-
Kumtegemea Yehova Kikamili Kunatuchochea Kuwa na UhakikaMnara wa Mlinzi—2011 | Mei 15
-
-
1, 2. (a) Daudi alipatwa na hali gani iliyokuwa hatari sana? (b) Tutazungumzia zaburi gani?
MFALME DAUDI amekuwa akitawala Israeli kwa muda fulani, lakini sasa anapatwa na hali hatari sana. Absalomu, mwana wake mwenye hila amejitangaza kuwa mfalme, na Daudi amelazimika kuondoka Yerusalemu. Amesalitiwa pia na rafiki wa karibu sana, na sasa, akiwa pamoja na watu wachache washikamanifu, anatembea akilia na akiwa miguu wazi kwenye Mlima wa Mizeituni. Zaidi ya hayo, Shimei, ambaye ni mtu wa familia ya Mfalme Sauli, anamtupia Daudi mawe na mavumbi huku akimlaani.—2 Sam. 15:30, 31; 16:5-14.
2 Je, hali hiyo itamwingiza Daudi ndani ya Sheoli au kaburi akiwa na huzuni na aibu? Hapana, kwa sababu anamtegemea Yehova. Hilo linaonekana wazi katika Zaburi ya 3, ambayo ilitungwa na Daudi akieleza jinsi alivyokimbia.
-
-
Kumtegemea Yehova Kikamili Kunatuchochea Kuwa na UhakikaMnara wa Mlinzi—2011 | Mei 15
-
-
Wakati ‘Wengi Wanapoinuka Juu Yetu’
3. Kama inavyoonyeshwa katika Zaburi 3:1, 2, Daudi alikuwa katika hali gani?
3 Mjumbe mmoja anasema hivi: “Moyo wa watu wa Israeli umekuwa nyuma ya Absalomu.” (2 Sam. 15:13) Akishangaa Absalomu amefanikiwa jinsi gani kupata wafuasi wengi hivyo, Daudi anauliza: “Ee Yehova, kwa nini adui zangu wamekuwa wengi? Kwa nini wengi wanainuka dhidi yangu? Wengi wanasema juu ya nafsi yangu: ‘Hakuna wokovu kwa ajili yake kutoka kwa Mungu.’” (Zab. 3:1, 2) Waisraeli wengi wanafikiri kwamba Yehova hatamkomboa Daudi kutoka katika msiba ambao umesababishwa na Absalomu na wafuasi wake.
4, 5. (a) Daudi alikuwa na uhakika gani? (b) Maneno “Mwenye kuinua kichwa changu” yanamaanisha nini?
4 Lakini Daudi ana uhakika kwa sababu anamtegemea Mungu kabisa. Anaimba hivi: “Na bado wewe, Ee Yehova, ni ngao inayonizunguka, utukufu wangu na Mwenye kuinua kichwa changu.” (Zab. 3:3) Daudi ana uhakika kwamba Yehova atamlinda kama vile ngao inavyomlinda askari-jeshi. Ndiyo, mfalme huyo anayeendelea kuzeeka anakimbia, kichwa chake kikiwa kimefunikwa na kuinama chini kwa sababu ya aibu. Lakini Aliye Juu Zaidi atabadili hali ya Daudi na kumtukuza. Yehova atamsaidia kusimama wima, kuinua kichwa chake na kukiinua juu zaidi kwa mara nyingine tena. Daudi anaita akiwa na uhakika kwamba Mungu atamjibu. Je, unaonyesha kwamba unamtegemea Yehova kwa njia hiyo?
5 Daudi anaposema “Mwenye kuinua kichwa changu,” anaonyesha kwamba Yehova ndiye atakayempa msaada anaohitaji. Biblia Habari Njema inasema hivi: “Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu u ngao yangu kila upande; kwako napata fahari na ushindi wangu.” Kuhusu usemi “Mwenye kuinua kichwa changu,” kitabu kimoja cha marejeo kinasema hivi: “Mungu anapoinua . . . ‘kichwa’ cha mtu, Anamjaza mtu huyo tumaini na uhakika.” Akiwa amelazimishwa kuacha kiti cha ufalme cha Israeli, Daudi ana sababu ya kuvunjika moyo. Hata hivyo, ‘kuinuliwa kwa kichwa chake’ kutampa tena ujasiri, uhakika, na ataweza kumtegemea Mungu kikamili.
‘Yehova Atajibu!’
6. Kwa nini Daudi alisema kwamba sala zake zingejibiwa kutoka katika mlima mtakatifu wa Yehova?
6 Akimtegemea Yehova na akiwa na uhakika kabisa, Daudi anaendelea kusema: “Kwa sauti yangu nitamwita Yehova, naye atanijibu kutoka katika mlima wake mtakatifu.” (Zab. 3:4) Kulingana na maagizo ya Daudi, sanduku la agano, ambalo linafananisha kuwapo kwa Mungu, limepelekwa kwenye Mlima Sayuni. (Soma 2 Samweli 15:23-25.) Basi, kwa kufaa Daudi anasema kwamba sala zake zitajibiwa kutoka katika mlima mtakatifu wa Yehova.
7. Kwa nini Daudi hakuogopa hata kidogo?
7 Akiwa na uhakika kwamba sala yake kwa Mungu si ya bure, Daudi haogopi hata kidogo. Badala yake, anaimba hivi: “Nami nitajilaza nipate kulala usingizi; hakika nitaamka, kwa maana Yehova anaendelea kunitegemeza.” (Zab. 3:5) Hata usiku, wakati ambapo kuna hatari zaidi ya kushambuliwa kwa ghafula, Daudi haogopi kulala usingizi. Ana uhakika kwamba ataamka, kwa kuwa mambo yaliyompata mapema yamemfanya awe na uhakika kabisa kwamba anaweza kutegemea msaada wa Mungu ambao hauwezi kushindwa. Sisi pia tunaweza kufanya hivyo tukishikamana na “njia za Yehova” na tusipomwacha kamwe.—Soma 2 Samweli 22:21, 22.
8. Andiko la Zaburi 27:1-4 linaonyesha jinsi gani kwamba Daudi alimtegemea Mungu?
8 Zaburi nyingine ya Daudi inaonyesha kwamba ana uhakika katika Mungu na anamtegemea kikamili, Zaburi hiyo ina maneno haya yaliyoongozwa na roho ya Mungu: “Yehova ni nuru yangu na wokovu wangu. Nitamwogopa nani? Yehova ni ngome ya uhai wangu. Nitamhofu nani? . . . Hata kambi ijapopiga hema dhidi yangu, moyo wangu hautaogopa. . . . Nimemwomba Yehova jambo moja—ndilo nitakalolitafuta, kwamba nipate kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yangu, ili kuuona uzuri wa Yehova na kulitazama kwa uthamini hekalu lake.” (Zab. 27:1-4) Ikiwa wewe pia unahisi vivyo hivyo na hali zako zinakuruhusu, utakusanyika kwa ukawaida pamoja na waabudu wenzako wa Yehova.—Ebr. 10:23-25.
9, 10. Ingawa Daudi alisema maneno yaliyo katika Zaburi 3:6, 7, kwa nini unaweza kusema kwamba hakuwa na roho ya kulipiza kisasi?
9 Ingawa Daudi anakabili udanganyifu wa Absalomu na ukosefu wa ushikamanifu wa watu wengine wengi sana, anaimba hivi: “Sitaogopa maelfu kumi ya watu ambao wamejipanga dhidi yangu kunizunguka pande zote. Usimame, Ee Yehova! Uniokoe, Ee Mungu wangu! Kwa maana utawapiga adui zangu wote kwenye taya. Utayavunja meno ya waovu.”—Zab. 3:6, 7.
10 Daudi hana roho ya kulipiza kisasi. Ikiwa adui zake ‘wangepigwa kwenye taya au mfupa wa kidevu,’ Mungu ndiye angefanya hivyo. Mfalme Daudi amejiandikia nakala yake mwenyewe ya Sheria na anajua kwamba katika Sheria hiyo Yehova anatangaza hivi: “Kisasi ni changu, na malipo.” (Kum. 17:14, 15, 18; 32:35) Pia, ni daraka la Mungu ‘kuvunja meno ya waovu.’ Kuvunja meno yao kunamaanisha kuwamaliza nguvu kabisa ili wasiwe na uwezo wa kusababisha madhara. Yehova anawajua watu waovu kwa sababu yeye “huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Sam. 16:7) Tunathamini kama nini kwamba Mungu anatupatia imani na nguvu za kumpinga Shetani, ambaye ni mwovu kuliko wote, na ambaye hivi karibuni atatupwa ndani ya abiso kama simba anayenguruma ambaye hana meno na ambaye anastahili tu kuharibiwa!—1 Pet. 5:8, 9; Ufu. 20:1, 2, 7-10.
“Wokovu Ni wa Yehova”
11. Kwa nini tunapaswa kusali kwa ajili ya waamini wenzetu?
11 Daudi anatambua kwamba Yehova peke yake ndiye anayeweza kuleta ukombozi ambao anauhitaji sana. Lakini mtunga-zaburi huyo hajifikirii yeye mwenyewe tu. Namna gani watu wa Yehova kwa ujumla ambao wana kibali chake? Kwa kufaa, Daudi anamalizia wimbo wake ulioongozwa na roho ya Mungu kwa maneno haya: “Wokovu ni wa Yehova. Baraka yako iko juu ya watu wako.” (Zab. 3:8) Ni kweli kwamba Daudi ana matatizo makubwa sana, lakini anawakumbuka watu wa Yehova kwa ujumla na ana hakika kwamba Mungu atawabariki. Je, sisi pia hatupaswi kuwakumbuka waabudu wenzetu? Acheni tuwakumbuke katika sala zetu, na kumwomba Yehova awape roho yake takatifu ili wawe na ujasiri na watende kwa uhakika wanapotangaza habari njema.—Efe. 6:17-20.
12, 13. Ni nini kilichompata Absalomu, na Daudi alitenda jinsi gani?
12 Absalomu anakufa kifo cha aibu—onyo kwa wote ambao wanawatendea wengine vibaya, hasa watiwa-mafuta wa Mungu, kama vile Daudi. (Soma Methali 3:31-35.) Vita vinatokea, na majeshi ya Absalomu yanashindwa. Absalomu anakimbia akiwa amepanda nyumbu, mnyama anayefanana na punda, wakati nywele zake nyingi zinaposhikwa na tawi la mti mkubwa. Ananing’inia juu ya mti huo akiwa hai, lakini hawezi kufanya lolote, kisha Yoabu anamuua Absalomu kwa kuchoma mikuki mitatu midogo ndani ya moyo wake.—2 Sam. 18:6-17.
13 Je, Daudi anashangilia anapopata habari kuhusu jambo ambalo limempata mwana wake? Hapana. Badala yake, anatembea huku na huku, akiomboleza, na kulia hivi kwa sauti: “Mwanangu Absalomu, mwanangu, mwanangu Absalomu! Laiti mimi mwenyewe ningekufa badala yako, Absalomu mwanangu, mwanangu!” (2 Sam. 18:24-33) Ni maneno ya Yoabu tu ndiyo yanayomwondolea Daudi huzuni ambayo ilikuwa karibu kumlemea kabisa. Ni mwisho wenye kuhuzunisha kama nini kwa Absalomu, ambaye aliruhusu tamaa ya kichoyo ya kutaka makuu imwongoze kupigana na baba yake mwenyewe—mtiwa-mafuta wa Yehova—na hivyo akajiletea msiba yeye mwenyewe!—2 Sam. 19:1-8; Met. 12:21; 24:21, 22.
-