Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uwe Mwenye Hekima—mwogope Mungu!
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Agosti 1
    • Ili kutusaidia kuelewa maana kamili ya kumwogopa Mungu, acheni tuzungumzie maisha ya mtu mmoja kati ya hao, yaani, Mfalme Daudi wa Israeli la kale.

      5. Kazi ya uchungaji ilimsaidiaje Daudi kujifunza kumwogopa Yehova?

      5 Yehova alimkataa Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli, kwa sababu ya kuwaogopa watu na kwa sababu ya kutomwogopa Mungu. (1 Samweli 15:24-26) Kwa upande mwingine, maisha ya Daudi na uhusiano wake wa karibu pamoja na Yehova yalionyesha kwamba alimwogopa Mungu kikweli. Tangu alipokuwa mdogo, mara nyingi Daudi alienda nje kulisha kondoo za baba yake. (1 Samweli 16:11) Haikosi kwamba pindi ambazo Daudi alitumia kuchunga kondoo usiku huku kukiwa na nyota zilimsaidia kuelewa maana ya kumwogopa Yehova. Ingawa Daudi angeweza kuona sehemu ndogo tu ya mfumo wa nyota, alikata kauli inayofaa kwamba Mungu anastahili kuheshimiwa na kuabudiwa. Baadaye, aliandika hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini, na mwana wa mtu wa udongo hivi kwamba umtunze?”—Zaburi 8:3, 4.

      6. Daudi alihisije alipotambua ukuu wa Yehova?

      6 Daudi alistaajabu alipolinganisha udogo wake na ukuu wa mbingu zinazoonekana. Badala ya kumwogopesha, ujuzi huo ulimchochea kumsifu Yehova na kusema: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake.” (Zaburi 19:1) Kumstahi Mungu kwa njia hiyo kulimfanya Daudi amkaribie Yehova zaidi na kulimchochea atake kujifunza na kufuata njia Zake kamilifu. Hebu wazia jinsi Daudi alivyohisi alipomwimbia Yehova hivi: “Wewe ni mkuu na unafanya mambo ya ajabu; wewe ni Mungu, wewe peke yako. Unifundishe, Ee Yehova, juu ya njia yako. Nitatembea katika kweli yako. Unganisha moyo wangu ili kuliogopa jina lako.”—Zaburi 86:10, 11.

      7. Kumwogopa Mungu kulimsaidiaje Daudi kupigana na Goliathi?

      7 Wafilisti waliposhambulia nchi ya Israeli, shujaa wao Goliathi mwenye urefu wa futi tisa na nusu, aliwadhihaki Waisraeli. Ni kana kwamba alisema hivi: ‘Nipeni mwanamume wa kupigana naye! Akishinda, tutawatumikia.’ (1 Samweli 17:4-10) Sauli na jeshi lake lote waliogopa, lakini Daudi hakuogopa. Daudi alijua kwamba Yehova ndiye anayepaswa kuogopwa, bali si mwanadamu, hata awe na nguvu nyingi kadiri gani. Daudi alimwambia Goliathi hivi: “Mimi naja kwako nikiwa na jina la Yehova wa majeshi . . . . Na kutaniko hili lote watajua kwamba Yehova haokoi kwa upanga wala kwa mkuki, kwa sababu vita ni vya Yehova.” Kwa msaada wa Yehova, Daudi aliliua jitu hilo akitumia kombeo na jiwe moja tu.—1 Samweli 17:45-47.

      8. Tunajifunza nini kutokana na mifano inayotajwa katika Biblia kuhusu watu waliomwogopa Mungu?

      8 Kama Daudi, labda tunakabili vizuizi au maadui wenye kuogopesha. Tunaweza kufanya nini? Tunaweza kushughulikia hali hizo kama Daudi na waaminifu wengine wa kale, yaani, kwa kumwogopa Mungu. Kumwogopa Mungu kunaweza kutusaidia tusiwaogope wanadamu. Nehemia, mtumishi mwaminifu wa Mungu, aliwahimiza hivi Waisraeli wenzake ambao walikuwa wakikabili upinzani: “Msiogope kwa sababu yao. Mkumbukeni Yehova, Yeye ambaye ni mkuu na Mwenye kuogopesha.” (Nehemia 4:14) Daudi, Nehemia, na watumishi wengine waaminifu wa Mungu walifanikiwa kutimiza kazi walizopewa na Mungu kwa sababu Mungu aliwasaidia. Tukimwogopa Mungu, hata sisi tutafanikiwa.

      Kukabili Matatizo kwa Kumwogopa Mungu

      9. Daudi alionyesha kwamba anamwogopa Mungu akiwa chini ya hali gani?

      9 Baada ya Daudi kumuua Goliathi, Yehova alimpa ushindi mwingine mbalimbali. Hata hivyo, Sauli mwenye wivu alijaribu kumuua Daudi. Kwanza, alifanya hivyo bila kupangia, kisha, akatumia ujanja, na hatimaye, akatumia jeshi. Ingawa Yehova alikuwa amemhakikishia Daudi kwamba angekuwa mfalme, kwa miaka mingi Daudi alilazimika kukimbia, kupigana, na kungojea wakati wa Yehova wa kumtawaza kuwa mfalme. Licha ya majaribu yote hayo, Daudi alionyesha kwamba anamwogopa Mungu wa kweli.—1 Samweli 18:9, 11, 17; 24:2.

      10. Daudi alipokabili hatari, alionyeshaje kwamba anamwogopa Mungu?

      10 Wakati fulani, Daudi alikimbilia kwa Akishi, mfalme wa jiji la Gathi la Wafilisti, ambako Goliathi aliishi. (1 Samweli 21:10-15) Watumishi wa mfalme huyo walimshutumu Daudi kuwa adui wa taifa lao. Daudi alitendaje alipokabili hali hiyo hatari? Alisali kwa Yehova na kumweleza mambo waziwazi. (Zaburi 56:1-4, 11-13) Ingawa ilimbidi Daudi ajifanye kuwa mwenda-wazimu ili aponyoke, alitambua kwamba Yehova ndiye aliyemkomboa kwa kubariki jitihada zake. Kwa kumtegemea Yehova kwa moyo wote na kumwamini, Daudi alionyesha kwamba anamwogopa Mungu.—Zaburi 34:4-6, 9-11.

      11. Kama Daudi, tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamwogopa Mungu wakati tunapokabili jaribu?

      11 Kama Daudi, tunaweza kuonyesha kwamba tunamwogopa Mungu kwa kuamini ahadi yake ya kutusaidia kukabiliana na matatizo. Daudi alisema hivi: “Mkabidhi Yehova njia yako, na kumtegemea, naye mwenyewe atatenda.” (Zaburi 37:5) Hilo halimaanishi kwamba tumwachie Yehova matatizo yetu bila kujitahidi kuyatatua, huku tukitarajia kwamba atatusaidia. Daudi hakukaa kitako baada ya kumwomba Mungu msaada. Alitumia uwezo wa kimwili na wa kiakili ambao alipewa na Yehova ili kushughulikia tatizo lake. Hata hivyo, Daudi alijua kwamba wanadamu hawawezi kufanikiwa wanapotegemea jitihada zao tu. Sisi pia tunapaswa kufanya hivyo. Baada ya kujitahidi tuwezavyo, tunapaswa kumwachia Yehova matatizo yetu. Naam, mara nyingi hatuwezi kufanya lolote ila kumtegemea Yehova. Huo ndio wakati wa kuonyesha kwamba tunamwogopa Mungu. Tunaweza kufarijiwa na maneno haya ya Daudi aliyoyasema kutoka moyoni: “Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wanaomwogopa.”—Zaburi 25:14.

      12. Kwa nini tunapaswa kuchukua kwa uzito sala zetu, nasi hatupaswi kamwe kuwa na mtazamo gani?

      12 Basi, tunapaswa kuchukua kwa uzito sala zetu na uhusiano wetu pamoja na Mungu. Tunaposali kwa Yehova, lazima ‘tuamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.’ (Waebrania 11:6; Yakobo 1:5-8) Na anapotusaidia, tunapaswa ‘kujionyesha kuwa wenye shukrani,’ kama mtume Paulo alivyotushauri. (Wakolosai 3:15, 17) Hatupaswi kamwe kuwa kama watu ambao walitajwa na Mkristo mmoja mtiwa-mafuta mwenye uzoefu mwingi: “Watu fulani wanadhani kwamba Mungu ni kama mhudumu wa hoteli. Wanapohitaji kitu, wanatoa ishara fulani ya kumwita. Na wakiisha kupata kile wanachohitaji, wanataka aondoke.” Huo si mtazamo wa kumwogopa Mungu.

      Wakati Ambapo Daudi Hakumwogopa Mungu

      13. Ni wakati gani ambapo Daudi hakuiheshimu Sheria ya Mungu?

      13 Daudi alipoona Yehova akimsaidia wakati wa taabu, hilo lilimfanya amwogope Yehova zaidi na kumwamini zaidi. (Zaburi 31:22-24) Hata hivyo, katika visa vitatu vya pekee, Daudi hakumwogopa Mungu, na hilo lilisababisha msiba. Kisa cha kwanza ni wakati ambapo alipanga sanduku la agano la Yehova lisafirishwe kwa gari la kukokotwa hadi Yerusalemu badala ya kuwatumia Walawi kulibeba juu ya mabega yao, kama Sheria ya Mungu ilivyoagiza. Uza ndiye aliyeliendesha gari hilo. Wakati alipolishika Sanduku ili kuzuia lisianguke, alikufa papo hapo kwa sababu ya “tendo [hilo] lisilo la heshima kwa Mungu.” Naam, Uza alitenda dhambi nzito, lakini msiba huo ulitukia hasa kwa sababu Daudi hakuiheshimu Sheria ya Mungu. Kumwogopa Mungu kunamaanisha kufanya mambo kwa njia yake.—2 Samweli 6:2-9; Hesabu 4:15; 7:9.

      14. Matokeo yalikuwa nini baada ya Daudi kuhesabu Israeli?

      14 Baadaye, Daudi alichochewa na Shetani kuhesabu idadi ya wanaume wa vita wa Israeli. (1 Mambo ya Nyakati 21:1) Kwa kufanya hivyo, Daudi alionyesha kwamba hakumwogopa Mungu wakati huo, na hilo likasababisha kifo cha Waisraeli 70,000. Ingawa Daudi alitubu mbele za Yehova, yeye na watu wake waliteseka sana.—2 Samweli 24:1-16.

      15. Ni jambo gani lililomfanya Daudi atumbukie katika dhambi ya uzinzi?

      15 Tena, kwa sababu ya kutomwogopa Mungu kwa muda fulani, Daudi alifanya uzinzi pamoja na Bath-sheba, mke wa Uria. Daudi alijua kwamba ni kosa kufanya uzinzi au hata kumtamani mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine. (Kutoka 20:14, 17) Tatizo lilianza wakati Daudi alipomwona Bath-sheba akioga. Kumwogopa Mungu kikweli kungemchochea Daudi aache papo hapo kumtazama Bath-sheba na badala yake afikirie mambo mengine. Lakini, inaonekana Daudi ‘aliendelea kumtazama’ Bath-sheba mpaka tamaa yake ikamfanya asimwogope Mungu. (Mathayo 5:28; 2 Samweli 11:1-4) Daudi alisahau kwamba Yehova ndiye aliyekuwa akiongoza maisha yake yote.—Zaburi 139:1-7.

      16. Daudi alipatwa na nini kwa sababu ya dhambi yake?

      16 Daudi na Bath-sheba walipata mwana kupitia uhusiano wao haramu. Muda mfupi baadaye, Yehova alimtuma nabii wake Nathani ili afunue dhambi ya Daudi. Aliporudia fahamu zake, Daudi alianza tena kumwogopa Mungu, naye akatubu. Alimsihi Yehova asimtupilie mbali wala asimnyang’anye roho Yake takatifu. (Zaburi 51:7, 11) Yehova alimsamehe Daudi na kupunguza adhabu ambayo angepata, lakini Hakumkinga kutokana na matokeo yote mabaya ya matendo yake. Mwana wa Daudi alikufa, na kuanzia wakati huo familia yake ikapatwa na huzuni na misiba. Hayo ni matokeo mabaya kama nini ya kutomwogopa Mungu kwa muda fulani!—2 Samweli 12:10-14; 13:10-14; 15:14.

  • Mwogope Yehova, Uwe Mwenye Furaha!
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Agosti 1
    • Kupata Furaha Tena

      3. Ni jambo gani lililomsaidia Daudi kurudia hali nzuri baada ya kutenda dhambi?

      3 Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, katika visa vitatu muhimu, Daudi alikosa kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa, naye akatenda dhambi. Hata hivyo, jinsi alivyotenda alipoadhibiwa na Yehova kulionyesha kwamba licha ya dhambi alizofanya, alikuwa mtu anayemwogopa Mungu. Kwa sababu alimstahi na kumheshimu Mungu alichochewa kukubali kwamba ana hatia, akajirekebisha, na kuwa tena na uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Ingawa Daudi na watu wengine waliumia kwa sababu ya makosa yake, Yehova aliendelea kumtegemeza na kumbariki kwa sababu alitubu kikweli. Bila shaka, mfano wa Daudi unaweza kuwaimarisha Wakristo ambao wanatumbukia katika dhambi nzito leo.

  • Mwogope Yehova, Uwe Mwenye Furaha!
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Agosti 1
    • Ni Afadhali Kuteseka Kuliko Kutenda Dhambi

      5, 6. Eleza jinsi Daudi alivyoepuka mara mbili kumuua Sauli na kwa nini alifanya hivyo.

      5 Bila shaka, ni afadhali kuepuka kutenda dhambi kwa sababu ya kumwogopa Mungu. Daudi alifanya hivyo pia. Pindi moja, Sauli na wanajeshi elfu tatu walikuwa wakimfuata Daudi. Sauli aliingia ndani ya pango ambamo Daudi na watu wake walikuwa wamejificha. Watu wa Daudi walimhimiza amuue Sauli. Kwa maoni yao, Yehova alikuwa amemtia Sauli, adui yake mkubwa, mikononi mwake! Daudi alimnyemelea Sauli kimyakimya na kukata upindo wa vazi lake. Kwa kuwa Daudi alimwogopa Mungu, hata tendo hilo lililoonekana kuwa lisilodhuru lilichoma dhamiri yake. Daudi aliwatawanya watu wake wenye hasira, akisema hivi: “Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba nimfanyie bwana wangu jambo hili, mtiwa-mafuta wa Yehova.”b—1 Samweli 24:1-7.

      6 Katika pindi nyingine baadaye, Sauli alipiga kambi usiku. Yeye na watu wake ‘wakashikwa na usingizi mzito kutoka kwa Yehova.’ Daudi pamoja na mpwa wake mwenye ujasiri aliyeitwa Abishai walinyemelea mpaka katikati kabisa ya kambi na kusimama mahali ambapo Sauli alikuwa amelala. Abishai alitaka kumkatilia mbali Sauli. Lakini Daudi akamzuia Abishai, kwa kuuliza hivi: “Ni nani amepata kunyoosha mkono wake juu ya mtiwa-mafuta wa Yehova, naye akabaki bila hatia?”—1 Samweli 26:9, 12.

      7. Ni jambo gani lililomzuia Daudi asitende dhambi?

      7 Kwa nini Daudi hakutumia nafasi hizo mbili kumuua Sauli? Kwa sababu alimwogopa Yehova kuliko Sauli. Kwa sababu ya kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa, Daudi alikuwa tayari kuteseka badala ya kutenda dhambi. (Waebrania 11:25) Aliamini kabisa kwamba Yehova huwatunza watu Wake na kwamba atamtunza. Daudi alijua kwamba angepata furaha na baraka nyingi kwa kumtii na kumtegemea Mungu, na kwamba ikiwa angempuuza Mungu basi angekosa kibali chake. (Zaburi 65:4) Pia, Daudi alijua kwamba Mungu angetimiza ahadi Yake ya kumfanya awe mfalme na kwamba angemwondoa Sauli asiwe mfalme kwa wakati wake na kwa njia yake.—1 Samweli 26:10.

  • Mwogope Yehova, Uwe Mwenye Furaha!
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Agosti 1
    • ‘Jitie Nguvu kwa Yehova’

      12. Daudi aliimarishwaje kwa kumwogopa Mungu?

      12 Kumwogopa Yehova hakukumzuia tu Daudi asitende dhambi. Kulimwimarisha achukue hatua na kutenda kwa hekima katika hali ngumu. Kwa muda wa mwaka mmoja na miezi minne, Daudi na watu wake walikimbilia Siklagi, katika maeneo ya mashambani ya Ufilisti, ili kumwepuka Sauli. (1 Samweli 27:5-7) Wakati mmoja ambapo wanaume hao walikuwa wameondoka, Waamaleki walishambulia na kuliteketeza jiji na kuchukua wake wote wa wanaume hao, watoto, na mifugo yao yote. Daudi na watu wake waliporudi na kuona kile kilichotukia, walilia sana. Kwa ghafula, huzuni yao ikageuka kuwa hasira, na watu wa Daudi wakataka kumpiga Daudi kwa mawe. Ingawa Daudi alitaabishwa na jambo hilo, hakuvunjika moyo. (Methali 24:10) Alimtegemea Yehova kwa sababu alimwogopa, naye “akajitia nguvu kwa Yehova.” Kwa msaada wa Mungu, Daudi na watu wake waliwafuata Waamaleki na kukomboa vitu vyote vilivyoporwa.—1 Samweli 30:1-20.

  • Mwogope Yehova, Uwe Mwenye Furaha!
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Agosti 1
    • Urithi Wenye Thamani

      15. Daudi alitaka kuwapa watoto wake nini, naye alifanyaje hivyo?

      15 Daudi aliandika hivi: “Njooni, enyi wana, nisikilizeni; nitawafundisha kumwogopa Yehova.” (Zaburi 34:11) Akiwa baba, Daudi alikusudia kuwapa watoto wake urithi wenye thamani, yaani, kumwogopa Yehova kikweli kwa njia inayofaa. Kwa maneno na kwa matendo, Daudi alionyesha kwamba Yehova si Mungu anayedai mengi mno, anayeogopesha, na aliye tayari kuwaadhibu wale wanaovunja sheria Zake, bali ni Baba mwenye upendo, anayejali, na anayewasamehe watoto Wake walio duniani. Daudi aliuliza hivi: “Makosa—ni nani anayeweza kuyatambua?” Kisha, akionyesha uhakika wake kwamba Yehova hachunguzi makosa yetu kila wakati, aliongeza hivi: “Unitangaze kuwa sina hatia ya dhambi zilizofichwa.” Daudi alikuwa na uhakika kwamba ikiwa angejitahidi awezavyo, basi maneno na mawazo yake yangempendeza Yehova.—Zaburi 19:12, 14.

  • Mwogope Yehova, Uwe Mwenye Furaha!
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Agosti 1
    • 18. Tutapata nini tukimwogopa Mungu wa kweli?

      18 Tunasoma hivi katika “maneno ya mwisho ya Daudi”: “Wakati yeye anayetawala juu ya wanadamu ni mwadilifu, akitawala kwa kumwogopa Mungu, basi ni kama nuru ya asubuhi, jua linapoangaza.” (2 Samweli 23:1, 3, 4) Inaonekana Sulemani, ambaye alikuwa mwana wa Daudi na mtawala aliyemfuata, alielewa maana ya maneno hayo kwa kuwa alimwomba Yehova ampe “moyo mtiifu” na uwezo wa ‘kutambua kati ya mema na mabaya.’ (1 Wafalme 3:9) Sulemani alitambua kwamba kumwogopa Yehova ni jambo la hekima na la kufurahisha. Baadaye, Sulemani alitoa muhtasari wa kitabu cha Mhubiri kwa maneno haya: “Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu. Kwa maana Mungu wa kweli ataleta kila kazi katika hukumu, kuhusiana na kila jambo lililofichwa, liwe jema au baya.” (Mhubiri 12:13, 14) Tukitii shauri hilo, tutajionea kwamba “matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova” si hekima na furaha tu, bali pia ni “utajiri na utukufu na uzima.”—Methali 22:4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki