-
Kutoa Kupita Uwezo WakoMnara wa Mlinzi—2002 | Desemba 1
-
-
Kutoa Kupita Uwezo Wako
“UNAWEZA kuniita omba-omba; lakini sijali. Mimi naomba pesa kwa ajili ya Yesu.” Maneno hayo ya kasisi Mprotestanti yanafunua mabishano yaliyopo kuhusu ugharimiaji wa shughuli za kidini. Yaonekana dini kubwa-kubwa huhitaji pesa nyingi ili kuweza kuendeleza shughuli zao. Mishahara inahitaji kulipwa, mahekalu yanahitaji kujengwa na kudumishwa, nayo kazi ya kueneza injili inahitaji kugharimiwa. Pesa hizo za lazima zitapatikanaje?
Makanisa mengi hutegemea fungu la kumi.a “Kutoa fungu la kumi ni njia ya Mungu ya kugharimia ufalme Wake duniani,” anasema mwinjilisti Norman Robertson. ‘Mungu hutumia njia hiyo ili kugharimia kuhubiriwa kwa Injili.’ Akiwakumbusha wafuasi wake kinaganaga kwamba wana daraka la kutoa, anasema hivi kwa mkazo: ‘Hutoi fungu la kumi kwa sababu unaweza. Ni tendo la utii. Unavunja amri za Mungu kwa kutotoa fungu la kumi, na huo ni wizi.’—Tithing—God’s Financial Plan.
Yaelekea unakubali kwamba kutoa michango kunapaswa kuwa sehemu ya ibada ya Kikristo. Hata hivyo, je, unasumbuliwa, labda hata kuudhika, unapoombwa tena na tena utoe pesa? Mwanatheolojia Inácio Strieder, kutoka Brazili, anashutumu makanisa kwa kutegemea fungu la kumi ili ‘kutatua matatizo yao ya kifedha’ na anataja zoea hilo kuwa “haramu, lenye uonevu, na lisilopatana na imani ya kidini.” Anasema matokeo yanakuwa kwamba “watu wasioajiriwa, wajane, wakazi wa mitaa ya mabanda, na wale wasioweza kuchanganua mambo watafikiri kwamba Mungu amewaacha na kwamba wanalazimika kumpa ‘mhubiri’ pesa nyingi sana kiasi cha kwamba familia zao zinakosa chakula.”
Huenda ukajiuliza: ‘Je, makanisa yanayolazimisha watu watoe fungu la kumi yanafuata Maandiko? Au yawezekana dini fulani zinatumia woga wa kuadhibiwa na Mungu ili kuwapokonya waumini pesa zao? Je, kwa kweli Mungu anatarajia tutoe kupita uwezo wetu?’
[Maelezo ya Chini]
a Fungu la kumi limefafanuliwa kuwa sehemu ya kumi ya mapato yote ya mtu.
-
-
Utoaji Unaoleta FurahaMnara wa Mlinzi—2002 | Desemba 1
-
-
Utoaji Unaoleta Furaha
GENIVAL anayeishi katika mtaa wa mabanda huko kaskazini-mashariki mwa Brazili, alimruzuku mke na watoto wake kwa mshahara mdogo aliopata akiwa askari mlinda-usalama kwenye hospitali moja. Licha ya magumu aliyokuwa nayo, Genival aliendelea kutoa fungu lake la kumi kwa uaminifu. “Wakati mwingine familia yangu ilikosa chakula,” anasema huku akishika-shika tumbo lake, “lakini nilitaka kumpa Mungu kilicho bora, haidhuru kungenigharimu nini.”
Hata baada ya kupoteza kazi yake, Genival aliendelea kutoa fungu la kumi. Kasisi wake alimhimiza amjaribu Mungu kwa kutoa mchango mkubwa, akimhakikishia kwamba Mungu angembariki sana kama angefanya hivyo. Kwa hiyo, Genival akaamua kuuza nyumba yake na kupeleka pesa zote kanisani.
Mbali na Genival watu wengi walio maskini sana hutoa fungu la kumi kwa unyofu. Wanafanya hivyo kwa sababu wanafundishwa na makanisa yao kwamba hilo ni takwa la Biblia.
-