-
Chukua Msimamo Upande wa Ibada ya KweliBiblia Inafundisha Nini Hasa?
-
-
11. Kwa nini watu fulani husherehekea sikukuu, hata hivyo, ni jambo gani lililo muhimu zaidi kwetu?
11 Watu fulani hukubali kwamba sikukuu kama vile Krismasi zilianzishwa na wapagani, hata hivyo, wanahisi kwamba si vibaya kuzisherehekea. Kwani, watu wengi wanaposherehekea sikukuu hizo hawafikirii ibada ya uwongo. Pia, pindi hizo huwezesha familia kuwa pamoja. Je, hivyo ndivyo unavyohisi? Ikiwa ndivyo, huenda sababu inayokufanya uone ugumu kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli ni upendo wako kwa familia wala si kwa dini ya uwongo. Uwe na hakika kwamba Yehova aliyeanzisha familia anataka uwe na uhusiano mzuri na watu wako wa ukoo. (Waefeso 3:14, 15) Hata hivyo, unaweza kuimarisha vifungo hivyo kwa njia ambayo Mungu anakubali. Mtume Paulo alisema hivi kuhusu jambo lililo muhimu zaidi maishani mwetu: “Endeleeni kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.”—Waefeso 5:10.
-
-
Chukua Msimamo Upande wa Ibada ya KweliBiblia Inafundisha Nini Hasa?
-
-
TUMIA UTAMBUZI UNAPOSHUGHULIKA NA WENGINE
13. Ni magumu gani yanayoweza kutokea usiposherehekea sikukuu?
13 Magumu yanaweza kutokea unapoamua kutosherehekea sikukuu. Kwa mfano, huenda wafanyakazi wenzako wakataka kujua ni kwa nini husherehekei sikukuu fulani zinazofanywa kazini. Vipi ukipewa zawadi ya Krismasi? Je, ni vibaya kuikubali? Vipi ikiwa mwenzi wako wa ndoa ana imani tofauti? Unaweza kuhakikishaje kwamba watoto wako hawahisi kwamba wamekosa kitu fulani kwa kutosherehekea sikukuu hizo?
14, 15. Unaweza kufanya nini ukipewa salamu ya sikukuu au ikiwa mtu anataka kukupa zawadi?
14 Unahitaji utambuzi ili kushughulikia kila hali inayotokea. Mtu akikupa salamu za sikukuu, unaweza tu kumshukuru kwa kukutakia heri. Lakini vipi ikiwa wewe humwona au kufanya kazi na mtu huyo kila siku. Basi, huenda ukaamua kumweleza mengi zaidi. Vyovyote vile, tumia busara. Biblia inashauri: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:6) Uwe mwangalifu usije ukawavunjia wengine heshima. Badala yake, waeleze msimamo wako kwa busara. Waeleze waziwazi kwamba hakuna ubaya wa kutoa au kupokea zawadi na kuwa na sherehe, hata hivyo ungependa kufanya mambo hayo wakati mwingine.
15 Vipi ikiwa mtu anataka kukupa zawadi? Inategemea hali mbalimbali. Huenda mwenye kukupa zawadi akasema: “Najua kwamba husherehekei sikukuu. Hata hivyo, ningependa kukupa zawadi hii.” Basi, huenda ukaamua kwamba kupokea zawadi hiyo si sawa na kushiriki katika sikukuu. Bila shaka, ikiwa mwenye kukupa zawadi hajui imani yako, unaweza kumtajia kwamba wewe husherehekei sikukuu hiyo. Hilo litamsaidia kuelewa ni kwa nini ingawa unakubali kupokea zawadi yake, hutampa zawadi yoyote. Kwa upande mwingine, huenda isifae kupokea zawadi ikiwa yule anayekupa zawadi hiyo anataka kuonyesha kwamba hushikamani na imani yako au kwamba unaweza kuvunja imani yako ili kupata vitu vya kimwili.
NAMNA GANI WASHIRIKI WA FAMILIA?
16. Unawezaje kutumia busara unaposhughulikia mambo yanayohusiana na sikukuu?
16 Namna gani ikiwa washiriki wa familia wana imani tofauti? Unapaswa kuwa na busara. Hakuna haja ya kubishania kila desturi au sherehe ambayo watu wako wa ukoo wanaamua kusherehekea. Badala yake, heshimu maoni yao, kama vile ungependa waheshimu maoni yako. (Mathayo 7:12) Epuka mambo yoyote ambayo yangefanya uonekane kwamba unasherehekea sikukuu. Lakini utumie busara katika mambo ambayo hayahusiani moja kwa moja na sherehe za sikukuu. Bila shaka, sikuzote unapaswa kutenda kwa njia itakayokuacha ukiwa na dhamiri njema.—1 Timotheo 1:18, 19.
17. Unawezaje kuwasaidia watoto wako wasihisi kwamba wanakosa kitu fulani wanapowaona wengine wakisherehekea sikukuu fulani?
17 Unaweza kufanya nini ili watoto wako wasihisi kwamba wamekosa kitu fulani kwa sababu ya kutosherehekea sikukuu isiyopatana na Maandiko? Inategemea sana mambo unayofanya nyakati nyingine. Wazazi fulani hutenga nyakati za kuwapa watoto wao zawadi. Mojawapo ya zawadi bora zaidi ambazo unaweza kuwapa watoto wako ni kuwa pamoja nao na kuwaonyesha upendo.
-