-
Yehova Anawakutanisha Watu Wake Wenye ShangweMnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 15
-
-
2 Kwa maelfu ya miaka iliyopita, watu wa Mungu walifanya pia makusanyiko matakatifu. Tutachunguza makusanyiko fulani yanayotajwa katika Maandiko ambayo ni kielelezo kwa makusanyiko ya leo. Angalia ulinganifu uliopo kati ya makusanyiko hayo na makusanyiko ya leo, na ukazie fikira faida tunazopata tunapohudhuria makusanyiko hayo.—Zab. 44:1; Rom. 15:4.
MAKUSANYIKO MUHIMU YA ZAMANI NA YA LEO
3. (a) Ni nini kilichotukia katika kusanyiko la kwanza la watu wa Yehova linalotajwa katika Biblia? (b) Ni nini kilichotumiwa kuwaita Waisraeli wakusanyike pamoja?
3 Kusanyiko lililofanywa chini ya Mlima Sinai ndilo kusanyiko la kwanza kubwa zaidi la watu wa Mungu. Walikusanyika ili kupata maagizo ya kiroho. Kwa kweli lilikuwa kusanyiko muhimu katika historia ya ibada safi. Katika pindi hiyo yenye kusisimua, ambayo bila shaka wahudhuriaji hawangeweza kamwe kuisahau, Yehova aliwaonyesha Waisraeli nguvu zake alipowapa Sheria yake. (Kut. 19:2-9, 16-19; soma Kutoka 20:18; Kumbukumbu la Torati 4:9, 10.) Tukio hilo lilikuwa msingi wa jinsi Mungu alivyoshughulika na taifa la Israeli baadaye. Muda mfupi baadaye, Yehova alianzisha njia mpya ya kuwakusanya watu wake. Alimwagiza Musa atengeneze tarumbeta mbili za fedha ambazo zingetumiwa kuliita “kusanyiko lote” ili likutane “kwenye mwingilio wa hema la mkutano.” (Hes. 10:1-4) Wazia msisimuko uliokuwapo katika pindi hizo!
4, 5. Kwa nini makusanyiko yaliyofanywa na Musa na Yoshua yalikuwa muhimu sana?
4 Walipokuwa wakikaribia mwisho wa safari yao ya miaka 40 nyikani, Musa aliwakusanya Waisraeli wenzake. Huo ulikuwa wakati muhimu zaidi katika historia ya taifa hilo jipya. Walikuwa karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi. Huo ulikuwa wakati unaofaa kabisa wa Musa kuwakumbusha ndugu zake mambo yote ambayo Yehova alikuwa amewafanyia na yale ambayo angewafanyia.—Kum. 29:1-15; 30:15-20; 31:30.
5 Labda katika kusanyiko hilohilo, Musa alizungumza kuhusu mipango ya kawaida ya makusanyiko na ya kuwaelimisha watu wa Mungu. Katika miaka ya Sabato, wakati wa Sherehe ya Vibanda, wanaume, wanawake, watoto, na wakaaji wageni katika Israeli walipaswa kukutana mahali ambapo Yehova alichagua ‘ili wasikilize na ili wajifunze kumwogopa Yehova na kuwa waangalifu kuyatimiza maneno yote ya sheria.’ (Soma Kumbukumbu la Torati 31:1, 10-12.) Kwa hiyo, mwanzoni kabisa mwa historia ya watu wa Mungu, ilikuwa wazi kwamba walipaswa kukusanyika kwa ukawaida ili kujifunza neno la Yehova na makusudi yake. Waisraeli walipoimiliki kikamili Nchi ya Ahadi huku wakiwa wamezungukwa na mataifa ya kipagani, Yoshua aliwakusanya Waisraeli wote ili kuimarisha azimio lao la kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova. Waisraeli walikubali na kuapa kumtumikia Mungu.—Yos. 23:1, 2; 24:1, 15, 21-24.
-
-
Yehova Anawakutanisha Watu Wake Wenye ShangweMnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 15
-
-
PINDI ZA KAWAIDA ZENYE SHANGWE
11. Mungu alianzisha mpango gani wa sherehe za kawaida za majira katika taifa la kale la Israeli?
11 Kila mwaka, Yehova aliwataka Waisraeli wakusanyike huko Yerusalemu kwa ajili ya sherehe tatu za majira, yaani, Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, Sherehe ya Majuma (baadaye iliitwa Pentekoste), na Sherehe ya Vibanda. Mungu aliamuru hivi kuhusu sherehe hizo: “Pindi tatu katika mwaka kila mwanamume wa kwako ataonekana mbele za uso wa Bwana wa kweli, Yehova.” (Kut. 23:14-17) Kwa kuwa walitambua thamani kubwa ya kiroho ya sherehe hizo, vichwa vingi vya familia walihudhuria pamoja na washiriki wote wa familia zao.—1 Sam. 1:1-7; Luka 2:41, 42.
12, 13. Waisraeli wengi walihitaji kufanya jitihada gani ili kuhudhuria sherehe za kila mwaka?
12 Hebu fikiria jitihada ambazo familia ya Mwisraeli ilihitaji kufanya ili kufunga safari hiyo. Kwa mfano, Yosefu na Maria walisafiri umbali wa kilomita 100 hivi kutoka Nazareti kwenda Yerusalemu. Unafikiri ingekuchukua muda gani kufunga safari hiyo, huku ukitembea pamoja na watoto wadogo? Simulizi kuhusu safari ya Yesu ya kwenda Yerusalemu akiwa mvulana linaonyesha kwamba nyakati nyingine watu wa ukoo na marafiki walifunga safari kama hizo wakiwa kikundi. Bila shaka, walifurahi sana kusafiri pamoja na kupika chakula pamoja na kutafuta mahali panapofaa pa kulala katika maeneo wasiyojua. Inaonekana kwamba kulikuwa na usalama wa kutosha kwa sababu mtoto mwenye umri wa miaka 12 kama Yesu alipewa kiasi fulani cha uhuru na wazazi wake. Wazia jinsi ambavyo sherehe hizo hazingeweza kusahaulika, hasa kwa watoto!—Luka 2:44-46.
13 Waisraeli walipotawanywa katika sehemu mbalimbali nje ya mipaka ya nchi yao, wale waliohudhuria sherehe hizo walitoka katika mataifa mengi. Wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Wayahudi na watu waliogeuzwa imani waliothamini sherehe hizo walisafiri kwenda Yerusalemu kutoka katika maeneo kama vile Italia, Libya, Krete, Asia Ndogo, na Mesopotamia.—Mdo. 2:5-11; 20:16.
14. Waisraeli walifaidikaje kwa kuhudhuria sherehe za kila mwaka?
14 Kwa Waisraeli waaminifu, jambo muhimu kuhusiana na safari hizo lilikuwa faida za kiroho, yaani, kumwabudu Yehova kwa bidii pamoja na maelfu ya waabudu wenzao waliothamini sherehe hizo. Matokeo yalikuwa nini kwa waliohudhuria? Jibu linapatikana katika maagizo ambayo Yehova aliwapa watu wake kuhusu Sherehe ya Vibanda: “Nawe utashangilia wakati wa sherehe yako, wewe na mwana wako na binti yako na mtumishi wako na kijakazi wako na Mlawi na mkaaji mgeni na mvulana asiye na baba na mjane, walio ndani ya malango yako. Siku saba utamfanyia Yehova Mungu wako sherehe katika mahali ambapo Yehova atapachagua, kwa sababu Yehova Mungu wako atakubariki katika mazao yako yote na katika kila tendo la mkono wako, nawe utakuwa na shangwe kwelikweli.”—Kum. 16:14, 15; soma Mathayo 5:3.
-