-
Kutumikia Kwa Shangwe Licha ya MagonjwaMnara wa Mlinzi—2006 | Juni 1
-
-
NILIZALIWA mnamo Oktoba 11, 1922, katika familia yenye watoto tisa, wavulana wanne na wasichana watano. Tuliishi katika kijiji cha Xylophagou, huko Saiprasi. Ingawa familia yetu ilikuwa na mali, bidii nyingi ilihitajiwa kufanya kazi shambani ili kutunza familia kubwa hivyo.
Baba yangu, Antonis, alipenda kusoma na alikuwa mdadisi. Muda mfupi baada ya mimi kuzaliwa, Baba alipokuwa akimtembelea mwalimu mmoja kijijini, aliona trakti Peoples Pulpit, iliyochapishwa na Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo). Alianza kuisoma, na baada ya muda, alipendezwa na ujumbe wake. Baba na Andreas Christou, mmoja wa rafiki zake, wakawa wa kwanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova katika kisiwa hicho.
Ongezeko Licha ya Upinzani
Baadaye, wote wawili walipata vitabu vingine vinavyofafanua Biblia kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Punde si punde, Baba na Andreas walichochewa kuwaambia wanakijiji wenzao kweli za Biblia walizokuwa wakijifunza. Kwa sababu ya kuhubiri, walipingwa vikali na makasisi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki na watu wengine waliofikiri kwamba Mashahidi wa Yehova ni hatari.
Wanakijiji wengi waliwaheshimu walimu hao wawili wa Biblia. Baba yangu alijulikana kuwa mwenye fadhili na mkarimu. Mara nyingi alisaidia familia maskini. Nyakati nyingine angeondoka nyumbani kisiri wakati wa usiku na kupeleka ngano au mkate milangoni mwa familia zenye uhitaji. Ujumbe wa wahudumu hao wawili uliwavutia watu kwa sababu ya mwenendo wao wa Kikristo usio na ubinafsi.—Mathayo 5:16.
Hivyo, karibu watu 12 walipendezwa na ujumbe wa Biblia. Walipoendelea kuelewa kweli, waliona uhitaji wa kukutana katika nyumba mbalimbali wakiwa kikundi ili kujifunza Biblia. Karibu mwaka wa 1934, Nikos Matheakis, mhudumu wa wakati wote kutoka Ugiriki alifika Saiprasi na akakutana na kikundi cha Xylophagou. Akiwa mwenye subira na bidii, Ndugu Matheakis alikipanga kikundi hicho na kukisaidia kuelewa Maandiko vizuri. Kikundi hicho ndicho kilichokuwa kutaniko la kwanza la Mashahidi wa Yehova huko Saiprasi.
Kazi ya Kikristo ilipoendelea na watu wengi kukubali kweli ya Biblia, akina ndugu waliona uhitaji wa kuwa na mahali pa kufanyia mikutano. Ndugu yangu mkubwa George, na mke wake, Eleni, walikubali chumba walichotumia kama ghala kitumiwe kwa ajili ya mikutano. Ghala hiyo iliyokuwa karibu na nyumba yao, ilifanyiwa marekebisho na kuwa mahali panapofaa kufanyia mikutano. Hivyo, akina ndugu wakawa na Jumba la Ufalme la kwanza kisiwani. Walifurahi kama nini! Nacho kilikuwa kichocheo kilichoje cha ongezeko zaidi!
-
-
Kutumikia Kwa Shangwe Licha ya MagonjwaMnara wa Mlinzi—2006 | Juni 1
-
-
[Picha katika ukurasa wa 17]
Jumba la Ufalme la kwanza huko Xylophagou linalotumiwa mpaka leo
-