Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu Wetu
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Mikusanyiko ya Mapema ya Wanafunzi wa Biblia

      Mipango ya mikusanyiko ya Wanafunzi wa Biblia kutoka majiji na nchi mbalimbali ilisitawi hatua kwa hatua. Tofauti na vikundi vya makanisa ya kimapokeo, Wanafunzi wa Biblia, kwa njia ya mikusanyiko yao, walipata kujua upesi waamini wenzao katika sehemu nyinginezo. Mwanzoni, mikusanyiko hiyo ilifanywa Allegheny, Pennsylvania, kuhusiana na mwadhimisho wa kila mwaka wa kifo cha Bwana. Katika 1891 tangazo lilitolewa hususa kwamba kungekuwako na “mkusanyiko kwa ajili ya funzo la Biblia na kwa ajili ya kuadhimisha Ukumbusho wa Mlo wa Jioni wa Bwana.” Mwaka uliofuata Watch Tower lilikuwa na kichwa chenye kutokeza kikitangaza “MKUSANYIKO WA WAAMINI, ALLEGHENY, PA., . . . APRILI 7 HADI 14, KUTIA NDANI TAREHE HIZO MBILI, 1892.”

      Umma kwa ujumla haukualikwa kwenye mikusanyiko hiyo ya mapema. Lakini, katika 1892, watu kama 400 waliokuwa wametoa uthibitisho wa imani katika fidia na kupendezwa kwa moyo mweupe na kazi ya Bwana walikuwapo. Programu ilitia ndani siku tano za funzo la Biblia lenye bidii na siku nyingine mbili za shauri lenye kusaidia kwa makolpota.

      Mwanamume mmoja aliyekuwapo kwa mara ya kwanza kwenye mikusanyiko hiyo alisema hivi: “Nimekuwa kwenye Mikusanyiko mingi, lakini sijapata kamwe kabla ya hapo kuwa kwenye mmoja kama huu, ambapo mapenzi na mpango wa Mungu ndiyo mazungumzo pekee na yasiyokoma tokea kuamka hadi kwenda kulala; nyumbani, barabarani, kwenye mkutano, kwenye chakula cha mchana na kila mahali.” Kuhusu roho iliyoonyeshwa na wajumbe, mwanamume mmoja kutoka Wisconsin, Marekani, aliandika: “Nilivutiwa sana na roho ya upendo na fadhili za kidugu zilizodhihirishwa katika pindi zote.”

      Badiliko katika mipango kwa ajili ya mkusanyiko wa kila mwaka lilitukia katika 1893. Ili kujifaidi na nauli zenye nafuu za garimoshi kuhusiana na Columbian Exposition kiangazi hicho Wanafunzi wa Biblia walikusanyika katika Chicago, Illinois, kuanzia Agosti 20 hadi 24. Huo ulikuwa ndio mkusanyiko wao wa kwanza nje ya eneo la Pittsburg. Hata hivyo, ili kutumia vizuri zaidi iwezekanavyo wakati na pesa kwa kazi ya Bwana, hakuna mikusanyiko zaidi mikuu iliyofanywa kwa miaka kadhaa.

      Halafu, kuanzia 1898, Wanafunzi wa Biblia katika sehemu mbalimbali walianza kuchukua hatua ya kwanza katika sehemu zao kupanga makusanyiko, ambayo yangehudhuriwa na watu katika eneo dogo. Katika 1900 kulikuwa mikusanyiko 3 iliyopangwa na Sosaiti; lakini kulikuwa pia makusanyiko 13 ya mahali katika Marekani na Kanada, iliyo mingi yayo ilikuwa ya siku moja tu na mara nyingi ilifanywa kuhusiana na ziara ya mmoja wa mapilgrimu. Hesabu ilizidi kukua. Kufikia 1909 kulikuwa angalau makusanyiko 45 ya mahali katika Amerika Kaskazini kuongezea mikusanyiko iliyotumikiwa na Ndugu Russell katika safari za pekee zilizompeleka kwenye sehemu mbalimbali za bara hilo. Sehemu ya programu kwenye makusanyiko ya siku moja ilikusudiwa hasa kuchochea kupendezwa upande wa umma. Hudhurio lilikuwa la kuanzia labda mia moja kufika maelfu kadhaa.

      Kwa upande mwingine, mikusanyiko mikuu, iliyohudhuriwa sanasana na Wanafunzi wa Biblia, ilikazia funzo kwa ajili ya wale walioimarika kwa kadiri fulani katika njia ya kweli. Kwa ajili ya mikusanyiko hiyo, magarimoshi ya pekee yakiwa yamejaa wajumbe yalikuwa yakija kutoka majiji makubwa. Pindi kwa pindi hudhurio lilikuwa juu kama 4,000, hata kutia wajumbe wachache kutoka Ulaya. Hizo zilikuwa nyakati za kiburudisho cha kweli cha kiroho kilichotokeza bidii na upendo ulioongezeka upande wa watu wa Yehova. Mwishoni mwa mkusanyiko mmoja katika 1903 kama huo ndugu mmoja alisema hivi: “Singepokea dola elfu kwa ajili ya wema ambao nimepokea kutoka Mkusanyiko huu;—ingawa mimi ni mtu maskini.”

      Ndugu mapilgrimu ambao huenda wakawa katika eneo hilo walisema kwenye makusanyiko hayo. Ndugu Russell pia alijitahidi kuhudhuria na kutumikia katika programu kwenye makusanyiko ya mahali na kwenye mikusanyiko mikubwa zaidi katika Marekani na mara nyingi katika Kanada. Hilo lilihusisha kusafiri sana. Kwingi kati ya huko kulifanywa katika safari za mwisho wa juma. Lakini, katika 1909, ndugu mmoja katika Chicago alikodi mabehewa kadhaa ya garimoshi ili kusafirisha wajumbe waliosafiri pamoja na Ndugu Russell kutoka mkusanyiko mmoja hadi mwingine katika safari. Katika 1911 na 1913, magarimoshi mazima yalikodiwa na ndugu huyohuyo ili kupeleka mamia ya wajumbe katika safari za mkusanyiko zilizoendelea kwa mwezi mmoja au zaidi na kuenea magharibi mwa Marekani na Kanada.

      Safari katika garimoshi la mkusanyiko kama hilo lilikuwa jambo la kukumbukwa. Katika 1913, Malinda Keefer alipanda moja katika Chicago, Illinois. Miaka mingi baadaye, alisema hivi: “Haikuchukua muda mrefu kujua kwamba tulikuwa familia moja kubwa . . . na garimoshi lilikuwa makao yetu kwa mwezi mmoja.” Garimoshi lilipokuwa likiondoka kituoni, wale waliokuja kuaga waliimba “Mungu Awe Nanyi Hadi Tuonanapo Tena,” muda wote huo wakipungapunga kofia na vitambaa vyao mpaka garimoshi lilipotoweka. Dada Keefer aliongeza: “Kwenye kila kituo safarini ilikuwako mikusanyiko iliyokuwa ikifanywa—mingi ilikuwa ya siku tatu, nasi tulikaa siku moja na kila mkusanyiko. Wakati wa vituo hivyo Ndugu Russell alitoa hotuba mbili, moja kwa akina ndugu alasiri, na nyingine kwa umma jioni juu ya kichwa ‘Baada ya Kifo.’”

      Pia katika nchi nyingine makusanyiko yalikuwa yakiongezeka. Mara nyingi yalikuwa madogo sana. Kama 15 walikuwapo kwa ajili ya ule wa kwanza katika Norway, katika 1905; lakini ulikuwa mwanzo tu. Miaka sita baadaye, wakati Ndugu Russell alipotembelea Norway, jitihada ya pekee ilifanywa kualika umma, na hudhurio katika pindi hiyo lilikadiriwa kuwa 1,200. Wakati wa 1909, alipohudhuria mikusanyiko katika Scotland, alisema kwa watu karibu 2,000 katika Glasgow na wengine 2,500 katika Edinburgh juu ya habari yenye kuamsha kupendezwa “Mwivi Katika Paradiso, Tajiri Katika Helo, na Lazaro Kifuani mwa Abrahamu.”

      Kwenye umalizio wa mikusanyiko ya mapema, ndugu walikuwa na kile walichokiita karamu ya upendo, kuonyesha hisia yao ya udugu wa Kikristo. Hiyo “karamu ya upendo” ilitia ndani nini? Kama kielelezo, wasemaji walikuwa wakipanga mstari wakiwa na sahani za mikate iliyokatwakatwa kuwa vipande vya umbo la dadu, kisha wasikilizaji walikuwa wakipita kwa mstari wakishiriki mkate, kusalimu kwa mkono, na kuimba “Na Vibarikiwe Vifungo Vifungavyo Mioyo Yetu Katika Upendo wa Kikristo.” Mara nyingi machozi ya shangwe yalikuwa yakitiririka mashavuni mwao walipokuwa wakiimba. Baadaye, kadiri hesabu zao zilivyokua, waliacha kusalimu kwa mkono na kushiriki mkate lakini walikuwa wakimalizia kwa wimbo na sala na, mara nyingi, kupiga makofi sana kuonyesha uthamini wao.

      Kuanzisha Kampeni ya Duniani Pote ya Kupiga Mbiu ya Ufalme

      Mkusanyiko mkubwa wa kwanza baada ya Vita ya Ulimwengu 1 ulifanywa Cedar Point, Ohio (kwenye Ziwa Erie, kilometa 96 magharibi mwa Cleveland), kutoka Septemba 1 hadi 8 katika 1919. Kufuatia kifo cha Ndugu Russell, baadhi ya wale waliokuwa wameshirikiana kimashuhuri na tengenezo waliacha kweli. Ndugu walipatwa na mitihani mikali. Mapema kidogo katika 1919, msimamizi wa Sosaiti na washirika wake walikuwa wamefunguliwa kutoka kifungo chao kisicho cha haki gerezani. Hivyo kulikuwa tarajio kubwa sana. Ijapokuwa hudhurio la siku ya kwanza lilikuwa chini, baadaye katika siku hiyo wajumbe zaidi waliwasili kwa magarimoshi ya pekee. Ndipo mameneja wa hoteli mbalimbali waliokuwa wamejitolea kuwapa wajumbe mahali pa kulala wakalemewa sana na kazi. R. J. Martin na A. H. Macmillan (wote wawili walikuwa miongoni mwa kile kikundi kilichofunguliwa toka gerezani karibuni) wakajitolea kusaidia. Walifanya kazi kuwagawia wajumbe vyumba mpaka kupita usiku wa manane, na Ndugu Rutherford na wengi kati ya wale wengine walifurahia kutumikia wakiwa wabeba-mizigo, wakibeba mizigo na kusindikiza akina ndugu kwenye vyumba vyao. Mlikuwamo roho yenye kuenea ya idili miongoni mwao wote.

      Kama 2,500 walitazamiwa kuhudhuria. Hata hivyo, katika kila njia mkusanyiko ulithibitika kuwa zaidi ya ilivyotarajiwa. Kufikia siku ya pili, tayari jumba lilikuwa limejaa kupita kiasi na majumba zaidi yalitumiwa. Hilo lilipothibitika kuwa halitoshi, vipindi vilihamishwa kupelekwa nje katika eneo lililokuwa na bustani nzuri ya miti. Wanafunzi wa Biblia kama 6,000 kutoka Marekani na Kanada walikuwapo.

      Kwa ajili ya hotuba kuu Jumapili, angalau 1,000 wa umma walikuja pia, hiyo iliongeza wasikilizaji kufikia 7,000 kamili, ambao msemaji alihutubia peupe bila msaada wowote wa maikrofoni au mfumo wa vikuza-sauti. Katika hotuba hiyo, “Tumaini kwa Ajili ya Wanadamu Wenye Kutaabika,” J. F. Rutherford alionyesha wazi kwamba Ufalme wa Kimesiya wa Mungu ndio utatuzi kwa matatizo ya wanadamu, na alionyesha pia kwamba Ushirika wa Mataifa (uliokuwa wakati huo ukizaliwa na ambao ulikuwa tayari umepewa kibali na makasisi) haukuwa hata kidogo wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu. Register gazeti la Sandusky lilikuwa na ripoti ndefu juu ya hotuba hiyo, pamoja na muhtasari wa utendaji wa Wanafunzi wa Biblia. Nakala za gazeti hilo zilipelekwa kwenye mashirika ya magazeti ya habari kotekote katika Marekani na Kanada. Lakini kulikuwako mengi zaidi yaliyomaanishwa na utangazaji uliotokana na mkusanyiko huo.

      Upeo halisi wa mkusanyiko wote ulikuwa “Hotuba kwa Wafanyakazi Wenzi” ya Ndugu Rutherford, ambayo baadaye ilitangazwa chini ya kichwa “Kuutangaza Ufalme.” Ilielekezwa kwa Wanafunzi wa Biblia wenyewe. Wakati wa hotuba hiyo umaana wa herufi GA zilizokuwa zimeonekana katika programu ya mkusanyiko na katika mahali mbalimbali katika mahali pa mkusanyiko ulipata kuwa wazi. Tangazo lilitolewa kuhusu kuchapwa kwa gazeti jipya kulikokuwa kukikaribia, The Golden Age, ambalo lingetumiwa katika kuelekeza fikira za watu kwenye Ufalme wa Kimesiya. Baada ya kueleza kazi ipasayo kufanywa, Ndugu Rutherford aliambia wasikilizaji hivi: “Mlango wa fursa unafunguka mbele yenu. Uingieni upesi. Kumbukeni kwamba mwendapo mbele katika kazi hii hamsihi watu mkiwa mawakili wa gazeti tu, bali nyinyi ni mabalozi wa Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana, mkitangazia watu kwa njia hiyo yenye kuheshimikia kuja kwa Enzi Bora Kabisa, ufalme wenye utukufu wa Bwana na Mkubwa wetu, ambao Wakristo wa kweli wameutumaini na kuuomba kwa karne nyingi.” (Ona Ufunuo 3:8.) Msemaji alipouliza ni wangapi waliotaka kushiriki katika kazi hiyo, itikio lenye idili lilikuwa lenye kuchochea kuliona. Wasikilizaji 6,000, wakasimama kwa umoja. Kufikia mwaka uliofuata, zaidi ya 10,000 walikuwa wakishiriki katika utumishi wa shambani. Mkusanyiko mzima ulikuwa na matokeo yenye kuleta umoja na kutia nguvu wahudhuriaji.

      Miaka mitatu baadaye, katika 1922, mkusanyiko mwingine wenye kukumbukwa ulifanywa Cedar Point. Ilikuwa programu ya siku tisa, tokea Septemba 5 hadi 13. Kuongezea wajumbe kutoka Marekani na Kanada, wengine walikuja kutoka Ulaya. Mikutano iliongozwa katika lugha kumi. Wastani wa hudhurio kila siku ulikuwa kama 10,000; na kwa ajili ya hotuba “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” wengi sana kati ya umma walikuwamo kati ya wasikilizaji hivi kwamba hudhurio lilikaribia kuwa mara mbili.

      Wanafunzi wa Biblia hawakukusanyika kwenye mkusanyiko huo wakiwa na wazo la kwamba walikuwa wakipangia kazi hapa duniani ambayo ingeendelea kwa makumi ya miaka katika wakati ujao. Kwa kweli, walisema kwamba huenda ukawa ndio mkusanyiko wao mkuu wa mwisho kabla ya “kanisa kukombolewa . . . kuingizwa katika sehemu ya kimbingu ya ufalme wa Mungu, na kwa kweli katika kuwapo kwenyewe na kuliko halisi kwa Bwana wetu na Mungu wetu.” Lakini hata wakati uwe mfupi jinsi gani, kufanya mapenzi ya Mungu kulikuwa ndilo hangaiko lao la kwanza. Akifikiria hilo, katika Ijumaa, Septemba 8, Ndugu Rutherford alitoa hotuba yenye kukumbukwa “Ule Ufalme.”

      Kabla ya hapo, beramu kubwa zenye herufi ADV zilikuwa zimeangikwa katika sehemu mbalimbali za uwanja. Wakati wa hotuba maana ya herufi hizo ikawa wazi msemaji alipohimiza hivi: “Iweni mashahidi waaminifu na wa kweli wa Bwana. Songeni mbele katika vita mpaka kila kisehemu cha Babiloni kiwe ukiwa. Utangazeni ujumbe kotekote. Lazima ulimwengu ujue kwamba Yehova ni Mungu na kwamba Yesu Kristo ni Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Hii ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme atawala! Nyinyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Wakati huo beramu kubwa, yenye urefu wa meta 11, ikakunjuka mbele ya wasikilizaji. Juu yake ilikuwapo ile shime yenye kuchochea “Mtangazeni [Kiingereza: ‘Advertise,’ ikiwakilishwa na ‘ADV’] Mfalme na Ufalme.” Ulikuwa muda wenye kutazamisha. Wasikilizaji walipiga makofi kwa idili. Ndugu Pfannebecker mwenye umri mkubwa, katika okestra ya kusanyiko, alipungapunga zeze lake juu ya kichwa chake na kusema kwa sauti kubwa kwa lahaja yake nzito ya Kijerumani: “Ach, Ya! Und now ve do it, no [Naam, na sasa tutaifanya, sivyo?]?” Nao waliifanya.

      Siku nne baadaye, wakati mkusanyiko ulipokuwa ungali unaendelea, Ndugu Rutherford alishiriki binafsi pamoja na wakusanyikaji wengine walipokuwa wakishiriki kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme nyumba hadi nyumba katika eneo ambalo halikuzidi umbali wa kilometa 72 kutoka uwanja wa mkusanyiko. Haikuishia hapo. Kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme ilikuwa imepewa msukumo wenye nguvu ambao ungefika duniani pote. Mwaka huo zaidi ya wafanyakazi 17,000 wenye bidii katika nchi 58 walishiriki kutoa ushahidi. Miongo mingi ya miaka baadaye, George Gangas aliyekuwa kwenye mkusanyiko huo na ambaye baadaye akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alisema hivi kuhusu programu katika Cedar Point: “Ni jambo lililokazwa kikiki katika akili na moyo wangu, ambalo sitasahau kamwe maadamu ninaishi.”

      Hatua za Maana Katika Ukuzi wa Kiroho

      Mikusanyiko yote imekuwa nyakati za burudisho na funzo katika Neno la Mungu. Lakini baadhi yayo imekumbukwa kwa miongo ya miaka kuwa ilikuwa hatua kubwa za kiroho.

      Mikusanyiko saba kati ya hiyo, ilifanywa mwaka mmoja baada ya mwingine, kuanzia 1922 hadi 1928, katika Marekani, Kanada, na Uingereza. Sababu moja ya umaana wa mikusanyiko hiyo ilikuwa yale maazimio yenye nguvu yaliyokubaliwa, yote saba yanaorodheshwa katika kisanduku katika ukurasa ufuatao. Ijapokuwa Mashahidi walikuwa wachache, waligawanya nakala nyingi kufikia milioni 45 za azimio moja, na nyingine kadhaa milioni 50, katika lugha nyingi ulimwenguni pote. Baadhi yayo yalisambazwa katika redio za kimataifa zilizounganishwa. Hivyo ushahidi wenye kutokeza ukatolewa.

      Mkusanyiko mwingine tena wenye kufanyiza historia ulifanywa Columbus, Ohio, katika 1931. Jumapili, Julai 26, baada ya Wanafunzi wa Biblia kusikia hoja za Kimaandiko walikubali jina jipya—Mashahidi wa Yehova. Lilifaa kama nini! Hapa palikuwa na jina ambalo huelekeza uangalifu wa kwanza kwa Muumba mwenyewe na ambalo hutambulisha daraka la wale wamwabuduo. (Isa. 43:10-12) Kukubaliwa kwa jina hilo kuliwatia akina ndugu bidii nyingi zaidi ya vile walivyopata kuwa wakati wowote wakiwa wapiga-mbiu wa jina na Ufalme wa Mungu. Kama vile barua moja iliyoandikwa mwaka huo na Shahidi Mdenmark ilivyolieleza jambo hilo: “Oh, ni jina tukufu kama nini, Mashahidi wa Yehova, naam, kwelikweli sisi sote na tuwe hivyo.”

  • Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu Wetu
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 261]

      Maazimio Saba ya Mkusanyiko Yenye Umaana

      Katika 1922, azimio lenye kichwa “Mwito kwa Viongozi wa Ulimwengu” uliwataka wathibitishe kwamba wanadamu wana hekima ya kutawala dunia hii, la sivyo wakubali kwamba amani, uhai, uhuru, na furaha isiyo na mwisho vyaweza kuja tu kutoka kwa Yehova kupitia Yesu Kristo.

      Katika 1923, kulikuwa “Onyo kwa Wakristo Wote” juu ya uhitaji wa haraka wa kukimbia matengenezo yanayodai kwa kusingizia kumwakilisha Mungu na Kristo.

      Katika 1924, “Makasisi Washtakiwa” lilifunua wazi mafundisho na mazoea yasiyo ya Kimaandiko ya makasisi wa Jumuiya ya Wakristo.

      Katika 1925, “Ujumbe wa Tumaini” lilionyesha kwa nini wale ambao hudai kuwa mianga yenye kuongoza ya ulimwengu wameshindwa kutosheleza uhitaji mkubwa zaidi wa mwanadamu na jinsi ni Ufalme wa Mungu tu uwezao kufanya hivyo.

      Katika 1926, “Ushuhuda kwa Watawala wa Ulimwengu” liliwajulisha kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli na kwamba sasa Yesu Kristo atawala akiwa Mfalme wa dunia anayestahili. Liliwahimiza watawala watumie uvutano wao wageuze akili za watu kuelekea Mungu wa kweli ili wasipatwe na msiba.

      Katika 1927, “Azimio kwa Watu wa Jumuiya ya Wakristo” lilifunua wazi muungano wa kifedha, kisiasa, na kidini ambao hukandamiza wanadamu. Lilihimiza watu waiache Jumuiya ya Wakristo na kuweka tumaini lao katika Yehova na Ufalme wake ulio mikononi mwa Kristo.

      Katika 1928, “Tangazo Dhidi ya Shetani na la Kusimama Upande wa Yehova” lilionyesha wazi kwamba Mfalme mtiwa-mafuta wa Yehova, Yesu Kristo, atamzuia Shetani karibuni na kuharibu tengenezo lake bovu, nalo lilihimiza wote wapendao uadilifu wachukue msimamo wao upande wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki