Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Utoaji Unaoleta Furaha
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Desemba 1
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

      Je, Waandishi wa Kanisa wa Mapema Walifundisha Kuhusu Kutoa Fungu la Kumi?

      “Wale walio matajiri kati yetu huwasaidia walio na uhitaji . . . Walio na mali na wanaotaka, hutoa wanachoona kinafaa.”—Kichapo The First Apology cha Justin Martyr, cha mwaka wa 150 hivi W.K.

      “Wayahudi waliweka wakfu kwa Mungu fungu la kumi la mali zao, lakini wale walio huru huweka kando mali zao zote kwa ajili ya kazi za Mungu, . . . kama yule mjane maskini ambaye alitia katika sanduku la hazina ya Mungu riziki yake yote.”—Kichapo Against Heresies, cha Irenaeus cha mwaka wa 180 hivi W.K.

      “Ingawa tuna sanduku la michango, pesa tunazochanga si za kununua wokovu kama ilivyo katika dini nyingine. Kila mmoja hutoa mchango mdogo mara moja kwa mwezi; lakini hufanya hivyo akipenda, na ikiwa tu anaweza: kwa kuwa watu hawalazimishwi; wanatoa kwa hiari.”—Kichapo Apology cha Tertullian cha mwaka wa 197 hivi W.K.

  • Utoaji Unaoleta Furaha
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Desemba 1
    • Utoaji wa Kikristo

      Hata hivyo, michango ya kutegemeza ibada ya kweli bado ilihitajiwa. Yesu aliwatuma wanafunzi wake ‘wawe mashahidi hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.’ (Matendo 1:8) Uhitaji wa kuwa na walimu Wakristo na waangalizi wa kutembelea na kuyatia nguvu makutaniko uliongezeka kadiri idadi ya waamini ilivyoongezeka. Wajane, mayatima, na watu wengine wenye uhitaji walipaswa kutunzwa nyakati nyingine. Wakristo wa karne ya kwanza waligharimiaje mambo hayo?

      Mnamo mwaka wa 55 W.K., Wakristo wasio Wayahudi wa Ulaya na Asia Ndogo waliombwa wasaidie kutaniko maskini la Yudea. Katika barua zake kwa kutaniko la Korintho, mtume Paulo anaeleza jinsi ukusanyaji wa ‘mchango kwa ajili ya watakatifu’ ulivyopangwa. (1 Wakorintho 16:1) Huenda ukashangazwa na yale Paulo aliyosema kuhusu utoaji wa Kikristo.

      Mtume Paulo hakuwabembeleza waamini wenzake watoe. Kwa kweli Wakristo wa Makedonia waliokuwa “chini ya taabu kubwa” na katika “umaskini wa kina kirefu” walilazimika ‘kufuliza kumwomba kwa kusihi sana ili wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili na kuwa na ushiriki katika huduma waliyokusudiwa watakatifu.’—2 Wakorintho 8:1-4.

      Ni kweli kwamba Paulo aliwatia moyo Wakorintho waliokuwa matajiri waige ndugu zao wa Makedonia waliokuwa wakarimu. Hata hivyo, kitabu kimoja cha kitaalamu kinasema kwamba ‘alikataa kutoa maagizo, na badala yake akawaomba, akawatolea madokezo, akawatia moyo, na kuwasihi. Wakorintho hawangetoa kwa hiari wala kwa uchangamfu kama wangelazimishwa.’ Paulo alijua kwamba “Mungu hupenda mpaji mchangamfu,” hapendi yule anayetoa “kwa kinyongo au kwa shurutisho.”—2 Wakorintho 9:7.

      Imani yao kubwa, ujuzi, pamoja na upendo wa kweli kwa Wakristo wenzao ungewachochea Wakorintho watoe kwa hiari.—2 Wakorintho 8:7, 8.

      “Kama Vile Ameazimia Moyoni Mwake”

      Badala ya kutaja kiasi hususa cha pesa, Paulo alipendekeza tu kwamba ‘kila mmoja atenge kiasi cha fedha kadiri ya mapato yake’ katika siku ya kwanza ya juma. (1 Wakorintho 16:2, Biblia Habari Njema) Kwa kupanga na pia kutenga kando kiasi fulani kwa ukawaida, Wakorintho hawangehisi kwamba wanashurutishwa kutoa michango yao, wala hawangeitoa kwa sababu ya msisimuko tu wakati Paulo alipofika. Kila Mkristo angeamua kibinafsi ni kiasi gani angetoa, kulingana na ‘alichokuwa ameazimia moyoni mwake.’—2 Wakorintho 9:5, 7.

      Wakorintho walihitaji kupanda kwa wingi ili wavune kwa wingi. Paulo hakusema lolote kuhusu kutoa kupita uwezo wa mtu. ‘Sikusudii iwe vigumu kwenu,’ Paulo akawahakikishia. Michango ‘ilikubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.’ (2 Wakorintho 8:12, 13; 9:6) Katika barua fulani aliyoandika baadaye, mtume alionya: “Ikiwa yeyote hawaandalii kitu . . . wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Paulo hakuwahimiza watu watoe kwa njia iliyovunja kanuni hiyo.

      Inafaa kuona kwamba Paulo alisimamia ukusanyaji wa ‘mchango kwa ajili ya watakatifu’ waliokuwa na uhitaji. Maandiko hayasemi popote pale kwamba Paulo au mitume wengine walipanga michango itolewe au walipokea fungu la kumi ili kugharimia huduma zao wenyewe. (Matendo 3:6) Paulo alishukuru daima kwa zawadi ambazo makutaniko yalimpelekea, naye alikuwa mwangalifu asiwatwike ndugu zake “mzigo ulemeao wenye gharama.”—1 Wathesalonike 2:9; Wafilipi 4:15-18.

      Kutoa kwa Hiari Leo

      Ni wazi kwamba wafuasi wa Kristo katika karne ya kwanza walitoa michango ya hiari, wala si fungu la kumi.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki