Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Useja—Mlango Uelekeao Kwenye Utendaji Pasipo Kukengeushwa Fikira
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Oktoba 15
    • “[Ni] kumhudumia Bwana pasipo kuvutwa [“kukengeushwa fikira,” “NW”] na mambo mengine.”—1 WAKORINTHO 7:35.

      1. Ni habari gani ya kushtua iliyomfikia Paulo kuhusu Wakristo katika Korintho?

      MTUME Paulo aliwahangaikia ndugu zake Wakristo katika Korintho, Ugiriki. Karibu miaka mitano mapema, alikuwa ameanzisha kutaniko katika jiji hilo lenye usitawi lililojulikana sana kwa ajili ya ukosefu walo wa adili. Sasa, karibu mwaka wa 55 W.K., alipokuwa Efeso, Asia Ndogo, alipokea ripoti za kushtua kutoka Korintho kuhusu migawanyiko iliyosababishwa na hali ya kufuata mwanadamu na kule kuvumilia kwa kisa cha ukosefu mbaya wa adili. Zaidi ya hayo, Paulo alikuwa amepokea barua kutoka kwa Wakristo Wakorintho wakiomba mwongozo juu ya mahusiano ya kingono, useja, ndoa, kutengana, na kuoa au kuolewa tena.

      2. Ukosefu wa adili uliokuwa umeenea katika Korintho ulikuwa unaathirije Wakristo katika jiji hilo?

      2 Ukosefu mzito wa adili ulioenea Korintho ulionekana kuathiri kutaniko la mahali hapo katika njia mbili. Wakristo fulani walikuwa wakishindwa na hali ya ulegevu wa kiadili na walikuwa wakiruhusu ukosefu wa adili. (1 Wakorintho 5:1; 6:15-17) Yaonekana wengine, kwa kuitikia kuwapo kwa anasa za kimwili zilizokuwapo kila mahali katika jiji hilo, walipita kiasi kwa kupendekeza hali ya kuepukana na ngono, hata kwa wenzi waliofunga ndoa.—1 Wakorintho 7:5.

      3. Paulo alishughulikia mambo gani kwanza katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho?

      3 Katika ile barua ndefu aliyoandika Paulo kwa Wakorintho, kwanza alishughulikia tatizo la ukosefu wa muungano. (1 Wakorintho, sura 1-4) Aliwahimiza waepuke kufuata wanadamu, jambo liwezalo kuongoza tu kwenye mafarakano yenye kudhuru. Wapaswa wawe na muungano wakiwa “wafanya kazi pamoja” na Mungu. Halafu akawapa maagizo hususa juu ya kudumisha kutaniko likiwa safi kiadili. (Sura 5, 6) Mtume huyo alishughulikia barua yao baada ya hayo.

      Useja Wapendekezwa

      4. Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba “ni heri mwanamume asimguse mwanamke”?

      4 Alianza hivi: “Basi kwa habari ya mambo yale mliyoandika, ni heri mwanamume asimguse mwanamke.” (1 Wakorintho 7:1) Hapa maneno “asimguse mwanamke” yamaanisha kuepuka kugusana na mwanamke kimwili ili kupata raha ya kingono. Kwa kuwa Paulo alikuwa amelaumu uasherati tayari, sasa alikuwa akirejezea mahusiano ya kingono katika mpango wa ndoa. Kwa hiyo, sasa Paulo alikuwa akipendekeza hali ya useja. (1 Wakorintho 6:9, 16, 18; linganisha Mwanzo 20:6; Mithali 6:29.) Mbele kidogo, aliandika hivi: “Nawaambia wale wasiooa bado, na wajane, Ni heri wakae kama mimi nilivyo.” (1 Wakorintho 7:8) Paulo hakuwa amefunga ndoa, labda alikuwa mjane.—1 Wakorintho 9:5.

      5, 6. (a) Kwa nini ni wazi kwamba Paulo hakuwa akipendekeza mtindo-maisha wa watawa? (b) Kwa nini Paulo alipendekeza useja?

      5 Yamkini Wakristo katika Korintho walikuwa wamepata kujua jambo fulani kuhusu falsafa ya Kigiriki, iliyokuwa na vikundi fulani vilivyotukuza hali ya kujinyima anasa za mwili au kujizuia kupita kiasi. Je, hilo laweza kuwa sababu iliyowafanya Wakorintho wamuulize Paulo ikiwa ni “heri” kwa Wakristo kuepuka ngono kabisa? Jibu la Paulo halikuonyesha falsafa ya Kigiriki. (Wakolosai 2:8) Tofauti na wanatheolojia Wakatoliki, yeye hakupendekeza popote maisha ya useja yenye kujinyima anasa za mwili katika makao ya watawa wa kiume au makao ya watawa wa kike, kana kwamba waseja walikuwa watakatifu hasa na wangeweza kuchangia wokovu wao wenyewe kwa mtindo maisha wao na sala zao.

      6 Paulo alipendekeza useja “kwa ajili ya shida iliyopo.” (1 Wakorintho 7:26) Huenda ikawa alikuwa akirejezea zile nyakati ngumu ambazo Wakristo walikuwa wakipitia, zilizoweza kuongezwa na ndoa. (1 Wakorintho 7:28) Shauri lake kwa Wakristo wasiofunga ndoa lilikuwa: “Ni heri wakae kama mimi nilivyo.” Aliwaambia wajane hivi: “Umefunguliwa? usitafute mke.” Kuhusu Mkristo mjane mwanamke, aliandika hivi: “Heri yeye zaidi akikaa kama alivyo; ndivyo nionavyo mimi, nami nadhani ya kuwa mimi nami nina Roho wa Mungu.”—1 Wakorintho 7:8, 27, 40.

      Si Shurutisho Kudumu Ukiwa Mseja

      7, 8. Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo hakuwa akimshurutisha Mkristo yeyote adumu akiwa mseja?

      7 Bila shaka roho takatifu ya Yehova ilikuwa ikimwongoza Paulo alipotoa shauri hilo. Utoaji wake wote kuhusu useja na ndoa waonyesha usawaziko na uzuifu. Halifanyi liwe jambo la kuwa mwaminifu au kutokuwa mwaminifu. Badala ya hivyo, hilo ni swali la uhuru wa kuchagua, likipendekeza useja kwa wale wawezao kudumu wakiwa safi kiadili wakiwa katika hali hiyo.

      8 Mara baada ya kutaarifu “ni heri mwanamume asimguse mwanamke,” Paulo aliongeza hivi: “Lakini kwa sababu ya zinaa kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe, na kila mwanamke na awe na mume wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 7:1, 2) Baada ya kuwashauri watu wasiofunga ndoa na wajane “wakae kama mimi nilivyo,” alifanya upesi kuongeza hivi: “Lakini ikiwa hawawezi kujizuia, na waoe; maana ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa.” (1 Wakorintho 7:8, 9) Tena, shauri lake kwa wajane lilikuwa: “Usitafute mke. Lakini, kama ukioa, huna hatia.” (1 Wakorintho 7:27, 28) Shauri hilo lenye usawaziko laonyesha uhuru wa kuchagua.

      9. Kulingana na Yesu na Paulo, ndoa na pia useja ni zawadi zitokazo kwa Mungu jinsi gani?

      9 Paulo alionyesha kwamba ndoa na pia useja ni zawadi zitokazo kwa Mungu. “Nipendalo ni kwamba watu wote wawe kama mimi nilivyo; walakini kila mtu ana karama [“zawadi,” NW] yake mwenyewe itokayo kwa Mungu, huyu hivi na huyu hivi.” (1 Wakorintho 7:7) Bila shaka alikuwa akifikiria yale aliyosema Yesu. Baada ya kuthibitisha kwamba ndoa ilitoka kwa Mungu, Yesu alionyesha kwamba useja wa hiari kwa ajili ya kutumikia masilahi ya Ufalme ni zawadi hususa: “Si watu wote wafanyao nafasi kwa huo usemi, ila tu wale walio na hiyo zawadi. Kwa maana kuna matowashi waliozaliwa namna hiyo kutoka katika tumbo la uzazi la mama yao, na kuna matowashi waliofanywa matowashi na watu, na kuna matowashi ambao wamejifanya wenyewe matowashi kwa sababu ya ufalme wa mbingu. Acheni yeye awezaye kufanyia hilo nafasi alifanyie hilo nafasi.”—Mathayo 19:4-6, 11, 12.

      Kufanyia Nafasi Zawadi ya Useja

      10. Mtu aweza ‘kufanyiaje nafasi’ (NW) zawadi ya useja?

      10 Ingawa Yesu na Paulo pia walisema juu ya useja kuwa “zawadi,” hakuna aliyesema kwamba ni zawadi ya kimuujiza ambayo ni watu fulani tu walio nayo. Yesu alisema kwamba “si watu wote wafanyao nafasi” kwa ajili ya zawadi hiyo, naye waliwahimiza wale wawezao “kufanyia hilo nafasi,” jambo ambalo Yesu na Paulo walilifanya. Ni kweli, Paulo aliandika hivi: “Ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa,” lakini alikuwa akisema kuhusu wale ambao “hawawezi kujizuia.” (1 Wakorintho 7:9) Katika maandishi ya mapema, Paulo alionyesha kwamba Wakristo waweza kuepuka kuwaka tamaa. (Wagalatia 5:16, 22-24) Kutembea kwa roho kwamaanisha kuruhusu roho ya Yehova iongoze kila moja ya hatua zetu. Je, Wakristo wachanga waweza kufanya hivyo? Ndiyo, wakifuata Neno la Yehova kwa ukaribu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Jinsi gani kijana aisafishe njia yake? Kwa kutii, akilifuata neno lako.”—Zaburi 119:9.

      11. ‘Kutembea kwa kufuata roho’ kunamaanisha nini?

      11 Hilo lahusisha kulinda dhidi ya mawazo yenye uendekevu yanayoenezwa kupitia programu nyingi za televisheni, sinema, makala za magazeti, vitabu, na maneno ya nyimbo. Mawazo hayo yanakazia mambo ya mwili. Mkristo mchanga wa jinsia yoyote anayetaka kufanyia nafasi useja hapaswi “[kutembea] kwa kufuata mambo ya mwili, bali mambo ya roho. Kwa maana wale waufuatao mwili huyafikiri mambo ya mwili; bali wale waifuatao roho huyafikiri mambo ya roho.” (Warumi 8:4, 5, italiki ni zetu.) Mambo ya roho ni yenye uadilifu, yenye usafi kiadili, yenye kupendeka, yenye wema wa adili. Wakristo, vijana kwa wazee, hufanya vema “[kuendelea] kufikiria mambo haya.”—Wafilipi 4:8, 9, NW.

      12. Ni jambo gani hasa linalohusika katika kufanyia nafasi zawadi ya useja?

      12 Kufanyia nafasi zawadi ya useja ni jambo hasa la kukazia moyo mradi huo na kusali kwa Yehova ili apate msaada wa kuufuatia. (Wafilipi 4:6, 7) Paulo aliandika hivi: “Yeye aliyesimama kwa uthabiti wa moyo wake, hana sharti, lakini aweza kuyatawala mapenzi yake, tena amekusudia moyoni mwake kumlinda mwanamwali wake, atatenda vema. Basi, hivyo na amwozaye mwanamwali wake afanya vema; na yeye asiyemwoza atazidi kufanya vema.”—1 Wakorintho 7:37, 38.

      Useja Wenye Kusudi

      13, 14. (a) Mtume Paulo alifanya ulinganifu gani kati ya Wakristo wasiofunga ndoa na wale waliofunga ndoa? (b) Mkristo mseja aweza “kufanya vema” kuliko wale waliofunga ndoa katika njia gani pekee?

      13 Useja si wenye kustahili heshima wenyewe. Basi huo ni ‘wema’ katika maana ipi? Yategemea hasa jinsi mtu anavyoutumia uhuru ambao huo huleta. Paulo aliandika hivi: “Lakini nataka msiwe na masumbufu. Yeye asiyeoa hujishughulisha na mambo ya Bwana, ampendezeje Bwana; bali yeye aliyeoa hujishughulisha na mambo ya dunia hii, jinsi atakavyompendeza mkewe [“amegawanyika,” NW]. Tena iko tofauti hii kati ya mke na mwanamwali. Yeye asiyeolewa hujishughulisha na mambo ya Bwana, apate kuwa mtakatifu mwili na roho. Lakini yeye aliyeolewa hujishughulisha na mambo ya dunia hii, jinsi atakavyompendeza mumewe. Nasema hayo niwafaidie, si kwamba niwategee tanzi, bali kwa ajili ya vile vipendezavyo, tena mpate kumhudumia Bwana pasipo kuvutwa [“kukengeushwa fikira,” NW] na mambo mengine.”—1 Wakorintho 7:32-35.

      14 Mkristo mseja anayetumia hali yake ya kutofunga ndoa ili kufuatia miradi yenye ubinafsi hafanyi “vema” kuliko Wakristo waliofunga ndoa. Anadumu akiwa mseja, si “kwa ajili ya ufalme,” bali kwa sababu za kibinafsi. (Mathayo 19:12) Mwanamume au mwanamke asiyefunga ndoa apaswa ‘kujishughulisha na mambo ya Bwana,’ ahangaikie ‘kumpendeza Bwana,’ na “[amhudumie] Bwana pasipo kuvutwa [“kukengeushwa fikira,” NW] na mambo mengine.” Hilo lamaanisha kukazia uangalifu usiogawanyika kumtumikia Yehova na Kristo Yesu. Ni kwa kufanya hivyo tu ndipo wanaume na wanawake Wakristo wasiofunga ndoa wafanyavyo “vema” kuliko Wakristo waliofunga ndoa.

      Utendaji Pasipo Kukengeushwa Fikira

      15. Ni lipi jambo kuu la hoja ya Paulo katika 1 Wakorintho sura ya 7?

      15 Hii ndiyo hoja yote ya Paulo katika sura hii: Ingawa ndoa ni halali na, chini ya hali fulani, ni jambo lifaalo kwa watu fulani, bila shaka useja ni wenye faida kwa mwanamume au mwanamke Mkristo anayetaka kumtumikia Yehova pasipo kukengeushwa fikira hata kidogo. Hali mtu aliyefunga ndoa “amegawanyika,” Mkristo asiyefunga ndoa yu huru kukazia uangalifu “mambo ya Bwana.”

      16, 17. Mkristo mseja aweza kukazaje uangalifu juu ya “mambo ya Bwana” vizuri zaidi?

      16 Ni yapi mambo ya Bwana ambayo Mkristo asiyefunga ndoa aweza kukazia uangalifu kwa uhuru zaidi kuliko watu waliofunga ndoa? Katika muktadha mwingine, Yesu alisema juu ya “yaliyo ya Mungu”—mambo ambayo Mkristo hawezi kumpa Kaisari. (Mathayo 22:21) Kwa jumla mambo hayo huhusu maisha, ibada, na huduma ya Mkristo.—Mathayo 4:10; Warumi 14:8; 2 Wakorintho 2:17; 3:5, 6; 4:1.

      17 Kwa kawaida waseja wana uhuru zaidi wa kutolea wakati utumishi wa Yehova, uwezao kunufaisha hali yao ya kiroho na kadiri ya huduma yao. Wanaweza kutumia wakati mwingi zaidi kwa funzo la kibinafsi na kutafakari. Mara nyingi Wakristo waseja waweza kutia ndani usomaji wao wa Biblia katika ratiba yao kwa urahisi zaidi kuliko wale waliofunga ndoa wawezavyo. Huenda wakatayarisha vizuri zaidi kwa ajili ya mikutano na utumishi wa shambani. Yote hayo ni kwa ‘faida yao ya kibinafsi.’—1 Wakorintho 7:35, NW.

      18. Ndugu wengi waseja waweza kuonyeshaje kwamba wanataka kumtumikia Yehova pasipo “kukengeushwa fikira” (NW)?

      18 Ndugu wengi waseja wanaotumikia tayari wakiwa watumishi wa huduma wako huru kumwambia Yehova: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isaya 6:8) Wanaweza kujaza ombi la kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, iwezayo kuhudhuriwa tu na watumishi wa huduma na wazee walio waseja ambao wako huru kutumikia mahali palipo na uhitaji mkubwa zaidi. Hata ndugu ambao hawako huru kuacha kutaniko lao waweza kuwa tayari kutumikia ndugu zao wakiwa watumishi wa huduma au wazee.—Wafilipi 2:20-23.

      19. Dada waseja wengi wanabarikiwaje, na ni ipi njia moja wawezayo kuwa baraka kwa makutaniko?

      19 Dada waseja, wakiwa hawana mtu aliye kichwa chao, wa kushauriana naye na wa kumwambia siri, huenda wakaelekea zaidi ‘kumtwika BWANA mizigo yao.’ (Zaburi 55:22; 1 Wakorintho 11:3) Hilo ni jambo la maana hasa kwa dada ambao ni waseja kwa sababu ya kumpenda Yehova. Wakifunga ndoa hatimaye, ingekuwa “katika Bwana tu,” yaani, wangefunga ndoa tu na mtu aliyejiweka wakfu kwa Yehova. (1 Wakorintho 7:39) Wazee wanashukuru kuwa na dada wasiofunga ndoa kutanikoni mwao; mara nyingi hao hutembelea na kusaidia wagonjwa na wazee-wazee. Hilo hufurahisha wote wanaohusika.—Matendo 20:35.

      20. Wakristo wengi wanaonyeshaje kwamba ‘wanamhudumia Bwana pasipo [“kukengeushwa fikira,” NW]’?

      20 Wakristo wengi wachanga wamepanga mambo yao ili waweze “kumhudumia Bwana pasipo kuvutwa [“kukengeushwa fikira,” NW] na mambo mengine.” (1 Wakorintho 7:35) Wanamtumikia Yehova wakiwa wahudumu mapainia wa wakati wote, wamishonari, au kwenye mojawapo ofisi za tawi za Watch Tower Society. Nao ni kikundi chenye furaha kama nini! Kuwapo kwao kwaburudisha kama nini! Machoni pa Yehova na Yesu, wao ni kama “umande.”—Zaburi 110:3.

      Hakuna Nadhiri ya Useja wa Daima

      21. (a) Kwa nini ni wazi kwamba Paulo hakutia moyo kuweka nadhiri ya useja? (b) Alidokeza nini aliposema juu ya ‘kupita mchanuko wa ujana’?

      21 Jambo kuu katika shauri la Paulo ni kwamba Wakristo wangefanya “vema” kufanyia nafasi useja maishani mwao. (1 Wakorintho 7:1, 8, 26, 37) Hata hivyo, yeye hawaaliki kwa vyovyote waweke nadhiri ya useja. Kinyume cha hilo, aliandika hivi: “Ikiwa yeyote afikiri anajiendesha isivyofaa kuelekea ubikira wake, ikiwa huo umepita mchanuko wa ujana, na hiyo ndiyo njia ambayo yapasa kutukia, acheni afanye lile atakalo; hafanyi dhambi. Acheni waoe au waolewe.” (1 Wakorintho 7:36, NW) Lile neno moja la Kigiriki (hy·peʹra·kmos) ambalo limetafsiriwa “umepita mchanuko wa ujana” lamaanisha kihalisi “kupita kilele cha juu zaidi” na hurejezea kupita kilele cha msukumo wa tamaa ya kingono. Kwa hiyo wale ambao wamekuwa katika hali ya useja kwa miaka kadhaa na wanaohisi hatimaye kwamba wapaswa kufunga ndoa wako huru kabisa kufunga ndoa na mwamini mwenzao.—2 Wakorintho 6:14.

  • Mume na Mzee—Kusawazisha Hayo Madaraka
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Oktoba 15
    • 1, 2. Kwa nini useja wa mapadri si wa Kimaandiko?

      KATIKA karne ya kwanza, Wakristo waaminifu walihangaikia kusawazisha madaraka yao mbalimbali. Mtume Paulo aliposema kwamba Mkristo anayedumu akiwa mseja “atazidi kufanya vema,” je, alimaanisha kwamba mwanamume huyo angefaa zaidi kutumikia akiwa mwangalizi katika kutaniko la Kikristo? Je, alikuwa akifanya useja kuwa takwa la kuwa mzee? (1 Wakorintho 7:38) Useja ni takwa kwa makasisi Wakatoliki. Lakini je, useja wa mapadri ni wa Kimaandiko? Makanisa ya Othodoksi ya Mashariki huruhusu mapadri wao wa parokia wawe wanaume waliooa, lakini hawaruhusu maaskofu wao wafanye hivyo. Je, hilo lapatana na Biblia?

      2 Wengi wa mitume 12 wa Kristo, washiriki wa msingi wa kutaniko la Kikristo, walikuwa wanaume waliooa. (Mathayo 8:14, 15; Waefeso 2:20) Paulo aliandika hivi: “Je, hatuna ruhusa kumchukua mke Mkristo katika ziara zetu, kama vile wafanyavyo mitume wengine, ndugu zake Bwana, na pia Kefa [Petro]?” (1 Wakorintho 9:5, Habari Njema kwa Watu Wote) Kichapo New Catholic Encyclopedia chakubali kwamba “chanzo cha sheria ya useja ni cha kikanisa” na kwamba “wahudumu katika AJ [Agano Jipya] hawakuwa chini ya wajibu wa useja.” Mashahidi wa Yehova hufuata kigezo cha Kimaandiko badala ya sheria ya kikanisa.—1 Timotheo 4:1-3.

      Kuwa Mzee na Ndoa Ni Mambo Yanayopatana

      3. Ni mambo gani ya hakika ya Kimaandiko yaonyeshayo kwamba waangalizi Wakristo waweza kuwa wanaume waliooa?

      3 Badala ya kutaka kwamba wanaume waliowekwa rasmi wawe waangalizi wasioe, Paulo alimwandikia Tito hivi: “Kwa sababu hii nalikuacha Krete, ili uyatengeneze yaliyopunguka, na kuweka wazee [Kigiriki, pre·sbyʹte·ros] katika kila mji kama vile nilivyokuamuru; ikiwa mtu hakushitakiwa neno, naye ni mume wa mke mmoja, ana watoto waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii. Maana imempasa askofu [“mwangalizi,” NW] [Kigiriki, e·piʹsko·pos, litokapo neno “askofu”] awe mtu asiyeshitakiwa neno, kwa kuwa ni wakili wa Mungu.”—Tito 1:5-7.

      4. (a) Twajuaje kwamba ndoa si takwa kwa waangalizi Wakristo? (b) Ndugu mseja aliye mzee ana faida gani?

      4 Kwa upande mwingine, ndoa si takwa la Kimaandiko la kuwa mzee. Yesu alidumu akiwa mseja. (Waefeso 1:22) Paulo, mwangalizi mwenye kutokeza katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, alikuwa asiyeoa wakati huo. (1 Wakorintho 7:7-9) Leo, kuna Wakristo wengi waseja wanaotumikia wakiwa wazee. Hali yao ya useja labda huwaruhusu wawe na wakati mwingi zaidi kushughulikia wajibu wao mbalimbali wakiwa waangalizi.

      ‘Mtu Aliyeoa Amegawanyika’

      5. Ndugu waliooa wakubali jambo gani la hakika la Kimaandiko?

      5 Mwanamume Mkristo anapooa, yeye apaswa kung’amua kwamba anajipatia madaraka mapya yatakayotaka wakati na uangalifu wake. Biblia hutaarifu hivi: “Yeye asiyeoa hujishughulisha na mambo ya Bwana, ampendezeje Bwana; bali yeye aliyeoa hujishughulisha na mambo ya dunia hii, jinsi atakavyompendeza mkewe [“naye amegawanyika,” NW].” (1 Wakorintho 7:32-34) Kugawanyika katika maana ipi?

      6, 7. (a) Mwanamume aliyeoa “amegawanyika” (NW) katika njia gani moja? (b) Paulo awatolea shauri gani Wakristo waliofunga ndoa? (c) Hilo lingeweza kuathirije uamuzi wa mwanamume wa kukubali mgawo wa kazi?

      6 Kwanza, mtu aliyeoa anamkabidhi mtu mwingine mamlaka juu ya mwili wake mwenyewe. Paulo alieleza jambo hilo kwa wazi sana: “Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe.” (1 Wakorintho 7:4) Watu fulani wanaofikiria ndoa huenda wakahisi kwamba onyo hilo la upole halina maana sana kwa sababu ngono haitakuwa jambo kuu katika ndoa yao. Hata hivyo, kwa kuwa usafi wa kiadili kabla ya ndoa ni takwa la Kimaandiko, kwa kweli Wakristo hawajui mahitaji ya kindani ya atakayekuwa mwenzi wao wakati ujao.

      7 Paulo aonyesha kwamba hata wenzi ‘wanaofikiri mambo ya roho’ lazima wafikirie mahitaji ya ngono ya mmoja na mwenzake. Aliwashauri Wakristo katika Korintho hivi: “Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi kwenu.” (Warumi 8:5; 1 Wakorintho 7:3, 5) Kwa kuhuzunisha, kumekuwa na visa vya uzinzi wakati ambapo shauri hilo halikufuatwa. Kwa sababu hiyo, Mkristo aliyefunga ndoa apaswa achunguze mambo kwa uangalifu kabla ya kukubali mgawo wa kazi utakaomtenganisha na mkewe kwa kipindi kirefu cha wakati. Yeye hana tena uhuru uleule wa kutenda aliokuwa nao alipokuwa mseja.

      8, 9. (a) Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba Wakristo waliofunga ndoa “hujishughulisha na mambo ya dunia hii”? (b) Wakristo waliofunga ndoa wajishughulishe kufanya nini?

      8 Yaweza kusemwa katika maana gani kwamba wanaume Wakristo waliooa, kutia na wazee, “hujishughulisha na mambo ya dunia hii [“ulimwengu,” NW] [koʹsmos]”? (1 Wakorintho 7:33) Ni dhahiri sana kwamba Paulo hakuwa akisema juu ya mambo mabaya ya ulimwengu huu, ambayo Wakristo wote wa kweli wapaswa kuepuka. (2 Petro 1:4; 2:18-20; 1 Yohana 2:15-17) Neno la Mungu hutuagiza “kukataa ubaya na tamaa za kidunia [“kilimwengu,” NW] [ko·smi·kosʹ]; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa.”—Tito 2:12.

      9 Kwa hiyo, Mkristo aliyefunga ndoa “hujishughulisha na mambo ya dunia hii” kwa habari ya kwamba yeye huhangaikia kihalali mambo ya kimwili ambayo ni sehemu ya maisha ya kawaida ya ndoa. Hayo yatia ndani nyumba, chakula, mavazi, tafrija—kuongezea mahangaiko mengine yasiyohesabika ikiwa kuna watoto. Lakini hata kwa wenzi wasio na watoto, ikiwa ndoa hiyo itafanikiwa, mume na pia mke lazima ajishughulishe ili apate ‘kumpendeza’ mwenzi wake wa ndoa. Hilo ni la upendezi mahususi kwa wazee Wakristo wasawazishapo madaraka yao.

      Waume Wema na pia Wazee Wema

      10. Ili Mkristo astahili kuwa mzee, ndugu zake na watu walio nje wapaswa kuweza kuona nini?

      10 Ingawa ndoa si takwa la kuwa mzee, ikiwa mwanamume Mkristo alioa, kabla ya kupendekezwa kwa ajili ya kuwekwa rasmi kuwa mzee, kwa hakika apaswa kutoa uthibitisho wa kujitahidi kuwa mume mwema, mwenye upendo, huku akitumia ukichwa ifaavyo. (Waefeso 5:23-25, 28-31) Paulo aliandika hivi: “Ni neno la kuaminiwa; mtu akitaka kazi ya askofu [“mwangalizi,” NW], atamani kazi njema. Basi imempasa askofu [“mwangalizi,” NW] awe mtu asiyelaumika, mume wa mke mmoja.” (1 Timotheo 3:1, 2) Yapaswa iwe dhahiri kwamba mzee anafanya kadiri awezavyo ili kuwa mume mwema, mke wake awe ni Mkristo mwenzake au la. Kwa kweli, hata watu walio nje ya kutaniko wapaswa kuweza kuona kwamba anamtunza mke wake vizuri na yale madaraka yake mengine. Paulo aliongeza hivi: “Imempasa kushuhudiwa mema na watu walio nje; ili asianguke katika lawama na mtego wa Ibilisi.”—1 Timotheo 3:7.

      11. Fungu la maneno “mume wa mke mmoja” ladokeza nini, kwa hiyo wazee wachukue hatua zipi za kujihadhari?

      11 Bila shaka, fungu la maneno “mume wa mke mmoja” lakataza ndoa ya wake wengi, na pia ladokeza uaminifu wa ndoa. (Waebrania 13:4) Wazee wahitaji hasa kuwa waangalifu wanaposaidia dada kutanikoni. Wapaswa kuepuka kuwa peke yao wanapomtembelea dada fulani anayehitaji shauri na faraja. Wangefanya vema kuandamana na mzee mwingine, mtumishi wa huduma, au hata mke wao ikiwa ni jambo la kufanya ziara ya kutia moyo tu.—1 Timotheo 5:1, 2.

      12. Wake wa wazee na wa watumishi wa huduma wajitahidi kufaana na ufafanuzi upi?

      12 Kama ilivyo, mtume Paulo alipokuwa akiorodhesha matakwa ya wazee na watumishi wa huduma, alikuwa na shauri pia la kuwapa wake wa wale wanaofikiriwa kwa ajili ya mapendeleo hayo. Aliandika hivi: “Vivyo hivyo wake zao na wawe wastahivu; si wasingiziaji; watu wa kiasi, waaminifu katika mambo yote.” (1 Timotheo 3:11) Mume Mkristo aweza kuchangia sana kumsaidia mkewe afaane na ufafanuzi huo.

      Wajibu Mbalimbali wa Kimaandiko kwa Mke

      13, 14. Hata ikiwa mke wa mzee si Shahidi mwenzake, kwa nini akae naye na awe mume mwema?

      13 Bila shaka, shauri hili wanalopewa wake wa wazee au wa watumishi wa huduma latarajia kwamba wake hao wenyewe ni Wakristo waliojiweka wakfu. Kwa ujumla, ndivyo ilivyo kwa sababu Wakristo wanatakwa wafunge ndoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Lakini namna gani ndugu aliyekuwa tayari ameoa mke asiyeamini alipoweka maisha yake wakfu kwa Yehova, au yule ambaye mke wake aiacha kweli kwa kosa lisilo la mume?

      14 Jambo hilo lenyewe, lisingemzuia asiwe mzee. Hata hivyo, lisingempa haki ya kutengana na mkewe kwa sababu tu yeye hashiriki itikadi zake. Paulo alishauri hivi: “Je! umefungwa kwa mke? usitake kufunguliwa.” (1 Wakorintho 7:27) Aliendelea kutaarifu hivi: “Iwapo ndugu mmoja ana mke asiyeamini, na mke huyo anakubali kukaa naye asimwache. Lakini yule asiyeamini akiondoka, na aondoke. Hapo huyo ndugu mume au ndugu mke hafungiki. Lakini Mungu ametuita katika amani. Kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo?” (1 Wakorintho 7:12, 15, 16) Hata ikiwa mkewe si Shahidi, mzee apaswa kuwa mume mwema.

      15. Mtume Petro hutolea shauri gani waume Wakristo, na matokeo yaweza kuwa nini mzee akithibitika kuwa mume mwenye kumpuuza mke?

      15 Mkewe awe ni mwamini mwenzake au la, mzee Mkristo apaswa kutambua kwamba mke wake ahitaji uangalifu wake wenye upendo. Mtume Petro aliandika hivi: “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.” (1 Petro 3:7) Mume ambaye kwa kukusudia anakosa kushughulikia mahitaji ya mkewe huhatarisha uhusiano wake mwenyewe pamoja na Yehova; hilo laweza kumzuia asimfikie Yehova kama kwamba ‘kwa wingu, maombi yasipite.’ (Maombolezo 3:44) Hilo lingeweza kuongoza kwenye kutostahili kwake tena kutumikia akiwa mwangalizi Mkristo.

      16. Paulo atoa jambo gani kuu, na wazee wahisije juu ya hilo?

      16 Kama ilivyoonyeshwa, jambo kuu la hoja ya Paulo ni kwamba mwanamume anapooa, anaacha kiasi fulani cha uhuru aliokuwa nao akiwa mwanamume mseja uliomruhusu ‘amhudumie Bwana pasipo [“kukengeushwa fikira,” NW].’ (1 Wakorintho 7:35) Ripoti zaonyesha kwamba wazee fulani waliooa hawajakuwa na usawaziko siku zote katika kusababu juu ya maneno ya Paulo yaliyopuliziwa. Katika tamaa yao ya kutimiza yale wanayohisi kwamba wazee wema wanapaswa kufanya, huenda wakapuuza baadhi ya wajibu wao mbalimbali wa kimume. Huenda wengine wakapata ugumu wa kukataa pendeleo la kutaniko, hata ikiwa kulikubali kungekuwa na madhara ya kiroho kwa wake zao. Wanafurahia mapendeleo yanayoambatana na ndoa, lakini je, wako tayari kutimiza madaraka yanayoambatana nayo?

      17. Ni jambo gani ambalo limewapata wake fulani, na hilo lingaliwezaje kuepukwa?

      17 Bila shaka, kuwa na bidii akiwa mzee ni jambo linalostahili pongezi. Hata hivyo, je, Mkristo amesawazika ikiwa, katika kutimiza wajibu wake mbalimbali kutanikoni, anapuuza madaraka yake ya Kimaandiko kwa mke wake? Huku akitamani kuwategemeza walio kutanikoni, mzee mwenye usawaziko atahangaikia pia hali ya kiroho ya mke wake. Baadhi ya wake wa wazee wamekuwa dhaifu kiroho, na wengine ‘wameangamia’ kiroho. (1 Timotheo 1:19) Ingawa mke ana daraka la kufanyia kazi wokovu wake mwenyewe, katika visa vingi hilo lingaliweza kuepukwa ikiwa mzee ‘angalimlisha na kumtunza’ mkewe, “kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa.” (Waefeso 5:28, 29) Kwa hakika, ni lazima wazee ‘watunze nafsi zao, na lile kundi lote nalo.’ (Matendo 20:28) Ikiwa wameoa, hilo latia ndani wake zao.

      “Dhiki Katika Mwili”

      18. Ni zipi baadhi ya sehemu za “dhiki” ambazo Wakristo waliofunga ndoa hupatwa nazo, na hilo lingeweza kuathirije utendaji mbalimbali wa wazee?

      18 Mtume aliandika hivi pia: “Mwanamwali akiolewa, hana hatia; lakini watu kama hao watakuwa na dhiki katika mwili nami nataka kuwazuilia hayo.” (1 Wakorintho 7:28) Paulo alitamani kuwazuilia wale walioweza kufuata kielelezo chake cha useja wasiwe na mahangaiko yasiyoepukika yanayoambatana na ndoa. Hata kwa wenzi wasio na watoto, huenda mahangaiko hayo yakatia ndani matatizo ya afya au ya kifedha na pia madaraka ya Kimaandiko kwa wazazi waliozeeka wa mwenzi. (1 Timotheo 5:4, 8) Lazima mzee akabiliane na madaraka hayo kwa njia ya kuweka kielelezo chema, na nyakati nyingine hilo laweza kuathiri utendaji wake mbalimbali akiwa mwangalizi Mkristo. Kwa kufurahisha, wazee wanafanya kazi bora katika kutimiza madaraka yao ya familia na ya kutaniko.

      19. Paulo alimaanisha nini aliposema: “Wale walio na wake na wawe kama hawana”?

      19 Paulo aliongeza hivi: “Muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa wale walio na wake na wawe kama hawana.” (1 Wakorintho 7:29) Bila shaka, kwa sababu ya yale aliyokuwa ameandika tayari katika sura hii ya Wakorintho, ni dhahiri kwamba hakumaanisha kwamba Wakristo waliofunga ndoa kwa njia fulani wawapuuze wake zao. (1 Wakorintho 7:2, 3, 33) Alionyesha alichomaanisha, alipoandika hivi: “[Acha] wale wautumiao ulimwengu huu, [wawe] kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita.” (1 Wakorintho 7:31) Sasa, hata zaidi kuliko katika siku ya Paulo au katika siku ya mtume Yohana, ‘ulimwengu unapita.’ (1 Yohana 2:15-17, HNWW) Kwa hiyo, Wakristo waliofunga ndoa wanaoona uhitaji wa kutoa dhabihu katika kumfuata Kristo hawawezi kujishughulisha kabisa katika shangwe na mapendeleo ya ndoa.—1 Wakorintho 7:5.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki