Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Niko Tayari Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 1

      Je, Niko Tayari Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?

      “Kuna mkazo mwingi sana wa kuwa na mpenzi. Isitoshe kuna wavulana wengi sana wenye kuvutia.”—Whitney.

      “Wasichana fulani hawasiti kusema kwamba wangependa tuwe wapenzi, nami ningependa pia. Lakini nikiwauliza wazazi wangu, ninajua hawatakubali.”—Phillip.

      TAMAA ya kuwa pamoja na mtu fulani anayekuvutia, ambaye pia anavutiwa na wewe, inaweza kuwa na nguvu sana, nayo inaweza kuanza mapema sana maishani. Jenifer anakumbuka hivi: “Nilianza kupata mkazo wa kuwa na rafiki wa kiume nilipokuwa na umri wa miaka 11.” Brittany anasema: “Shuleni, usipokuwa na mpenzi, unaonwa kuwa hufai. Ni afadhali uwe na mpenzi yeyote yule, angalau uonekane kuwa una mpenzi!”

      Namna gani wewe? Je, uko tayari kuanzisha urafiki wa kimapenzi? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kwanza kufikiria swali moja la msingi:

      “Urafiki wa Kimapenzi” Ni Nini?

      Jibu maswali yanayofuata kwa kutia alama mahali panapofaa:

      Una kawaida ya kwenda matembezi pamoja na mtu wa jinsia tofauti. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?

      □ Ndiyo

      □ Hapana

      Unavutiwa na mtu wa jinsia tofauti ambaye anavutiwa nawe pia. Mara kadhaa kwa siku mnatumiana ujumbe mfupi kwenye simu au kupigiana simu. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?

      □ Ndiyo

      □ Hapana

      Kila mara mnapokuwa katika tafrija pamoja na marafiki, unatumia muda mwingi pamoja na mtu yuleyule wa jinsia tofauti. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?

      □ Ndiyo

      □ Hapana

      Labda haikuwa vigumu kwako kujibu swali la kwanza. Lakini huenda ulisita kidogo kabla ya kujibu swali la pili na la tatu. Urafiki wa kimapenzi ni nini hasa? Urafiki wa kimapenzi ni urafiki kati ya watu wawili wanaovutiana kimahaba na unatia ndani shughuli yoyote ya kirafiki ambayo wanafanya pamoja. Kwa hiyo, jibu la maswali yote matatu ni ndiyo. Iwe kwa simu, uso kwa uso, mbele ya watu, au mahali pasipo na watu, ikiwa wewe na rafiki yako wa jinsia tofauti mnaonyeshana mahaba na mnawasiliana kwa ukawaida, basi huo ni urafiki wa kimapenzi. Je, uko tayari kuanzisha urafiki wa aina hiyo? Kufikiria maswali matatu kutakusaidia kujua kama uko tayari.

      Kwa Nini Unataka Kuanzisha Urafiki wa Kimapenzi?

      Katika jamii nyingi, urafiki wa kimapenzi unaonwa kuwa njia inayofaa ya watu wawili kufahamiana vizuri. Hata hivyo, urafiki huo unapaswa kuwa na kusudi lenye kuheshimika, yaani, kumsaidia mwanamume na mwanamke kujua ikiwa wanaweza kufunga ndoa.

      Labda vijana wenzako hawauoni urafiki huo kuwa jambo zito. Pengine wanafurahia tu kuwa na rafiki wa pekee wa jinsia tofauti bila kusudi lolote la kufunga ndoa. Huenda hata wengine wao wanawaona rafiki hao kuwa “tuzo” au “pambo” ambalo linawafanya waheshimiwe. Hata hivyo, mara nyingi urafiki huo usio na msingi mzuri haudumu. Msichana mmoja anayeitwa Heather alisema hivi: “Vijana wengi ambao wanaanzisha urafiki wa kimapenzi, wanauvunja baada ya juma moja au mawili. Wanaanza kuwa na maoni ya kwamba urafiki kama huo ni wa muda tu, na maoni hayo yanawatayarisha kwa talaka badala ya ndoa.”

      Ni wazi kwamba unapoanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu fulani, hisia zake zinahusika. Kwa hiyo, hakikisha kwamba una nia nzuri. Hebu fikiria: Je, ungependa mtu fulani achezee hisia zako kama vile mtoto anavyocheza-cheza na kitu cha kuchezea kisha anakiacha? Msichana anayeitwa Chelsea anasema hivi: “Wakati mwingine ninaona kwamba urafiki wa kimapenzi unapaswa kuwa jambo la kujifurahisha tu, lakini haliwezi kuwa jambo la kujifurahisha tu ikiwa mtu mmoja anauchukulia urafiki huo kwa uzito naye yule mwingine anauona kuwa mchezo tu.”

      Ati Una Miaka Mingapi?

      Unafikiri kijana anapaswa kuanzisha urafiki wa kimapenzi akiwa na umri gani? ․․․․․

      Sasa muulize mmoja wa wazazi wako au wote wawili swali hilohilo kisha uandike jibu. ․․․․․

      Inawezekana kwamba namba ya kwanza uliyoandika ni ndogo kuliko ya pili. Au labda sivyo! Labda wewe ni mmoja kati ya vijana wengi ambao kwa busara wameahirisha kuanzisha urafiki wa kimapenzi mpaka watakapokuwa na umri wa kutosha kujielewa vizuri. Hivyo ndivyo Danielle, aliye na umri wa miaka 17, alivyoamua kufanya. Anasema hivi: “Miaka miwili iliyopita, sifa ambazo nilitaka rafiki yangu wa karibu awe nazo ni tofauti sana na zile ambazo ninapendezwa nazo sasa. Kwa kweli, hata sasa sina hakika kwamba ninaweza kufanya uamuzi mzito kama huo. Baada ya miaka kupita, nikiona kwamba utu wangu umekomaa, nitafikiria kuanzisha urafiki wa kimapenzi.”

      Kuna sababu nyingine nzuri ya kungoja. Biblia inatumia maneno “upeo wa ujana” kufafanua kipindi cha maisha ambapo tamaa za ngono na hisia za mahaba zinaanza kuwa zenye nguvu. (1 Wakorintho 7:36) Kuwa na urafiki wa karibu na mtu yuleyule wa jinsia tofauti ukiwa katika kipindi hicho kunaweza kuwasha tamaa hizo na kukufanya utumbukie katika mwenendo mbaya. Ni kweli kwamba huenda marafiki wako wasione hilo kuwa jambo zito. Wengi wao wanatamani sana kufanya ngono. Lakini unaweza kuwa tofauti na wao! (Waroma 12:2) Biblia inakuhimiza “uukimbie upotovu wa kingono.” (1 Wakorintho 6:18, New International Version) Ukingoja mpaka upite upeo wa ujana, unaweza ‘kuuondolea mbali msiba.’—Mhubiri 11:10.

      Je, Uko Tayari Kufunga Ndoa?

      Ili uweze kujibu swali hilo, jichunguze kwa makini. Fikiria mambo haya:

      Uhusiano wako na wengine. Wewe huwatendea wazazi wako na ndugu na dada zako jinsi gani? Je, mara nyingi unashindwa kujizuia unaposhughulika nao, labda kwa kutumia maneno makali au ya dhihaka unapotoa maoni? Wao wanaweza kusema nini kuhusu jambo hilo? Jinsi unavyoshughulika na watu wa familia yenu ndivyo utakavyomtendea mwenzi wako.—Soma Waefeso 4:31.

      Mtazamo. Je, wewe hutazamia mema au unaona mambo yote kuwa mabaya? Je, una usawaziko, au sikuzote unasisitiza mambo yafanywe kwa njia yako? Je, wewe huwa mtulivu chini ya mkazo? Je, una subira? Kukuza matunda ya roho ya Mungu sasa kutakusaidia ujitayarishe kuwa mume au mke.—Soma Wagalatia 5:22, 23.

      Matumizi ya Pesa. Je, unatumia pesa vizuri? Je, una madeni mengi? Je, wewe huachishwa kazi mara kwa mara? Ikiwa ndivyo, ni kwa nini? Je, ni kwa sababu ya kazi yenyewe au yule aliyekupa kazi? Au ni kwa sababu ya zoea au tabia fulani ambayo unapaswa kurekebisha? Ikiwa hutumii vizuri pesa zako mwenyewe, je, utaweza kutumia vizuri pesa za familia?—Soma 1 Timotheo 5:8.

      Hali ya Kiroho. Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, una sifa gani za kiroho? Je, una mpango wa kusoma Neno la Mungu, kuhubiri, na kushiriki katika mikutano ya Kikristo? Mtu ambaye utafunga ndoa pamoja naye anastahili kupata mwenzi aliye imara kiroho.—Soma Mhubiri 4:9, 10.

      Mambo Ambayo Unaweza Kufanya

      Kuwa chini ya mkazo wa kuanzisha urafiki wa kimapenzi kabla ya kuwa tayari ni kama kulazimishwa kufanya mtihani wa somo ambalo umeanza tu kujifunza. Bila shaka, utahisi kwamba umeonewa! Unahitaji wakati wa kujifunza somo hilo ili uwe na habari zitakazokuwezesha kupita mtihani huo.

      Ndivyo ilivyo pia kuhusiana na urafiki wa kimapenzi. Kama tulivyoona, urafiki wa kimapenzi si mchezo. Kwa hiyo, kabla ya kuwa tayari kumkazia fikira mtu mmoja hususa, unahitaji kujifunza “somo” muhimu sana—jinsi ya kujenga urafiki. Baadaye, utakapompata mtu anayekufaa, utakuwa tayari kujenga urafiki wenye kudumu. Kusema kweli, ndoa nzuri ni muungano wa marafiki wawili wakubwa.

      Kungoja muda upite kabla ya kuanzisha urafiki wa kimapenzi hakukunyimi uhuru. Badala yake, kunakupa uhuru zaidi wa ‘kushangilia katika ujana wako.’ (Mhubiri 11:9) Nawe utakuwa na wakati wa kujitayarisha kwa kuboresha utu wako, na zaidi ya yote, hali yako ya kiroho.—Maombolezo 3:27.

      Kwa sasa, unaweza kufurahia kushirikiana na watu wa jinsia tofauti. Jinsi gani? Njia bora ni kushirikiana nao mkiwa katika vikundi vyenye mchanganyiko wa wavulana na wasichana ambavyo vinasimamiwa vizuri. Msichana anayeitwa Tammy anasema: “Nafikiri inafurahisha zaidi mambo yanapofanywa kwa njia hiyo. Ni afadhali kuwa na marafiki wengi.” Monica anakubaliana naye. Anasema: “Kushirikiana katika vikundi ni wazo zuri, kwa sababu unaona watu wenye nyutu tofauti-tofauti.”

      Kwa upande mwingine, ukimkazia fikira mtu mmoja tu mapema sana maishani, huenda ukavunjwa moyo. Kwa hiyo, usiwe na haraka. Tumia wakati huu wa maisha yako kujifunza jinsi ya kusitawisha na kudumisha urafiki. Baadaye, ukichagua kuanzisha urafiki wa kimapenzi, utakuwa umejifahamu vizuri zaidi na kufahamu sifa ambazo ungependa mwenzi wa ndoa awe nazo.

      PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 29 NA 30

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Je, unataka kuanzisha urafiki wa kimapenzi bila wazazi wako kujua? Huenda usijue kwamba kuna hatari nyingi za kufanya hivyo.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

      PENDEKEZO

      Ili kujitayarisha kwa ajili ya urafiki wa kimapenzi na ndoa, soma 2 Petro 1:5-7 na uchague sifa moja ambayo unahitaji kufanyia kazi. Baada ya mwezi mmoja, jichunguze uone kadiri ambavyo umejifunza kuhusu sifa hiyo na kuiboresha.

      JE, WAJUA . . .

      Uchunguzi mbalimbali umeonyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa ndoa ya watu wenye umri wa chini ya miaka 20 kuvunjika kwa talaka kabla ya miaka mitano kuisha.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Ili kujitayarisha kwa ajili ya ndoa, ninahitaji kufanyia kazi sifa hizi: ․․․․․

      Ninaweza kufanyia kazi sifa hizo kwa ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Unaweza kuchangamana na watu wa jinsia tofauti katika hali gani zinazofaa?

      ● Unaweza kufanya nini ili kumsaidia ndugu au dada yako ambaye anataka kuanzisha urafiki wa kimapenzi akiwa na umri mdogo sana?

      ● Ukianzisha urafiki wa kimapenzi bila nia ya kufunga ndoa, unaweza kuathiri jinsi gani hisia za mwenzako?

      [Babu katika ukurasa wa 18]

      “Nafikiri unapaswa kuanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu ambaye kwa kweli unampenda na unaona kwamba uhusiano wenu unaweza kukua. Unamjali mtu mwenyewe bali si msisimuko tu wa kuwa na urafiki wa kimapenzi.’’—Amber

      [Picha katika ukurasa wa 16, 17]

      Ukianzisha urafiki wa kimapenzi bila nia ya kufunga ndoa, unatenda kama mtoto anayecheza-cheza na kitu cha kuchezea kisha anakiacha

  • Kuna Ubaya Gani Kuwa na Urafiki wa Kimapenzi wa Siri?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 2

      Kuna Ubaya Gani Kuwa na Urafiki wa Kimapenzi wa Siri?

      Jessica alijikuta mashakani. Kijana mmoja darasani anayeitwa Jeremy alianza kupendezwa naye. “Alikuwa na sura nzuri sana,” Jessica anasema, “na marafiki wangu walisema kwamba sitapata kamwe mvulana mwingine mzuri kama huyo. Wasichana wengi walikuwa wamejaribu kuanzisha urafiki naye, lakini hakupendezwa nao. Alipendezwa na mimi tu.”

      Muda si muda, Jeremy alimwomba Jessica wawe marafiki. Jessica alijibu kwamba kwa kuwa yeye ni Shahidi wa Yehova hangeruhusiwa kuanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu ambaye si wa dini yake. “Hata hivyo,” Jessica anasema, “Jeremy alikuwa na wazo lingine. Aliuliza, ‘Kwa nini tusiwe na urafiki bila wazazi wako kujua?’”

      IKIWA mtu fulani ambaye wewe unavutiwa naye angependekeza muwe na urafiki wa aina hiyo, ungefanya nini? Huenda ukashangaa kujua kwamba Jessica alikubali wazo la Jeremy. “Nilisadiki kwamba tukiwa marafiki, ninaweza kumsaidia ajifunze kumpenda Yehova,” Jessica anasema. Matokeo yalikuwa nini? Tutaona baadaye. Kwanza, acheni tuone jinsi ambavyo wengine wameingia katika mtego wa kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri.

      Kwa Nini Wanafanya Urafiki Wao Uwe Siri?

      Kwa nini wengine huanzisha urafiki wa siri? Kijana anayeitwa David anasema hivi waziwazi: “Wanajua kwamba wazazi wao hawatakubali, kwa hiyo hawawaambii.” Jane anaeleza sababu nyingine. Anasema: “Urafiki wa kimapenzi wa siri ni ishara ya uasi. Ukiona kwamba hutendewi kama mtu mzima, unaamua kufanya jambo lolote unalotaka bila kuwaambia wazazi wako.”

      Je, unaweza kufikiria sababu nyingine zinazowafanya wengine wawe na urafiki wa kimapenzi wa siri? Ikiwa unajua, ziorodheshe hapa chini.

      ․․․․․

      Bila shaka, unajua kwamba Biblia inakuagiza uwatii wazazi wako. (Waefeso 6:1) Na ikiwa wazazi wako wanaona kwamba hupaswi kuanzisha urafiki wa kimapenzi, bila shaka wana sababu nzuri. Hata hivyo, si ajabu ukiwa na maoni haya:

      ● Ninaona kwamba ninakosa kitu fulani kwa sababu kila mtu isipokuwa mimi ana mpenzi.

      ● Ninavutiwa na mtu ambaye si wa dini yangu.

      ● Ningependa kuwa na urafiki wa kimapenzi pamoja na Mkristo mwenzangu, hata ingawa sijafikia umri wa kufunga ndoa.

      Huenda unajua maoni ya wazazi wako kuhusu taarifa zilizo juu. Nawe unajua moyoni kwamba wazazi wako wana haki ya kuwa na maoni hayo. Hata hivyo, huenda ukawa na maoni kama ya msichana anayeitwa Manami, anayesema: “Mkazo wa kuwa na urafiki wa kimapenzi ni wenye nguvu sana hivi kwamba nyakati nyingine mimi huwa na mashaka kuhusu msimamo wangu. Kwa maoni ya vijana wa leo, kutokuwa na mpenzi ni jambo lisilowazika. Isitoshe, hakuna raha yoyote maishani ukiwa peke yako!” Wengine walio katika hali kama hiyo wameanzisha urafiki wa kimapenzi na kuwaficha wazazi wao. Jinsi gani?

      “Tuliambiwa Tusimwambie Yeyote”

      Ili kuendeleza urafiki wa kimapenzi wa siri, udanganyifu fulani unahusika. Wengine wanadumisha urafiki wao ukiwa siri kwa kuwasiliana hasa kupitia simu au Intaneti. Wakiwa mbele ya watu wanaonekana kuwa marafiki tu, lakini barua-pepe, ujumbe mfupi wa simu, na mazungumzo yao kwenye simu yanaonyesha hali tofauti kabisa.

      Njia nyingine ya ujanja ambayo vijana wanatumia ni kupanga tafrija huku wakiwa na lengo la kujitenga wakiwa wawili-wawili baadaye. James anasema hivi: “Siku moja tulialikwa mahali tukiwa kikundi, lakini baadaye tukagundua kwamba tafrija hiyo ilipangwa ili tu vijana fulani wawili waweze kuwa pamoja. Tuliambiwa tusimwambie yeyote.”

      Kama James alivyosema, kwa kawaida marafiki husaidia kuendeleza urafiki huo ukiwa siri. Carol anasema: “Angalau rafiki mmoja hujua kinachoendelea lakini anaamua kunyamaza kwa sababu aliahidi kutomwambia yeyote.” Nyakati nyingine udanganyifu ulio wazi unahusika. Beth, mwenye umri wa miaka 17, anasema: “Wengi huendeleza urafiki wao wa siri kwa kuwadanganya wazazi wao kuhusu mahali ambapo wanaenda.” Misaki, mwenye umri wa miaka 19, alifanya hivyo. Anasema: “Ilinibidi nitunge hadithi za uwongo kwa makini. Nilikuwa mwangalifu nisiseme uwongo kuhusu mambo mengine isipokuwa tu yale yanayohusiana na urafiki wangu wa siri ili wazazi wangu waendelee kuniamini.”

      Hatari za Urafiki wa Siri

      Ukishawishiwa kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri, au ikiwa tayari umeanzisha urafiki wa aina hiyo, inafaa ujiulize maswali mawili yafuatayo:

      Udanganyifu wangu utakuwa na matokeo gani? Je, unakusudia kufunga ndoa pamoja na mtu huyo hivi karibuni? Evan, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Mtu anayeanzisha urafiki wa kimapenzi bila kuwa na nia ya kufunga ndoa, ni kama mtu anayepeleka kitu fulani sokoni bila nia ya kukiuza.” Ni nini kinachoweza kutokea? Methali 13:12 inasema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” Je, kwa kweli ungependa kumfanya mtu unayemjali augue moyoni? Unapaswa kufikiria jambo hili pia: Kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri kunakunyima mashauri yenye upendo kutoka kwa wazazi wako na watu wazima wengine wanaokujali. Kwa sababu hiyo kuna uwezekano mkubwa wa kutumbukia katika upotovu wa kingono.—Wagalatia 6:7.

      Yehova Mungu ana maoni gani kuhusu yale ninayofanya? Biblia inasema: “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13) Kwa hiyo, ikiwa unaficha urafiki wako wa kimapenzi au wa rafiki yako, tayari Yehova anajua jambo hilo. Na ikiwa umedanganya, unapaswa kuhangaishwa na jambo hilo. Yehova Mungu anachukia sana udanganyifu. Kwa kweli, Biblia inataja waziwazi kwamba “ulimi wa uwongo” ni kati ya mambo ambayo anachukia!—Methali 6:16-19.

      Kufunua Siri

      Bila shaka ingekuwa vema uzungumze na wazazi wako au Mkristo mkomavu ikiwa una urafiki wowote wa siri. Na ikiwa una rafiki aliye na rafiki wa kimapenzi wa siri, usishiriki katika matendo yake kwa kumsaidia kuficha urafiki huo. (1 Timotheo 5:22) Ungehisi jinsi gani ikiwa urafiki huo ungesababisha madhara? Je, hungelaumika kwa kiasi fulani?

      Tuseme rafiki yako ambaye ana ugonjwa wa kisukari anakula keki kwa siri. Utafanya nini ukijua jambo hilo lakini rafiki yako anakusihi usimwambie mtu yeyote? Utachukua hatua gani—utaficha jambo hilo au utachukua hatua ambayo inaweza kuokoa uhai wake?

      Ndivyo ilivyo ikiwa unajua kwamba rafiki yako ana urafiki wa kimapenzi wa siri. Usiogope kwamba urafiki wenu utavunjika. Baada ya muda, rafiki wa kweli atatambua kwamba ulichukua hatua kwa sababu unamjali.—Zaburi 141:5.

      Ni Siri au Ni Faragha?

      Si siri zote zinazohusiana na urafiki wa kimapenzi zinazohusisha udanganyifu. Tuseme mwanamume kijana na mwanamke kijana wangependa kujuana vizuri zaidi lakini wanataka kufanya hivyo kwa siri kwa muda fulani. Labda kama kijana anayeitwa Thomas anavyosema, “hawataki kuulizwa-ulizwa maswali kama, ‘Mtafunga ndoa siku gani?’”

      Mikazo kutoka kwa wengine inaweza kuwa hatari. (Wimbo wa Sulemani 2:7) Hivyo, mwanzoni mwa uhusiano, huenda kwa busara watu fulani wakaamua kutowajulisha wengine kuhusu urafiki wao. (Methali 10:19) Anna, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Hilo linawawezesha watu hao wawili kuwa na wakati wa kuamua ikiwa wanataka kuendeleza urafiki huo. Baada ya kufanya uamuzi huo, ndipo wanaweza kuwajulisha wengine.”

      Wakati huohuo, haifai kuwaficha watu ambao wana haki ya kujua kuhusu urafiki huo, kama vile wazazi wako au wazazi wa rafiki yako. Ikiwa hutaki urafiki huo ujulikane, unapaswa kujiuliza ni kwa nini. Je, tayari umeona kwamba wazazi wako wana sababu ya kuukataa?

      “Nilijua Hatua Ambayo Ninapaswa Kuchukua”

      Jessica, aliyetajwa mwanzoni, alibadili maoni yake kuhusu kuwa na urafiki wa kimapenzi wa siri pamoja na Jeremy aliposikia kuhusu Mkristo mwingine ambaye alikuwa katika hali kama hiyo. “Baada ya kusikia jinsi Mkristo huyo alivyovunja urafiki huo,” Jessica anasema, “nilijua hatua ambayo ninapaswa kuchukua.” Je, ilikuwa rahisi kuvunja urafiki huo? Hapana! Jessica anasema: “Hakuna mvulana mwingine ambaye nimepata kumpenda kama nilivyompenda huyo. Nililia kila siku kwa majuma kadhaa.”

      Hata hivyo, Jessica alijua kwamba anampenda Yehova. Na ingawa alikuwa amekengeushwa, alitaka sana kufanya lililo sawa. Baadaye, uchungu wa kuuvunja urafiki huo ulipungua. Jessica anasema: “Sasa uhusiano wangu pamoja na Yehova umekuwa mzuri sana kuliko wakati mwingine wowote. Ninashukuru sana kwamba anatupa mwongozo tunaohitaji kwa wakati unaofaa!”

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Tuseme kwamba uko tayari kuanzisha urafiki wa kimapenzi na umempata mtu unayempenda. Unaweza kujua jinsi gani kwamba anakufaa?

      MAANDIKO MUHIMU

      “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.

      PENDEKEZO

      Si lazima utangazie ulimwengu mzima kuhusu urafiki wenu. Lakini waambie wale walio na haki ya kujua. Kwa kawaida watu hao wanatia ndani wazazi wako na wazazi wa rafiki yako.

      JE, WAJUA . . .?

      Ili uwe na urafiki wenye kudumu ni lazima uwe mwenye kutumainika. Wazazi wako hawatakutumaini ikiwa una urafiki wa kimapenzi wa siri, na kufanya hivyo kunadhoofisha msingi wa uhusiano wako pamoja na rafiki yako.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Ikiwa nina urafiki wa kimapenzi wa siri na Mkristo mwenzangu, nita ․․․․․

      Ikiwa rafiki yangu ana urafiki wa kimapenzi wa siri nita ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Fikiria tena mambo matatu ambayo yameandikwa kwa herufi nzito katika ukurasa wa 22. Ni jambo gani kati ya mambo hayo linalofafanua jinsi unavyohisi nyakati fulani?

      ● Unaweza kushughulikia jinsi gani jambo hilo bila kuanzisha urafiki wa kimapenzi wa siri?

      ● Ikiwa ungejua kwamba rafiki yako ana urafiki wa kimapenzi wa siri, ungeshughulikia jambo hilo jinsi gani, na kwa nini ungechagua kulishughulikia hivyo?

      [Blabu katika ukurasa wa 27]

      “Nilivunja urafiki wa kimapenzi wa siri. Kusema kweli, haikuwa rahisi kwenda shuleni na kumwona mvulana huyo kila siku. Hata hivyo, Yehova Mungu anaona kila kitu, lakini sisi hatuwezi. Tunahitaji tu kumtegemea Yehova.’’—Jessica

      [Picha katika ukurasa wa 25]

      Kuficha urafiki wa kimapenzi wa rafiki yako ni kama kujua kwamba rafiki yako mwenye ugonjwa wa kisukari anakula keki lakini husemi

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki