Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Miujiza” Miwili Kwenye Kusanyiko Moja Huko Georgia
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Agosti 1
    • Mnamo Januari (Mwezi wa 1) 2006, jitihada zilifanywa ili kupata mahali panapofaa kwa ajili ya kusanyiko hilo la maelfu ya watu katika jiji kuu, Tbilisi, mji mkuu wa Georgia. Mahali pengine pa kusanyiko pangeunganishwa kwa simu.

      Kwa miaka mingi sasa, watu wamepewa uhuru wa ibada hatua kwa hatua huko Georgia. Hivyo, ingawa kulikuwa na upinzani wakati uliopita, Mashahidi walisonga mbele, wakiwa na uhakika kwamba wangepata mahali ambapo wangefanyia kusanyiko katika mji mkuu. Kwa kawaida, watu wa Georgia ni wachangamfu sana na wakarimu. Hata hivyo, wakuu fulani wa serikali wana ubaguzi mwingi wa kidini. Je, wangebadili maoni yao na hivyo kuwaruhusu Mashahidi wakodi mahali pa kufanyia kusanyiko?

      Ndugu wa Halmashauri ya Kusanyiko walitembelea viwanja mbalimbali na majumba makubwa ya michezo. Wasimamizi waliahidi kwamba Mashahidi wangetumia viwanja na majumba yao lakini wakakataa wakati ndugu walipoomba tarehe hususa ya kukodi. Hivyo, halmashauri ilishangaa wakati wasimamizi wa Tbilisi Philharmonic walipokubali Mashahidi wa Yehova wakodi jumba lao. Jumba hilo la maonyesho liko katikati ya jiji, mahali ambapo matukio mengi maarufu sana yanafanyiwa.

      Wakiwa wametiwa moyo kwamba mwishowe jitihada zao zilikuwa zimefanikiwa, ndugu wa halmashauri hiyo walianza matayarisho ya kusanyiko la Tbilisi, na pia makusanyiko katika miji na majiji nchini kote, kutia ndani Tsnori, Kutaisi, Zugdidi, Kaspi, na Gori. Kazi kubwa ilifanywa ili kuunganisha kwa njia ya simu maeneo yote hayo ya makusanyiko ili programu iendeshwe wakati uleule. Kila kitu kilikuwa tayari kwa ajili ya kusanyiko. Kisha, kwa ghafula, juma moja tu kabla ya kusanyiko kuanza, wasimamizi wa jumba la maonyesho la Tbilisi Philharmonic wakafutilia mbali mapatano yaliyofanywa. Hawakueleza sababu ya kufanya hivyo.

      “Muujiza” wa Kwanza

      Ndugu wangefanya nini kwa siku chache tu zilizobaki? Uwezekano pekee ulikuwa kwenda kwenye mji wa Marneuli, eneo la mashambani lililo umbali wa kilomita 40 nje ya jiji la Tbilisi. Makusanyiko mengi yalikuwa yamefanywa huko kwenye uwanja wa familia moja ambayo ni ya Mashahidi wa Yehova. Zamani uwanja huo ulikuwa shamba kubwa. Kwa miaka kumi iliyopita, hapo ndipo mahali pekee ambapo makutaniko ya Tbilisi yalifanyia makusanyiko. Hata hivyo, Marneuli pia ni mahali ambapo Mashahidi wa Yehova wameshambuliwa mara nyingi na umati wa watu wenye hasira.

  • “Miujiza” Miwili Kwenye Kusanyiko Moja Huko Georgia
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Agosti 1
    • Halmashauri ya Kusanyiko ilipaswa kukabiliana si tu na tishio la jeuri bali pia ugumu wa kufanyia kusanyiko la watu 5,000 mahali ambapo kwa kawaida panatoshea watu 2,500 hivi. Tatizo hilo lingetatuliwa jinsi gani kwa muda huo mfupi? Ilionekana kama muujiza wakati wamiliki wa mashamba mawili yaliyokuwa karibu na mahali hapo walipowaendea akina ndugu na kupendekeza kwamba wakodi mashamba yao.

      Kugeuza mashamba hayo yawe mahali panapofaa kufanyia kusanyiko ilikuwa kazi ngumu. Hali ya hewa ilifanya mambo yawe magumu sana, kwa kuwa mvua ilinyesha juma zima kabla ya kusanyiko. Viazi vilikuwa vimepandwa katika mashamba hayo, navyo vilipaswa kuvunwa. Kwanza, wajitoleaji walichimbua viazi huku mvua ikinyesha. Kisha, nyua ziliondolewa na paa zikajengwa za kuwakinga wasikilizaji na jua na mvua. Viti zaidi vya mbao vilihitaji kutengenezwa, na vifaa vya sauti vya ziada kuwekwa. Wajitoleaji walikata na kutoboa mbao, nao wakapigilia misumari. Walifanya kazi hiyo usiku na mchana, na wengine hata walijinyima usingizi.

      Kila mtu alijiuliza, “Itakuwa namna gani ikiwa mvua itaendelea wakati wa kusanyiko? Je, wajumbe watazama na kutoweka ndani ya matope ya eneo hili?” Majani makavu yalinunuliwa ili kufunika udongo uliolowa. Mwishowe, jua liliangaza! Kwa siku zote tatu za kusanyiko, udongo ulipigwa na joto la jua jangavu.

      Wajumbe walipofika, mazingira yalikuwa mazuri sana. Mazingira hayo yenye utulivu yalionekana kama yale ya ulimwengu mpya. Wakiwa wameketi kwa starehe, wajumbe walizungukwa na mitini, miti mingine ya matunda, mashamba ya mahindi, na nyanya. Sehemu ya nyuma ya jukwaa ilipambwa kwa mizabibu. Pindi kwa pindi wakati wa programu, wasikilizaji walisikia majogoo yakiwika na sauti za kuku wakati mayai yao yalipokuwa yakikusanywa. Kulikuwa na sauti nyingine zinazosikika tu mashambani, lakini kwa wahudhuriaji, sauti hizo zote zilikuwa zenye kuburudisha. Wasikilizaji hawakukengeushwa na sauti hizo kwa sababu walitaka kusikiliza kwa makini programu bora iliyotegemea Biblia.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki