-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Jitihada za Kuhudhuria
Makusanyiko mengi yalifanywa katika maeneo yaliyo mbali na barabara kuu yasiyofikika kwa urahisi. Robinson Shamuluma anakumbuka kusanyiko alilohudhuria mnamo 1959. Anasema: “Tukiwa watu 15 hivi, tuliendesha baiskeli hadi Kabwe katika Mkoa wa Kati. Tulibeba unga wa mahindi na samaki waliokaushwa. Usiku tulilala vichakani. Tulipofika Kabwe tulipanda gari-moshi, na hatimaye tukafika kusanyikoni baada ya kusafiri kwa karibu siku nne.”
Lamp Chisenga anamkumbuka ndugu mmoja ambaye pamoja na watoto wake sita, alitembea na kuendesha baiskeli kwa karibu kilometa 130 ili kuhudhuria kusanyiko. Anasema: “Walitayarisha mihogo iliyochomwa, njugu-karanga, na siagi ya njugu kwa ajili ya safari. Mara nyingi walilazimika kupiga kambi vichakani bila ulinzi wowote.”
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Wakati wa makusanyiko ya wilaya mwaka fulani, tulisafiri kwa gari kaskazini mwa nchi. Katika sehemu hiyo kuna barabara chache. Tulikiona kikundi cha watu barabarani, umbali wa kilometa kadhaa kutoka kijiji fulani. Mmoja wao alikuwa mzee mkongwe aliyetembea kwa kutumia bakora. Alibeba viatu vyake pamoja na mfuko mdogo wenye vitu vichache mgongoni. Tulipowakaribia tuliona kwamba mzee huyo na wale wengine walikuwa na beji za kusanyiko. Tulisimama na kuwauliza walikotoka. Yule ndugu mzee alijinyoosha kidogo na kusema: “Umesha sahau. Tulikuwa pamoja nanyi kusanyikoni huko Chansa. Sasa tumekaribia nyumbani.”
“Mlitoka kusanyikoni lini?” tukauliza.
“Tulitoka Jumapili mara tu kusanyiko lilipomalizika.”
“Lakini leo ni Jumatano. Je, mmetembea kwa siku tatu?”
“Naam, na jana usiku tuliwasikia simba wakinguruma.”
“Nyote mnastahili pongezi kwa roho yenu bora na jinsi mnavyojitolea ili kuhudhuria makusanyiko.”
Huyo ndugu mzee alichukua vitu vyake, akaanza kutembea, na kusema: “Hilo ni jambo dogo tu. Nenda ukawashukuru ndugu kwenye ofisi ya tawi kwa kutupangia mahali papya pa kusanyiko. Mwaka uliopita tulichapa miguu kwa siku tano, lakini mwaka huu tumetembea kwa siku tatu tu.”
Wengi wanakumbuka ile njaa iliyokumba Zambia mwaka wa 1992. Tulikuwa kwenye kusanyiko lililofanywa kando ya Mto Zambezi, umbali wa kilometa 200 kutoka Maporomoko ya Victoria. Jioni moja tulizungumza na watu wa familia mbalimbali ambao wengi wao walikuwa wakiota moto nje ya vibanda vyao vidogo. Kikundi kimoja cha watu 20 hivi kilikuwa kikiimba nyimbo za Ufalme. Walituambia kwamba walikuwa wametembea kwa siku nane ili wahudhurie kusanyiko. Hawakuliona hilo kuwa jambo kubwa. Wanyama wao walibeba vifurushi vya chakula, vyombo vya kupikia, na vitu vingine vya lazima, na vilevile watoto wadogo. Walilala popote pale walipokuwa wamefika giza lilipoingia.
-