-
Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu WetuMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Kupanga Kitengenezo Mikusanyiko ya Kimataifa
Kwa zaidi ya nusu karne, Mashahidi wa Yehova wamefanya mikusanyiko mikubwa, mikusanyiko iliyofanywa sawia katika majiji mengi katika nchi nyingi. Hisi yao ya udugu wa kimataifa imeongezeka katika pindi hizo walipokuwa wameweza wote kusikia hotuba kuu zikitoka jiji moja kuu.
Hata hivyo, haikuwa mpaka 1946, wakati mkusanyiko mkubwa wa kimataifa ulipoleta pamoja katika jiji moja wajumbe kutoka sehemu nyingi za dunia. Hiyo ilikuwa katika Cleveland, Ohio. Ijapokuwa bado ilikuwa vigumu kusafiri baada ya vita, hudhurio lilifika 80,000, kutia wajumbe 302 kutoka nchi 32 nje ya Marekani. Vipindi viliongozwa kwa lugha 20. Mafunzo mengi mazuri yenye kutumika yalitolewa kwa lengo la kupanua kazi ya kueneza evanjeli. Mojawapo mambo makuu ya mkusanyiko lilikuwa hotuba ya Ndugu Knorr juu ya matatizo ya kujenga upya na kupanua. Wasikilizaji walipiga makofi kwa idili waliposikia mipango ya kuongeza vifaa vya uchapaji na vya ofisi vya makao makuu ya Sosaiti, pamoja na vifaa vyao vya usambazaji wa redio na kuanzisha ofisi za tawi katika nchi kubwakubwa za ulimwengu, kupanua vifaa vyayo vya usambazaji wa redio, kuongezea kazi ya mishonari. Mara baada ya mkusanyiko huo, mambo mengi yalitayarishwa ili Ndugu Knorr na Ndugu Henschel waweze kufunga safari ya ulimwenguni pote kutekeleza yaliyokuwa yamezungumzwa.
Katika miaka iliyofuata, mikusanyiko yenye kufanyiza historia kwelikweli ilifanywa katika Yankee Stadium ya New York City. Kwenye ule wa kwanza wayo, kuanzia Julai 30 hadi Agosti 6, 1950, wajumbe walikuwapo kutoka nchi 67. Programu ilitia ndani ripoti fupi zilizotolewa na watumishi wa matawi, wamishonari, na wajumbe wengine. Hao waliupa mkusanyiko mambo yenye kusisimua kuonyesha ile kazi ya bidii ya kueneza evanjeli iliyokuwa ikifanywa katika nchi zote walikokuwa wametoka. Siku ya mwisho, hudhurio lilipanda kufika 123,707 kwa ajili ya hotuba “Je, Unaweza Kuishi Milele kwa Furaha Duniani?” Kichwa cha mkusanyiko kilikuwa “Ongezeko la Theokrasi.” Uangalifu ulielekezwa kwenye ongezeko kubwa la idadi. Hata hivyo, kama vile mwenyekiti, Grant Suiter, alivyoonyesha kwa mkazo, hilo halikufanywa ili kusifu watu wenye akili sana katika tengenezo lionekanalo. Bali, alijulisha: “Yehova ndiye wa kusifiwa kwa ajili ya idadi hiyo kubwa. Yapaswa kuwa hivyo, nasi hatungetaka iwe vingine.”
Katika 1953, mkusanyiko mwingine ulifanywa Yankee Stadium katika New York. Wakati huo hudhurio lilikuwa na kilele cha 165,829. Kama ilivyokuwa kwa mkusanyiko wa kwanza hapo, programu ilijaa mazungumzo ya unabii mbalimbali wa Biblia wenye kusisimua, shauri lenye kutumika juu ya jinsi ya kufanya kazi ya kuhubiri habari njema, na ripoti kutoka nchi nyingi. Ijapokuwa vipindi vilianza kama saa 3:30 asubuhi, kwa kawaida havikumalizika mpaka 3:00 au 3:30 usiku. Mkusanyiko huo uliandaa siku nane kamili za karamu ya kiroho yenye shangwe.
Kwa ajili ya mkusanyiko wao mkubwa kupita yote, katika New York katika 1958, ilikuwa lazima kutumia Yankee Stadium na pia Polo Grounds ulio karibu pamoja na maeneo ya ziada nje ya stediamu ili umati wa ziada wa mkusanyiko upate mahali pa kukaa. Siku ya mwisho, wakati kila kiti kilipokuwa kimekaliwa, ruhusa ya pekee ilitolewa kutumia hata sehemu ya ndani ya uwanja wa michezo wa Yankee Stadium, na ilisisimua kama nini kuona maelfu yakimiminika, yakatoa viatu, na kuketi kwenye nyasi! Idadi ilionyesha kuwa 253,922 walihudhuria kusikia hotuba ya watu wote. Uthibitisho zaidi wa baraka ya Yehova juu ya huduma ya watumishi wake ulionwa wakati 7,136 kwenye mkusanyiko huo walipoonyesha wakfu wao kwa uzamisho wa maji—zaidi ya mara mbili ya idadi ya waliobatizwa katika ile pindi yenye kufanyiza historia ya Pentekoste 33 W.K., kama ilivyoripotiwa katika Biblia!—Mdo. 2:41.
Uendeshaji wote wa mikusanyiko hiyo ulitoa uthibitisho wa jambo lililo zaidi ya tengenezo lenye ufanisi. Ulikuwa udhihirisho wa roho ya Mungu ikifanya kazi miongoni mwa watu wake. Upendo wa kidugu ambao msingi wao ni kumpenda Mungu ulionekana wazi kila mahali. Hakukuwa na wapangaji mambo wenye kulipwa mshahara. Kila idara iliendeshwa na wenye kujitolea wasiolipwa. Ndugu na dada Wakristo, mara nyingi vikundi vya familia, walishughulikia viburudisho. Pia walitayarisha milo yenye moto, na katika mahema makubwa nje ya stediamu, walipakulia wajumbe milo kwa mwendo wa kufikia elfu moja kwa dakika moja. Makumi ya maelfu—wote wakiwa na furaha ya kushiriki kazi—walitumikia wakiwa wakaribishaji na wakashughulikia ujenzi wote uliohitajiwa, upishi na upakuaji wa milo, usafi, na mengi zaidi.
Wenye kujitolea wengine wengi walitumia mamia ya maelfu ya saa ili kutimiza mahitaji ya mahali pa kulala ya wajumbe. Katika miaka fulani, ili kutimiza mahitaji ya angalau baadhi ya wakusanyikaji, majiji yalipangwa kwa kutumia mahema na trela. Katika 1953 Mashahidi walimvunia mkulima mmoja katika New Jersey hekta 16 za nafaka bila malipo, ambaye aliwakodisha shamba lake kwa ajili ya jiji lao la trela. Vyoo, umeme, mabafu, madobi, kafeteria, na maduka, yalijengwa ili kutimiza mahitaji ya idadi iliyozidi 45,000. Walipoingia mahali hapo, jiji lilijengwa kwa usiku mmoja. Maelfu mengi zaidi walipata mahali pa kulala katika mahoteli na nyumba za watu binafsi katika New York. Ilikuwa kazi kubwa mno. Kwa baraka za Yehova, ilitimizwa kwa mafanikio.
Mikusanyiko Katika Mwendo
Washiriki wa udugu huu wa kimataifa wanapendezwa sana na Mashahidi wenzao katika nchi nyinginezo. Likiwa tokeo, wametumia fursa ili kuhudhuria mikusanyiko nje ya nchi za nyumbani kwao.
Wakati kusanyiko la kwanza kati ya ule mfululizo wa Ibada Safi Kusanyiko lilipofanywa katika Wembley Stadium katika London, Uingereza, katika 1951, Mashahidi kutoka nchi 40 walikuwapo. Programu ilikazia upande wenye kufaa wa ibada ya kweli na kufaa kwa mtu kufanya huduma kuwa kazi yake ya maisha. Kutoka Uingereza, Mashahidi wengi walisafiri kwenda Bara Ulaya, ambapo mikusanyiko mingine tisa ilifanywa wakati wa miezi miwili iliyofuata. Mkubwa kupita yote kati yayo ulikuwa katika Frankfurt am Main, Ujerumani, ambapo 47,432 walikuwapo kutoka nchi 24. Uchangamfu wa akina ndugu ulionyeshwa mwishoni mwa programu wakati okestra ilipoanza kupiga muziki nao ndugu Wajerumani wakaanza ghafula kuimba kutoka moyoni wimbo wa kuaga wakiwakabidhi kwa Mungu Mashahidi wenzao waliokuwa wamekuja kutoka ng’ambo kujiunga nao. Vitambaa vya mkononi vilipungwapungwa, na mamia wakamiminika uwanjani kuonyesha uthamini wao binafsi kwa ajili ya karamu hiyo nzuri ya kitheokrasi.
Katika 1955, Mashahidi zaidi walipanga kutembelea ndugu zao Wakristo katika ng’ambo wakati wa mkusanyiko. Kwa njia ya meli mbili zilizokodiwa (kila moja ikiwa na abiria 700) na ndege 42 zilizokodiwa, wajumbe kutoka Marekani na Kanada walienda Ulaya. Chapo la Ulaya la gazeti The Stars and Stripes, lililosambazwa katika Ujerumani, lilieleza mmiminiko wa Mashahidi kuwa ‘labda ndio Waamerika wengi zaidi waliopata kwenda Ulaya tangu uvamizi wa Mataifa Marafiki wakati wa Vita ya Ulimwengu 2.’ Wajumbe wengine walikuja kutoka Amerika ya Kati na ya Kusini, Asia, Afrika, na Australia. Zijapokuwa jitihada za makasisi wa Jumuiya ya Wakristo za kuzuia Mashahidi wasifanye mikusanyiko yao katika Roma na Nuremberg, hiyo miwili na mingine sita ilifanywa katika Ulaya wakati wa kiangazi. Hudhurio lilikuwa kuanzia 4,351 katika Roma kufika 107,423 katika Nuremberg. Kikundi kingine cha 17,729 kilikusanyika Waldbühner katika ile iliyokuwa wakati huo Berlin Magharibi, ambapo ndugu kutoka eneo la Mashariki la enzi hiyo wangeweza kufika bila hatari kubwa. Wengi kati yao walikuwa wamekuwa katika gereza kwa ajili ya imani yao au walikuwa na washiriki wa familia waliokuwa gerezani wakati huo, lakini walikuwa wangali thabiti katika imani. Kichwa cha mkusanyiko kilifaa kama nini—“Ufalme Wenye Kushinda”!
Ingawa tayari kulikuwa kumekuwa mikusanyiko mingi ya kimataifa, lililotukia katika 1963 lilikuwa la kwanza la aina yake. Ulikuwa mkusanyiko wa ulimwenguni pote. Ukianzia Milwaukee, Wisconsin, katika Marekani, ulisonga mbele kwenda New York; kisha, kwenye majiji makubwa manne katika Ulaya; kupitia Mashariki ya Kati; kusonga mbele hadi India, Burma (sasa Myanmar), Thailand, Hong Kong, Singapore, Filipino, Indonesia, Australia, Taiwan, Japani, New Zealand, Fiji, Jamhuri ya Korea, na Hawaii; na kisha kurudi kwenye bara la Amerika Kaskazini. Kwa ujumla, wajumbe kutoka nchi 161 walikuwapo. Jumla ya hudhurio ilizidi 580,000. Walikuwapo 583, kutoka nchi kama 20, walioandamana na mkusanyiko, wakihudhuria katika nchi moja baada ya nyingine, duniani pote. Safari za utalii za pekee ziliwawezesha kuona sehemu za kidini zenye kupendeza, na pia walishiriki pamoja na ndugu na dada wenyeji katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Wasafiri hao walijilipia gharama zao wenyewe.
Wajumbe wa Amerika ya Latin walikuwa wamewakilishwa vizuri kwenye mingi ya mikusanyiko hiyo ya kimataifa. Lakini katika 1966-1967, ilikuwa zamu yao ya kuwa wakaribishaji wa mikusanyiko. Wale waliohudhuria hawatasahau kamwe ile drama iliyolifanya kuwa na uhai lile simulizi la Biblia kuhusu Yeremia na ambayo ilisaidia kila mtu kuthamini maana yalo kwa siku yetu.a Vifungo vya upendo wa Kikristo viliimarishwa wageni walipokuwa wakijionea wenyewe hali ambazo katika kampeni kubwa ya elimu ya Biblia ilikuwa ikitimizwa katika Amerika ya Latin. Walivutwa sana na imani yenye nguvu ya waamini wenzao, wengi wao walikuwa wameshinda vizuizi vilivyoelekea kutoshindika—upinzani wa familia, mafuriko, kupoteza mali—ili wahudhurie. Walitiwa moyo sana na mambo yaliyoonwa kama lile la dada painia wa pekee kutoka Uruguai dhaifu aliyehojiwa na ambaye alikuwa jukwaani na wengi kati ya watu 80 ambao tayari alikuwa amesaidia kufanya maendeleo kufikia hatua ya ubatizo wa Kikristo! (Kufikia 1992, dada huyo alikuwa amesaidia watu 105 kufikia hatua ya ubatizo. Yeye alikuwa angali dhaifu na angali ni painia wa pekee!) Pia ilichangamsha moyo kama nini kukutana na wamishonari kutoka yale madarasa ya mapema zaidi ya Gileadi wakiwa wangali wanafanya kazi katika migawo yao! Mikusanyiko hiyo ilikuwa kichocheo kizuri kwa kazi iliyokuwa ikifanywa katika sehemu hiyo ya ulimwengu. Katika nyingi za nchi hizo, sasa kuna wasifaji wa Yehova wengi kama mara 10, 15, au hata 20 kama wale waliokuwako wakati ule.
Miaka michache baadaye, katika 1970-1971, iliwezekana kwa Mashahidi kutoka ng’ambo kuwa na ushirika pamoja na ndugu zao kwenye mikusanyiko ya kimataifa iliyofanywa barani Afrika. Mkubwa kupita yote kati ya mikusanyiko hiyo ya Kiafrika ulikuwa Lagos, Nigeria, ambapo ilikuwa lazima kujenga vifaa vyote kuanzia chini kwenda juu. Ili kukinga wajumbe na jua kali, jiji la mianzi lilijengwa—maeneo ya kuketi, mabweni, kafeteria, na idara nyinginezo. Ilitaka nguzo za mianzi 100,000 na mikeka mikubwa 36,000, iliyofumwa kwa matete—yote ikiwa imetayarishwa na ndugu na dada. Programu ilitolewa katika lugha 17 wakati uleule mmoja. Hudhurio lilifika 121,128, na Mashahidi wapya 3,775 wakabatizwa. Vikundi vingi vya Kikabila viliwakilishwa, na wengi wa wale waliokuwapo walikuwa watu waliozoea kupigana. Lakini sasa, ilikuwa shangwe kama nini kuwaona wakiwa wameungana katika vifungo vya udugu halisi wa Kikristo!
Baada ya mkusanyiko, baadhi ya wajumbe wa nchi za kigeni walisafiri kwa basi kwenda nchi ya Waigbo kuona lile eneo lililoathiriwa vibaya sana na vita ya hivi karibuni ya wenyewe kwa wenyewe. Udadisi mwingi ulitokezwa katika mji baada ya mji wageni walipokuwa wakisalimiwa na kukumbatiwa na Mashahidi wenyeji. Watu walikimbia barabarani kutazama. Wonyesho huo wa upendo na umoja kati ya weusi na weupe ulikuwa jambo ambalo hawakuwa wamepata kuona kamwe.
Katika nchi fulani idadi ya Mashahidi wa Yehova hufanya isiwezekane kwao wote kukusanyika pamoja katika mahali pamoja. Hata hivyo, pindi kwa pindi, mikusanyiko kadhaa imefanywa kwa wakati mmoja, mingine zaidi ikifuata, juma baada ya juma. Katika 1969, umoja uliohisiwa kwenye mikusanyiko iliyopangwa kwa njia hiyo ulizidishwa na uhakika wa kwamba baadhi ya wasemaji wakuu walisafiri kwa ndege kwenda na kurudi kati ya mikusanyiko hiyo, hivyo kuitumikia yote. Katika 1983 na 1988, umoja kama huo ulihisiwa wakati idadi fulani ya mikusanyiko mikubwa yenye kutumia lugha moja ilipounganishwa pamoja, hata kimataifa, kwa kupisha kwa njia ya simu hotuba kuu zilizotolewa na washiriki wa Baraza Linaloongoza. Hata hivyo, msingi halisi wa umoja miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ni uhakika wa kwamba wote humwabudu Yehova akiwa ndiye Mungu wa pekee wa kweli, wote hushikamana na Biblia ikiwa mwongozo wao, wote hunufaika kutokana na programu ileile moja ya ulishaji wa kiroho, wote humtegemea Yesu Kristo akiwa Kiongozi wao, wote hutafuta kudhihirisha matunda ya roho ya Mungu katika maisha zao, wote huweka tumaini lao katika Ufalme wa Mungu, na wote hushiriki katika kupelekea wengine habari njema za Ufalme huo.
Wamefanywa Tengenezo ili Wamsifu Yehova Kimataifa
Mashahidi wa Yehova wameongezeka idadi kiasi cha kuzidi idadi ya watu wa mataifa mengi moja moja. Ili mikusanyiko yao itimize mengi zaidi yaliyo mema, mipango mingi ya uangalifu hutakwa. Hata hivyo, maombi sahili yaliyochapwa kuhusu mahali ambapo Mashahidi kutoka maeneo mbalimbali wapaswa kuhudhuria kwa kawaida ndiyo tu huhitajiwa ili kuhakikisha kwamba kutakuwa nafasi ya kutosha kwa kila mtu. Mikusanyiko ya kimataifa inapopangwa, mara nyingi sasa Baraza Linaloongoza linahitaji kufikiria idadi ya Mashahidi kutoka nchi nyingine ambao wangependa kwenda na walio katika hali ya kuweza kufanya hivyo na pia ukubwa wa vifaa vipatikanavyo vya mkusanyiko, idadi ya Mashahidi wenyeji ambao watahudhuria, na kiasi cha mahali pa kulala panapopatikana kwa ajili ya wajumbe; kisha tarakimu isiyopasa kuzidi yaweza kugawiwa kila nchi. Ndivyo ilivyokuwa kuhusu ile Mikusanyiko mitatu ya “Ujitoaji Kimungu” iliyofanywa Poland katika 1989.
Kwa ajili ya mikusanyiko hiyo Mashahidi wa Yehova kama 90,000 walitazamiwa kutoka Poland kuongezea maelfu ya watu wapya wenye kupendezwa. Pia wengi walialikwa wahudhurie kutoka Uingereza, Kanada, na Marekani. Vikundi vikubwa vya wajumbe vilikaribishwa kutoka Italia, Ufaransa, na Japani. Vingine vilikuja kutoka nchi za Skandinevia na Ugiriki. Angalau nchi 37 ziliwakilishwa. Kwa ajili ya sehemu fulani za programu, ilikuwa lazima kutafsiri Kipoland au Kiingereza katika lugha nyingine nyingi kama 16. Jumla ya hudhurio ilikuwa 166,518.
Vikundi vikubwa vya Mashahidi kwenye mikusanyiko hiyo vilikuwa vimekuja kutoka ule uliokuwa wakati huo Muungano wa Sovieti na kutoka Chekoslovakia; vikundi vikubwa vilikuwapo pia kutoka nchi nyingine za Ulaya Mashariki. Hoteli na mabweni ya shule hayangeweza kuwaandalia wote mahali pa kulala. Kwa ukaribishaji-wageni, Mashahidi Wapoland walifungua mioyo na makao yao, wakishiriki kwa furaha walivyokuwa navyo. Kutaniko moja la wahubiri 146 liliandalia wajumbe zaidi ya 1,200 mahali pa kulala. Kwa baadhi ya wale waliohudhuria mikusanyiko hiyo, ilikuwa mara ya kwanza ambayo walipata wakati wowote kuwa kwenye mkusanyiko mkubwa wa watu wa Yehova zaidi ya 15 au 20. Mioyo yao ilijaa uthamini walipokuwa wakitazama makumi ya maelfu katika stediamu hizo, wakijiunga katika sala, na kuunganisha sauti zao katika nyimbo za sifa kwa Yehova. Walipochangamana pamoja kati ya vipindi, kulikuwako kukumbatiana kwa uchangamfu, hata ingawa tofauti za lugha mara nyingi ziliwazuia kusema kwa maneno yale yaliyokuwa mioyoni mwao.
Mkusanyiko ulipokuwa ukifikia mwisho, mioyo yao ilijaa shukrani kwa Yehova, aliyeyawezesha yote. Katika Warsaw, baada ya maelezo ya kuaga ya mwenyekiti, wasikilizaji walipiga makofi ghafula ambayo yaliendelea bila kupungua kwa angalau dakika kumi. Baada ya wimbo na sala ya mwisho, makofi yakarudiwa, nao wasikilizaji walikawiakawia vitini kwa muda mrefu. Walikuwa wamengojea pindi hiyo kwa miaka mingi, nao hawakutaka iishe.
Mwaka uliofuata, 1990, muda ulio punde kuliko miezi mitano baada ya kuondolewa marufuku ya miaka 40 juu ya Mashahidi wa Yehova katika ile iliyokuwa wakati ule Ujerumani Mashariki, mkusanyiko mwingine wa kimataifa wenye kusisimua ulifanywa, huo katika Berlin. Miongoni mwa wale 44,532 waliokuwapo mlikuwamo wajumbe kutoka nchi 65 tofauti. Kutoka nchi fulani, ni wachache tu waliokuwa wamekuja; kutoka Poland, kama 4,500 walikuja. Maneno hayangeweza kueleza zile hisia zenye kina za wale ambao hawakuwa wamepata kamwe uhuru wa kuhudhuria mkusanyiko kama huo, na wakati wasikilizaji wote walipojiunga katika nyimbo za sifa kwa Yehova, hawangeweza kuzuia machozi ya shangwe.
Baadaye mwaka huo, mkusanyiko kama huo ulipofanywa katika São Paulo, Brazili, stediamu mbili kubwa zilihitajiwa kukaliwa na wasikilizaji wa kimataifa 134,406. Hiyo ilifuatwa na mkusanyiko katika Argentina, ambako kwa mara nyingine tena stediamu mbili zilitumiwa sawia kuandaa mahali pa kuketi kwa ajili ya wasikilizaji wa Kimataifa. Mwaka 1991 ulipokuwa ukianza, mikusanyiko zaidi ya kimataifa ilikuwa ikianza katika Filipino, Taiwan, na Thailand. Idadi kubwa za wasikilizaji kutoka mataifa mengi zilikuwapo pia mwaka huo kwa ajili ya mikusanyiko katika Ulaya Mashariki—katika Hungaria, Chekoslovakia, na ile ambayo sasa ni Kroatia. Na katika 1992, wajumbe kutoka nchi 28 waliliona kuwa pendeleo la pekee kuwa miongoni mwa wale 46,214 waliokuwa katika St. Petersburg kwa ajili ya mkusanyiko wa kwanza ulio wa kimataifa kwelikweli wa Mashahidi wa Yehova katika Urusi.
-
-
Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu WetuMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Picha katika ukurasa wa 270, 271]
Katika 1958 idadi ya wasikilizaji 253,922, walijaa pomoni na wakazidi stediamu mbili kubwa katika New York, walisikia ujumbe “Ufalme wa Mungu Watawala—Je, Mwisho wa Ulimwengu U Karibu?”
Polo Grounds
Yankee Stadium
[Picha katika ukurasa wa 274]
Grant Suiter, mwenyekiti wa mkusanyiko katika Yankee Stadium katika 1950
[Picha katika ukurasa wa 274]
John Groh, (aketiye), akizungumzia mipango ya mkusanyiko pamoja na George Couch katika 1958
[Picha katika ukurasa wa 277]
Katika 1963 mkusanyiko wa ulimwenguni pote ulifanywa, wajumbe kutoka nchi zipatao 20 wakisafiri nao duniani pote
Kyoto, Japani, (chini kushoto), lilikuwa moja la majiji 27 ya mkusanyiko. Wajumbe katika Jamhuri ya Korea walipata kujuana (katikati). Salamu ya Kimaori katika New Zealand (chini kulia)
[Picha katika ukurasa wa 279]
Mkusanyiko uliotumikia vikundi 17 vya lugha wakati uleule mmoja, katika jiji la mianzi lililojengwa kwa ajili ya pindi hiyo (Lagos, Nigeria, 1970)
[Picha katika ukurasa wa 280]
Mikusanyiko mikubwa mitatu ilifanywa Poland katika 1989, wajumbe wakiwepo kutoka nchi 37
T. Jaracz (kulia) alihutubia wajumbe katika Poznan
Maelfu walibatizwa katika Chorzów
Wasikilizaji walipiga makofi kwa muda mrefu sana katika Warsaw
Wajumbe kutoka iliyokuwa wakati huo U.S.S.R. (chini)
Visehemu vya programu katika Chorzów vilitafsiriwa katika lugha 15
-
-
Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu WetuMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 272, 273]
Pande za Baadhi ya Mikusanyiko Mikubwa
Mamia ya wajumbe wenye idili waliwasili kwa meli, maelfu kwa ndege, makumi ya maelfu kwa magari na basi
Mpango mzuri wa kitengenezo ulihitajiwa na wafanyakazi wengi wenye moyo wa kupenda walitakwa ili kupata na kugawa mahali pa kulala pa kutosha
Wakati wa mikusanyiko hiyo ya siku nane, milo yenye moto—makumi ya maelfu yayo—walipakuliwa wajumbe kwa ukawaida
Katika 1953, jiji la trela na la mahema liliwapa makao wajumbe zaidi ya 45,000
New York City, katika 1958, watu 7,136 walibatizwa—wengi zaidi ya wakati mwingine wowote tangu Pentekoste ya 33 W.K.
Ishara zenye salamu kutoka nchi nyingi zilionyeshwa, na vipindi viliongozwa katika lugha 21, New York City katika 1953
-