-
Je, Sayansi Inapingana na Masimulizi ya Mwanzo?Amkeni!—2006 | Septemba
-
-
Maoni ya Biblia
Je, Sayansi Inapingana na Masimulizi ya Mwanzo?
WATU wengi hudai kwamba sayansi inapinga masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji. Lakini, sayansi haipingani na Biblia bali inapingana na maoni ya Wakristo wenye imani kali. Baadhi ya Wakristo hao husisitiza kwa uwongo kwamba, kulingana na Biblia, vitu vyote vinavyoonekana viliumbwa katika kipindi cha siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja, yapata miaka 10,000 hivi iliyopita.
Hata hivyo, Biblia haiungi mkono fundisho hilo. Iwapo ingefanya hivyo, uvumbuzi mwingi wa kisayansi, ambao umefanywa katika muda wa miaka mia moja iliyopita, ungefanya Biblia itiliwe shaka. Kuchunguza Biblia kwa makini kumethibitisha kwamba mambo hakika ya sayansi hayapingani na Biblia. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova hawakubaliani na “Wakristo” wenye imani kali wala wanauumbaji, yaani, watu wanaodai kwamba vitu vyote vinavyoonekana viliumbwa katika kipindi cha siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja, yapata miaka 10,000 hivi iliyopita. Habari ifuatayo inaonyesha kile ambacho Biblia inafundisha hasa.
“Mwanzo” Ulikuwa Lini?
Masimulizi ya Mwanzo yanaanza kwa taarifa hii fupi yenye nguvu: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Wasomi wa Biblia wanakubali kwamba taarifa hiyo inafafanua jambo tofauti na matukio yaliyotendeka katika zile siku sita za uumbaji. Matukio hayo yanasimuliwa kuanzia mstari wa 3 na kuendelea. Hilo ni jambo muhimu sana. Kulingana na taarifa ya ufunguzi ya Biblia, ulimwengu wote, kutia ndani Dunia, ulikuwapo kwa kipindi kisichojulikana kabla ya zile siku sita za uumbaji.
Wanajiolojia wanakadiria kwamba dunia imekuwapo kwa miaka bilioni 4, nao wanaanga wanasema huenda ulimwengu umekuwapo kwa miaka bilioni 15. Je, kauli hizo, au marekebisho yoyote ya ufahamu wetu kuhusu muda ambao ulimwengu, kutia ndani dunia, umekuwapo, zinapingana na Mwanzo 1:1? La. Biblia haisemi chochote kuhusu muda ambao “mbingu na dunia” zimekuwapo. Sayansi haipingi masimulizi ya Biblia.
Siku za Uumbaji Zilikuwa na Urefu Gani?
Vipi zile siku za uumbaji? Je, zilikuwa siku halisi zenye urefu wa saa 24 kila moja? Watu fulani hudai kwamba kwa kuwa Musa—aliyeandika kitabu cha Mwanzo—alirejelea siku iliyofuata siku sita za uumbaji kuwa mfano wa Sabato ya kila juma, lazima kila mojawapo ya siku hizo za uumbaji iwe ilikuwa na urefu wa saa 24. (Kutoka 20:11) Je, maneno ya Mwanzo yanaunga mkono kauli hiyo?
La hasha. Ukweli ni kwamba, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “siku” halimaanishi tu kipindi cha saa 24, bali pia linamaanisha vipindi vya wakati vyenye urefu tofauti. Kwa mfano, akieleza kwa ufupi kazi ya Mungu ya uumbaji, Musa anarejelea kipindi hicho cha siku sita kuwa siku moja tu. (Mwanzo 2:4) Bila shaka, hatuna msingi wowote wa Kimaandiko wa kukata kauli kwamba kila mojawapo ya siku za uumbaji ilikuwa na urefu wa saa 24.
Hivyo basi, siku hizo zilikuwa na urefu gani? Maneno ya Mwanzo sura ya 1 na ya 2 yanaonyesha zilikuwa vipindi virefu sana vya wakati.
-
-
Je, Sayansi Inapingana na Masimulizi ya Mwanzo?Amkeni!—2006 | Septemba
-
-
Kinyume na madai ya watu fulani, kitabu cha Mwanzo hakifundishi kwamba ulimwengu, kutia ndani dunia na viumbe hai vilivyomo, viliumbwa katika kipindi kifupi cha wakati, muda usio mrefu sana uliopita. Badala yake, masimulizi ya Mwanzo kuhusu kuumbwa kwa ulimwengu na vitu hai duniani yanapatana na uvumbuzi wa karibuni wa kisayansi.
-