-
Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya DuniaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Ukubwa wa mikusanyiko yao na mwenendo wa Kikristo wa wale wanaohudhuria umevuta fikira. Mikusanyiko miwili kama hiyo, iliyofanywa wakati uleule katika São Paulo na Rio de Janeiro, Brazili, katika 1985, ilikuwa na kilele cha hudhurio cha 249,351. Baadaye, mikusanyiko 23 zaidi, iliyofanywa ili watu wanaopendezwa katika sehemu nyinginezo za Brazili waweze kuhudhuria, iliinua jumla ya hudhurio kuwa 389,387. Matokeo ya kazi ambayo Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakifanya katika Brazili wakiwa walimu wa Neno la Mungu yalikuwa dhahiri sana wakati watu 4,825 walipofananisha wakfu wao kwa Yehova kwa uzamisho wa maji kwenye mfululizo huo wa mikusanyiko. Miaka mitano tu baadaye, katika 1990, ilihitaji kufanywe mikusanyiko 110 kotekote katika Brazili ili watu 548,517 waliohudhuria waweze kutoshea. Wakati huo, 13,448 walijitokeza kwa ajili ya uzamisho wa maji. Kotekote nchini mamia ya maelfu ya watu mmoja-mmoja na familia walikuwa wakiwakaribisha Mashahidi wa Yehova wawafunze kutokana na Neno la Mungu.
Namna gani kuhusu Argentina? Baada ya miongo ya vizuizi vya serikali, Mashahidi wa Yehova waliweza tena kukusanyika kwa uhuru katika 1985. Ilikuwa furaha iliyoje kwa 97,167 waliohudhuria kwenye mfululizo wa kwanza wa mikusanyiko! Chini ya kichwa “Ufalme Ambao Unakua—Ule wa Mashahidi wa Yehova,” gazeti la huko liitwalo Ahora lilishangazwa na utaratibu wa umati wa mkusanyiko katika Buenos Aires, kutokuwa kwao na chuki za kikabila au kijamii, hali yao ya amani, na upendo walioonyesha. Kisha likamalizia hivi: “Iwe tunashiriki mawazo na mafundisho yao au la, halaiki hii yote yastahili staha yetu nyingi sana.” Hata hivyo, Waargentina wengi walifanya zaidi ya hiyo. Walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, na kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme ili kuchunguza jinsi Mashahidi hutumia kanuni za Biblia maishani mwao. Kisha wachunguzi hao wakafanya uamuzi. Katika miaka saba iliyofuata, mamia ya maelfu yao waliweka maisha zao wakfu kwa Yehova, na idadi ya Mashahidi katika Argentina imeongezeka kwa asilimia 71!
-
-
Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya DuniaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Kisha, katika 1985 Mashahidi wa Yehova waliweza kufanya mikusanyiko minne mikubwa katika stediamu kubwa zaidi nchini Poland wakati wa mwezi wa Agosti. Wakati mjumbe kutoka Austria alipowasili kwa ndege, alishangaa kusikia tangazo kutoka kwa vikuza-sauti la kuwakaribisha Mashahidi wa Yehova nchini Poland kwa mkusanyiko wao. Akijua kwamba hilo lilionyesha kulikuwa na badiliko katika mtazamo wa serikali, Shahidi Mpoland mzee-mzee aliyekuwa hapo kuwakaribisha wageni hangeweza kujizuia kutokwa na machozi ya shangwe. Waliohudhuria mikusanyiko hiyo walikuwa wajumbe 94,134, kutia vikundi kutoka nchi 16. Je, umma ulijua kile kilichokuwa kikiendelea? Naam, ulijua! Wakati na baada ya mikusanyiko hiyo, walisoma ripoti katika magazeti yao makuu, wakaona umati wa mkusanyiko kwenye televisheni, na kusikia sehemu za programu kwenye redio zao. Wengi wao walipenda yale waliyoona na kusikia.
Mipango kwa ajili ya mikusanyiko mikubwa hata zaidi katika Poland ilikuwa inaendelea, mnamo Mei 12, 1989, serikali ilipotoa utambulisho wa kisheria kwa Mashahidi wa Yehova kuwa shirika la kidini. Katika muda wa miezi mitatu, mikusanyiko mitatu ya kimataifa ilikuwa ikiendelea—katika Chorzów, Poznan, na Warsaw—kukiwa na jumla ya hudhurio la 166,518. Kwa kustaajabisha, maelfu ya Mashahidi kutoka zile nchi zilizokuwa Muungano wa Sovieti (U.S.S.R.) na Chekoslovakia waliweza kupata ruhusa iliyohitajiwa ya kusafiri na walihudhuria. Je, kazi ya kufanya wanafunzi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa inazaa matokeo katika nchi hizo ambako kutoamini kuwako kwa Mungu kulikuwa kumeungwa mkono sana na Serikali kwa miongo ya miaka? Jibu lilikuwa wazi wakati 6,093, kutia na vijana wengi, walipojitoa kwa ajili ya uzamisho wa maji kwenye mikusanyiko hiyo.
Umma ungeweza kuona wazi sana kwamba Mashahidi walikuwa tofauti—kwa njia yenye kufaa sana. Kwenye magazeti ya umma, walisoma taarifa kama zile zifuatazo: “Wale wanaoabudu Yehova Mungu—kama vile wanavyosema wenyewe—huthamini sana vikusanyiko vyao, ambavyo kwa kweli ni udhihirisho wa umoja miongoni mwao. . . . Kuhusu utaratibu, hali ya amani, na usafi, washiriki wa mkusanyiko ni mifano ya kuigwa.” (Życie Warszawy) Baadhi ya watu wa Poland waliamua kufanya zaidi ya kuchunguza tu wakusanyikaji. Walitaka Mashahidi wa Yehova wajifunze Biblia nao. Kama tokeo la mafunzo hayo katika Neno la Mungu, idadi ya Mashahidi wa Yehova nchini Poland iliongezeka kutoka 72,887 katika 1985 hadi 107,876 katika 1992; na wakati wa mwaka huo uliotajwa mwisho, walitoa zaidi ya muda wa saa milioni 16,800,000 kuwaambia wengine kuhusu tumaini la ajabu lililoonyeshwa katika Maandiko.
-