Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Wafu Watafufuliwa”
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
    • Hata hivyo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Msiwe na hofu, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa nyinyi ufalme.” (Luka 12:32) Ufalme wa Mungu ni wa kimbingu. Kwa sababu hiyo, ahadi hiyo humaanisha kwamba “kundi dogo” lingepaswa kuwa mbinguni pamoja na Yesu likiwa viumbe wa roho. (Yohana 14:2, 3; 1 Petro 1:3, 4) Ni tazamio lenye utukufu kama nini! Yesu alizidi kumfunulia mtume Yohana kwamba, idadi ya ‘kundi hilo dogo’ ingekuwa watu 144,000 tu.—Ufunuo 14:1.

      4 Ingawa hivyo, hao 144,000 wangeingiaje katika utukufu wa kimbingu? Yesu “ametoa nuru juu ya uhai na kutoharibika kupitia habari njema.” Kwa kutumia damu yake, alianzisha “njia mpya na yenye uhai” ya kuingia mbinguni. (2 Timotheo 1:10; Waebrania 10:19, 20) Kwanza, alikufa, kama vile Biblia ilivyotabiri angefanya. (Isaya 53:12) Kisha, kama vile mtume Petro alivyotangaza, “Yesu huyu Mungu alimfufua.” (Matendo 2:32) Ingawa hivyo, Yesu hakufufuliwa akiwa binadamu. Alikuwa amesema hivi: “Mkate ambao nitatoa ni mwili wangu kwa ajili ya uhai wa ulimwengu.” (Yohana 6:51) Kuuchukua mwili wake tena kungebatilisha dhabihu hiyo. Hivyo Yesu ‘aliuawa katika mwili wenye nyama, lakini akafanywa kuwa hai katika roho.’ (1 Petro 3:18) Hivyo Yesu “[ali]pata ukombozi udumuo milele kwa ajili yetu,” yaani “kundi dogo.” (Waebrania 9:12) Alimtolea Mungu thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ukiwa fidia kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi, na wale 144,000 ndio waliokuwa wa kwanza kunufaika na fidia hiyo.

      5. Wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza walitolewa tumaini gani?

      5 Si Yesu pekee ambaye angefufuliwa kwenye uhai wa kimbingu. Paulo aliwaambia Wakristo wenzake katika Roma kwamba walikuwa wametiwa mafuta kwa roho wawe wana wa Mungu na warithi-washirika pamoja na Kristo ikiwa wangethibitisha kutiwa mafuta kwao kwa kuvumilia mpaka mwisho. (Waroma 8:16, 17) Paulo pia alieleza hivi: “Ikiwa tumekuwa wenye kuungana pamoja naye katika ufanani wa kifo chake, hakika sisi pia tutaunganishwa pamoja naye katika ufanani wa ufufuo wake.”—Waroma 6:5.

      Kutetea Tumaini la Ufufuo

      6. Kwa nini imani katika ufufuo ilishambuliwa katika Korintho, na mtume Paulo aliitikiaje?

      6 Ufufuo ni sehemu ya “fundisho la msingi” la Ukristo. (Waebrania 6:1, 2) Hata hivyo, fundisho hilo lilikuwa likishambuliwa huko Korintho. Watu fulani katika kutaniko, waliokuwa kwa wazi wameathiriwa na falsafa za Kigiriki, walikuwa wakisema hivi: “Hakuna ufufuo wa wafu.” (1 Wakorintho 15:12) Wakati ripoti za usemi huo zilipomfikia mtume Paulo, alitetea tumaini la ufufuo, hasa tumaini la Wakristo watiwa-mafuta. Acheni tuchunguze maneno ya Paulo kama yalivyorekodiwa katika 1 Wakorintho sura ya 15. Litakuwa jambo lenye kusaidia ukiwa umesoma hiyo sura yote, kama ambavyo ilipendekezwa katika makala iliyotangulia.

      7. (a) Ni suala gani kuu ambalo Paulo alikazia? (b) Ni nani waliomwona Yesu aliyekuwa amefufuliwa?

      7 Katika mistari ya kwanza miwili ya 1 Wakorintho sura ya 15, Paulo ataja kichwa cha mazungumzo yake: “Nawajulisha nyinyi, akina ndugu, habari njema niliyowatangazia, mliyoipokea pia, ambayo katika hiyo mwasimama pia, ambayo kupitia hiyo nyinyi pia mnaokolewa, . . . isipokuwa, kwa kweli, mwe mlipata kuwa waamini bila kusudi lolote.” Wakorintho walikuwa wameipokea kweli bure, ikiwa walishindwa kusimama imara katika habari njema. Paulo aliendelea kusema hivi: “Niliwapa nyinyi, miongoni mwa mambo ya kwanza, lile nililolipokea pia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba amefufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko; na kwamba alionekana kwa Kefa, kisha kwa wale kumi na wawili. Baada ya hilo alionekana kwa zaidi ya ndugu mia tano kwa wakati mmoja, ambao walio wengi kati yao wabaki hadi wakati wa sasa, lakini baadhi yao wamelala usingizi katika kifo. Baada ya hilo alionekana kwa Yakobo, kisha kwa mitume wote; lakini mwisho wa wote alionekana pia kwangu kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati wake.”—1 Wakorintho 15:3-8.

      8, 9. (a) Itikadi katika ufufuo ni ya maana kadiri gani? (b) Yaelekea ni wakati gani Yesu alionekana kwa “zaidi ya ndugu mia tano”?

      8 Kwa waliokuwa wamepokea habari njema, imani katika ufufuo wa Yesu halikuwa jambo la kuchagua. Kulikuwa na mashahidi wengi waliojionea kwa macho waliothibitisha kwamba “Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu” na kwamba alikuwa amefufuliwa. Mmoja wao alikuwa Kefa, au Petro, jina linalojulikana zaidi. Baada ya Petro kumkataa Yesu usiku wa kusalitiwa na kukamatwa kwa Yesu, lazima awe alifarijiwa sana kumwona Yesu. Pia Yesu aliyekuwa amefufuliwa aliwatembelea “wale kumi na wawili,” yaani wale mitume wakiwa kikundi—jambo lililoonwa ambalo bila shaka liliwasaidia kushinda hofu yao na kuwa mashahidi wajasiri wa ufufuo wa Yesu.—Yohana 20:19-23; Matendo 2:32.

      9 Kristo pia alionekana kwa kikundi kikubwa zaidi, “ndugu zaidi ya mia tano.” Kwa kuwa ni katika Galilaya tu alikokuwa na idadi kubwa hivyo ya wafuasi, huenda huo ukawa ni ule wakati ambao umeelezwa kwenye Mathayo 28:16-20, Yesu alipotoa amri ya kufanya wanafunzi. Hao watu wangeweza kutoa ushuhuda wenye nguvu kama nini! Baadhi yao walikuwa bado hai mwaka wa 55 W.K. wakati Paulo alipotunga barua yake ya kwanza kwa Wakorintho. Ingawa hivyo, ona kwamba wale waliokuwa wamekufa walitajwa kuwa “wamelala usingizi katika kifo.” Walikuwa bado hawajafufuliwa ili kupokea thawabu yao ya kimbingu.

      10. (a) Mkutano wa mwisho wa Yesu pamoja na wanafunzi wake ulikuwa na matokeo gani? (b) Yesu alionekanaje kwa Paulo “kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati”?

      10 Shahidi mwingine mwenye kutokeza wa ufufuo wa Yesu alikuwa Yakobo, mwana wa Yosefu na Maria, mama yake Yesu. Kabla ya huo ufufuo ni wazi kwamba Yakobo hakuwa amekuwa mwamini. (Yohana 7:5) Lakini baada ya Yesu kuonekana kwake, Yakobo akawa mwamini na labda akatimiza fungu fulani katika kugeuza imani ya ndugu zake. (Matendo 1:13, 14) Katika mkutano wake wa mwisho pamoja na wanafunzi wake, wakati alipopaa kwenda mbinguni, Yesu aliwapa utume wa ‘kuwa mashahidi wake hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.’ (Matendo 1:6-11) Baadaye, alionekana kwa Sauli wa Tarso, aliyekuwa mnyanyasaji wa Wakristo. (Matendo 22:6-8) Yesu alionekana kwa Sauli “kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati wake.” Ilikuwa kama kwamba Sauli alikuwa tayari amefufuliwa kwenye uhai wa roho na angeweza kumwona Bwana aliyetukuzwa, karne nyingi kabla ya ufufuo huo kutokea. Jambo hilo lilifanya Sauli aache mara moja upinzani wa hata kuua kimakusudi washiriki wa kutaniko la Kikristo na kufanya badiliko lenye kutokeza. (Matendo 9:3-9, 17-19) Sauli alipata kuwa mtume Paulo, mmojawapo wa watetezi mashuhuri wa imani ya Kikristo.—1 Wakorintho 15:9, 10.

      Imani Katika Ufufuo Ni Muhimu

      11. Paulo alifichuaje kosa la kusema kwamba “hakuna ufufuo”?

      11 Kwa hiyo kufufuliwa kwa Yesu kulikuwa jambo la hakika lililothibitishwa vizuri. “Sasa ikiwa Kristo anahubiriwa kwamba amefufuliwa kutoka kwa wafu,” Paulo atoa hoja, “ni jinsi gani wengine miongoni mwenu husema hakuna ufufuo wa wafu?” (1 Wakorintho 15:12) Watu hao hawakuwa na shaka za kibinafsi au maswali kuhusu ufufuo tu, bali pia walisema waziwazi kwamba hawauamini. Hivyo Paulo afichua kusababu kwao kwenye kosa. Alisema kwamba ikiwa Kristo hakufufuliwa, ule ujumbe wa Kikristo ulikuwa uwongo, na walioshuhudia kufufuliwa kwa Kristo walikuwa “mashahidi wasio wa kweli wa Mungu.” Ikiwa Kristo hakuwa amefufuliwa, Mungu hakuwa amelipwa fidia yoyote; Wakristo walikuwa ‘bado wamo katika dhambi zao.’ (1 Wakorintho 15:13-19; Waroma 3:23, 24; Waebrania 9:11-14) Na Wakristo waliokuwa “wamelala usingizi katika kifo” katika visa vingine wakiwa wafia-imani, walikuwa wameangamia bila tumaini la kweli. Wakristo wangekuwa katika hali yenye kusikitisha kama nini ikiwa uhai huu ndio tu wangeweza kutarajia! Kuteseka kwao kwote hakungekuwa na maana.

      12. (a) Ni nini linalodokezwa na kumwita Kristo “matunda ya kwanza katika wale wamelala usingizi katika kifo?” (b) Kristo alifanyaje ufufuo uwezekane?

      12 Hata hivyo, hali haikuwa hivyo. Paulo aendelea kusema hivi: “Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu.” Zaidi ya hayo, yeye ni “matunda ya kwanza kati ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” (1 Wakorintho 15:20) Yehova aliwabariki Waisraeli kwa mavuno makubwa, wakati ambapo walimpa kwa utii matunda ya kwanza ya mazao yao. (Kutoka 22:29, 30; 23:19; Mithali 3:9, 10) Kwa kumwita Kristo “matunda ya kwanza,” Paulo adokeza kwamba mavuno zaidi ya watu wangefufuliwa kutoka kwa wafu wakaishi mbinguni. “Kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu,” Paulo asema, “ufufuo wa wafu pia ni kupitia mwanadamu. Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, ndivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” (1 Wakorintho 15:21, 22) Yesu alifanya ufufuo uwezekane kwa kutoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ukiwa fidia, ikiwafungulia wanadamu njia watoke katika utumwa wa dhambi na kifo.—Wagalatia 1:4; 1 Petro 1:18, 19.a

      13. (a) Ufufuo wa kimbingu unatukia lini? (b) Inakuwaje kwamba watiwa-mafuta fulani ‘hawalali usingizi katika kifo’?

      13 Paulo aendelea kusema hivi: “Lakini kila mmoja katika daraja lake mwenyewe: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake.” (1 Wakorintho 15:23) Kristo alifufuliwa mwaka wa 33 W.K. Hata hivyo, wafuasi wake watiwa-mafuta—“wale walio wa Kristo”—wangelazimika kungoja hadi punde baada ya Yesu kuanza kuwapo kwake kwa kifalme, ambako unabii wa Biblia waonyesha kulitukia mwaka wa 1914. (1 Wathesalonike 4:14-16; Ufunuo 11:18) Namna gani wale ambao wangekuwa hai wakati wa kuwapo kwake? Paulo asema hivi: “Tazama! Nawaambia nyinyi siri takatifu: Hatutalala usingizi katika kifo sisi sote, bali sisi sote tutabadilishwa, kwa dakika, katika kupepeseka kwa jicho, wakati wa tarumbeta ya mwisho. Kwa maana hiyo tarumbeta itavuma, na wafu watafufuliwa wakiwa wasioharibika, nasi tutabadilishwa.” (1 Wakorintho 15:51, 52) Kwa wazi, si watiwa-mafuta wote ambao hulala kaburini wakingojea ufufuo. Wanaokufa wakati wa kuwapo kwa Kristo hugeuzwa umbo mara moja.—Ufunuo 14:13.

      14. Watiwa-mafuta ‘hubatizwaje kwa kusudi la kuwa wafu’?

      14 “Kama sivyo,” Paulo auliza, “watafanya nini wao wanaobatizwa kwa kusudi la kuwa wafu? Ikiwa wafu hawapaswi kufufuliwa hata kidogo, kwa nini pia wanabatizwa kwa kusudi la kuwa hivyo? Kwa nini sisi pia tumo hatarini kila saa?” (1 Wakorintho 15:29, 30) Paulo hakumaanisha kwamba watu waliokuwa hai walibatizwa kwa niaba ya wafu, kama vile tafsiri nyingine za Biblia hufanya jambo hilo lionekane. Hata hivyo, ubatizo wahusiana na uanafunzi wa Kikristo, na nafsi zilizokufa haziwezi kuwa wanafunzi. (Yohana 4:1) Badala yake, Paulo alikuwa akizungumza juu ya Wakristo waliokuwa hai, ambao wengi wao, kama Paulo mwenyewe, walikuwa “hatarini kila saa.” Wakristo watiwa-mafuta ‘walibatizwa katika kifo cha Kristo.’ (Waroma 6:3) Tangu walipotiwa mafuta, walikuwa ‘wakibatizwa’ kitamathali, na kuingia katika mwendo ambao ungewaongoza kwenye kifo kama kile cha Kristo. (Marko 10:35-40) Wangekufa wakiwa na tumaini la ufufuo mtukufu wa kimbingu.—1 Wakorintho 6:14; Wafilipi 3:10, 11.

      15. Huenda Paulo alipatwa na hatari gani, na imani katika ufufuo ilitimizaje fungu katika kuzivumilia?

      15 Paulo sasa aeleza kwamba yeye mwenyewe alikuwa amekabili hatari kiasi cha kuweza kusema hivi: “Kila siku nakabili kifo.” Ili wengine wasije wakamshtaki kuwa mwenye kutia chumvi, Paulo aongeza kusema hivi: “Hili nathibitisha kwa mchachawo nilio nao juu yenu, akina ndugu, katika Kristo Yesu Bwana wetu.” Biblia Habari Njema hutafsiri mstari huu hivi: “Ndugu, mimi ninakabili kifo kila siku! Fahari niliyo nayo juu yenu katika kuungana na Kristo Yesu Bwana wetu inanifanya nitangaze jambo hili.” Ukiwa mfano wa hatari alizokabili, katika mstari wa 32, Paulo asema juu ya ‘kupigana na mahayawani-mwitu katika Efeso.’ Mara nyingi Waroma walifisha wahalifu kwa kuwatupa kwa mahayawani-mwitu katika viwanja vya michezo. Ikiwa Paulo alivumilia pigano na mahayawani-mwitu halisi, angeweza kuwa aliokoka tu kwa msaada wa Yehova. Bila tumaini la ufufuo, kuchagua njia ya maisha iliyomweka katika hatari kama hiyo kwa kweli kungalikuwa kujihatarisha kipumbavu. Bila tumaini la uhai wa wakati ujao, kuvumilia shida na kujidhabihu kulikoambatana na kumtumikia Mungu hakungekuwa na maana. “Ikiwa wafu hawapaswi kufufuliwa,” Paulo asema, “‘acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa.’”—1 Wakorintho 15:31, 32; ona 2 Wakorintho 1:8, 9; 11:23-27.

      16. (a) Huenda usemi “acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa” ukawa umetokana na nini? (b) Ni zipi zilizokuwa hatari za kukubali maoni hayo?

      16 Huenda ikawa Paulo alinukuu andiko la Isaya 22:13, ambalo lafafanua mtazamo wa nadharia-ajali wa wakazi wa Yerusalemu wasiotii. Au huenda akawa alikuwa akifikiria yale Waepikurea waliyoamini, waliodharau tumaini lolote la uhai baada ya kifo na kuamini raha ya kimwili ndiyo iliyokuwa jambo lenye faida kubwa maishani. Kwa vyovyote vile, “tule na tunywe” ilikuwa falsafa ya kutomwogopa Mungu. Kwa sababu hiyo Paulo aonya hivi: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33) Kushirikiana na wale ambao walikataa ufufuo kungeweza kuwa jambo lenye sumu. Kushirikiana kama huko kulitimiza fungu fulani katika matatizo ambayo Paulo alikuwa ashughulikie katika kutaniko la Korintho, kama vile ukosefu wa adili katika ngono, migawanyiko, mashtaka ya kisheria, na kutostahi Mlo wa Jioni wa Bwana.—1 Wakorintho 1:11; 5:1; 6:1; 11:20-22.

      17. (a) Paulo aliwatolea Wakorintho onyo gani lenye upole? (b) Ni maswali gani yanayobaki kujibiwa?

      17 Hivyo Paulo awapa Wakorintho himizo hili lenye upole ambalo lafaa: “Amkeni mwe na utimamu wa akili katika njia ya uadilifu na msizoee dhambi, kwa maana wengine hawana ujuzi juu ya Mungu. Ninasema ili kuwasukuma mwone aibu.” (1 Wakorintho 15:34) Maoni yasiyofaa juu ya ufufuo yaliongoza wengine kuingia katika kuzubaa kiroho, kama kwamba walikuwa wamelewa. Walihitaji kuamka, kuwa timamu kiakili. Hivyohivyo, Wakristo watiwa-mafuta leo wanahitaji kuwa macho kiroho, bila kuathiriwa na maoni yenye kutilia shaka ya ulimwengu. Lazima washikamane kabisa na tumaini lao la ufufuo wa kimbingu. Lakini maswali bado yalibaki—kwa Wakorintho wakati huo na kwetu wakati wa sasa. Kwa kielelezo, wale 144,000 hufufuliwa kwenda mbinguni katika umbo gani? Na namna gani mamilioni ya wengine waliomo kaburini na ambao hawana tumaini la kimbingu? Ufufuo utamaanisha nini kwa watu kama hao? Katika makala yetu inayofuata, tutachunguza mazungumzo ya Paulo yanayobaki juu ya ufufuo.

  • “Kifo Kitafanywa Kuwa Si Kitu”
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
    • “Kifo Kitafanywa Kuwa Si Kitu”

      “Kikiwa ni adui wa mwisho, kifo kitafanywa kuwa si kitu.” —1 WAKORINTHO 15:26.

      1, 2. (a) Mtume Paulo aliwatolea wafu tumaini gani? (b) Paulo alizungumzia swali gani kuhusu ufufuo?

      “NINAAMINI katika . . . ufufuo wa mwili, na uhai udumuo milele.” Hivyo ndivyo isemavyo ile taarifa ya itikadi iitwayo Imani ya Mitume. Wakatoliki na vilevile Waprotestanti huikariri kwa utiifu, wasing’amue kwamba mambo wanayoamini yafanana zaidi na falsafa za Kigiriki kuliko chochote kile ambacho mitume waliwahi kuamini. Hata hivyo, mtume Paulo alikataa falsafa ya Kigiriki na hakuamini kwamba nafsi haiwezi kufa. Hata hivyo, aliamini kwa dhati kuwako kwa uhai wakati ujao na kupuliziwa kuandika hivi: “Kikiwa ni adui wa mwisho, kifo kitafanywa kuwa si kitu.” (1 Wakorintho 15:26) Hilo lamaanisha nini hasa kwa wanadamu wanaokufa?

      2 Kwa kujibu, acheni turudi kwenye mazungumzo ya Paulo juu ya ufufuo yaliyorekodiwa katika 1 Wakorintho sura 15. Utakumbuka kwamba katika mistari ya kufungua, Paulo alithibitisha ufufuo kuwa sehemu muhimu ya fundisho la Kikristo. Sasa anazungumzia swali mahususi: “Hata hivyo, mtu fulani atasema: ‘Wafu watafufuliwaje? Ndiyo, wanakuja wakiwa na mwili wa namna gani?’”—1 Wakorintho 15:35.

      Mwili wa Aina Gani?

      3. Kwa nini watu fulani waliukataa ufufuo?

      3 Kwa kuzusha swali hilo, huenda Paulo akawa alinuia kukinza uvutano wa falsafa ya Plato. Plato alifundisha kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa ambayo hubaki hai baada ya mwili kufa. Wale waliokua wakiwa na wazo kama hilo, bila shaka fundisho la Kikristo la ufufuo halikuonekana kuwa jambo la lazima. Ikiwa nafsi iliendelea kuwa hai baada ya kifo, ufufuo una maana gani? Na zaidi, yaelekea ufufuo ulionekana kuwa jambo lisilo la akili. Mwili unapooza na kuwa mavumbi, kunaweza kuwaje na ufufuo? Mwelezaji wa Biblia, Heinrich Meyer, asema kwamba ugomvi wa Wakorintho fulani labda ulitegemea “msingi wa falsafa ya kwamba, lilikuwa jambo lisilowezekana kurudisha vitu vinavyoufanyiza mwili.”

      4, 5. (a) Kwa nini vipingamizi vya wasio na imani vilikuwa mambo yasiyo ya akili? (b) Eleza kielezi cha Paulo cha “punje tupu.” (c) Mungu huwapa watiwa-mafuta wenye kufufuliwa miili ya aina gani?

      4 Paulo afichua upumbavu wa kusababu kwao: “Wewe mtu asiye na akili! Kile upandacho hakifanywi kuwa hai isipokuwa kwanza kife; na kwa habari ya kile upandacho, wapanda, si mwili utakaositawi, bali punje tupu, huenda ikawa, ya ngano au yoyote moja kati ya zile nyingine; lakini Mungu huipa mwili kama vile imempendeza, na kwa kila moja ya hizo mbegu mwili wayo yenyewe.” (1 Wakorintho 15:36-38) Mungu hangefufua miili ambayo watu walikuwa nayo walipokuwa duniani. Badala yake, kungekuwa na mgeuzo umbo.

      5 Paulo alinganisha ufufuo na kumea kwa mbegu. Mbegu ndogo ya ngano huwa haifanani kwa vyovyote na mmea utakaoota kutoka kwake. Kichapo The World Book Encyclopedia chasema hivi: “Mbegu ianzapo kuota, hufyoza maji mengi sana. Hayo maji husababisha mabadiliko mengi ya kemikali ndani ya hiyo mbegu. Pia husababisha sehemu ya ndani ya mbegu kuvimba na kupasua ngozi ya nje ya mbegu.” Kwa kweli hiyo mbegu hufa ikiwa mbegu na kuwa mmea unaoibuka. “Mungu huipa mwili” kwa kuwa alizipanga sheria za kisayansi zinazoongoza kusitawi kwake, na kila mbegu hupokea mwili kulingana na aina yake. (Mwanzo 1:11) Vivyo hivyo, Wakristo watiwa-mafuta kwanza hufa wakiwa binadamu. Kisha, kwenye wakati wa Mungu uliowekwa, yeye huwafufua katika miili mipya kabisa. Kama vile Paulo alivyowaambia Wafilipi, “Yesu Kristo . . . ataufanya upya mwili wetu uliotwezwa ili upatanishwe na umbo la mwili wake wenye utukufu.” (Wafilipi 3:20, 21; 2 Wakorintho 5:1, 2) Wao hufufuliwa katika miili ya roho na huishi katika makao ya roho.—1 Yohana 3:2.

      6. Kwa nini ni jambo la akili kuamini kwamba Mungu aweza kuwapa wenye kufufuliwa miili ifaayo ya roho?

      6 Je, jambo hilo ni gumu mno kuamini? La. Paulo anasababu kwamba, wanyama wana miili mingi tofauti. Kwa kuongezea, yeye atofautisha malaika wa kimbingu na wanadamu wenye nyama na damu, akisema: “Kuna miili ya kimbingu, na miili ya kidunia.” Pia kuna tofauti kubwa kati ya uumbaji wa vitu visivyo na uhai. “Nyota hutofautiana na nyota kwa utukufu,” Paulo akasema, muda mrefu kabla sayansi haijagundua nyota kubwa kwa ndogo na zenye rangi tofauti-tofauti. Kwa kufikiria hilo, je, si jambo la akili kwamba Mungu aweza kuandaa miili ya roho ifaayo kwa ajili ya watiwa-mafuta wenye kufufuliwa?—1 Wakorintho 15:39-41.

      7. Ni nini maana ya kutoharibika? na ya kutoweza kufa?

      7 Kisha Paulo asema hivi: “Ndivyo pia ulivyo ufufuo wa wafu. Hupandwa katika uharibifu, hufufuliwa katika kutoharibika.” (1 Wakorintho 15:42) Mwili wa kibinadamu, hata unapokuwa mkamilifu, waweza kuharibika. Waweza kuuawa. Kwa mfano, Paulo alisema kwamba Yesu aliyefufuliwa “[ali]kusudiwa asirudi tena kwenye uharibifu.” (Matendo 13:34) Hangefufuliwa katika mwili wa kibinadamu wenye kuharibika, hata ingawa ni mkamilifu. Mungu huwapa watiwa-mafuta wenye kufufuliwa miili isiyoharibika—isiyoweza kufa au kuoza. Paulo aendelea kusema hivi: “Hupandwa katika fedheha, hufufuliwa katika utukufu. Hupandwa katika udhaifu, hufufuliwa katika nguvu. Hupandwa ukiwa mwili wa nyama, hufufuliwa ukiwa mwili wa kiroho.” (1 Wakorintho 15:43, 44) Na zaidi, Paulo asema hivi: “Huu uwezao kufa lazima uvae hali ya kutokufa.” Kutokufa humaanisha uhai wa milele usioweza kuhabiriwa. (1 Wakorintho 15:53; Waebrania 7:16) Katika njia hiyo, wenye kufufuliwa huchukua “mfano wa yule wa kimbingu,” yaani Yesu, aliyewezesha kufufuliwa kwao.—1 Wakorintho 15:45-49.

      8. (a) Twajuaje kwamba wenye kufufuliwa watakuwa watu walewale waliokuwa hai duniani? (b) Ni unabii gani mbalimbali unaotimizwa ufufuo utokeapo?

      8 Licha ya mgeuzo umbo huo, wenye kufufuliwa bado watakuwa watu walewale waliokuwa kabla ya kufa. Watafufuliwa na kumbukumbu zilezile na sifa zilezile bora za Kikristo. (Malaki 3:3; Ufunuo 21:10, 18) Katika hilo wanafanana na Yesu Kristo. Umbo lake la roho lilibadilika kuwa la kibinadamu. Kisha akafa na kufufuliwa akiwa roho. Hata hivyo, “Yesu Kristo ni yuleyule jana na leo, na milele.” (Waebrania 13:8) Watiwa-mafuta wana pendeleo lililoje! Paulo asema hivi: “Lakini wakati huu ulio wenye kuharibika uvaapo kutoharibika na huu uwezao kufa uvaapo hali ya kutokufa, ndipo usemi utakapotukia ambao umeandikwa: ‘Kifo kimemezwa milele.’ ‘Kifo, ushindi wako uko wapi? Kifo, kichomeo chako kiko wapi?’”—1 Wakorintho 15:54, 55; Isaya 25:8; Hosea 13:14.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki