuka kwa tumaini kumekuwa dhahiri katika nyanja nyinginezo mbali na za siasa, uchumi, na dini—nguzo tatu za jamii ya kibinadamu. Utekelezaji wa sheria ni kielelezo kingine. Njia za kuepa mifumo ya sheria ya uhalifu, matatizo katika kutekeleza sheria kwa haki, na maamuzi ya mahakama yenye kutilika shaka, yamedhoofisha vibaya tumaini la watu. Kulingana gazeti la Time, “kukatishwa tamaa kwa raia na kwa polisi kumefikia kiwango cha kutokuwa na tumaini lolote na mfumo ambao huwaachilia wahalifu hatari kutoka gerezani baada ya muda mfupi tu.” Hata kuwatumaini polisi kumeshuka kwa sababu wameshutumiwa kuwa wafisadi na wakatili.

      Kuhusiana na siasa za kimataifa, mazungumzo ya amani yasiyofanikiwa na kuvunjika kwa usimamishaji mapigano, hudhihirisha ukosefu wa tumaini. Bill Richardson, balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, alionyesha wazi kikwazo kikuu cha kupatikana kwa amani katika Mashariki ya Kati, akisema tu hivi: “Kuna ukosefu wa tumaini.”

      Wakati uleule, watu binafsi walio wengi hukosa tumaini hata katika watu wa jamaa na marafiki wa karibu, watu hasa ambao wanadamu huwaendea ili kupata msaada na faraja wanapokuwa na matatizo. Hali hiyo ni sawa na ile iliyofafanuliwa na nabii Mwebrania Mika: “Msimwamini rafiki, msimwekee kiongozi tumaini; ilinde milango ya midomo ya kinywa chako ili mkeo alalaye kifuani mwako asijue habari.”—Mika 7:5.

      Ishara ya Nyakati

      Hivi majuzi mwanasaikolojia Mjerumani aitwaye Arthur Fischer, alinukuliwa akisema hivi: “Tumaini katika maendeleo ya jamii na katika wakati ujao wa mtu binafsi, kwa kweli limeshuka kwa kutazamisha katika nyanja zote. Vijana hushuku kama mashirika ya jamii yanaweza kuwasaidia. Hawana tumaini kamwe, liwe la kisiasa, kidini, au katika shirika jingine lolote.” Si ajabu kwamba mwanasoshiolojia aitwaye Ulrich Beck huzungumzia “utamaduni wa shaka” kuelekea mamlaka za muda mrefu, mashirika, na wataalamu.

      Katika utamaduni kama huo, watu huwa na maelekeo ya kujitenga, kukataa mamlaka yote, na kuishi kulingana na viwango vyao binafsi, wakifanya maamuzi yasiyotegemea shauri au mwongozo kutoka kwa wengine. Wengine huwa wenye shaka kupita kiasi, labda hata kukosa ufikirio, wanaposhughulika na wale wasioweza kuwatumaini tena. Mtazamo huo hukuza hali hatari, kama ile iliyofafanuliwa katika Biblia: “Katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu, wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo.” (2 Timotheo 3:1-5; Mithali 18:1) Kwa kweli, tatizo la siku hizi la ukosefu wa tumaini ni ishara ya nyakati, ishara ya “siku za mwisho.”

      Kwa hakika, maisha hayawezi kufurahiwa kikamili katika ulimwengu unaosumbuliwa na tatizo la ukosefu wa tumaini na uliojaa watu kama wale waliofafanuliwa hapo juu. Lakini inawezekana kufikiri kwamba mambo yatabadilika? Je, tatizo la siku hizi la ukosefu wa tumaini linaweza kushindwa? Ikiwa ndivyo, ni lini na jinsi gani?

  • Tumaini Laweza Kupatikana Tena!
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Agosti 15
    • Tumaini Laweza Kupatikana Tena!

      IJAPOKUWA tatizo la sasa la ukosefu wa tumaini ni ishara ya “siku za mwisho,” ukosefu wa tumaini pia ulidhihirika maelfu ya miaka iliyopita. (2 Timotheo 3:1) Ulitokea mara ya kwanza katika paradiso, mahali ambapo hapakutarajiwa kabisa utokee. Biblia husema hivi juu ya mahali hapo: “BWANA Mungu akapanda bustani upande wa mashariki wa Edeni, akamweka ndani yake huyo mtu aliyemfanya. BWANA Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa; na mti wa uzima katikati ya bustani, na mti wa ujuzi wa mema na mabaya.”—Mwanzo 2:8, 9.

      Mistari inayofuata yafafanua jinsi jambo hilo linavyohusiana na tatizo la siku ya kisasa la ukosefu wa tumaini. Twasoma hivi: “BWANA Mungu akamwagiza huyo mtu, akisema, Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Je, Adamu alikuwa na sababu ya kushuku yale aliyosema Yehova?

      Twaendelea kusoma hivi: “Basi nyoka alikuwa mwerevu kuliko wanyama wote wa mwitu aliowafanya BWANA Mungu. Akamwambia mwanamke, Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani? Mwanamke akamwambia nyoka, Matunda ya miti ya bustanini twaweza kula; lakini matunda ya mti ulio katikati ya bustani Mungu amesema, Msiyale wala msiyaguse, msije mkafa. Nyoka akamwambia mwanamke, Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya. Mwanamke alipoona ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa, basi alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala.”—Mwanzo 3:1-6.

      Kwa kupuuza onyo la Mungu lililokuwa wazi, Adamu na Hawa walionyesha ukosefu wa tumaini katika Yehova. Walionyesha sifa za Shetani, mpinzani wa Mungu aliyekuwa amezungumza na Hawa kupitia nyoka halisi. Shetani alikosa tumaini katika njia ya Yehova ya kutawala. Kwa sababu hiyo na kwa kuwa na moyo wenye kiburi uliotamani makuu, Shetani aliasi Mungu na kuwaongoza wanadamu vibaya wafanye hivyohivyo. Aliwashawishi wafikiri kwamba Mungu hakupaswa kutumainiwa.

      Matokeo Yalikuwaje? Mahusiano Yenye Shida

      Huenda ukawa umeona kwamba watu wasiowatumaini wengine huliona kuwa jambo gumu kudumisha urafiki. Publilius Syrus, mwandishi wa Kilatini wa karne ya kwanza K.W.K., aliandika hivi: “Tumaini ndilo kifungo cha pekee cha urafiki.” Kwa kuasi, Adamu na Hawa walionyesha kutomtumaini Mungu. Kwa sababu hiyo, bila shaka Mungu hakuwa na sababu ya kuwatumaini. Kama tokeo la kuvunjika kwa tumaini, wanadamu wa kwanza walipoteza urafiki wa Mungu. Hakuna chochote kionyeshacho kwamba Yehova alizungumza nao tena kamwe baada ya kuwahukumia adhabu kwa sababu ya uasi wao.

      Uhusiano baina ya Adamu na Hawa ulipatwa na madhara pia. Yehova alimwonya Hawa: “Kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala.” (Mwanzo 3:16, italiki ni zetu.) Biblia ya The Jerusalem Bible husema: “Atapiga ubwana juu yako.” Badala ya kutumia ukichwa kwa upendo juu ya mke wake, kama vile Mungu alivyotaka, sasa Adamu akawa bwana wake, akipiga ubwana juu yake.

      Baada ya kufanya dhambi, Adamu alijaribu kumlaumu mke wake. Kwa maoni yake, yale Hawa aliyokuwa amefanya ndiyo yaliyosababisha kufukuzwa kwao kutoka katika bustani kamilifu na kuingia katika dunia isiyo kamilifu, wakiwa wamehukumiwa kufanya kazi kama watumwa chini ya hali zisizo kamilifu kabla ya kurudi mavumbini. (Mwanzo 3:17-19) Basi tunaweza kuwazia kwamba jambo hilo lilitokeza kutopatana baina yao. Huenda Adamu akawa alitenda kwa kupita kiasi, akisema kwamba hangemsikiliza Hawa tena kamwe. Labda alihisi kwa kweli alikuwa na sababu halali ya kumwambia, ‘Kuanzia sasa na kuendelea, mimi ndiye mwenye mamlaka!’ Kwa upande mwingine, huenda Hawa akawa aliona kwamba Adamu alikuwa ameshindwa na daraka lake akiwa kichwa cha familia, akimfanya akose kumtumaini. Kwa vyovyote, kwa kutomtumaini Mungu, wanadamu walipoteza urafiki wao naye na kuharibu uhusiano kati yao wenyewe.

      Twaweza Kumtumaini Nani?

      Kama vile kielelezo cha Adamu na Hawa kionyeshavyo, si kila mtu astahiliye kutumainiwa. Twaweza kujuaje wale wastahilio kutumainiwa na wale wasiostahili?

      Andiko la Zaburi 146:3 latushauri hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” Na kwenye Yeremia 17:5-7, twasoma hivi: ‘Amelaaniwa mtu yule amtumainiye mwanadamu, amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake na moyoni mwake amemwacha BWANA.’ Kwa upande mwingine, “amebarikiwa mtu yule anayemtegemea BWANA, ambaye BWANA ni tumaini lake.”

      Ni kweli kwamba, si kosa sikuzote kuwatumaini wanadamu. Maandiko hayo yanatoa hoja kwamba kumtumaini Mungu kwafaa kabisa, lakini nyakati nyingine kuwatumaini wanadamu wasio wakamilifu kwaweza kutokeza msiba. Kwa kielelezo, watu ambao huwatumaini wanadamu watimize yale ambayo Mungu pekee ndiye awezaye kutimiza—kutoa wokovu na kuleta amani na usalama kamili—wanaelekea kukatishwa tamaa.—Zaburi 46:9; 1 Wathesalonike 5:3.

      Kwa kweli, wanadamu na mashirika ya kibinadamu yanastahili kutumainiwa tu kwa kadiri wanadamu hao na mashirika hayo hutenda kupatana na makusudi ya Mungu na kudhihirisha kanuni za kimungu. Hivyo, ikiwa tutawachochea wengine watutumaini, ni lazima tuseme kweli, tukiwa wanyofu na wenye kutegemeka. (Mithali 12:19; Waefeso 4:25; Waebrania 13:18) Ni kwa kujiendesha kwa kupatana na kanuni za Biblia tu ndipo wengine watakuwa na sababu halali ya kututumaini na pia kuthibitika kuwa chanzo cha nguvu na kitia-moyo kwa mmoja na mwenzake.

      Kurudisha Tumaini

      Mashahidi wa Yehova wana msingi thabiti wa kumtumaini Mungu na kuwatia wengine moyo wafanye hivyohivyo. Yehova ni mwaminifu na mwenye uaminifu-mshikamanifu, yeye ambaye sikuzote aweza kutegemeka afanye yale ambayo amesema, kwa sababu “haiwezekani Mungu kusema uwongo.” Kumtumaini Mungu wa upendo hakutaongoza kamwe kwenye kukatishwa tamaa.—Waebrania 6:18; Zaburi 94:14; Isaya 46:9-11; 1 Yohana 4:8.

      Watu ambao wameunganishwa na tumaini lao katika Yehova na wanaoishi kwa kutegemea kanuni zake wamechochewa kabisa kutumainiana. Katika ulimwengu unaosumbuliwa na tatizo la ukosefu wa tumaini, ni furaha iliyoje kupata watu wanaotumainika! Ebu wazia jinsi ambavyo ulimwengu ungekuwa kama tungeweza kutumaini kabisa yale ambayo kila mtu mwingine husema au kufanya! Katika ulimwengu mpya unaokuja ambao Mungu ameahidi, hali itakuwa hivyo. Hakutakuwa kamwe tatizo lolote la ukosefu wa tumaini!

      Je, ungetaka kuishi wakati huo? Ikiwa ndivyo, Mashahidi wa Yehova wanakualika uimarishe tumaini lako katika Mungu na ahadi zake kwa kujifunza mengi kuhusu anayokutaka ufanye maishani. Funzo la Biblia hutoa uthibitisho kwamba Mungu yuko na kwamba yeye anapendezwa na hali njema ya wanadamu, na kwamba karibuni atachukua hatua ya kusahihisha matatizo ya ulimwengu kupitia Ufalme wake. Mamilioni ya watu wamejifunza kumtumaini Mungu na Neno lake, Biblia. Kwa furaha Mashahidi wa Yehova watakufafanulia utumishi wautoleao watu wote kupitia mtaala wa funzo la Biblia bila malipo. Au uandikie wachapishaji wa gazeti hili ili upate habari zaidi.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki