Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuwa Hodari Kupitia Imani na Kumwogopa Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Oktoba 1
    • Kuwa Hodari Kupitia Imani na Kumwogopa Mungu

      “Uwe hodari na mwenye nguvu . . . Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe.”—YOSHUA 1:9.

      1, 2. (a) Kwa maoni ya wanadamu, je, kulikuwa na matumaini yoyote kwamba Waisraeli wangewashinda Wakanaani? (b) Yoshua alipewa uhakikisho gani?

      KATIKA mwaka wa 1473 K.W.K., taifa la Israeli lilikuwa tayari kuingia Nchi ya Ahadi. Kuhusiana na matatizo ambayo wangekabili, Musa aliwakumbusha watu hao hivi: ‘Leo mnavuka Yordani mwingie ndani na kuyafukuza mataifa makubwa zaidi na yenye nguvu zaidi kuliko ninyi, majiji makubwa na yenye ngome zinazofika mbinguni, watu wakubwa na warefu, wana wa Waanaki, ambao mmesikia ikisemwa juu yao, “Ni nani anayeweza kusimama imara mbele ya wana wa Anaki?”’ (Kumbukumbu la Torati 9:1, 2) Naam, mashujaa hao ambao walikuwa majitu walijulikana sana! Isitoshe, Wakanaani fulani walikuwa na majeshi yenye silaha za kutosha, pamoja na farasi na magari ya vita yenye miundu ya chuma kwenye magurudumu.—Waamuzi 4:13.

      2 Kwa upande mwingine, hapo awali Israeli lilikuwa taifa la watumwa, nao walikuwa wamekaa nyikani kwa miaka 40. Hivyo, kwa maoni ya wanadamu, haikuonekana kwamba wangeshinda vita. Hata hivyo, Musa alikuwa na imani; angeweza ‘kumwona’ Yehova akiwaongoza. (Waebrania 11:27) Musa aliwaambia watu hivi: ‘Yehova Mungu wenu anavuka mbele yenu. Atawaangamiza hao, na yeye mwenyewe atawatiisha mbele yenu.’ (Kumbukumbu la Torati 9:3; Zaburi 33:16, 17) Baada ya kifo cha Musa, Yehova alimhakikishia Yoshua kwamba angemtegemeza, aliposema hivi: “Simama sasa, vuka huu mto Yordani, wewe na watu hawa wote, mwingie katika nchi ambayo ninawapa wao, wana wa Israeli. Hakuna yeyote atakayesimama imara mbele yako siku zote za maisha yako. Nitakuwa pamoja nawe, kama vile nilivyokuwa pamoja na Musa.”—Yoshua 1:2, 5.

      3. Ni nini kilichomsaidia Yoshua kuwa na imani na uhodari?

      3 Ili kupata msaada na mwongozo wa Yehova, Yoshua alipaswa kusoma na kutafakari Sheria ya Mungu na kuishi kulingana nayo. Yehova alisema hivi: “Kwa maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima. Je, mimi sikukuamuru wewe? Uwe hodari na mwenye nguvu. Usitetemeke wala usiwe na hofu, kwa maana Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe kila mahali unapoenda.” (Yoshua 1:8, 9) Kwa kuwa Yoshua alimsikiliza Mungu, alikuwa hodari, mwenye nguvu, naye alifanikiwa. Hata hivyo, watu wengi wa kizazi chake hawakusikiliza. Hivyo, hawakufanikiwa, nao walikufa nyikani.

      Watu Wasio na Imani Wakosa Uhodari

      4, 5. (a) Mtazamo wa wale wapelelezi kumi ulitofautianaje na ule wa Yoshua na Kalebu? (b) Yehova alitendaje watu hao walipokosa imani?

      4 Miaka 40 mapema Waisraeli walipokaribia Kanaani kwa mara ya kwanza, Musa aliwatuma wanaume 12 ili waipeleleze nchi. Kumi kati yao walirudi wakiwa na woga. Walipaaza sauti hivi: “Watu wote tuliowaona katikati yake ni watu wenye ukubwa usio wa kawaida. Na humo tuliwaona Wanefili, wana wa Anaki, waliotoka kwa Wanefili; hivi kwamba sisi tukawa machoni petu wenyewe kama panzi.” Je, kweli “watu wote” walikuwa majitu au ni Waanaki tu? Si watu wote waliokuwa majitu. Je, Waanaki walikuwa wazao wa Wanefili walioishi kabla ya Gharika? Hapana! Hata hivyo, kwa sababu ya kutilia chumvi, woga ulitanda kambini. Hata watu walitaka kurudi Misri, ambako walikuwa watumwa!—Hesabu 13:31–14:4.

      5 Lakini, wapelelezi wawili Yoshua na Kalebu, walitamani kuingia Nchi ya Ahadi. Walisema hivi: “[Wakanaani] ni mkate kwetu. Ulinzi wao umegeuka kutoka juu yao, na Yehova yuko pamoja nasi. Msiwaogope.” (Hesabu 14:9) Je, uhakika wa Yoshua na Kalebu ulikuwa na msingi? Ndiyo! Wao pamoja na taifa lote, walikuwa wameona Yehova akifedhehesha taifa la Misri lenye nguvu na miungu yao kupitia Mapigo Kumi. Kisha, walimwona Yehova akimzamisha Farao na majeshi yake katika Bahari Nyekundu. (Zaburi 136:15) Ni wazi kwamba, wapelelezi kumi na wale walioathiriwa nao hawakupaswa kuogopa. Yehova alisema hivi kwa huzuni nyingi: “Watakosa kuniamini mpaka wakati gani ijapokuwa ishara zote ambazo nilifanya katikati yao?”—Hesabu 14:11.

      6. Kuna uhusiano gani kati ya uhodari na imani, na hilo limeonekanaje katika nyakati za sasa?

      6 Yehova alitaja chanzo cha tatizo, yaani, woga wa watu hao ulionyesha kwamba hawakuwa na imani. Naam, kuna uhusiano wa karibu sana kati ya imani na uhodari, hivi kwamba mtume Yohana aliandika hivi kuhusu kutaniko la Kikristo na vita vyake vya kiroho: “Huu ndio ushindi ambao umeushinda ulimwengu, imani yetu.” (1 Yohana 5:4) Leo, imani kama ya Yoshua na Kalebu imewezesha habari njema ya Ufalme ihubiriwe ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni sita, vijana kwa wazee, wenye nguvu na walio dhaifu. Hakuna adui ambaye amefaulu kunyamazisha jeshi hilo lenye nguvu na lililo hodari.—Waroma 8:31.

      ‘Usirudi Nyuma’

      7. ‘Kurudi nyuma’ kunamaanisha nini?

      7 Leo, watumishi wa Yehova wanahubiri habari njema kwa uhodari kwa sababu wana mtazamo kama wa mtume Paulo aliyeandika hivi: “Sisi si namna ya watu wanaorudi nyuma kwenye maangamizi, bali sisi ni namna ya watu walio na imani ya kuihifadhi hai nafsi.” (Waebrania 10:39) Kama Paulo alivyotaja ‘kurudi nyuma’ hakumaanishi kuogopa kwa muda mfupi, kwa kuwa kuna wakati ambapo watumishi wengi waaminifu wa Mungu wameogopa. (1 Samweli 21:12; 1 Wafalme 19:1-4) Badala yake, kamusi moja ya Biblia inasema kwamba kurudi nyuma kunamaanisha “kusonga nyuma, kuacha,” “kulegea katika kufuata kweli.” Pia, inasema kwamba huenda ikawa ‘kurudi nyuma’ ni maneno ya mfano yanayotokana na “kushusha tanga ya meli na hivyo kupunguza mwendo” katika utumishi wa Mungu. Bila shaka, wale walio na imani yenye nguvu hawafikirii kamwe “kupunguza mwendo” wakati matatizo yanapotokea, yawe ni mateso, magonjwa, au majaribu mengine. Badala yake, wanasonga mbele kwa kumtumikia Yehova, wakijua kwamba anawajali sana na anajua udhaifu wao. (Zaburi 55:22; 103:14) Je, una imani kama hiyo?

      8, 9. (a) Yehova aliimarishaje imani ya Wakristo wa mapema? (b) Tunaweza kufanya nini ili tuimarishe imani yetu?

      8 Wakati mmoja mitume walihisi kwamba imani yao ilikuwa imepungua, hivyo wakamwambia Yesu hivi: “Tupe imani zaidi.” (Luka 17:5) Ombi lao la unyoofu lilijibiwa, hasa siku ya Pentekoste 33 W.K., wakati roho takatifu iliyoahidiwa ilipokuja juu ya wanafunzi na kuwapa ufahamu mwingi wa Neno la Mungu na kusudi lake. (Yohana 14:26; Matendo 2:1-4) Imani ya wanafunzi hao ikiwa imeimarishwa, walianza kampeni ya kuhubiri, na licha ya upinzani walihubiri habari njema katika “uumbaji wote ulio chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23; Matendo 1:8; 28:22.

      9 Ili kuimarisha imani yetu na kuendelea na huduma yetu, ni lazima sisi pia tujifunze na kutafakari kuhusu Maandiko na kusali ili tupate roho takatifu. Kama vile Yoshua, Kalebu, na wanafunzi Wakristo wa mapema, tukikazia kweli ya Mungu katika akili na moyo wetu tutapata imani inayotuwezesha kuwa hodari ili kuvumilia na kushinda katika vita vyetu vya kiroho.—Waroma 10:17.

      Imani Si Kuamini Tu Kwamba Kuna Mungu

      10. Imani ya kweli inahusisha nini?

      10 Kama ilivyoonyeshwa na watu wa zamani wenye utimilifu, imani inayomsaidia mtu kuwa hodari na kuvumilia inatia ndani mengi kuliko kuamini tu kwamba kuna Mungu. (Yakobo 2:19) Imani hiyo inahusisha kumjua Yehova kuwa mtu halisi na kumwamini kabisa. (Zaburi 78:5-8; Methali 3:5, 6) Inamaanisha kuamini kwa moyo wetu wote kwamba tunafaidika sana tunapotii sheria na kanuni za Mungu. (Isaya 48:17, 18) Pia, imani inahusisha kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatimiza ahadi zake zote na kuwa “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:1, 6; Isaya 55:11.

      11. Yoshua na Kalebu walibarikiwaje kwa sababu ya imani na uhodari wao?

      11 Imani hiyo hukua. Inakua tunapoishi kulingana na kweli, ‘tunapoonja’ faida zake, ‘tunapoona’ sala zetu zikijibiwa, na kutambua mwongozo wa Yehova maishani mwetu kwa njia nyingine. (Zaburi 34:8; 1 Yohana 5:14, 15) Tunaweza kuwa na hakika kwamba imani ya Yoshua na Kalebu iliimarishwa walipoonja wema wa Mungu. (Yoshua 23:14) Fikiria mambo haya: Waliokoka safari ya miaka 40 nyikani kama Mungu alivyoahidi. (Hesabu 14:27-30; 32:11, 12) Walipewa kazi ya pekee wakati wa ile miaka sita ya kuteka Kanaani. Hatimaye, walifurahia maisha marefu na afya nzuri na hata wakapewa urithi wao. Yehova huwapa thawabu wale walio waaminifu na wanaomtumikia kwa uhodari!—Yoshua 14:6, 9-14; 19:49, 50; 24:29.

      12. Yehova ‘hulitukuzaje neno lake’?

      12 Fadhili zenye upendo ambazo Mungu aliwaonyesha Yoshua na Kalebu zinatukumbusha maneno haya ya mtunga-zaburi: “Umeyatukuza maneno yako hata juu ya jina lako lote.” (Zaburi 138:2) Yehova anapotumia jina lake kuonyesha uhakika wa ahadi fulani, utimizo wa ahadi hiyo ‘hutukuzwa’ katika maana ya kwamba ahadi hiyo hutimia hata zaidi ya vile inavyotarajiwa. (Waefeso 3:20) Naam, kamwe Yehova hawavunji moyo wale ambao ‘hupata furaha tele’ katika yeye.—Zaburi 37:3, 4.

      Mtu ‘Aliyempendeza Mungu Vema’

      13, 14. Kwa nini Enoko alihitaji imani na uhodari?

      13 Tunaweza kujifunza mengi kuhusu imani na uhodari kwa kufikiria mfano wa shahidi mwingine wa kabla ya Ukristo, yaani, Enoko. Hata kabla ya kuanza kutoa unabii, huenda Enoko alijua kwamba imani na uhodari wake ungejaribiwa. Kwa nini? Kwa sababu Yehova alikuwa amesema katika Edeni kwamba kungekuwa na uadui au chuki kati ya wale wanaomtumikia Mungu na wale wanaomtumikia Shetani Ibilisi. (Mwanzo 3:15) Enoko alijua pia kwamba chuki hiyo ilikuwa imetokea mapema katika historia ya wanadamu wakati Kaini alipomuua Abeli ndugu yake. Adamu, baba yao, aliendelea kuishi miaka 310 hivi baada ya Enoko kuzaliwa.—Mwanzo 5:3-18.

      14 Hata hivyo, licha ya mambo hayo, Enoko ‘aliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli’ kwa uhodari na kushutumu ‘mambo yenye kushtua’ ambayo watu walisema dhidi ya Yehova. (Mwanzo 5:22; Yuda 14, 15) Inaonekana msimamo huo thabiti kwa ajili ya ibada ya kweli ulifanya Enoko awe na maadui wengi na kuhatarisha maisha yake. Wakati huo, Yehova alimlinda nabii wake asipate maumivu ya kifo. Baada ya kumfunulia Enoko “kwamba amempendeza Mungu vema,” Yehova ‘alimhamisha’ toka uhai hadi kifo, huenda akiwa katika maono ya kinabii.—Waebrania 11:5, 13; Mwanzo 5:24.

      15. Enoko aliwawekea watumishi wa kisasa wa Yehova mfano gani mzuri?

      15 Mara tu baada ya kutaja jinsi Enoko alivyohamishwa, Paulo alikazia tena umuhimu wa imani aliposema hivi: “Zaidi ya hayo, bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema.” (Waebrania 11:6) Naam, kuwa na imani kulimwezesha Enoko kuwa hodari ili atembee pamoja na Yehova na kutangaza ujumbe wa Yehova wa hukumu kwa ulimwengu usiomwogopa Mungu. Kwa njia hiyo, Enoko alituwekea mfano mzuri. Tuna kazi kama hiyo katika ulimwengu unaopinga ibada ya kweli na uliojaa kila namna ya ubaya.—Zaburi 92:7; Mathayo 24:14; Ufunuo 12:17.

      Kuwa Hodari kwa Kumwogopa Mungu

      16, 17. Obadia alikuwa nani, naye alikabili hali gani?

      16 Zaidi ya imani, kuna jambo lingine linalotuwezesha kuwa hodari, yaani, kumwogopa na kumheshimu Mungu. Acheni tuone mfano bora wa mtu aliyemwogopa Mungu, na ambaye aliishi katika siku za nabii Eliya na Mfalme Ahabu, aliyetawala ufalme wa kaskazini wa Israeli. Wakati wa utawala wa Ahabu, ibada ya Baali iliathiri sana ufalme wa kaskazini. Hata manabii 450 wa Baali na manabii wengine 400 wa mti mtakatifu, ambao ulikuwa ishara ya kiungo cha uzazi cha kiume, ‘walikula mezani pa Yezebeli,’ mke wa Ahabu.—1 Wafalme 16:30-33; 18:19.

      17 Akiwa adui mkatili wa Yehova, Yezebeli alijaribu kukomesha ibada ya kweli nchini. Aliwaua baadhi ya manabii wa Yehova na hata akajaribu kumuua Eliya, ambaye kulingana na mwongozo wa Mungu alikimbia na kuvuka Mto Yordani. (1 Wafalme 17:1-3; 18:13) Je, unaweza kuwazia jinsi ambavyo ingekuwa vigumu kuunga mkono ibada safi katika ufalme wa kaskazini wakati huo? Namna gani ikiwa ungekuwa unafanya kazi katika jumba la mfalme? Obadiaa alikabili hali hiyo. Alikuwa mtumishi wa nyumba ya Ahabu, naye alimwogopa Mungu.—1 Wafalme 18:3.

      18. Ni jambo gani lililomwezesha Obadia kuwa mwabudu wa pekee wa Yehova?

      18 Bila shaka, Obadia alikuwa mwenye tahadhari na busara katika ibada yake kwa Yehova. Lakini, hakukana imani yake. Andiko la 1 Wafalme 18:3 linatuambia hivi: “Obadia alikuwa amejionyesha kuwa mtu anayemwogopa Yehova sana.” Naam, Obadia alimwogopa Mungu sana! Woga huo unaofaa ulimwezesha Obadia kuwa hodari sana, kama ilivyoonekana baada tu ya Yezebeli kuwaua manabii wa Yehova.

      19. Obadia alifanya mambo gani yaliyoonyesha kwamba alikuwa hodari?

      19 Tunasoma hivi: “Ikawa kwamba Yezebeli alipowakatilia mbali manabii wa Yehova, Obadia aliwachukua manabii 100, akawaficha wakiwa vikundi viwili vya watu 50 pangoni, naye akawapa mkate na maji.” (1 Wafalme 18:4) Kama unavyoweza kuwazia, ilikuwa hatari sana kuwalisha kisiri wanaume 100. Mbali na kuepuka kutambuliwa na Ahabu na Yezebeli, Obadia alipaswa pia kuepuka kugunduliwa na wale manabii wa uwongo 850 ambao walitembelea jumba la mfalme kwa ukawaida. Isitoshe, wale waabudu wengine wengi wa uwongo katika Israeli, kuanzia watu wa hali ya chini hadi wakuu, wangetumia nafasi hiyo kumfichua Obadia ili kupata kibali cha mfalme na malkia. Hata hivyo, Obadia aliwahudumia manabii wa Yehova kwa uhodari bila kuogopa kuonwa na waabudu hao wa sanamu. Naam, kumwogopa Mungu kunaweza kumwimarisha mtu sana!

      20. Kumwogopa Mungu kulimsaidiaje Obadia, na mfano wake unakufaidije?

      20 Kwa kuwa Obadia alionyesha uhodari kwa kumwogopa Mungu, inaonekana Yehova alimlinda dhidi ya maadui wake. Andiko la Methali 29:25 linasema hivi: “Kutetemeshwa na wanadamu ndiko huleta mtego, lakini yeye anayemtegemea Yehova atalindwa.” Obadia alikuwa mwanadamu tu kama sisi; aliogopa kukamatwa na kuuawa. (1 Wafalme 18:7-9, 12) Lakini, kumwogopa Mungu kulimwezesha awe hodari na kushinda woga wowote ambao angekuwa nao kuelekea wanadamu. Obadia ni mfano bora kwetu sote, hasa kwa wale wanaohatarisha uhuru wao au maisha yao ili wamwabudu Yehova. (Mathayo 24:9) Naam, acheni sisi sote tujitahidi kumtumikia Yehova “kwa woga wa kimungu na heshima.”—Waebrania 12:28.

      21. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

      21 Uhodari haupatikani tu kwa kuwa na imani na kumwogopa Mungu; upendo unaweza kutuimarisha hata zaidi. Paulo aliandika hivi: “Mungu hakutupa sisi roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.” (2 Timotheo 1:7) Katika makala inayofuata, tutaona jinsi upendo unavyoweza kutusaidia kumtumikia Yehova kwa uhodari katika siku hizi za mwisho zenye hatari.—2 Timotheo 3:1.

      [Maelezo ya Chini]

      a Huyo si yule nabii Obadia.

  • Uhodari Waimarishwa kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Oktoba 1
    • Uhodari Waimarishwa kwa Upendo

      “Mungu hakutupa sisi roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.”—2 TIMOTHEO 1:7.

      1, 2. (a) Upendo unaweza kumchochea mtu kufanya nini? (b) Kwa nini uhodari wa Yesu ulikuwa wa pekee sana?

      MUME na mke waliooana karibuni walikuwa wakipiga mbizi karibu na mji fulani ulio kwenye pwani ya mashariki ya Australia. Walikuwa karibu kutoka majini wakati samaki mkubwa anayeitwa papa aliposonga haraka kumwelekea mke. Kwa ushujaa, mume huyo alimsukuma mke wake kando, naye akaacha samaki huyo amshambulie. Mwanamke huyo alisema hivi wakati wa mazishi ya mume wake: “Alitoa uhai wake kwa ajili yangu.”

      2 Naam, upendo unaweza kuwachochea wanadamu kuonyesha uhodari wa hali ya juu. Yesu Kristo mwenyewe alisema hivi: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Muda usiozidi saa 24 baada ya Yesu kusema maneno hayo, alitoa uhai wake, si kwa ajili ya mtu mmoja tu, bali kwa ajili ya wanadamu wote. (Mathayo 20:28) Isitoshe, Yesu hakutoa uhai wake kwa kushtukia. Alijua kimbele kwamba angedhihakiwa, angetendewa vibaya, angehukumiwa isivyo haki, na kuuawa kwenye mti wa mateso. Hata aliwatayarisha wanafunzi wake kwa ajili ya hilo, akisema: “Tazama, tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani, na waandishi, nao watamhukumia kifo na kumtia mikononi mwa watu wa mataifa, nao watamdhihaki, watamtemea mate, watampiga mijeledi na kumuua.”—Marko 10:33, 34.

      3. Ni nini kilichomwezesha Yesu kuwa hodari sana?

      3 Ni nini kilichomwezesha Yesu kuonyesha uhodari usio wa kawaida? Hasa ni kwa sababu ya imani na kumwogopa Mungu. (Waebrania 5:7; 12:2) Hata hivyo, zaidi ya yote, uhodari wa Yesu ulitokana na upendo wake kwa Mungu na kwa wanadamu wenzake. (1 Yohana 3:16) Tukisitawisha upendo kama huo pamoja na imani na kumwogopa Mungu, sisi pia tutakuwa hodari kama Kristo. (Waefeso 5:2) Tunaweza kusitawishaje upendo kama huo? Tunapaswa kutambua Chanzo cha upendo huo.

      “Upendo Unatoka kwa Mungu”

      4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova ndiye Chanzo cha upendo?

      4 Yehova ndiye mfano bora zaidi wa upendo na Chanzo cha sifa hiyo. Mtume Yohana aliandika hivi: “Wapendwa, acheni tuendelee kupendana, kwa sababu upendo unatoka kwa Mungu, na kila mtu ambaye hupenda amezaliwa kutokana na Mungu na hupata kumjua Mungu. Yeye ambaye hapendi hajamjua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:7, 8) Hivyo, mtu anaweza kusitawisha upendo kama wa Mungu ikiwa tu anamkaribia Yehova kupitia ujuzi sahihi na kutenda kulingana na ujuzi huo kwa kutii kutoka moyoni.—Wafilipi 1:9; Yakobo 4:8; 1 Yohana 5:3.

      5, 6. Ni nini kilichowasaidia wafuasi wa Yesu wa mapema kusitawisha upendo kama wa Kristo?

      5 Katika sala yake ya mwisho pamoja na mitume wake waaminifu 11, Yesu alionyesha uhusiano kati ya kumjua Mungu na kukua katika upendo aliposema hivi: “Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda nao upate kuwa ndani yao nami katika muungano pamoja nao.” (Yohana 17:26) Yesu aliwasaidia wanafunzi wake kusitawisha upendo kama ule uliokuwapo kati yake na Baba yake, akionyesha kwa maneno na kwa mfano kile ambacho jina la Mungu linawakilisha, yaani, sifa nzuri ajabu za Mungu. Hiyo ndiyo sababu Yesu alisema hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yohana 14:9, 10; 17:8.

      6 Upendo kama wa Kristo unatokana na roho takatifu ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Siku ya Pentekoste 33 W.K., wakati Wakristo wa mapema walipopokea roho takatifu iliyoahidiwa, hawakukumbuka tu mambo mengi ambayo Yesu aliwafundisha, bali pia walielewa zaidi maana ya Maandiko. Inaonekana kwamba ufahamu huo ulioongezeka uliimarisha upendo wao kwa Mungu. (Yohana 14:26; 15:26) Ikawaje? Hata uhai wao ulipokuwa hatarini, walihubiri habari njema kwa ujasiri na kwa bidii.—Matendo 5:28, 29.

      Kuonyesha Uhodari na Upendo

      7. Paulo na Barnaba walivumilia mambo gani katika safari yao ya umishonari?

      7 Mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu hakutupa sisi roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.” (2 Timotheo 1:7) Paulo alikuwa akisema mambo aliyojionea. Fikiria yale yaliyompata yeye na Barnaba walipokuwa katika safari yao ya umishonari. Walihubiri katika majiji mengi, kutia ndani Antiokia, Ikoniamu, na Listra. Katika kila jiji, watu fulani walipata kuwa waamini, lakini wengine walikuwa wapinzani wakali. (Matendo 13:2, 14, 45, 50; 14:1, 5) Huko Listra, watu wenye hasira hata walimpiga Paulo kwa mawe na kumwacha wakifikiri kwamba amekufa! “Hata hivyo, wanafunzi walipomzunguka, akasimama na kuingia ndani ya jiji. Na siku iliyofuata akaondoka pamoja na Barnaba kwenda Derbe.”—Matendo 14:6, 19, 20.

      8. Uhodari wa Paulo na Barnaba ulionyeshaje kwamba waliwapenda watu sana?

      8 Je, jaribio hilo la kumuua Paulo lilimwogopesha yeye na Barnaba kuacha kuhubiri? Hapana! Baada ya “kufanya wanafunzi wengi” huko Derbe, wanaume hao wawili “wakarudi Listra na Ikoniamu na Antiokia.” Kwa nini? Ili kuwatia moyo wapya wabaki wakiwa imara katika imani. Paulo na Barnaba walisema hivi: “Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.” Ni wazi kwamba walikuwa hodari kwa sababu walipenda sana “wana-kondoo” wa Kristo. (Matendo 14:21-23; Yohana 21:15-17) Baada ya kuwaweka rasmi wazee katika kila moja ya makutaniko mapya, ndugu hao wawili walitoa sala na “kuwakabidhi kwa Yehova ambaye walikuwa wamemwamini.”

      9. Upendo wa Paulo uliwachocheaje wazee wa Efeso?

      9 Paulo alikuwa mtu mwenye upendo na uhodari hivi kwamba Wakristo wengi wa mapema walimpenda sana. Kumbuka yaliyotukia kwenye mkutano ambao Paulo alifanya pamoja na wazee wa Efeso, ambako alikuwa amekaa kwa miaka mitatu na kukabili upinzani mwingi. (Matendo 20:17-31) Baada ya kuwatia moyo kulichunga kundi la Mungu walilokabidhiwa, Paulo alipiga magoti pamoja nao na kusali. Kisha, “wote wakalia sana, nao wakamwangukia Paulo shingoni na kumbusu kwa wororo, kwa sababu waliumizwa hasa na neno alilosema kwamba hawangemwona uso wake tena.” Ndugu hao walimpenda Paulo sana! Kwa kweli, wakati wa kuagana ulipofika, ilibidi Paulo na wale waliosafiri pamoja naye ‘wajiondoe kwao.’ Naam, wazee wa huko hawakutaka kuwaruhusu waondoke.—Matendo 20:36–21:1.

      10. Mashahidi wa Yehova leo wameonyeshaje kwa uhodari kwamba wanapendana?

      10 Leo, waangalizi wanaosafiri, wazee wa makutaniko, na wengine wengi wanapendwa sana kwa sababu ya uhodari wanaoonyesha wanaposhughulikia kondoo za Yehova. Kwa mfano, katika nchi zinazokumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe au katika maeneo ambako kazi ya kuhubiri imepigwa marufuku, waangalizi wanaosafiri na wake zao wamehatarisha maisha yao na uhuru wao ili kuyatembelea makutaniko. Vivyo hivyo, Mashahidi wengi wameteswa na watawala wakatili pamoja na wafuasi wao kwa sababu wamekataa kuwasaliti Mashahidi wenzao au kusema mahali wanapotoa chakula cha kiroho. Maelfu ya Mashahidi wengine wameteswa, wamenyanyaswa, na hata kuuawa kwa sababu wamekataa kuacha kuhubiri habari njema au kukutana na waamini wenzao kwenye mikutano ya Kikristo. (Matendo 5:28, 29; Waebrania 10:24, 25) Acheni tuige imani na upendo wa ndugu na dada hao hodari!—1 Wathesalonike 1:6.

      Usiache Upendo Wako Upoe

      11. Shetani hutumia njia gani kupigana vita vya kiroho dhidi ya watumishi wa Yehova, nao wanahitaji kufanya nini?

      11 Shetani alipotupwa duniani, aliazimia kuelekeza hasira yake kwa watumishi wa Yehova kwa sababu ‘wanashika amri za Mungu na wana kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.’ (Ufunuo 12:9, 17) Mojawapo ya mbinu za Ibilisi ni mateso. Hata hivyo, mara nyingi mbinu hiyo haifanikiwi kwa sababu inawafanya watu wa Mungu wawe na uhusiano wa karibu zaidi unaotegemea upendo wa Kikristo na inawachochea wengi wao kuwa na bidii zaidi. Mbinu nyingine ya Shetani ni kuchochea mielekeo ya wanadamu ya kutenda dhambi. Tunahitaji kuwa hodari kwa njia nyingine ili kushinda mbinu hiyo kwa sababu pambano letu ni la ndani, dhidi ya tamaa mbaya katika ‘moyo wetu wenye hila ambao ni hatari.’—Yeremia 17:9; Yakobo 1:14, 15.

      12. Shetani anatumiaje “roho ya ulimwengu” ili kujaribu kudhoofisha upendo wetu kwa Mungu?

      12 Shetani anatumia silaha nyingine yenye nguvu, yaani, “roho ya ulimwengu,” ambayo ni mwelekeo au uvutano wake wenye nguvu zaidi ambao unapinga moja kwa moja roho takatifu ya Mungu. (1 Wakorintho 2:12) Roho ya ulimwengu huchochea pupa na tamaa ya mali, naam, “tamaa ya macho.” (1 Yohana 2:16; 1 Timotheo 6:9, 10) Ingawa mali na pesa zenyewe haziwezi kutudhuru, tukizipenda badala ya kumpenda Mungu, basi Shetani atakuwa ameshinda. Nguvu au “mamlaka” ya roho ya ulimwengu, hutokana na jinsi inavyochochea mwili wenye dhambi, jinsi ilivyo yenye hila, jinsi inavyowachochea watu tena na tena, na jinsi inavyoenea sana kama hewa. Usiache roho ya ulimwengu iathiri moyo wako!—Waefeso 2:2, 3; Methali 4:23.

      13. Uhodari wetu wa kudumisha usafi wa kiadili unaweza kujaribiwaje?

      13 Hata hivyo, ili kupinga na kuchukia roho mbovu ya ulimwengu, tunahitaji kuwa hodari ili kudumisha usafi wa kiadili. Kwa mfano, uhodari unahitajiwa ili kuondoka kwenye jumba la sinema au kuzima kompyuta au televisheni wakati picha chafu zinapoonyeshwa. Tunahitaji kuwa hodari ili kukataa msongo wa marika na kuacha mashirika mabaya. Vivyo hivyo, tunahitaji kuwa hodari ili kufuata sheria na kanuni za Mungu licha ya kudhihakiwa na wanashule, wafanyakazi, majirani, au watu wa ukoo.—1 Wakorintho 15:33; 1 Yohana 5:19.

      14. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tumeathiriwa na roho ya ulimwengu?

      14 Basi, ni muhimu kama nini tuimarishe upendo wetu kwa Mungu na kwa ndugu na dada zetu wa kiroho! Chunguza miradi yako na maisha yako ili uone ikiwa roho ya ulimwengu imekuathiri kwa njia yoyote ile. Ikiwa imekuathiri, hata kwa kiasi kidogo, mwombe Yehova akupe uhodari ili uiondolee mbali kabisa na kutoiruhusu ikuathiri tena. Yehova hatapuuza maombi hayo ya unyoofu. (Zaburi 51:17) Isitoshe, roho yake ina nguvu zaidi kuliko roho ya ulimwengu.—1 Yohana 4:4.

      Kukabili Majaribu kwa Uhodari

      15, 16. Upendo kama wa Kristo unaweza kutusaidiaje kukabiliana na majaribu? Toa mfano.

      15 Matatizo mengine ambayo watumishi wa Yehova wanakabili yanatia ndani matokeo ya kutokamilika na uzee, ambayo mara nyingi husababisha magonjwa, ulemavu, kushuka moyo, na matatizo mengine mengi. (Waroma 8:22) Upendo kama wa Kristo unaweza kutusaidia kukabiliana na majaribu hayo. Fikiria mfano wa Namangolwa aliyelelewa katika familia ya Kikristo huko Zambia. Alipokuwa na umri wa miaka miwili, Namangolwa alilemaa. Anasema hivi: “Nilikuwa nikijifikiria sana, nikifikiri kwamba watu watashtuliwa na umbo langu. Lakini ndugu zangu wa kiroho walinisaidia kuona mambo kwa njia tofauti. Kwa hiyo, niliacha kujifikiria sana, na baada ya muda nikabatizwa.”

      16 Ingawa Namangolwa ana kiti cha magurudumu, mara nyingi yeye hulazimika kutembea kwa mikono na magoti anapokuwa kwenye barabara ya mchanga. Hata hivyo, yeye hufanya upainia msaidizi angalau miezi miwili kila mwaka. Mwenye nyumba mmoja alilia wakati Namangolwa alipomhubiria. Kwa nini? Kwa sababu alichochewa sana na imani na uhodari wa dada yetu. Yehova amembariki sana Namangolwa kwa kuwa watano kati ya wanafunzi wake wa Biblia wamebatizwa, na mmoja ni mzee wa kutaniko. Namangolwa anasema hivi: “Mara nyingi miguu yangu huniuma sana, lakini siachi jambo hilo linizuie.” Dada huyo ni mmoja wa Mashahidi wengi ulimwenguni walio dhaifu kimwili lakini wenye bidii nyingi kwa sababu wanampenda Mungu na jirani. Watu kama hao ni wenye kutamanika sana machoni pa Yehova!—Hagai 2:7.

      17, 18. Ni nini huwasaidia wengi kuvumilia magonjwa na majaribu mengine? Toa mifano ya kwenu.

      17 Ugonjwa wa kudumu unaweza pia kumfanya mtu avunjike moyo, na hata kushuka moyo. Mzee mmoja wa kutaniko anasema hivi: “Katika funzo la kitabu ninalohudhuria, dada mmoja ana ugonjwa wa sukari na ugonjwa wa figo, mwingine ana kansa, wengine wawili wana ugonjwa wa baridi yabisi, na mmoja ana ugonjwa fulani wa misuli na ugonjwa mwingine (unaoitwa lupus). Wakati mwingine wao huvunjika moyo. Hata hivyo, wao hukosa mikutano wakati tu wanapokuwa wagonjwa sana au wanapolazwa hospitalini. Wote huhubiri kwa ukawaida. Wao hunikumbusha Paulo, aliyesema hivi: ‘Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.’ Ninavutiwa na upendo wao na uhodari wao. Labda hali yao huwawezesha kuwa na maoni yanayofaa maishani na kutambua mambo yaliyo muhimu zaidi.” —2 Wakorintho 12:10.

      18 Ikiwa unapambana na ugonjwa au tatizo lingine ‘sali bila kuacha’ upate msaada ili usivunjike moyo. (1 Wathesalonike 5:14, 17) Bila shaka, huenda ukavunjika moyo mara kwa mara, lakini jitahidi kukazia fikira mambo yanayofaa, yaani, mambo ya kiroho, hasa tumaini letu la Ufalme lenye thamani. Dada mmoja alisema hivi: “Ninaona kuhubiri kuwa dawa.” Kuwahubiria wengine habari njema humsaidia kudumisha mtazamo unaofaa.

      Upendo Huwasaidia Wakosaji Kumrudia Yehova

      19, 20. (a) Ni nini kinachoweza kuwasaidia wale ambao wametenda dhambi kupata uhodari ili kumrudia Yehova? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

      19 Wengi ambao wamekuwa dhaifu kiroho au wametenda dhambi huona ni vigumu kumrudia Yehova. Lakini watapata uhodari unaohitajiwa ikiwa watatubu kikweli na kuanza tena kumpenda Mungu. Fikiria mfano wa Marioa ambaye anaishi Marekani. Mario aliacha kutaniko la Kikristo, akawa mlevi na akazoea kutumia dawa za kulevya, na baada ya miaka 20 akafungwa gerezani. Mario anasema hivi: “Nilianza kufikiri sana kuhusu wakati wangu ujao na kusoma Biblia tena. Baada ya muda, nilithamini sifa za Yehova, hasa rehema yake, ambayo nilimwomba mara nyingi. Baada ya kutoka gerezani, nilijiepusha na mashirika yangu ya zamani, nikahudhuria mikutano ya Kikristo, na mwishowe nikarudishwa. Ninavuna mwilini mwangu kile nilichopanda, lakini sasa angalau nina tumaini zuri ajabu. Ninamshukuru sana Yehova kwa huruma zake na msamaha wake.”—Zaburi 103:9-13; 130:3, 4; Wagalatia 6:7, 8.

      20 Bila shaka, wale wanaokabili hali kama za Mario wanapaswa kujitahidi sana ili wamrudie Yehova. Lakini upendo wao uliochochewa upya kwa sababu ya kujifunza Biblia, kusali, na kutafakari, utawapa uhodari na bidii. Pia, Mario aliimarishwa na tumaini la Ufalme. Naam, zaidi ya upendo, imani, na kumwogopa Mungu, tumaini pia linaweza kutuchochea kutenda mema maishani. Katika makala inayofuata, tutachunguza kwa undani zawadi hiyo ya kiroho yenye thamani.

      [Maelezo ya Chini]

      a Jina limebadilishwa.

  • Mtumaini Yehova na Uwe Hodari
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Oktoba 1
    • Mtumaini Yehova na Uwe Hodari

      “Mtumaini Yehova; uwe hodari na moyo wako uwe na nguvu. Naam, mtumaini Yehova.”—ZABURI 27:14.

      1. Tumaini ni muhimu kadiri gani, na neno hilo linatumiwaje katika Maandiko?

      TUMAINI la kweli ni kama mwangaza mwingi. Linatusaidia kuvumilia majaribu na kutazamia wakati ujao tukiwa na uhodari na shangwe. Ni Yehova peke yake anayeweza kutupa tumaini hakika, na anafanya hivyo kupitia Neno lake lililoongozwa kwa roho. (2 Timotheo 3:16) Neno “tumaini” linapatikana mara nyingi katika Biblia nalo linarejelea kutazamia jambo zuri kwa hamu na uhakika na vilevile kusudi la tazamio hilo.a Tumaini hilo si tamaa tu ambayo haina msingi wala uwezekano wa kutimizwa.

      2. Tumaini lilikuwa na umuhimu gani katika maisha ya Yesu?

      2 Yesu alipokabili majaribu na matatizo, alifikiria wakati ujao naye akamtumaini Yehova. “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake, yeye alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.” (Waebrania 12:2) Kwa kuwa alikazia fikira tazamio la kutetea enzi kuu ya Yehova na kulitakasa jina Lake, Yesu hakuacha kamwe kumtii Mungu licha ya mambo ambayo alikabili.

      3. Tumaini lina umuhimu gani katika maisha ya watumishi wa Mungu?

      3 Mfalme Daudi anataja uhusiano kati ya tumaini na uhodari, akisema: “Mtumaini Yehova; uwe hodari na moyo wako uwe na nguvu. Naam, mtumaini Yehova.” (Zaburi 27:14) Ikiwa tunataka moyo wetu uwe na nguvu, hatupaswi kamwe kuacha tumaini letu liwe hafifu bali tunapaswa kuendelea kulifanya liwe wazi akilini na kulithamini sana. Kufanya hivyo kutatusaidia kumwiga Yesu katika kuonyesha uhodari na bidii tunapofanya kazi ambayo aliwapa wanafunzi wake. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kwa kweli, tumaini linatajwa pamoja na imani na upendo likiwa sifa muhimu ya watumishi wa Mungu ambayo huwasaidia kuvumilia.—1 Wakorintho 13:13.

      Je, ‘Unazidi Katika Tumaini’?

      4. Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao wa “kondoo wengine” wanatazamia nini kwa hamu?

      4 Watu wa Mungu wana wakati ujao mzuri. Wakristo watiwa-mafuta wanangoja kwa hamu kutumikia pamoja na Kristo mbinguni, na “kondoo wengine” wanatumaini ‘kuwekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu’ wa kidunia. (Yohana 10:16; Waroma 8:19-21; Wafilipi 3:20) ‘Uhuru huo wenye utukufu’ unatia ndani kukombolewa kutoka katika dhambi na matokeo yake mabaya. Naam, Yehova ambaye ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu” atawapa washikamanifu wake zawadi bora zaidi.—Yakobo 1:17; Isaya 25:8.

      5. ‘Tunazidije katika tumaini’?

      5 Tumaini la Kikristo linapaswa kuwa muhimu kadiri gani maishani mwetu? Tunasoma hivi kwenye Waroma 15:13: “Mungu anayetoa tumaini na awajaze ninyi shangwe yote na amani kwa kuamini kwenu, ili mzidi katika tumaini kwa nguvu za roho takatifu.” Naam, tumaini haliwezi kulinganishwa na mshumaa ulio gizani, bali linaweza kulinganishwa na miale miangavu ya jua la asubuhi, likifanya maisha ya mtu kuwa na amani, furaha, kusudi, na uhodari. Ona kwamba ‘tunazidi katika tumaini’ tunapoamini Neno la Mungu lililoandikwa na kupokea roho yake takatifu. Andiko la Waroma 15:4 linasema hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” Basi jiulize hivi: ‘Je, mimi hudumisha tumaini langu kwa kujifunza Biblia kwa bidii, kwa kuisoma kila siku? Je, mimi husali mara nyingi ili kupata roho ya Mungu?’—Luka 11:13.

      6. Ili tudumishe tumaini letu, tunapaswa kujilinda dhidi ya nini?

      6 Yesu, Kielelezo chetu, aliimarishwa na Neno la Mungu. Tunapomfikiria sana, tunaepuka ‘kuchoka na kuzimia katika nafsi zetu.’ (Waebrania 12:3) Tumaini letu kutoka kwa Mungu likififia akilini na moyoni mwetu au tukikengeushwa, labda na vitu vya kimwili au miradi ya kilimwengu, huenda tukachoka kiroho, na hatimaye kukosa nguvu na uhodari wa kudumisha maadili. Tukiwa na mtazamo huo, hata ‘imani yetu inaweza kuvunjika.’ (1 Timotheo 1:19) Kwa upande mwingine, tumaini la kweli huimarisha imani yetu.

      Tumaini Ni Muhimu kwa Imani

      7. Ni kwa njia gani tumaini ni muhimu kwa imani?

      7 Biblia inasema hivi: “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Hivyo, tumaini si sifa inayoongeza tu imani; bali ni sehemu muhimu ya imani. Fikiria Abrahamu. Kwa maoni ya kibinadamu, yeye na mke wake Sara, walikuwa wamepita umri wa kupata watoto wakati Yehova alipowaahidi mrithi. (Mwanzo 17:15-17) Abrahamu alitendaje? “Ijapokuwa alikuwa amepita hali ya kuwa na tumaini, bado kwa kutegemea tumaini alikuwa na imani, ili awe baba ya mataifa mengi.” (Waroma 4:18) Naam, tumaini ambalo Abrahamu alipata kutoka kwa Mungu lilifanya imani yake ya kupata mzao iwe na msingi imara. Hivyo, imani yake iliimarisha tumaini lake na kulifanya liwe hakika. Abrahamu na Sara hata walikuwa na uhodari wa kuondoka nyumbani kwao na kuacha watu wao wa ukoo na kuishi miaka ya mwisho ya maisha yao katika mahema ugenini!

      8. Kuvumilia kwa uaminifu huimarishaje tumaini?

      8 Abrahamu alidumisha tumaini lake kwa kumtii Yehova kabisa hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. (Mwanzo 22:2, 12) Vivyo hivyo, kwa kutii na kuvumilia katika utumishi wa Yehova, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutapata thawabu yetu. Paulo aliandika kwamba matokeo ya “uvumilivu,” ni “hali yenye kukubaliwa,” ambayo hutokeza tumaini, “nalo tumaini halikatishi tamaa.” (Waroma 5:4, 5) Hiyo ndiyo sababu Paulo aliandika hivi pia: “Tunatamani kila mmoja wenu aonyeshe bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho.” (Waebrania 6:11) Mtazamo huo unaofaa ambao unategemea uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, unaweza kutusaidia kukabili tatizo lolote kwa uhodari, hata kwa shangwe.

      “Shangilieni Katika Tumaini”

      9. Tunapaswa kufanya nini kwa ukawaida ili ‘tushangilie katika tumaini’?

      9 Tumaini letu tulilopewa na Mungu ni muhimu zaidi kuliko chochote ambacho ulimwengu unaweza kutoa. Andiko la Zaburi 37:34 linasema hivi: “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake, naye atakuinua uimiliki dunia. Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.” Naam, tuna kila sababu ya ‘kushangilia katika tumaini.’ (Waroma 12:12) Hata hivyo, ili tufanye hivyo, ni lazima tuendelee kufikiria tumaini letu. Je, wewe hufikiria kwa ukawaida tumaini lako ulilopewa na Mungu? Je, unaweza kuwazia ukiwa katika Paradiso, ukiwa na afya nzuri, bila wasiwasi, ukizungukwa na wapendwa wako, na ukifanya kazi yenye kuridhisha? Je, wewe hutafakari kuhusu picha za Paradiso zinazoonyeshwa katika vichapo vyetu? Kutafakari hivyo kwa ukawaida ni kama kusafisha dirisha ili kuweza kuona mandhari yenye kupendeza. Tukipuuza kusafisha dirisha hilo, baada ya muda mfupi litapata uchafu ambao utatuzuia tusione waziwazi mandhari hiyo na kuvutiwa nayo. Kisha, tutavutiwa na mambo mengine. Tusiruhusu kamwe hilo litukie!

      10. Kwa nini kutazamia thawabu kunaonyesha kwamba tuna uhusiano mzuri pamoja na Yehova?

      10 Bila shaka, sababu yetu kuu ya kumtumikia Yehova ni kwamba tunampenda. (Marko 12:30) Hata hivyo, tunapaswa kutazamia kwa hamu thawabu. Kwa kweli, Yehova anatutazamia tufanye hivyo! Andiko la Waebrania 11:6 linasema hivi: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” Kwa nini Yehova anataka tumwone kuwa Mthawabishaji? Kwa sababu tunapofanya hivyo, tunaonyesha tunamjua vizuri Baba yetu wa mbinguni. Yeye ni mkarimu na anawapenda watoto wake. Fikiria jinsi ambavyo tungehuzunika na kuvunjika moyo kwa urahisi ikiwa hatungekuwa na “wakati ujao na tumaini.”—Yeremia 29:11.

      11. Tumaini ambalo Musa alipewa na Mungu lilimsaidiaje kufanya maamuzi kwa hekima?

      11 Musa ni kielelezo kizuri cha mtu ambaye alikazia fikira tumaini lake alilopewa na Mungu. Akiwa “mwana wa binti ya Farao” Musa angeweza kupata mamlaka, umashuhuri, na utajiri wa Misri. Je, angefuatilia mambo hayo au angemtumikia Yehova? Kwa uhodari, Musa aliamua kumtumikia Yehova. Kwa nini? Kwa sababu “alikaza macho kwenye malipo ya thawabu.” (Waebrania 11:24-26) Naam, Musa hakupuuza tumaini ambalo Yehova alikuwa ameweka mbele yake.

      12. Kwa nini tumaini la Kikristo ni kama kofia ya chuma?

      12 Mtume Paulo alilinganisha tumaini na kofia ya chuma. Kofia yetu ya chuma ya mfano hulinda nguvu zetu za kufikiri, linatuwezesha kufanya maamuzi kwa hekima, kutanguliza mambo yanayofaa, na kudumisha utimilifu. (1 Wathesalonike 5:8) Je, wewe huvaa kofia yako ya chuma ya mfano kila wakati? Ikiwa ndivyo, basi, kama Musa na Paulo, utaweka tumaini lako “si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie.” Ni kweli kwamba uhodari unahitajiwa ili kukataa kufuata mambo ya ubinafsi yanayopendwa sana, lakini kuna faida kubwa kufanya hivyo! Kwa nini ukubali kitu chochote chenye thamani ndogo kuliko “uzima ulio wa kweli,” ambao wale wanaomtumaini na kumpenda Yehova watapata?—1 Timotheo 6:17, 19.

      ‘Sitakuacha Hata Kidogo’

      13. Yehova anawapa watumishi wake washikamanifu uhakikisho gani?

      13 Watu wanaoweka tumaini lao katika mfumo wa mambo wa sasa hufikiria sana mambo mabaya ambayo wanakabili huku ulimwengu ukizidi kupatwa na “maumivu ya taabu.” (Mathayo 24:8) Lakini wale wanaomtumaini Yehova hawaogopeshwi na mambo hayo. Wataendelea ‘kukaa salama wala hawatasumbuliwa na hofu ya msiba.’ (Methali 1:33) Kwa sababu hawaweki tumaini lao katika mfumo huu wa mambo, wanatii kwa shangwe shauri hili la Paulo: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana yeye amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’”—Waebrania 13:5.

      14. Kwa nini Wakristo hawapaswi kuhangaikia sana mahitaji yao ya kimwili?

      14 Maneno hayo ya mkazo “hata kidogo” yanathibitisha kabisa kwamba Mungu atatutunza. Yesu pia alituhakikishia kwamba Mungu anatuhangaikia kwa upendo, aliposema: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote [vitu vya lazima maishani]. Kwa hiyo, msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.” (Mathayo 6:33, 34) Yehova anajua kwamba ni vigumu kwetu kuwa na bidii kwa ajili ya Ufalme wake na wakati huohuo kutimiza daraka la kujiandalia mahitaji ya kimwili. Basi, acheni tuwe na uhakika kabisa kwamba anaweza na anatamani kutosheleza mahitaji yetu.—Mathayo 6:25-32; 11:28-30.

      15. Wakristo hudumishaje ‘jicho rahisi’?

      15 Tunaonyesha kwamba tunamtegemea Yehova kwa kuwa na ‘jicho rahisi.’ (Mathayo 6:22, 23) Jicho rahisi ni nyoofu, lina nia nzuri, na halina pupa wala ubinafsi wa kutaka makuu. Kuwa na jicho rahisi hakumaanishi kuwa maskini au kupuuza madaraka yetu ya Kikristo. Badala yake, kunamaanisha kuwa na “utimamu wa akili” tunapoendelea kutanguliza utumishi wa Yehova.—2 Timotheo 1:7.

      16. Kwa nini tunahitaji imani na uhodari ili kuwa na jicho rahisi?

      16 Tunahitaji imani na uhodari ili kudumisha jicho rahisi. Kwa mfano, ikiwa mwajiri wako anasisitiza kwamba ufanye kazi kwa ukawaida wakati wa mikutano ya Kikristo, je, utatanguliza mambo ya kiroho kwa uhodari? Ikiwa mtu ana shaka kwamba Yehova atatimiza ahadi Yake ya kuwatunza watumishi Wake, basi Shetani akizidisha mkazo, mtu huyo anaweza kuacha kabisa kuhudhuria mikutano. Naam, tukikosa imani tunaweza kumruhusu Shetani atuongoze na kutuonyesha mambo ya kutanguliza badala ya kumwacha Yehova afanye hivyo. Huo utakuwa msiba ulioje!—2 Wakorintho 13:5.

      “Mtumaini Yehova”

      17. Wale wanaomtumaini Yehova wanabarikiwaje hata sasa?

      17 Maandiko yanaonyesha tena na tena kwamba wale wanamtumaini na kumtegemea Yehova hawashindwi kamwe. (Methali 3:5, 6; Yeremia 17:7) Ni kweli kwamba kuna wakati ambapo huenda wakahitaji kutosheka na vitu vichache, lakini wanaona hilo kuwa dhabihu ndogo ikilinganishwa na baraka zilizo mbele yao. Hivyo, wanaonyesha kwamba ‘wanamtumaini Yehova’ na wana uhakika kwamba mwishowe atatosheleza tamaa zote za uadilifu za moyo wa washikamanifu wake. (Zaburi 37:4, 34) Hivyo, wana furaha nyingi hata sasa. “Tarajio la waadilifu ni kushangilia, lakini tumaini lenyewe la waovu litapotea.”—Methali 10:28.

      18, 19. (a) Yehova anatupa uhakikisho gani wenye upendo? (b) Tunamwekaje Yehova kwenye ‘mkono wetu wa kuume’?

      18 Mvulana mdogo anapotembea huku akiwa ameshikwa mkono na baba yake, yeye huhisi kwamba yuko salama salimini. Sisi pia huhisi hivyo tunapotembea pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Yehova aliliambia hivi taifa la Israeli: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. . . . Nitakusaidia kwelikweli. . . . Kwa maana mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”—Isaya 41:10, 13.

      19 Maneno hayo yanaonyesha jambo lenye kuvutia, yaani, Yehova akiushika mkono wa mtu! Daudi aliandika hivi: “Nimemweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yuko upande wa mkono wangu wa kuume, sitatikiswa.” (Zaburi 16:8) Tunamwekaje Yehova kwenye ‘mkono wetu wa kuume’? Tunafanya hivyo angalau kwa njia mbili. Kwanza, tunaacha Neno lake lituongoze katika sehemu zote za maisha yetu; na pili, tunatazamia zawadi tukufu ambayo Yehova ameweka mbele yetu. Mtunga-zaburi Asafu aliimba hivi: “Niko pamoja nawe daima; umeushika mkono wangu wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanipeleka kwenye utukufu.” (Zaburi 73:23, 24) Tukiwa na uhakikisho huo, tunaweza kutazamia wakati ujao kwa uhakika.

      “Ukombozi Wenu Unakaribia”

      20, 21. Wale wanaomtumaini Yehova wanatazamia wakati ujao wa aina gani?

      20 Kila siku inapopita, inakuwa muhimu zaidi tumweke Yehova kwenye mkono wetu wa kuume. Hivi karibuni, kuanzia na kuharibiwa kwa dini ya uwongo, ulimwengu wa Shetani utapatwa na dhiki ambayo haijawahi kutukia kamwe. (Mathayo 24:21) Wanadamu wasio na imani wataogopa. Hata hivyo, wakati huo wenye msukosuko, watumishi wa Yehova wenye uhodari watashangilia katika tumaini lao! Yesu alisema hivi: “Mambo haya yanapoanza kutukia, simameni wima na kuinua vichwa vyenu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.”—Luka 21:28.

      21 Basi, acheni tushangilie katika tumaini ambalo tumepewa na Mungu na tusidanganywe wala kushawishiwa na hila za Shetani za kutukengeusha. Wakati huohuo, acheni tujitahidi kusitawisha imani, upendo, na kumwogopa Mungu. Tukifanya hivyo, tutakuwa na uhodari wa kumtii Yehova chini ya hali zote na kumpinga Ibilisi. (Yakobo 4:7, 8) Naam, “iweni hodari, nayo mioyo yenu na iwe na nguvu, ninyi nyote mnaomngojea Yehova.”—Zaburi 31:24.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ingawa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo neno “tumaini” linatumiwa mara nyingi kurejelea thawabu ambayo Wakristo watiwa-mafuta watapata mbinguni, katika makala hii, neno tumaini litazungumziwa katika maana ya ujumla.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki