Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yaliyomo
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • Yaliyomo

      Ukurasa

      1. Je, Maisha Yenye Kuridhisha Ni Ndoto?

      2. Madokezo ya Kuishi Maisha Yenye Kuridhisha

      3. Kitabu Chenye Mwongozo Unaotegemeka

      4. Mtungaji wa Kitabu Hiki cha Pekee

      5. Kumjua Mungu

      6. Kwa Nini Yehova Alituumba?

      7. Kwa Nini Ni Vigumu Kuwa na Maisha Yenye Kuridhisha?

      8. Maisha Yenye Kuridhisha Yarudishwa

      9. Furahia Maisha Yenye Kuridhisha Sasa na Milele!

  • Utangulizi
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • Utangulizi

      Msichana tineja akitumia simu ya mkononi; mvulana tineja akisikiliza muziki; mke akiwa amefadhaika kwa sababu anapuuzwa na mume wake

      Hebu fikiria hali hizi zinazotofautiana: Katika nchi moja ambayo imeendelea, zaidi ya asilimia 90 ya watu wanaona kwamba wana furaha nyingi ama wana furaha ya kiasi fulani. Lakini kati ya aina 10 za dawa zinazotumiwa sana katika nchi hiyo, aina 3 ni za kutibu ugonjwa wa kushuka moyo. Katika nchi hiyohiyo, asilimia 91 ya watu huona maisha yao ya familia kuwa yenye kuridhisha. Lakini, karibu nusu ya watu waliofunga ndoa katika nchi hiyo hutalikiana!

      Utafiti uliohusisha watu katika nchi 18, ambazo zina karibu nusu ya idadi ya watu wote ulimwenguni, ulionyesha kwamba “ulimwenguni kote watu wana shaka kuhusu wakati ujao.” Basi, ni wazi kwamba watu wengi hawaishi maisha yenye kuridhisha kikamili. Namna gani wewe? Broshua hii imetayarishwa ikusaidie kufanya maisha yako yawe yenye kuridhisha kwelikweli.

  • Je, Maisha Yenye Kuridhisha Ni Ndoto?
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • SEHEMU YA 1

      Je, Maisha Yenye Kuridhisha Ni Ndoto?

      KATIKA nchi ambayo imesitawi, nyumba yenye vitu vya starehe inaweza kuonekana kuwa yenye ufanisi. Lakini unapotembelea nyumba hiyo utakuta hali gani? Hali ngumu isiyo na furaha. Utapata vijana wakiwa wamenuna wakiwajibu wazazi wao tu “Ndiyo,” au “La.” Mama anatamani mume wake amjali. Naye baba hataki kusumbuliwa. Wazazi waliozeeka wa familia hiyo ambao wanaishi kwingine wanatamani kuwaona, kwani hawajawaona kwa miezi kadhaa. Kwa upande mwingine, kuna familia zenye mikazo kama hiyo ambazo zimeweza kusuluhisha matatizo yao na ambazo kwa kweli zina furaha. Je, unajua sababu?

      2 Hebu fikiria familia fulani katika nchi inayositawi, labda katika sehemu nyingine ya ulimwengu. Familia hiyo ya watu saba inaishi katika nyumba mbovu inayoweza kuanguka wakati wowote. Hawajui watapata lini mlo mwingine—kikumbusha chenye kusikitisha kwamba mwanadamu bado hajaweza kuondoa njaa na umaskini ulimwenguni. Hata hivyo, kuna familia nyingi duniani ambazo ni maskini lakini zina furaha. Kwa nini?

      Mwanamke akiwa na mkazo kwa sababu ya pesa

      3 Hata katika nchi tajiri, matatizo ya kifedha yanaweza kutokea. Familia moja nchini Japani ilinunua nyumba uchumi ulipokuwa mzuri kabisa. Wakiwa na hakika kwamba wataongezewa mshahara, walinunua nyumba kwa deni kubwa. Lakini uchumi ulipoharibika walishindwa kulipa deni la nyumba hiyo na wakalazimika kuiuza kwa bei ya chini sana kuliko walivyoinunua. Ingawa sasa familia hiyo haiishi katika ile nyumba, bado wanalipa deni hilo. Isitoshe pia, wanang’ang’ana kulipa madeni yaliyotokana na kutumia vibaya kadi za mkopo. Baba anacheza kamari ya mbio za farasi, na familia inazidi kudidimia kwenye madeni. Lakini familia nyingi zimefanya marekebisho ambayo yamefanya wapate furaha. Je, ungependa kujua wameipataje?

      4 Hata uwe unaishi wapi, mahusiano kati ya wanadamu yanaweza kusababisha mikazo na kufanya usifurahie maisha. Huenda ukasengenywa kazini. Mambo ambayo umetimiza yanaweza kuwafanya wengine wakuonee wivu na kufanya uchambuliwe. Huenda mtu ambaye unashughulika naye kila siku anakuudhi kwa sababu anasisitiza sana maoni yake. Labda mtoto wako ananyanyaswa, anadhulumiwa au kupuuzwa shuleni. Ikiwa wewe ni mzazi asiye na mwenzi wa ndoa, unajua kwamba hali hiyo inaongeza mzigo wa matatizo yako maishani. Matatizo hayo yote yanawazidishia mikazo wanaume na wanawake wengi leo.

      Wenzi wa ndoa wanakabiliana na mkazo; mwanamume anakunywa pombe akiwa peke yake; familia maskini sana

      5 Bila kujua, athari za mikazo zinaweza kuongezeka polepole kwa muda fulani mpaka mtu alemewe kabisa. Hiyo ndiyo sababu mkazo umeitwa muuaji wa kimyakimya, na mkazo wa daima kuitwa sumu inayoua polepole. “Leo, mkazo na magonjwa yanayosababishwa na mkazo yanaathiri wafanyakazi karibu ulimwenguni kote,” ndivyo anavyosema Profesa Robert L. Veninga wa Chuo Kikuu cha Minnesota. Inasemekana kwamba magonjwa yanayoletwa na mkazo yanagharimu Marekani dola bilioni 200 kila mwaka. Mkazo umetoka Marekani na kuenea hata katika nchi nyinginezo, na maneno yanayorejelea “mkazo” yanapatikana katika lugha nyingi kubwa ulimwenguni. Ikiwa una mkazo na unashindwa kutimiza mambo uliyotaka kufanya, huenda ukaanza kuhisi hatia. Uchunguzi mmoja uliofanywa karibuni unaonyesha kwamba mtu wa kawaida hujiona ana hatia kwa muda wa saa mbili kila siku. Lakini, wengine wameweza kukabili mkazo na kufaulu maishani.

      6 Unawezaje kukabiliana na matatizo hayo ya kila siku na bado uishi maisha yenye kuridhisha? Wengine husoma vitabu vyenye ushauri mbalimbali na maagizo ya wataalamu. Je, vitabu hivyo vinategemeka? Dakt. Benjamin Spock, ambaye kitabu chake kuhusu kulea watoto kimetafsiriwa katika lugha 42 na ambacho nakala milioni 50 hivi zimeuzwa, alisema kwamba “kutokuwa thabiti . . . ndilo tatizo la kawaida zaidi la wazazi nchini Marekani leo.” Kisha akasema kwamba wataalamu, kutia ndani yeye mwenyewe, ndio wenye kulaumika sana. “Hatukutambua jambo hilo mpaka ikawa kuchelewa mno,” akasema, “mtazamo wetu kwamba tunajua mambo yote unafanya wazazi wasiwe na uhakika.” Basi, huenda tukajiuliza: ‘Tunaweza kufuata ushauri wa nani ili tuishi maisha yenye kuridhisha leo na wakati ujao?’

      UNAONAJE?

      1. 1-3. Tunakabili matatizo gani kila siku?

      2. 4. Uhusiano na watu wengine unakuathirije?

      3. 5. Ni mambo gani ambayo yanasababisha mkazo ulimwenguni leo?

      4. 6. Unaionaje hekima ya wanadamu ya kukusaidia uishi maisha yenye kuridhisha?

  • Madokezo ya Kuishi Maisha Yenye Kuridhisha
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • SEHEMU YA 2

      Madokezo ya Kuishi Maisha Yenye Kuridhisha

      UNAPOPATA tatizo, unatafuta ushauri wapi? Huenda ukazungumza na rafiki unayemwamini au mshauri mwenye ujuzi. Unaweza kupata msaada kwa kuchunguza habari kama vile kwenye maktaba. Ama unaweza kutafuta “hekima ya Nyanya (Bibi),” kama wanavyosema watu kutoka nchi za Mashariki, ujifunze kutokana na ujuzi wake wa miaka mingi. Iwe unapendelea njia gani, ni vizuri kufikiria ushauri hususa wenye hekima ambao hutoa madokezo yanayosaidia kusuluhisha tatizo hilo. Yafuatayo ni madokezo mazuri ambayo yatakusaidia.

      Baba akizungumza na mwanaye

      “Mzoeze mvulana njia anayopaswa kuifuata”

      2 Maisha ya Familia: Wazazi wengi wana wasiwasi kuhusu kuwalea watoto katika ulimwengu wenye uvutano mbaya. Unaweza kupata msaada ukifuata ushauri huu: “Mzoeze mvulana njia anayopaswa kuifuata; hata atakapozeeka hataiacha.”1 Watoto wanapoendelea kukua, wanahitaji “njia,” yaani kanuni wanazopaswa kufuata. Wataalamu wengi wametambua umuhimu wa kuwawekea watoto sheria zinazofaa. Kanuni zenye hekima za wazazi huwafanya watoto wajihisi wako salama. Isitoshe: “Fimbo na karipio hufunza hekima, lakini mtoto aliyeachiliwa humwaibisha mama yake.”2 “Fimbo” inamaanisha mamlaka ya mzazi ambayo inapaswa kutumiwa kwa upendo ili watoto wasipotoke. Kutumia mamlaka hiyo hakumaanishi kwamba unapaswa kumtendea mtoto vibaya. Wazazi wanashauriwa hivi: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”3

      Mume anamsikiliza mke wake

      “Kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe”

      3 Uhusiano mzuri kati ya mume na mke ndio msingi wa familia yenye furaha. Ni nini kinachohitajika ili kuwe na uhusiano kama huo? “Kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”4 Upendo na staha huboresha maisha ya familia. Ili ushauri huu utumike, ni muhimu kuwa na mawasiliano kwa sababu “mipango huvunjika watu wasiposhauriana.”5 Ili kuwa na mawasiliano ya waziwazi, tunapaswa kujitahidi kufahamu hisia za mwenzi wetu wa ndoa, tukimtia moyo azungumze ili tujue hisia zake. Ni jambo la hekima kukumbuka kwamba “Mawazo yaliyo moyoni mwa mtu ni kama maji yenye kina, lakini mtu mwenye utambuzi huyateka.”6

      Wenzi wa ndoa waliozeeka wakiwa pamoja

      Uwe na mtazamo unaofaa, na ujitahidi kuwa na uhusiano mzuri na wengine

      4 Watu wengi ambao wamezeeka huwa wapweke katika miaka yao ya baadaye kwa sababu ya kuachwa na watoto wao, hata katika nchi ambazo watoto walikuwa na desturi ya kuwaheshimu wazazi. Lakini, inafaa watoto wao wafikirie maneno haya yenye hekima: Mheshimu baba yako na mama yako.”7 “Usimdharau mama yako kwa sababu tu amezeeka.”8 “Yule anayemtendea vibaya baba yake na kumfukuza mama yake ni mwana anayeleta aibu na fedheha.”9 Kwa upande mwingine, wazazi ambao wamezeeka wanahitaji kuwa na maoni mazuri na kujaribu kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine. “Anayejitenga na wengine anafuatia tamaa zake mwenyewe za kichoyo; hukataa hekima yote inayotumika.”10

      5 Kunywa Pombe: Ni kweli kwamba “divai hufanya maisha yafurahishe,”11 na kunywa pombe kunaweza kumfanya mtu ‘ausahau umaskini wake.’12 Lakini kumbuka: “Divai ni mdhihaki, kileo ni vurugu; yeyote anayepotoshwa navyo hana hekima.”13 Hebu fikiria madhara ya kunywa kupita kiasi: “Mwishowe huuma kama nyoka, nayo hutoa sumu kama nyoka kipiri. Macho yako yataona mambo ya ajabu, na moyo wako utasema mambo yaliyopotoka. . . . Nitaamka lini? Nahitaji kinywaji kingine.”14 Kunywa pombe kwa kiasi kunaweza kunufaisha, lakini sikuzote tunapaswa kuepuka kunywa kupita kiasi.

      6 Matumizi ya Pesa: Katika hali fulani, tunaweza kuepuka matatizo ya pesa kwa kuzitumia vizuri. Hebu sikiliza ushauri huu: “Usiwe miongoni mwa watu wanaokunywa divai nyingi mno, miongoni mwa wale wanaokula nyama kwa pupa, kwa maana mlevi na mlafi watakuwa maskini, na kusinzia kutamvika mtu matambara.”15 Kwa kuepuka pombe na dawa za kulevya na vilevile mazoea kama kucheza kamari, tunaweza kutumia pesa zetu kuiandalia familia yetu ifaavyo. Lakini, wengine hushindwa kuishi kulingana na mapato yao na mwishowe hulazimika kufanya kazi kwa bidii ili walipe madeni. Wengine hata huchukua mkopo ili walipe riba ya mkopo mwingine. Kukumbuka maneno haya ya hekima kutatusaidia: “Anayefuatia vitu visivyo na thamani atakuwa na umaskini wa kutosha.”16 Tunaweza kujiuliza: ‘Je, kweli ninahitaji vitu ambavyo ninataka kununua? Ni vitu vingapi ambavyo hukaa tu nyumbani baada ya kuvitumia mara chache?’ Mwandishi mmoja alisema hivi: “Mambo ambayo mwanadamu anahitaji ni machache lakini yale anayotaka hayana mwisho.” Hebu sikiliza maneno haya ya hekima: “Hatukuleta chochote ulimwenguni, wala hatuwezi kuondoka na chochote. Basi, tukiwa na chakula na mavazi, tutaridhika na vitu hivyo. . . . Kupenda pesa ndicho chanzo cha mambo mabaya ya kila aina, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo, wengine . . . [wamejichoma] kila mahali kwa maumivu mengi.”17

      7 Bidii husaidia sana kusuluhisha matatizo ya kifedha. “Mwendee chungu, ewe mvivu; zichunguze njia zake uwe na hekima. . . . Lala kidogo, sinzia kidogo,kunja mikono kidogo ili upumzike, na umaskini wako utakuja kama jambazi,na uhitaji wako kama mwanamume mwenye silaha.”18 Kupanga mambo kwa uangalifu na kutumia pesa vizuri kunaweza kusaidia pia: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?”19

      Seremala

      “Je, umemwona mtu aliye stadi katika kazi yake??”

      8 Lakini namna gani ikiwa tunalazimika kuwa maskini kwa sababu ya hali? Kwa mfano, kwa sababu ya matatizo makubwa ya kiuchumi, huenda tukakosa kazi hata ingawa tuko tayari kufanya kazi kwa bidii. Au huenda tunaishi katika nchi ambayo watu wengi ni maskini. Tufanyeje? “Hekima ni ulinzi kama pesa zilivyo ulinzi, lakini hii ndiyo faida ya ujuzi: Hekima humhifadhi hai yule aliye nayo.”20 Isitoshe fikiria ushauri huu: “Je, umemwona mtu aliye stadi katika kazi yake? Atasimama mbele ya wafalme.”21 Je, tunaweza kujifunza ufundi fulani ambao unaweza kutusaidia kupata kazi?

      Wenzi wa ndoa wanakula chakula pamoja na familia

      “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, nanyi mtapewa”

      9 Ushauri ufuatao huenda ukaonekana kuwa unajipinga, lakini ni ushauri bora: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, nanyi mtapewa. . . . Kwa maana kwa kipimo mnachowapimia watu, ndicho watakachowapimia.”22 Hii haimaanishi kuwapa watu vitu ukitarajia kupewa vitu pia. Badala yake, tunashauriwa kuwa na roho ya ukarimu: “Mtu mkarimu atapata ufanisi, na yule anayewaburudisha wengine yeye mwenyewe ataburudishwa.”23 Tunapowasaidia wengine wanapokuwa na uhitaji, tunaendeleza roho ya kutoa ambayo hatimaye inaweza kutufaidi.

      10 Uhusiano wa wanadamu: Mfalme mmoja mwenye hekima alisema: “Nami nimeona jinsi ambavyo ushindani kati ya watu unavyowafanya wajitahidi sana na kufanya kazi kwa ustadi; hili pia ni ubatili, kukimbiza upepo.”24 Ushindani umewafanya wengi watende kwa njia isiyo ya hekima. Mtu anaona jirani yake amenunua televisheni ya inchi 32, naye anaenda kununua televisheni ya inchi 36, hata ingawa ile televisheni yake ya inchi 27 inafanya kazi vizuri. Kwa kweli ushindani kama huo ni ubatili, ni kama kufuata upepo tu—kukimbia huku na huku bila kutimiza chochote. Je, sivyo?

      Mwanamume anamtuliza mtu mwenye hasira

      Tunawezaje kudhibiti hasira kali?

      11 Huenda tukakasirishwa na mambo ambayo wengine wametuambia. Lakini hebu fikiria ushauri huu: “Usikasirike haraka, kwa maana hasira hukaa katika kifua cha wajinga.”25 Ni kweli kwamba kuna pindi ambazo una haki ya kukasirika. “Iweni na hasira,” mwandishi mmoja wa kale anasema, “lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa bado mmekasirika.”26 Lakini tunawezaje kudhibiti hasira kali? “Ufahamu wa mtu hakika hutuliza hasira yake, na ni fahari kwake kuachilia kosa.”27 Tunahitaji ufahamu. Tunaweza kujiuliza: ‘Kwa nini alifanya hivyo? Je, kuna mambo yaliyosababisha afanye hivyo?’ Zaidi ya kuwa na ufahamu, kuna sifa ambazo tunaweza kukuza ili kudhibiti hasira. “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu, upole, na subira. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari hata ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. . . . Lakini zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”28 Ndiyo, upendo husuluhisha matatizo mengi yanayohusu uhusiano wa wanadamu.

      12 Lakini, kuna “kiungo kidogo” ambacho kinaharibu amani kati ya watu—ulimi. Maneno yafuatayo ni ya kweli kabisa: “Lakini hakuna mwanadamu anayeweza kuufuga ulimi. Ulimi ni kitu kitundu chenye kudhuru, kilichojaa sumu yenye kuua.”29 Na kwa kweli ushauri huu unafaa: “Kila mtu lazima awe mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa hasira.”30 Na tunapotumia ulimi, tuwe waangalifu tusiseme mambo ambayo ni kweli nusu ili kudumisha amani ya kijuujuu. “Acheni ‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo, kwa maana linalozidi hayo linatoka kwa yule mwovu.”31

      13 Tunawezaje kudumisha uhusiano mzuri pamoja na wengine? Ona kanuni ifuatayo: “Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.”32 Kwa kufanya hivyo tutaishi kulingana na ile ambayo imeitwa na wengi Kanuni Bora: “Basi, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.”33

      Mwanamke anasafisha nyumba yake

      14 Mkazo: Tunaweza kudumishaje usawaziko wa kihisia katika ulimwengu huu uliojaa mikazo? “Moyo wenye shangwe hufanya uso uchangamke, lakini maumivu ya moyo huiponda roho.”34 Tunaweza kupoteza kwa urahisi “moyo wenye shangwe” tunapoona wengine wakipuuza mambo tunayoona kuwa sawa. Lakini ni vizuri tukumbuke maneno haya: “Usiwe mwadilifu kupita kiasi, wala kujifanya mwenye hekima kupita kiasi. Kwa nini ujiangamize?”35 Kwa upande mwingine, huenda sikuzote tukawa na mahangaiko ya maisha. Tufanye nini? Tukumbuke maneno haya: “Mahangaiko yaliyo moyoni mwa mtu huulemea moyo, lakini neno jema huuchangamsha.”36 Tunaweza kutafakari “neno jema,” neno lenye fadhili ambalo linatutia moyo. Kuwa na mtazamo unaofaa hata tunapokabili hali ngumu kunaweza kuchangia afya bora: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.”37 Tukishuka moyo kwa sababu inaonekana wengine hawatujali, inafaa tufuate dokezo hili: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”38 Tukiwa na mtazamo unaofaa, tunaweza kukabiliana na mikazo ya kila siku.

      15 Je, unafikiri kwamba maneno hayo ya hekima yaliyotajwa yanaweza kukusaidia leo katika karne ya 21? Maneno hayo yanapatikana katika kitabu fulani cha kale—Biblia. Lakini, kwa nini uchunguze Biblia badala ya vyanzo vingine vya hekima? Kwa kuwa, miongoni mwa sababu nyingine, kanuni zinazopatikana katika Biblia zimethibitika kuwa zenye faida nyakati zote. Kwa mfano, fikiria Yasuhiro na Kayoko, waliokuwa wanaharakati wa kutetea haki za wanawake. Walifunga ndoa kwa sababu tu Kayoko alishika mimba ya Yasuhiro. Lakini kwa sababu ya matatizo ya kifedha na kuona kwamba hawafaani, wakaamua kutalikiana. Baadaye, bila yeyote kati yao kujua, wote wawili walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kila mmoja wao aliona mabadiliko makubwa katika maisha ya mwenzake. Yasuhiro na Kayoko wakaamua kufunga ndoa tena. Ingawa bado wanakabili matatizo, sasa wanaishi kwa kufuata kanuni za Biblia, na wote wawili wanakubaliana kusuluhisha matatizo. Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, utaona matokeo mazuri ya kutumia kanuni za Biblia maishani. Mbona usihudhurie mojawapo ya mikutano yao ili uwafahamu watu ambao wanajitahidi kuishi kulingana na Biblia?

      16 Mashauri yaliyonukuliwa hapo juu ni sehemu tu ya hekima chungu nzima yenye faida unayoweza kupata katika hazina hii kubwa ya elimu, yaani Biblia. Kuna sababu zinazofanya Mashahidi wa Yehova watumie kanuni za Biblia kwa hiari maishani mwao. Kwa nini usijitahidi kujua sababu zinazofanya watumie kanuni hizo na ujifunze mambo ya msingi kuhusu Biblia?

      UNAONAJE?

      1. 1. Utafanya nini ukikabili tatizo maishani mwako?

      2. 2-4. Ni maneno gani ya hekima yanayoweza kuzuia familia isivunjike?

      3. 5. Inafaa utii onyo gani kuhusu kunywa pombe?

      4. 6-9. Toa mifano ya njia ambazo unaweza kuboresha matumizi yako ya pesa.

      5. 10, 11. Unaweza kufanya nini ili kuepuka hasira na mashindano?

      6. 12. Ni nini ambacho kitakusaidia kudhibiti ulimi wako?

      7. 13. Unawezaje kudumisha uhusiano mzuri na watu?

      8. 14. Ni nini kinachoweza kukusaidia kukabiliana na mkazo?

      9. 15, 16. Kwa nini unapaswa uchunguze Biblia?

      SOMA MANENO YA HEKIMA KATIKA BIBLIA

      1. Methali 22:6

      2. Methali 29:15

      3. Wakolosai 3:21

      4. Waefeso 5:28, 33

      5. Methali 15:22

      6. Methali 20:5

      7. Mathayo 19:19

      8. Methali 23:22

      9. Methali 19:26

      10. Methali 18:1

      11. Mhubiri 10:19

      12. Methali 31:6, 7

      13. Methali 20:1

      14. Methali 23:29-35

      15. Methali 23:20, 21

      16. Methali 28:19

      17. 1 Timotheo 6:7-10; Luka 12:15

      18. Methali 6:6-11

      19. Luka 14:28

      20. Mhubiri 7:12

      21. Methali 22:29

      22. Luka 6:38

      23. Methali 11:25; Mhubiri 11:1

      24. Mhubiri 4:4

      25. Mhubiri 7:9

      26. Waefeso 4:26, 27

      27. Methali 19:11

      28. Wakolosai 3:12-14

      29. Yakobo 3:5-8

      30. Yakobo 1:19

      31. Mathayo 5:37

      32. Wafilipi 2:4

      33. Mathayo 7:12

      34. Methali 15:13

      35. Mhubiri 7:16

      36. Methali 12:25

      37. Methali 17:22

      38. Matendo 20:35

  • Kitabu Chenye Mwongozo Unaotegemeka
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • SEHEMU YA 3

      Kitabu Chenye Mwongozo Unaotegemeka

      Biblia katika lugha mbalimbali

      “BIBLIA ni mkusanyo wa ustaarabu wa mwanadamu na mambo yaliyompata maishani, na ni kitabu cha pekee,” ndivyo linavyosema jarida moja lililochapishwa na Chuo Kikuu cha Chung Shang kule Guangzhou, China. Immanuel Kant, mwanafalsafa mashuhuri wa karne ya 18, alisema hivi: “Faida kubwa zaidi ambayo mwanadamu amewahi kupata ni Biblia, kitabu kwa ajili ya wanadamu. Jaribio lolote la kuipuuza . . . ni uhalifu dhidi ya binadamu.” Kitabu The Encyclopedia Americana kinasema: “Biblia haiwavutii Wayahudi na Wakristo tu. . . . Bali sasa [Biblia] inaonwa kuwa hazina ya mambo ya kiadili na ya kidini na mafundisho yake tele yanatarajiwa kuwa muhimu hata zaidi ulimwengu unapotazamiwa kufanya maendeleo makubwa zaidi.”

      2 Hata uwe mfuasi wa dini gani, je, hungependa kujifunza kuhusu kitabu hicho? Kufikia mwisho wa karne ya 20, Biblia ilikuwa imetafsiriwa katika lugha zaidi ya 2,200, ikiwa nzima au kwa sehemu. Watu wengi wanaweza kupata Biblia katika lugha wanayoweza kusoma na kuelewa. Tangu mashine ya kupiga chapa ivumbuliwe, inakadiriwa kwamba Biblia bilioni nne zimeenezwa ulimwenguni kote.

      3 Sasa, ikiwa una Biblia tafadhali fungua ukurasa wa yaliyomo. Utaona majina ya vitabu, Mwanzo hadi Ufunuo. Kwa kweli, Biblia ni maktaba yenye vitabu 66 vilivyoandikwa na watu wapatao 40. Sehemu ya kwanza, yenye vitabu 39 ambayo wengi wanaiita Agano la Kale, inaitwa kwa usahihi Maandiko ya Kiebrania kwa sababu iliandikwa hasa katika Kiebrania. Sehemu ya pili, yenye vitabu 27 ambayo wengi wanaiita Agano Jipya, inaitwa kwa usahihi Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kwa kuwa waandishi Wakristo waliiandika katika Kigiriki. Ilichukua zaidi ya miaka 1,600 kumaliza kuandika Biblia, kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. hadi 98 W.K. Waandishi hao hawakuketi ili washauriane, na vitabu vingine viliandikwa kwa wakati uleule katika maeneo tofauti yaliyotenganishwa na maelfu ya kilomita. Ingawa hivyo, Biblia ina kichwa kimoja kikuu nayo inapatana na haijipingi. Basi tunaweza kujiuliza, ‘Ingewezekanaje kwa zaidi ya wanaume 40 katika kipindi cha karne 16 kutokeza kitabu ambacho kinapatana hivyo?’

      Sayari ya dunia

      “[Mungu] hulitandaza anga la kaskazini mahali pasipo na kitu, na kuining’iniza dunia mahali pasipo na kitu.”

      4 Ingawa kitabu cha mwisho cha Biblia kiliandikwa zaidi ya miaka 1,900 iliyopita, bado ujumbe wa Biblia unapendwa na wanaume na wanawake wa nyakati zetu. Kwa mfano, hebu fungua Biblia yako kwenye Ayubu 26:7. Kumbuka kwamba andiko hilo liliandikwa karne ya 15 K.W.K. Linasema: “[Mungu] hulitandaza anga la kaskazini mahali pasipo na kitu, na kuining’iniza dunia mahali pasipo na kitu.” Kisha, fungua Isaya 40:22, na ukumbuke kwamba kitabu cha Isaya kiliandikwa karne ya nane K.W.K. Mstari huo unasema: “Kuna Yule anayekaa juu ya duara ya dunia, na wakaaji wake ni kama panzi. Anazitandaza mbingu kama wavu laini,naye huzitandaza kama hema la kuishi.” Unapata wazo gani unaposoma maandiko hayo mawili? Kitu chenye umbo la duara ‘kinachoning’inia’ angani. Huenda umeona picha kama hiyo iliyopigwa na vyombo vya kisasa vya angani. Labda unajiuliza, ‘Inawezekanaje kwa watu walioishi zamani sana hivyo kutoa taarifa sahihi za kisayansi?’

      5 Hebu tufikirie swali lingine kuhusu Biblia. Je, Biblia ni sahihi kihistoria? Wengine wanafikiri kwamba Biblia ni mkusanyo tu wa hadithi zisizoweza kuthibitishwa kihistoria. Kwa mfano, mfikirie Daudi, mfalme Mwisraeli anayejulikana sana. Hadi hivi karibuni, Biblia peke yake ndiyo iliyotaja kwamba kulikuwa na mtu aliyeitwa Daudi. Ingawa wanahistoria mashuhuri wanakubali kwamba ni mtu halisi, watu wengine wanaotilia shaka wanasema kwamba ni mtu wa kuwaziwa tu aliyebuniwa na Wayahudi waliotaka kueneza mawazo yao. Lakini ukweli wa mambo ni nini?

      Maandishi yanayotaja “Nyumba ya Daudi”

      Maandishi yanayotaja “Nyumba ya Daudi”

      6 Mwaka wa 1993, maandishi yanayotaja “Nyumba ya Daudi” yalipatikana kwenye magofu ya jiji la kale la Dani, la Waisraeli. Maandishi hayo yalikuwa sehemu ya mnara wa ukumbusho ulioharibika wa karne ya tisa K.W.K. ulioonyesha jinsi maadui walivyowashinda Waisraeli. Ghafla maandishi mengine kando na Biblia yanayomtaja Daudi yakapatikana. Je, hilo lilikuwa jambo muhimu? Israel Finkelstein, wa Chuo Kikuu cha Tel Aviv, alisema hivi kuhusu ugunduzi huo: “Wazo la kwamba maandishi ya Biblia hayana msingi likakoma ghafla baada ya maandishi hayo yanayomtaja Daudi kupatikana.” Jambo la kupendeza ni kwamba Profesa William F. Albright, mtaalamu wa mambo ya kale aliyeishi miaka mingi Palestina akichimbua vitu vya kale, alisema hivi: “Ugunduzi mmoja baada ya mwingine umethibitisha usahihi wa mambo mengi sana madogo-madogo, na kufanya Biblia itambuliwe zaidi kuwa kitabu cha kihistoria.” Tena, tunaweza kujiuliza, ‘Tofauti na hadithi na hekaya, kwa nini kitabu hiki cha kale ni sahihi sana kihistoria?’ Lakini kuna mengi zaidi.

      Sarafu inayoonyesha Aleksanda Mkuu

      Sarafu inayoonyesha Aleksanda Mkuu

      7 Biblia ni kitabu cha unabii pia. (2 Petro 1:20, 21) Neno “unabii” huenda likafanya ufikirie kuhusu unabii wa uwongo unaotolewa na wale wanaojiita manabii. Lakini usifikirie mawazo kama hayo, fungua Danieli sura ya 8 katika Biblia. Hapo Danieli anafafanua maono ya pambano kati ya kondoo dume mwenye pembe mbili na mbuzi dume mwenye manyoya mengi na “pembe iliyoonekana waziwazi.” Mbuzi dume anashinda, lakini pembe yake kuu inavunjika. Badala yake pembe nne zinatokea. Maono hayo yanamaanisha nini? Masimulizi ya Danieli yanaendelea kusema: “Yule kondoo dume mwenye pembe mbili uliyemwona anafananisha wafalme wa Umedi na Uajemi. Yule mbuzi dume mwenye manyoya anafananisha mfalme wa Ugiriki; na ile pembe kubwa iliyokuwa kati ya macho yake, inafananisha mfalme wa kwanza. Kuhusu ile pembe iliyovunjika, kisha pembe nne zikatokea badala yake, kuna falme nne kutoka katika taifa lake zitakazosimama, lakini hazitakuwa na nguvu kama zake.”—Danieli 8:3-22.

      “Ugunduzi mmoja baada ya mwingine umethibitisha usahihi wa mambo mengi sana madogo-madogo, na kufanya Biblia itambuliwe zaidi kuwa kitabu cha kihistoria.”—Profesa William F. Albright

      8 Je, unabii huu ulitimizwa? Kitabu cha Danieli kilikamilika kuandikwa mwaka wa 536 K.W.K. hivi. Mfalme wa Makedonia, Aleksanda Mkuu, aliyezaliwa miaka 180 baadaye, mnamo 356 K.W.K., alishinda Milki ya Uajemi. Yeye ndiye aliyekuwa ile “pembe kubwa” kati ya macho ya “mbuzi dume mwenye manyoya mengi.” Kulingana na Yosefo, mwanahistoria wa Kiyahudi, Aleksanda alionyeshwa kitabu cha Danieli alipoingia Yerusalemu kabla ya kuishinda Uajemi. Akafikia uamuzi kwamba unabii wa Danieli alioonyeshwa ulihusu vita yake dhidi ya Uajemi. Isitoshe, unaweza kusoma katika vitabu vya historia ya ulimwengu kilichoipata milki ya Aleksanda baada ya kifo chake mwaka wa 323 K.W.K. Hatimaye majenerali wanne wakatawala milki yake, na kufikia mwaka wa 301 K.W.K., zile “pembe nne” ambazo ziliinuka mahali pa “ile pembe kubwa” ziligawanya milki hiyo katika sehemu nne. Kwa mara nyingine tena, tuna sababu nzuri ya kujiuliza, ‘Kitabu kingewezaje kutabiri kwa njia sahihi na iliyo wazi mambo ambayo yangetokea miaka 200 baadaye?’

      Aleksanda Mkuu na “mbuzi dume mwenye manyoya”

      9 Biblia yenyewe inajibu maswali hayo: “Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.” (2 Timotheo 3:16) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa ‘ongozwa na roho ya Mungu’ hasa linamaanisha “-enye pumzi ya Mungu.” Mungu ‘aliweka pumzi’ katika akili za waandishi wapatao 40 nao wakaandika habari tunazopata sasa katika vitabu vya Biblia. Mifano michache ambayo tumezungumzia—kuhusu sayansi, historia, na unabii—inathibitisha jambo moja. Kitabu hiki cha pekee, Biblia, hakitokani na hekima ya wanadamu bali kimetokana na Mungu. Hata hivyo, watu wengi leo wanatilia shaka kama kweli Mtungaji wake—Mungu—yuko. Wewe unaonaje?

      UNAONAJE?

      1. 1, 2. Kwa nini unapaswa kuchunguza Biblia kwa makini?

      2. 3. Ni mambo gani kuhusu uandikaji wa Biblia yanayoshangaza?

      3. 4-6. Kwa nini uamini habari zilizo katika Biblia?

      4. 7, 8. Unaonaje unabii wa Biblia?

      5. 9. Ni nini kinachofanya mambo yaliyo katika Biblia yawe ya pekee?

  • Mtungaji wa Kitabu cha Pekee
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • SEHEMU YA 4

      Mtungaji wa Kitabu Hiki cha Pekee

      INGAWA asilimia 96 hivi ya Wamarekani wanadai kwamba wanamwamini Mungu, huko Ulaya na Asia ni watu wachache hata zaidi wanaoamini Mungu. Hata katika nchi ambazo watu wengi wanadai hawaamini kuna Mungu, kuna watu wengi wanaokubali kwamba nguvu fulani isiyojulikana ilisababisha ulimwengu uwepo. Yukichi Fukuzawa, mwalimu mashuhuri nchini Japani, ambaye picha yake iko kwenye noti ya yen 10,000 (pesa za Japani), aliandika hivi pindi moja: “Inasemekana kwamba mbingu haiumbi mwanadamu mmoja akiwa bora kuliko mwingine.” Kwa kutumia neno “mbingu,” Fukuzawa alitaja chanzo fulani cha asili ambacho alifikiri kilitokeza wanadamu. Watu wengi wanakubaliana na mshindi wa tuzo ya Nobel, Kenichi Fukui, kwamba kuna “mbingu” kama hiyo ya kuwaziwa. Alisema anaamini kwamba kuna nguzo kuu katika ulimwengu—ambayo kulingana na usemi wa kidini ni “Mungu” —lakini akaiita nguzo hiyo “tabia ya maumbile.”

      Yukichi Fukuzawa; Kenichi Fukui

      Kushoto: Yukichi Fukuzawa; Kulia: Kenichi Fukui

      2 Wasomi hao waliamini kuna kitu cha milele au mtu wa milele aliyeanzisha kila kitu katika ulimwengu mzima. Kwa nini? Fikiria jambo hili: Jua ni nyota kubwa sana hivi kwamba dunia milioni moja zinaweza kutoshea ndani yake, lakini jua lenyewe ni tone tu katika kundi la nyota la Kilimia. Kilimia ni kundi moja tu la nyota kati ya mabilioni ya makundi mengine ya nyota ulimwenguni pote. Inaonekana uchunguzi wa sayansi unaonyesha kwamba makundi hayo ya nyota yanaendelea kutawanyika kwa mwendo wa kasi sana. Bila shaka, nguvu nyingi sana zilihusika ili kuanzisha ulimwengu. Ni nani au ni nini chanzo cha nguvu hizo nyingi? “Inueni macho yenu mbinguni mwone. Ni nani aliyeviumba vitu hivi?” Biblia inasema. “Ni Yule anayelileta nje jeshi lao kwa hesabu; huziita zote kwa majina. Kwa sababu ya nguvu zake nyingi zenye msukumo na nguvu zake zenye kuogopesha, hakuna hata moja inayokosekana.” (Isaya 40:25, 26) Andiko hilo linaonyesha kwamba kuna mtu aliyeanzisha ulimwengu mzima—ambaye ndiye Chanzo cha “nguvu nyingi zenye msukumo.”

      Sombrero Galaxy

      Sombrero Galaxy

      3 Fikiria pia uhai duniani. Je, uhai ungeweza kuanza wenyewe tu, kama wanavyodai wanamageuzi? Mwanasayansi Michael Behe, anasema: “Sayansi imefanya maendeleo makubwa sana ya kujua jinsi mwili unavyofanya kazi, lakini usanifu na utata wa molekuli za mifumo inayofanya kazi mwilini umefanya majaribio ya sayansi ya kugundua jinsi zilivyoanza yasifanikiwe. . . . Wanasayansi wengi wamesisitiza kwamba tayari wana majibu, au kwamba watayapata majibu hayo baada ya muda, lakini madai yao hayaungwi mkono na vitabu vya wataalamu wa sayansi. Jambo muhimu zaidi ni kwamba kuna sababu zenye nguvu—zinazotegemea mifumo ya utendaji wa chembe zenyewe za mwili—zinazofanya tufikirie kwamba nadharia ya Darwin ya jinsi uhai ulivyoanza haitaeleweka milele.”

      Sehemu ya protini

      “Kujikunja kwa protini ya kawaida . . . kunaweza kulinganishwa na fumbo tata la maneno,” asema Michael Behe. Na bado mwili wa binadamu unaweza kuwa na mamia ya maelfu ya mafumbo kama hayo. Wanasayansi wanajaribu kufumbua mafumbo hayo, lakini ni nani aliyeyabuni?

      4 Je, kweli unakubaliana na nadharia inayosema kwamba uhai wa wanadamu ulianza bila mtu fulani mwenye akili kuuanzisha? Acheni tuchunguze mfano wa kiungo kinachoonekana kuwa “kitu tata zaidi ulimwenguni,” yaani, ubongo wa mwanadamu, na tuone tutafikia uamuzi gani. “Ubongo wa nzi unazidi mara elfu kumi uwezo wa kompyuta za hali ya juu zaidi ambazo zinaiga utendaji wa ubongo,” asema Dakt. Richard M. Restak. Ubongo wa mwanadamu una uwezo mkubwa sana kuliko ubongo wa nzi. Ubongo una uwezo wa kujifunza lugha nyingi. Ubongo unajirekebisha, unajiratibu, na kujiboresha. Bila shaka unakubali kwamba hata kompyuta yenye uwezo mkubwa zaidi ambayo ‘inashindwa na uwezo wa nzi mara elfu kumi’ imebuniwa na mtu mwenye akili. Je, si zaidi ubongo wa binadamu?a

      5 Miaka 3,000 hivi iliyopita, wakati ambapo wanadamu hawakujua kwamba wameumbwa kwa njia ya ajabu, mwandishi mmoja wa Biblia alitafakari jinsi ambavyo mwili wa binadamu umeumbwa akasema: “Ninakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia inayoogopesha na kustaajabisha. Kazi zako zinastaajabisha, ninajua vizuri sana jambo hilo.” Bila kujua kuhusu molekuli za DNA, aliandika hivi: “Macho yako hata yaliniona nikiwa kiinitete; sehemu zake zote ziliandikwa katika kitabu chako.” (Zaburi 139:14, 16) Alikuwa akizungumza juu ya nani? Ni nani aliyetokeza kila kitu ulimwenguni kwa “nguvu zake nyingi zenye msukumo”?

      Kompyuta zenye uwezo mkubwa na nzi

      Ni nini kilicho na uwezo zaidi, je, ni kompyuta za hali ya juu zaidi ambazo zinaiga utendaji wa ubongo au ni nzi?

      6 Mstari wa kwanza katika Biblia unasema: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Yeye pia ndiye Mtungaji wa Biblia, na alitumia roho yake kuongoza iandikwe. Anajitambulisha kuwa mtu ambaye tunaweza kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye.

      a Utafurahia kusoma habari zaidi katika sura ya 2 hadi ya 4 ya kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

      UNAONAJE?

      1. 1, 2. Una maoni gani kuhusu chanzo cha ulimwengu?

      2. 3. Unaamini nini kuhusu uwezekano wa uhai kujitokeza wenyewe kupitia mageuzi?

      3. 4. Uwezo wa ubongo wa mwanadamu unakufundisha nini kuhusu chanzo cha ubongo?

      4. 5, 6. Umefikia uamuzi gani kuhusu Chanzo cha uhai?

  • Kumjua Mungu
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • SEHEMU YA 5

      Kumjua Mungu

      UNAPOTAFUTA ushauri, je, huendi kwa mtu anayeaminika? Ukipata ushauri kutoka kwa mtu unayemwamini inaelekea utaufuata iwe utafaidika papo hapo au la. Ili ufaidike na ushauri wenye hekima ulio katika Biblia ni lazima umfahamu Mtungaji wake. Hata unaweza kuwa “rafiki” yake!—Isaya 41:8.

      Jina la Mungu katika maandishi ya Kiebrania ya Isaya

      Jina la Mungu linalopatikana katika maandishi ya Kiebrania ya kitabu cha Isaya

      2 Ukitaka kuwa rafiki ya mtu, bila shaka utataka kujua jina lake. Je, Biblia inataja jina la Mungu? Yeye alitangaza hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu; simpi yeyote utukufu wangu, wala kuzipa sanamu za kuchongwa sifa yangu.” (Isaya 42:8) Jina lake ni “Yehova,” ambalo linaandikwa יהוה (likisomwa kutoka kulia kwenda kushoto) katika Kiebrania. Jina hilo linapatikana mara 7,000 hivi katika Maandiko ya Kiebrania ya Biblia. Inaeleweka kwamba jina la Mungu linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa,” likidokeza kwamba Yehova anaweza kuwa chochote kile anachotaka ili atimize makusudi yake, au kuhusiana na uumbaji wake anaweza kusababisha chochote kinachohitajika ili kutimiza kusudi lake. Katika Kiebrania jina lake ni kitenzi kinachoonyesha kitendo kinachoendelea. Jambo hilo linaonyesha nini? Linatuambia kwamba Yehova amesababisha na bado anasababisha makusudi yake yatimizwe. Yeye ni Mungu aliye hai, si nguvu tu isiyo na utu!

      Ndege, ua, kipepeo, na ndovu

      3 Yehova akawa Muumba. (Mwanzo 1:1) Yeye ni “Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.” (Matendo 14:15) Yehova aliumba kila kitu, kutia ndani wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa. Kwa hiyo, Mungu ndiye “chanzo cha uhai.” (Zaburi 36:9) Akawa pia Mtegemezaji wa uhai. Kwa hiyo, “hakujiacha bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira ya mavuno, akiwashibisha kwa chakula na kuijaza mioyo yenu furaha.” (Matendo 14:17) Barani Afrika na Asia, wengi huabudu mababu zao kwa sababu uhai wao ulitokana nao. Je, hawapaswi kumwabudu Muumba na Mtegemezaji wa uhai, Yule aliyewaumba wanadamu wawili wa kwanza na kuwapa uwezo wa kuzaa? Ukitafakari jambo hilo, unaweza kusema hivi: “Unastahili, Ee Yehova Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilitokea navyo vikaumbwa.”—Ufunuo 4:11.

      4 Kupitia Biblia, unaweza kumjua Muumba wako, Yehova, na kujifunza yeye ni Mungu wa aina gani. Biblia inafunua kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:16; Kutoka 34:6, 7) Unaposoma Biblia kuanzia Mwanzo hadi Ufunuo, utapata masimulizi mengi yanayoonyesha kwamba kwa kweli yeye ni Mungu mwenye upendo. Mbona usiwe na mazoea ya kusoma Neno la Mungu kila siku ili umjue Muumba wako? Jifunze Biblia kwa makini ukisaidiwa na wale wanaoifahamu. (Matendo 8:26-35) Ukifanya hivyo, utaona kwamba yeye ni Mungu wa haki, ambaye hataruhusu uovu uendelee milele. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Si rahisi kwa mwanadamu kuonyesha upendo na haki kwa usawaziko, lakini kwa kuwa Yehova ana hekima anasawazisha sifa hizo kikamili. (Waroma 11:33; 16:27) Kwa kuwa yeye ni Mungu Mweza Yote, ana uwezo wa kufanya chochote anachotaka ili atimize makusudi yake. (Mwanzo 17:1) Jitahidi kutumia ushauri wenye hekima ulio katika Biblia, nawe utamfahamu Muumba wako vizuri zaidi, na utatambua kwamba nyakati zote ushauri wake hutufaidi.

      Familia ikisali pamoja

      Mbona usisali kwa Yehova?

      5 Bado kuna njia nyingine ya kuwasiliana na Mungu. Ni kupitia sala. Yehova ni “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Anaweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.” (Waefeso 3:20) Lakini, ungemwonaje “rafiki” anayekuja kwako wakati tu anapotaka umsaidie? Labda hungemwona kuwa rafiki wa kweli. Vivyo hivyo, bila shaka ungependa kutumia pendeleo la sala kumwomba Mungu mahitaji yako na vilevile kumshukuru na kumsifu.—Wafilipi 4:6, 7; 1 Wathesalonike 5:17, 18.

      UNAONAJE?

      1. 1. Kwa nini ni muhimu kumjua Mungu?

      2. 2. Kwa nini jina la Mungu na maana yake ni muhimu?

      3. 3. Una sababu gani za kumsifu Yehova?

      4. 4. Ni zipi baadhi ya sifa kuu za Yehova?

      5. 5. Wewe binafsi unawezaje kumjua Mungu?

  • Kwa Nini Yehova Alituumba?
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • SEHEMU YA 6

      Kwa Nini Yehova Alituumba?

      Mfalme Sulemani

      Mfalme Sulemani alichunguza swali lililohusu kusudi la uhai

      UTAFAIDIKAJE kwa kumjua Yehova? Miongoni mwa mambo mengine, utapata jibu la swali ambalo limewatatiza mabilioni ya watu: ‘Kwa nini niko hai?’ Huenda umewahi kujiuliza swali hilo. Mfalme mmoja mwenye hekima ambaye pia alikuwa tajiri “kuliko wafalme wengine wote duniani” katika siku zake, alichunguza swali hilo kuhusu kusudi la uhai. (2 Mambo ya Nyakati 9:22; Mhubiri 2:1-13) Mfalme huyo, Sulemani, alikuwa na mamlaka kubwa sana, mali nyingi sana, na hekima isiyo na kifani. Uchunguzi wake ulionyesha nini? “Huu ndio umalizio, baada ya mambo yote kusikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na ushike amri zake, kwa maana huu ndio wajibu wote wa mwanadamu.” (Mhubiri 12:13) Kwa kuwa Sulemani alikuwa na hekima kuliko watu wengi, tunapaswa kuchunguza uamuzi aliofikia.—Mhubiri 2:12.

      2 Sulemani alipotaja kumwogopa Mungu hakumaanisha hofu isiyofaa ya kuogopa roho isiyojulikana. Badala yake, ni woga unaofaa wa kutomkasirisha mtu unayempenda sana. Ikiwa unampenda mtu sana, utajitahidi kumfurahisha nyakati zote na kuepuka kufanya jambo lolote linaloweza kumkasirisha. Unapozidi kumpenda Yehova, utahisi hivyo kumhusu.

      3 Unaposoma Biblia, utajifunza mambo ambayo Muumba wetu anapenda na mambo ambayo hapendi, na pia kusudi lake la kuumba dunia. Biblia inasema Yehova ndiye “Yule aliyeiumba dunia, Yule aliyeitengeneza,” pia Biblia inamwita yule “[aliyeifanya] imara kabisa, ambaye hakuiumba tu bila sababu, lakini aliiumba ili ikaliwe.” (Isaya 45:18) Yehova alitayarisha dunia ili ikaliwe na wanadamu, ambao wangeitunza na kuwatunza viumbe wote ndani yake. (Mwanzo 1:28) Lakini, je, hilo ndilo kusudi pekee lililomfanya Yehova awaumbe wanadamu, yaani, kuwa watunzaji?

      Adamu na Hawa

      Adamu na Hawa walikuwa na uhusiano mzuri sana pamoja na Mungu

      4 Hapana, kulikuwa na kusudi kubwa hata zaidi. Mwanadamu wa kwanza, Adamu, alikuwa na uhusiano mzuri sana pamoja na Yehova. Adamu angeweza kuwasiliana moja kwa moja na Muumba. Angeweza kumsikiliza Mungu na kumwambia Yehova maoni yake. (Mwanzo 1:28-30; 3:8-13, 16-19; Matendo 17:26-28) Basi, Adamu na mkewe, Hawa, walikuwa na fursa nzuri sana ya kumjua Yehova vizuri na kuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja naye. Kumjua Yehova na kumwiga kungefanya maisha yao yawe yenye kuridhisha, kwa kuwa yeye ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Akiwa Mungu “ambaye hutupatia kwa wingi vitu vyote tunavyofurahia,” Yehova alimweka mwanadamu wa kwanza katika paradiso iliyoitwa bustani ya Edeni, akiwa na tumaini la kuishi milele.—1 Timotheo 6:17; Mwanzo 2:8, 9, 16, 17.

      Telomere na Kromosomu

      Ugunduzi wa hivi karibuni kuhusu chembe za binadamu unaonyesha nini?

      5 Milele? Huenda ukafikiri wazo la kuishi milele ni upuuzi mtupu, lakini je, ni upuuzi? Wanasayansi wanaamini kwamba sasa wanafahamu jambo linalosababisha chembe zizeeke. Visehemu vya chembe za urithi vinavyoitwa telomere, vinavyopatikana kwenye miisho ya kromosomu, huwa fupi kila mara chembe inapogawanyika. Baada ya chembe kugawanyika mara 50 hadi 100, telomere huchakaa, na chembe nyingi huacha kugawanyika. Lakini ugunduzi wa hivi karibuni wa kisayansi unadokeza kwamba kwa msaada wa kimeng’enya kinachoitwa telomerase, chembe za binadamu zinaweza kuendelea kugawanyika milele. Ingawa ugunduzi huo haumaanishi kwamba Yehova anaweza kufanya tuishi milele kupitia kimeng’enya hicho, unaonyesha jambo hili: Wazo la kuishi milele si upuuzi!

      6 Ndiyo, simulizi la Biblia linaloonyesha kwamba wanadamu wawili wa kwanza waliumbwa waishi milele ni la kweli. Wanadamu walipaswa kusitawisha uhusiano pamoja na Yehova milele. Walipaswa kuwa na uhusiano wa karibu sana na Baba yao wa mbinguni, wakijua kabisa kusudi lake kwa wanadamu duniani na kulitimiza. Maisha yao hayakupaswa kuwa yenye kuchosha. Adamu na Hawa walikuwa na tumaini zuri sana la kuijaza dunia wazao wakamilifu wenye furaha. Wangekuwa na kazi yenye maana na yenye kuridhisha milele. Hayo yangekuwa maisha yenye kuridhisha sana!—Mwanzo 1:28.

      UNAONAJE?

      1. 1. Sulemani alifikia uamuzi gani kuhusu kusudi la uhai?

      2. 2. Ni nini maana ya kumwogopa Mungu?

      3. 3. Yehova aliwaumba wanadamu kwa kusudi gani?

      4. 4. Ni nini ambacho kingefanya maisha ya wanadamu yawe yenye kuridhisha?

      5. 5, 6. Una maoni gani kuhusu uzima wa milele, na kwa nini?

  • Kwa Nini Ni Vigumu Kuwa na Maisha Yenye Kuridhisha?
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • SEHEMU YA 7

      Kwa Nini Ni Vigumu Kuwa na Maisha Yenye Kuridhisha?

      Mtu akiwa amelazwa hospitalini; msichana mdogo mlemavu; mwanamke akiwa katika kiti cha magurudumu

      KWA NINI watu wengi hujitahidi sana leo lakini hawapati kusudi maishani? “Mwanadamu anayezaliwa na mwanamke, maisha yake ni mafupi na yamejaa taabu. Huchanua kama ua na kisha hunyauka; hukimbia kama kivuli na kutoweka.” (Ayubu 14:1, 2) Jambo fulani lililowapata Adamu na Hawa katika Paradiso, liliwasababishia wanadamu matatizo.

      2 Ili wanadamu wawe na furaha ya kweli, ni lazima wawe na uhusiano mzuri pamoja na Mungu—uhusiano wa hiari bila kulazimishwa. (Kumbukumbu la Torati 30:15-20; Yoshua 24:15) Yehova anataka tumtii na kumwabudu kutoka moyoni, kwa sababu tunampenda. (Kumbukumbu la Torati 6:5) Basi katika bustani ya Edeni, Yehova alimpa Adamu maagizo ambayo yalimpa fursa ya kuthibitisha uaminifu wake wa moyoni. “Unaweza kula matunda ya kila mti,” Mungu akamwambia Adamu, “lakini kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya, usile matunda yake, kwa maana siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.” (Mwanzo 2:16, 17) Ulikuwa mtihani rahisi. Yehova alimkataza Adamu asile matunda ya mti mmoja tu kati ya miti yote iliyokuwa katika bustani. Mti huo uliwakilisha haki ya Muumba mwenye hekima yote ya kuamua mema na mabaya. Adamu akamwambia amri hiyo ya Mungu mke wake, ambaye Yehova alimpa awe “msaidizi” wake. (Mwanzo 2:18) Wote wawili waliridhika na mpango huo—kuishi chini ya utawala wa Mungu—wakifanya mapenzi yake kwa unyenyekevu na hivyo kuonyesha kwamba wanampenda Muumba wao na Mpaji Uhai.

      3 Kisha siku moja nyoka akaongea na Hawa, akauliza: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Hawa akasema walikatazwa kula tunda la “mti ulio katikati ya bustani,” mti wa ujuzi wa mema na mabaya, ‘wasije wakafa.’—Mwanzo 3:1-3.

      4 Huyo nyoka alikuwa nani? Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinamtambulisha “nyoka wa zamani” kuwa “Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Je, Mungu alimuumba Shetani Ibilisi? La, kazi za Yehova ni kamilifu na njema. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kiumbe huyu wa roho aligeuka mwenyewe akawa Ibilisi, yaani “Mchongezi,” na Shetani, yaani “Mpinzani.” ‘Alivutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe,’ alitamani kuwa kama Mungu, akaanza kumwasi Muumba.—Yakobo 1:14.

      Nyoka anazungumza na Hawa; Adamu anajaribu kulima ardhi iliyolaaniwa

      5 Shetani Ibilisi akaendelea kumwambia Hawa: “Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunguliwa nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:4, 5) Shetani alifanya wazo la kula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya livutie. Ni kana kwamba alisema: ‘Mungu anawanyima kitu kizuri. Onja tu matunda ya mti huu, nawe utakuwa kama Mungu na utaweza kujiamulia mema na mabaya.’ Leo Shetani bado anatumia njia hiyo ya kufikiri ili kuwazuia wengi wasimtumikie Mungu. ‘Fanya upendavyo,’ anasema. ‘Mpuuze Mungu aliyekupa uhai.’—Ufunuo 4:11.

      6 Ghafla matunda ya mti huo yakavutia, yakatamanika sana! Hawa akachukua tunda, akala, baadaye akampa mume wake. Ingawa Adamu alijua vizuri kabisa matokeo, alimsikiliza mke wake naye akala. Matokeo yakawaje? Yehova alimhukumu hivi mwanamke: “Nitazidisha sana uchungu wa mimba yako; utazaa watoto kwa uchungu, nawe utamtamani sana mume wako, naye atakutawala.” Namna gani mwanamume? “Ardhi imelaaniwa kwa sababu yako. Kwa maumivu utakula mazao yake sikuzote za maisha yako. Itakuzalia miiba na michongoma, nawe utakula mimea ya shambani. Kwa jasho la uso wako utakula chakula mpaka utakaporudi ardhini, kwa kuwa ulitolewa humo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” Sasa Adamu na Hawa waliachwa wajitafutie wenyewe furaha na kuridhika. Je, jitihada za wanadamu za kuishi maisha yenye kuridhisha bila kusudi la Mungu zingefanikiwa? Badala ya kufanya kazi yenye kufurahisha ya kutunza Paradiso iliyo kama bustani na kuipanua hadi miisho ya dunia, sasa walifanya kazi ya kuchosha ili tu waendelee kuishi, bila kufanya chochote cha kumtukuza Muumba.—Mwanzo 3:6-19.

      Hawa anahangaika na watoto wake wasio wakamilifu

      7 Siku waliyokula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya, machoni pa Mungu Adamu na Hawa walikufa wakaanza kudhoofika wakielekea kufa kihalisi. Walipatwa na nini walipokufa hatimaye? Biblia inatufahamisha hali ya wafu. “Walio hai wanajua kwamba watakufa, lakini waliokufa hawajui jambo lolote kamwe, wala hawana thawabu tena, kwa sababu kumbukumbu lote kuwahusu limesahauliwa.” (Mhubiri 9:5; Zaburi 146:4) “Nafsi” haiendelei kuishi mtu anapokufa. Adhabu ya dhambi ni kifo, wala si kuteswa katika moto wa milele. Isitoshe, mtu akifa haendi mbinguni kuishi raha mustarehe.a

      8 Kama vile sufuria iliyobonyea inayotumiwa kuokea mikate inavyotokeza mikate iliyobonyea, ndivyo Adamu na Hawa wasio wakamilifu wangetokeza wazao wasio wakamilifu. Biblia inafafanua hali hiyo: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, basi kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Kwa hiyo, sisi sote huzaliwa tukiwa na dhambi katika hali ya kutokamilika. Maisha ya wazao wa Adamu yakawa magumu na yenye kuchosha. Lakini, je, kuna suluhisho?

      a Unaweza kupata habari zenye kupendeza kuhusu hali ya wafu katika broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa?, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

      UNAONAJE?

      1. 1, 2. Kwa nini Mungu alikataza kula matunda ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya”?

      2. 3-6. Ni nini kilichowapata wanadamu na kufanya maisha yao yawe magumu?

      3. 7. Ni nini humpata mtu anapokufa?

      4. 8. Kwa nini sisi sote hufa?

  • Maisha Yenye Kuridhisha Yarudishwa
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • SEHEMU YA 8

      Maisha Yenye Kuridhisha Yarudishwa

      INGAWA mwanadamu alitumbukia katika maisha mabaya kwa sababu ya kuasi utawala wa Mungu, Mungu hakuwaacha wanadamu bila tumaini. Biblia inaeleza hivi: “Uumbaji ulitiishwa chini ya ubatili, si kwa mapenzi yake wenyewe bali kupitia yule aliyeutiisha, kwa msingi wa tumaini kwamba uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:20, 21) Naam, Mungu aliwapa tumaini wazao wa Adamu na Hawa. Lilikuwa tumaini hakika kwamba wanadamu wangewekwa huru kutokana na kifo na dhambi waliyorithi. Wangeweza kurudishwa kwenye uhusiano wa karibu na Yehova Mungu. Jinsi gani?

      Utumwa wa watoto

      Mungu aliwapa wanadamu tumaini ili waweze kukombolewa kutokana na utumwa wa dhambi na kifo

      2 Adamu na Hawa walipotenda dhambi, waliwanyima wazao wao fursa ya kuishi maisha yenye kuridhisha duniani milele. Kwa sababu ya kutaka haki ya kujiamulia mema na mabaya, waliiuza familia yao ya wakati ujao katika utumwa wa dhambi na kifo. Kwa kuwa walizaliwa katika familia hiyo, wazao wao wanaweza kufananishwa na watumwa waliofungiwa katika kisiwa cha mbali kinachotawaliwa na wafalme wakatili. Kwa kweli, kifo kimetawala kama mfalme juu ya wanadamu walio watumwa wa mfalme mwingine—dhambi. (Waroma 5:14, 21) Inaonekana hakuna mtu atakayewaokoa. Kwa sababu babu yao ndiye aliyewauza utumwani! Lakini mfadhili fulani anamtuma mwanawe, anayeleta malipo kamili yanayohitajika ili kuwakomboa wote ambao wamefungwa.—Zaburi 51:5; 146:4; Waroma 8:2.

      Yosefu na Maria pamoja na mtoto Yesu

      3 Katika mfano huo, mtu aliyewaokoa watumwa hao anawakilisha Yehova Mungu. Mwana aliyetoa malipo ili wawe huru ni Yesu Kristo. Kabla ya kuwa mwanadamu aliishi mbinguni akiwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. (Yohana 3:16) Yeye ndiye aliyeumbwa kwanza na Yehova, na viumbe wengine wote katika ulimwengu waliumbwa kupitia yeye. (Wakolosai 1:15, 16) Yehova alihamisha kimuujiza uhai wa Mwana huyo wa roho na kuuweka katika tumbo la uzazi la bikira fulani, na hivyo kufanya iwezekane mtoto huyo azaliwe akiwa mwanadamu mkamilifu, malipo yaliyohitajika ili kutimiza matakwa ya haki ya Mungu.—Luka 1:26-31, 34, 35.

      Yesu awafundisha wafuasi wake

      4 Yesu alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi, alibatizwa kwenye Mto Yordani. Alipobatizwa, alitiwa mafuta kwa roho takatifu, au nguvu za utendaji za Mungu. Basi, akawa Kristo, yaani “Mtiwa Mafuta.” (Luka 3:21, 22) Huduma ya Yesu duniani ilichukua miaka mitatu na nusu. Katika kipindi hicho, aliwafundisha wafuasi wake kuhusu “ufalme wa Mungu,” serikali ya mbinguni ambayo itawarudishia wanadamu uhusiano wenye amani pamoja na Yehova Mungu. (Luka 4:43; Mathayo 4:17) Yesu alijua jinsi wanadamu wanavyoweza kuishi kwa furaha, na akawapa wafuasi wake maagizo hususa kuhusu furaha. Kwa nini usisome Mathayo sura ya 5 hadi ya 7 katika Biblia yako uone baadhi ya mafundisho yake katika Mahubiri ya Mlimani?

      5 Tofauti na Adamu, Yesu alimtii Mungu kabisa. “Hakufanya dhambi.” (1 Petro 2:22; Waebrania 7:26) Hata alikuwa na haki ya kuishi milele duniani, lakini “alitoa uhai wake” ili amlipe Mungu kile ambacho Adamu alipoteza. Kwenye mti wa mateso, Yesu alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu. (Yohana 10:17; 19:17, 18, 28-30; Waroma 5:19, 21; Wafilipi 2:8) Kwa kufanya hivyo, Yesu aliandaa fidia, au malipo yanayohitajika ili kuwakomboa wanadamu kutoka kwenye utumwa wa dhambi na kifo. (Mathayo 20:28) Wazia kwamba unafanya kazi ngumu yenye mshahara mdogo katika kiwanda fulani, ukiishi kama mtumwa. Je, hungemshukuru sana mtu anayepanga kukukomboa kutoka kwenye kifungo hicho na yule anayejitolea kuutoa uhai wake kwa ajili ya uhai wako? Kupitia mpango wa fidia, ulipata nafasi ya kurudi kwenye familia ya Mungu ya ulimwenguni pote na kuishi maisha yanayoridhisha kwelikweli, ukiwa huru kutokana na utumwa wa dhambi na kifo.—2 Wakorintho 5:14, 15.

      Je, hungemshukuru sana mtu aliyekukomboa kutoka kifungoni?

      Wanajeshi wanamwinua Yesu kwenye mti wa mateso

      6 Kujua na kuthamini fadhili hizo zisizostahiliwa za Yehova kunakupa sababu kubwa zaidi ya kutumia maishani mwako maneno ya hekima yaliyo katika Biblia. Kwa mfano, fikiria mojawapo ya kanuni zilizo ngumu zaidi kufuata—kuwasamehe wengine wanapokuudhi. Je, unakumbuka maneno ya Wakolosai sura ya 3, mstari wa 12 hadi wa 14, ambayo tulizungumzia katika Somo la 2? Mistari hiyo ilikutia moyo uwasamehe wengine hata kama una sababu nzuri ya kulalamika juu yao. Muktadha unaonyesha ni kwa nini tunapaswa kufanya hivyo, unasema: “Kama vile Yehova alivyowasamehe kwa hiari, nanyi lazima mfanye vivyo hivyo.” Ukielewa vizuri mambo ambayo Yehova na Yesu Kristo wamewafanyia wanadamu, utachochewa kuwasamehe wengine makosa yoyote ambayo huenda wamefanya, hasa wanapotubu na kuomba msamaha.

      UNAONAJE?

      1. 1. Je, Yehova aliwaacha wanadamu bila tumaini?

      2. 2. Tunaweza kutumia mfano gani kufafanua jambo ambalo Adamu aliwatendea wazao wake?

      3. 3. Kwa nini Yesu Kristo alizaliwa na bikira?

      4. 4. Ni nini baadhi ya mafundisho ya Yesu Kristo, na kwa nini mafundisho hayo yana matokeo mazuri?

      5. 5, 6. Wewe binafsi una maoni gani kuhusu mambo ambayo Yehova na Yesu wamewafanyia wanadamu?

  • Furahia Maisha Yenye Kuridhisha Sasa na Milele!
    Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha
    • SEHEMU YA 9

      Furahia Maisha Yenye Kuridhisha Sasa na Milele!

      Unaweza kuishi maisha yenye kuridhisha ukisitawisha urafiki na Mungu

      ABRAHAMU, mtu mashuhuri mwenye imani anayetajwa katika historia ya Biblia, aliacha maisha mazuri katika jiji tajiri la Uru. Baada ya kuishi Harani kwa muda fulani, aliishi maisha yaliyobaki katika mahema naye alihamahama bila kuwa na makao maalumu. (Mwanzo 12:1-3; Matendo 7:2-7; Waebrania 11:8-10) Lakini, imeandikwa hivi kumhusu: “Abrahamu akakata pumzi na kufa baada ya kuishi maisha marefu, akiwa amezeeka na kuridhika.” (Mwanzo 25:8) Kwa nini maisha yake yaliridhisha sana? Akikaribia kufa, hakuwa tu mzee aliyeridhika kwa sababu ya mambo aliyotimiza maishani. Baadaye Abrahamu aliitwa “rafiki ya Yehova” kwa sababu alimwamini Mungu sana. (Yakobo 2:23; Isaya 41:8) Uhusiano mzuri ambao Abrahamu alisitawisha pamoja na Muumba wake ndio uliofanya awe na maisha yenye kuridhisha.

      Abrahamu akiwa karibu kufa

      Je, maisha yako yanaweza kuwa yenye kuridhisha kuliko ya Abrahamu?

      2 Ukisitawisha urafiki na Mungu kama Abrahamu alivyofanya miaka 4,000 hivi iliyopita, wewe pia unaweza kuishi maisha yenye maana na yenye kuridhisha. Huenda ukashangazwa sana na wazo la kuwa rafiki ya Muumba wa ulimwengu mzima, lakini inawezekana. Jinsi gani? Unahitaji kumjua na kumpenda. (1 Wakorintho 8:3; Wagalatia 4:9) Uhusiano kama huo na Muumba wako unaweza kuboresha maisha yako na kufanya yawe yenye kuridhisha.

      3 Yehova amewapa watu wanaokubali dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo mwongozo wa kuishi maisha yenye furaha. (Isaya 48:17) Kumbuka kwamba Adamu alimwasi Mungu kwa kujiamulia mema na mabaya. Ingawa Yehova aliwakomboa wanadamu kupitia dhabihu ya fidia ya Mwana wake, na kuwaweka huru kutoka kwa utumwa wa dhambi na kifo, ni lazima kila mtu akubali fidia hiyo na aache kujiamulia mwenyewe mema na mabaya. Ni lazima tutii sheria na kanuni ambazo Mungu anawapa wale wanaokubali dhabihu ya fidia ya Yesu.

      Kijana anasoma Biblia

      “Nifundishe njia zako”

      4 Unapoendelea kujifunza Biblia na kutumia kanuni zilizotajwa humo, bila shaka utaona umuhimu wa kufuata viwango vya Mungu kuhusu mema na mabaya. (Zaburi 19:7-9) Utachochewa kumwambia hivi Mungu, kama alivyofanya Musa, nabii wa Yehova: “Tafadhali, ikiwa nimepata kibali machoni pako, nifundishe njia zako ili nikujue.” (Kutoka 33:13; Zaburi 25:4) Biblia ina kanuni zinazoweza kukuongoza unapokabiliana na matatizo ya “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Utazipenda sana kanuni hizo, na kumfahamu Yehova zaidi na hivyo kuimarisha urafiki wako pamoja naye.

      5 Abrahamu alikufa akiwa “amezeeka na kuridhika,” lakini kwa kuwa bado wanadamu wanakufa, maisha ni mafupi sana. Hata tukizeeka sana, sisi sote tunatamani kuendelea kuishi. Hii ni kwa sababu “[Mungu] ameweka umilele katika moyo [wa wanadamu]; lakini bado wanadamu hawatajua kamwe kazi ambayo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.” (Mhubiri 3:11) Hata tukiishi milele, hatutaweza kamwe kujua uumbaji wote wa Yehova. Mambo tunayoweza kuona, kujifunza, na kufurahia kuhusu kazi za ajabu za Yehova hayana mwisho!—Zaburi 19:1-4; 104:24; 139:14.

      6 Labda hungependa kuishi milele katika dunia iliyojaa matatizo tunayoona leo. Lakini, hupaswi kuhangaishwa na jambo hilo. Biblia inaahidi hivi: “Tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Maneno “mbingu mpya” yanamaanisha serikali mpya ya mbinguni—Ufalme wa Mungu, ambao utatawala dunia nzima. “Dunia mpya” ni jamii mpya ya wanadamu ambao wanatii utawala wa Ufalme huo. Ili kutimiza jambo hilo, hivi karibuni Yehova atawachukulia hatua wale “wanaoiharibu dunia.”—Ufunuo 11:18; 2 Petro 3:10.

      Wanajeshi vitani; watoto wenye njaa; jengo lililoachwa

      7 Atachukua hatua lini? Alipotaja kuhusu “ishara . . . ya umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu Kristo alitia ndani vita kati ya mataifa, “upungufu wa chakula na matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali,” “magonjwa,” na “kuongezeka kwa uasi sheria.” (Mathayo 24:3-13; Luka 21:10, 11; 2 Timotheo 3:1-5) Kisha akatabiri hivi: “Mtakapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia.” (Luka 21:31) Kwa kweli, wakati ambapo Yehova atawaangamiza waovu unakaribia sana.a

      8 Baada ya “siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” Yehova atakapoondoa kabisa uovu duniani, dunia yetu itageuzwa kuwa paradiso. (Ufunuo 16:14, 16; Isaya 51:3) Kisha, “waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.” (Zaburi 37:29) Namna gani wale ambao wamekufa? Yesu alisema: “Msishangazwe na jambo hili, kwa maana saa inakuja ambayo wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka, wale waliotenda mema kwenye ufufuo wa uzima, na wale waliozoea kutenda maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:28, 29) Yehova, ambaye anapendezwa na kila mtu, anataka kuwafufua wale ambao wamelala katika kifo. Huenda wanasayansi wakajaribu kutokeza mwanadamu kupitia kurekebisha chembe za urithi, lakini Muumba hana haja ya kufanya hivyo. Anaweza kukumbuka kila jambo kuhusu kila mwanadamu anayeweza kukombolewa na kumfufua. Naam, una tumaini la kukutana na wapendwa wako waliokufa katika dunia paradiso!

      9 Maisha yatakuwaje katika Paradiso? Dunia itajaa wanaume na wanawake wenye furaha wanaomsifu Muumba kwa umoja. “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24; 54:13) Hakuna mtu atakayepatwa na matatizo ya kiafya kwa sababu ya mkazo na magonjwa ya kihisia na kiakili. Watu wote watakuwa na chakula kingi na watafurahia kazi ya maana kulingana na kusudi la Mungu. (Zaburi 72:16; Isaya 65:23) Watakuwa na amani pamoja na wanyama, amani pamoja na wanadamu wenzao na, zaidi ya yote, “amani pamoja na Mungu.”—Waroma 5:1; Zaburi 37:11; 72:7; Isaya 11:6-9.

      Watu katika Paradiso

      10 Unapaswa kufanya nini ili uishi katika Paradiso hiyo na kufurahia maisha yenye kuridhisha kabisa? Yesu Kristo alisema: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Basi endelea kupata ujuzi kumhusu Yehova na Yesu Kristo, na ujifunze mambo ambayo Mungu anataka ufanye. Kisha utampendeza Yehova Mungu, na hilo litafanya maisha yako yawe yenye kuridhisha sana.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki