Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kutegemeza Kazi ya Ufalme Kwenu na Ulimwenguni Pote
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • 11 Kila baada ya muda fulani, mipango hufanywa ili kukagua rekodi za pesa za mzunguko.

      KUWATUNZA MASKINI

      12 Kusudi moja la sanduku la pesa lililotunzwa na Yesu na wanafunzi wake lilikuwa kuwasaidia maskini. (Marko 14:3-5; Yoh. 13:29) Wajibu huo wa Kikristo unaendelea mpaka sasa, kwa kuwa Yesu alisema: “Maskini mnao sikuzote.” (Marko 14:7) Mashahidi wa Yehova hutimizaje wajibu huo leo?

      13 Nyakati nyingine, huenda washiriki waaminifu kutanikoni wakahitaji msaada kwa sababu ya uzee, udhaifu, au msiba mkubwa. Watu wa familia, na wengine ambao wanajua jambo hilo wanaweza kuwasaidia. Jambo hilo linapatana na maneno ya mtume Yohana: “Yeyote aliye na mali za ulimwengu huu akimwona ndugu yake akiwa na uhitaji naye akatae kumhurumia, anawezaje kuwa na upendo wa Mungu ndani yake? Watoto wadogo, tunapaswa kupendana, si kwa neno au kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yoh. 3:17, 18; 2 The. 3:6-12) Ibada ya kweli inahusisha kuwatunza waaminifu ambao huenda wanahitaji msaada wa kimwili.—Yak. 1:27; 2:14-17.

      14 Katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, mtume Paulo alieleza jinsi msaada unavyoweza kutolewa kwa wanaostahili. Unaweza kusoma ushauri wake kwenye 1 Timotheo 5:3-21. Ni jukumu la kila Mkristo kutunza mahitaji ya watu wa nyumbani mwake. Wazee kwa umri au walio dhaifu wanapaswa kusaidiwa na watoto wao, wajukuu wao, au watu wengine wa karibu wa ukoo. Nyakati nyingine, serikali au mashirika ya kijamii hutoa misaada, kwa hiyo watu wa ukoo au wengine wanaweza kumsaidia mwenye uhitaji aombe msaada huo kwa njia inayofaa. Huenda kukatokea hali inayolazimu kutaniko lote lifikirie kuwasaidia kwa njia fulani ndugu na dada wenye uhitaji ambao wamekuwa waaminifu kwa muda mrefu. Ikiwa watu wenye uhitaji hawana washiriki wa familia au watu wengine wa ukoo wanaoweza kuwasaidia, na serikali au mashirika ya kijamii hayatoi msaada wa kutosha, baraza la wazee linaweza kutoa mapendekezo yanayofaa ili kuwasaidia kwa njia fulani. Wakristo huona kuwa ni pendeleo kuwasaidia wenye uhitaji kwa mali zao.

      15 Huenda ndugu na dada wengi wakawa na uhitaji kwa sababu ya mateso, vita, matetemeko ya nchi, mafuriko, njaa, au misiba mingine ambayo ni ya kawaida katika siku hizi za hatari. (Mt. 24:7-9) Katika pindi hizo, huenda makutaniko yasiweze kuwasaidia, kwa hiyo Baraza Linaloongoza hupanga ili ndugu wa maeneo mengine wawasaidie. Wakristo wa Asia Ndogo walifanya vivyo hivyo walipowapa chakula ndugu wa Yudea kulipokuwa na njaa. (1 Kor. 16:1-4; 2 Kor. 9:1-5) Tunapoiga mfano wao, tunawathibitishia ndugu zetu kwamba tunawapenda na kuonyesha kwamba sisi ni wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo.—Yoh. 13:35.

      KUGAWA MACHAPISHO

      16 Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia husaidia sana kueneza ujumbe wa Ufalme. Kwa kawaida baraza la wazee humpa mtumishi wa huduma mgawo wa kutunza machapisho ya kutaniko. Ndugu waliopewa migawo hiyo huchukua majukumu yao kwa uzito. Wanaweka rekodi nzuri ya machapisho ili kutosheleza mahitaji ya kutaniko.

      17 Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, tunatambua kwamba wakati wetu, akili na nguvu, vipaji, mali zetu, hata uhai wetu wenyewe ni zawadi kutoka kwa Mungu na tunapaswa kuzitumia katika utumishi wake. (Luka 17:10; 1 Kor. 4:7) Tunapotumia vizuri kila kitu tulicho nacho, tunaonyesha kwamba tunampenda sana Yehova. Tunatamani sana kumheshimu Yehova kwa vitu vyetu vyenye thamani, tukijua kwamba anapendezwa na zawadi yoyote tunayomtolea ili kuonyesha kwamba tumejitoa kwake kwa nafsi yote. (Met. 3:9; Marko 14:3-9; Luka 21:1-4; Kol. 3:23, 24) Yesu alisema: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mt. 10:8) Tunapojitoa wenyewe na kila kitu tulicho nacho katika utumishi wa Yehova, tunapata shangwe kubwa sana.—Mdo. 20:35.

  • “Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • SURA YA 13

      “Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”

      TUKIWA watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna wajibu wa kusema na kufanya mambo yote kwa utukufu wa Yehova. Mtume Paulo alitoa kanuni inayotuongoza alipoandika hivi: “Iwe mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Hilo linatia ndani kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova vinavyoonyesha utu wake mkamilifu. (Kol. 3:10) Ni lazima tumwige Mungu tukiwa watu watakatifu.—Efe. 5:1, 2.

      2 Akikazia umuhimu wa Wakristo kuwa watakatifu, mtume Petro aliandika hivi: “Kama watoto watiifu, acheni kufinyangwa na tamaa mlizokuwa nazo zamani katika hali yenu ya kutojua, lakini iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote kama Yule Mtakatifu aliyewaita ninyi, kwa maana imeandikwa: ‘Lazima muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” (1 Pet. 1:14-16) Kama Waisraeli wa kale, wote katika kutaniko la Kikristo wanapaswa kudumisha utakatifu. Hilo linamaanisha kwamba wanapaswa kubaki safi na kuepuka kuchafuliwa na dhambi na mambo yasiyofaa ya ulimwengu. Hivyo wanatakaswa kwa ajili ya utumishi wa Yehova.—Kut. 20:5.

      3 Utakatifu unadumishwa kwa kufuata sheria na kanuni za Yehova zinazotajwa waziwazi katika Maandiko Matakatifu. (2 Tim. 3:16) Tulipojifunza Maandiko, tulifundishwa kumhusu Yehova na njia zake, na tukachochewa kumkaribia. Kujifunza Biblia kulitusadikisha kwamba tulihitaji kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na kutanguliza mapenzi ya Yehova maishani mwetu. (Mt. 6:33; Rom. 12:2) Ili kufanya hivyo, ilitubidi tuvae utu mpya.—Efe. 4:22-24.

      USAFI WA KIROHO NA WA MAADILI

      4 Si rahisi kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova nyakati zote. Adui yetu, Shetani Ibilisi, anajaribu kutukengeusha kutoka kwenye kweli. Pindi fulani ushawishi mbaya wa ulimwengu huu na mwelekeo wetu wa kutenda dhambi hufanya mambo yawe magumu. Ili tuishi kulingana na wakfu wetu tunahitaji kupigana vita vya kiroho. Maandiko yanatuambia kwamba tusishangae tunapopingwa au kujaribiwa. Tutateseka kwa ajili ya uadilifu. (2 Tim. 3:12) Tunaweza kufurahi tunapokuwa chini ya majaribu, tukijua kwamba majaribu hayo yanathibitisha kuwa tunafanya mapenzi ya Mungu.—1 Pet. 3:14-16; 4:12, 14-16.

      5 Ingawa Yesu alikuwa mkamilifu, alijifunza utii kutokana na mateso yaliyompata. Hakukubali kamwe kushindwa na vishawishi vya Shetani au kujitakia mambo makuu ya ulimwengu. (Mt. 4:1-11; Yoh. 6:15) Yesu hakufikiria kamwe kulegeza msimamo wake. Ingawa ulimwengu ulimchukia kwa sababu ya uaminifu wake, sikuzote alishikamana na viwango vya uadilifu vya Yehova. Muda mfupi kabla ya kufa, Yesu aliwatahadharisha wanafunzi wake kwamba ulimwengu ungewachukia wao pia. Tangu wakati huo, wafuasi wa Yesu wamepata dhiki nyingi, lakini wamejipa moyo kwa kujua kwamba Mwana wa Mungu aliushinda ulimwengu.—Yoh. 15:19; 16:33; 17:16.

      6 Ili tusiwe sehemu ya ulimwengu, tunahitaji kufuata viwango vya uadilifu vya Yehova kama alivyofanya Bwana wetu. Mbali na kuepuka mambo ya kisiasa na ya kijamii ya ulimwengu huu, tunapaswa kupinga maadili yake mapotovu. Tunapaswa kutii ushauri wa andiko la Yakobo 1:21: “Ondoeni uchafu wote na ubaya wote, na pokeeni kwa upole kupandwa kwa lile neno linaloweza kuwaokoa.” Tunapojifunza na kuhudhuria mikutano, ‘tunapanda lile neno’ la kweli akilini na mioyoni mwetu, na hatutatamani hata kidogo mambo ya ulimwengu. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.” (Yak. 4:4) Kwa sababu hiyo, Biblia inatuhimiza kwa uthabiti tufuate viwango vya uadilifu vya Yehova na kujitenga na ulimwengu.

      7 Neno la Mungu linatuonya kwamba tusishiriki katika mwenendo wa aibu na mpotovu. Linasema hivi: “Uasherati na kila namna ya ukosefu wa usafi au pupa visitajwe kamwe miongoni mwenu, kama inavyowafaa watu watakatifu.” (Efe. 5:3) Kwa hiyo, hatutaruhusu kamwe akili yetu iendelee kufikiria mambo machafu ya aibu au yaliyopotoka, wala hatutaruhusu kamwe mambo hayo yaingie katika mazungumzo yetu. Kwa kufanya hivyo, tunathibitisha kwamba tunataka kufuata viwango safi na vya uadilifu vya Yehova kuhusu maadili.

      USAFI WA KIMWILI

      8 Mbali na usafi wa kiroho na wa maadili, Wakristo hutambua umuhimu wa kuwa safi kimwili. Katika Israeli la kale, Mungu mtakatifu aliwaagiza wadumishe usafi kambini. Sisi pia tunapaswa kuwa safi ili Yehova “asione kitu chochote kichafu” ndani yetu.—Kum. 23:14.

      9 Katika Biblia, utakatifu unahusianishwa na usafi wa kimwili. Kwa mfano, Paulo aliandika hivi: “Wapendwa . . . acheni tujisafishe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Kor. 7:1) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli wanapaswa kujitahidi kuwa safi kimwili kwa kuoga na kufua nguo zao kwa ukawaida. Ijapokuwa hali hutofautiana katika nchi mbalimbali, kwa kawaida tunaweza kupata sabuni na maji ya kutosha kuoga na kuhakikisha kwamba watoto wetu ni wasafi.

      10 Tunajulikana sana katika jamii kwa sababu ya kazi yetu ya kutoa ushahidi. Kudumisha mpangilio mzuri na usafi, ndani na nje ya nyumba, ni njia mojawapo ya kuwatolea ushahidi jirani zetu. Familia nzima inaweza kushiriki kufanya hivyo. Akina ndugu wanapaswa kuzingatia usafi wa nyumba na mazingira yake, wakijua kwamba mazingira mazuri ya nyumbani huwavutia wengine. Kuzingatia usafi na pia kuongoza katika mambo ya kiroho, huonyesha kwamba wanasimamia vyema nyumba zao. (1 Tim. 3:4, 12) Akina dada pia wana jukumu la kudumisha usafi, hasa ndani ya nyumba. (Tito 2:4, 5) Watoto waliozoezwa vizuri hutimiza jukumu lao kwa kuwa wasafi na kudumisha mpangilio mzuri na usafi wa vyumba vyao. Hivyo, familia hushirikiana kusitawisha utaratibu wa usafi ambao tutafuata katika ulimwengu mpya chini ya Ufalme wa Mungu.

      11 Watumishi wengi wa Yehova leo hutumia magari kwenda kwenye mikutano. Katika maeneo fulani, inalazimu kuwa na gari katika huduma. Gari hilo linapaswa kuwa safi na kudumishwa vizuri. Nyumba na magari yetu yanapaswa kuonyesha kwamba sisi ni watu wa Yehova walio safi na watakatifu. Kanuni hiyo inahusu pia mikoba na Biblia tunazotumia katika utumishi wa shambani.

      12 Mavazi na mapambo yetu yanapaswa kupatana na kanuni za Mungu. Hatuwezi kwenda mbele ya watu mashuhuri tukiwa tumevaa isivyofaa au ovyoovyo. Je, hatupaswi kuvaa vizuri hata zaidi tunapomwakilisha Yehova katika utumishi wa shambani au jukwaani? Mavazi na mapambo yetu yanaweza kuathiri jinsi wengine wanavyoiona ibada ya Yehova. Bila shaka haingefaa kuvaa kwa njia isiyo na kiasi au bila kuwajali wengine. (Mika 6:8; 1 Kor. 10:31-33; 1 Tim. 2:9, 10) Kwa hiyo, tunapojitayarisha kwenda utumishi wa shambani, mikutanoni au makusanyikoni, tunapaswa kukumbuka yale ambayo Biblia husema kuhusu usafi wa kimwili, mavazi na mwonekano wetu. Sikuzote tunataka kumheshimu na kumtukuza Yehova.

      Tukiwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna wajibu wa kusema na kufanya mambo yote kwa utukufu wa Yehova

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki