-
Je, Kweli Uhai Udumuo Milele Wawezekana?Mnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 15
-
-
Tumebuniwa Tuishi Milele
3, 4. (a) Kwa nini watu wengine huamini kwamba twapaswa kuishi milele? (b) Daudi alisema nini kuhusu jinsi alivyoumbwa?
3 Sababu moja inayowafanya watu wengi waamini kwamba wanadamu wapaswa kuishi milele yahusiana na jinsi ambavyo tumeumbwa kwa namna ya ajabu. Kwa mfano, ni jambo la kimwujiza kweli jinsi tulivyoumbwa ndani ya tumbo la uzazi la mama yetu. Mtu mmoja mwenye ujuzi juu ya hali ya kuzeeka aliandika hivi: “Baada ya kufanya miujiza inayotupata kutoka kutungwa mimba hadi kuzaliwa kisha hadi upevuko wa kingono na utu uzima, hali-asili ilichagua kutounda kile kionekanacho kuwa mfumo wa utendaji ulio sahili zaidi ambao ungedumisha miujiza hiyo milele.” Ndiyo, tufikiriapo jinsi tulivyoumbwa kimwujiza, swali hili labaki, Kwa nini inakuwa lazima tufe?
4 Maelfu ya miaka iliyopita, Daudi, mwandishi wa Biblia, alifikiria kwa makini miujiza hiyo, ingawa hangeweza kuona kihalisi ndani ya tumbo la uzazi kama wanasayansi wawezavyo kuona leo. Daudi alitafakari juu ya jinsi alivyoumbwa alipoandika kwamba alikuwa ‘amefichwa tumboni mwa mama yake.’ Alisema ‘figo zake zilifanyizwa’ wakati huo. Pia, yeye alisema kuhusu kuumbwa kwa “mifupa” yake wakati, kama alivyosema, “Nilipoumbwa kwa siri.” Kisha Daudi akasema juu ya “kiinitete changu” na kutaarifu kuhusu kiinitete hicho katika tumbo la uzazi la mama yake hivi: “Chuoni mwako ziliandikwa zote.”—Zaburi 139:13-16, NW.
5. Ni miujiza gani huhusika katika kufanyizwa kwetu ndani ya tumbo la uzazi?
5 Kwa wazi, hakukuwa ramani halisi iliyoandikwa kwa mkono kwa ajili ya kufanyizwa kwa Daudi ndani ya tumbo la uzazi la mama yake. Lakini katika kutafakari kwa Daudi juu ya kufanyizwa kwa “figo” zake, “mifupa” yake, na sehemu nyingine za mwili wake, kwake ilionekana kana kwamba ukuzi wa vitu hivi uliendelea kwa mpango—kwamba kila kitu kilikuwa, kusema kitamathali, ‘kimeandikwa chuoni.’ Ilikuwa kana kwamba chembe iliyotungishwa mimba ndani ya mama yake ilikuwa na chumba kikubwa kilichojaa vitabu vikiwa na maagizo mengi mno kuhusu namna ya kufanyiza mtoto wa kibinadamu na maagizo hayo tata yakapitishwa hadi kwa kila chembe iliyokuwa ikifanyizwa. Hivyo, gazeti Science World latumia mfano wa ‘kila chembe katika kiinitete kinachokua kuwa ina kabati iliyojaa ramani.’
6. Kuna uthibitisho gani kwamba sisi, kama alivyoandika Daudi, ‘tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha’?
6 Je, umewahi kufikiria jinsi mwili wetu unavyofanya kazi kimwujiza? Mwanabiolojia Jared Diamond alitaarifu hivi: “Sisi hubadilisha chembe zilizo ukutani mwa matumbo yetu mara moja baada ya siku chache, zile zilizo ukutani mwa kibofu cha mkojo mara moja baada ya miezi miwili, na chembe zetu nyekundu za damu mara moja kwa miezi minne.” Alimalizia kusema hivi: “Nguvu za asili zatutawanya vipande-vipande na kutuunganisha tena kila siku.” Hilo lamaanisha nini hasa? Lamaanisha kwamba haidhuru huenda tukaishi miaka mingapi—iwe 8, 80, au hata 800—mwili wetu wabaki ukiwa mchanga sana. Wakati mmoja, mwanasayansi fulani alikadiria hivi: “Kwa mwaka mmoja atomi ambazo sisi hupata kupitia hewa, chakula, na maji tunayotumia, zitachukua mahali pa zile atomi zipatazo asilimia 98 tulizo nazo sasa.” Kwa kweli, kama Daudi alivyosifu, tumeumbwa kwa “jinsi ya ajabu ya kutisha.”—Zaburi 139:14.
7. Kwa kutegemea jinsi ambavyo miili yetu imebuniwa, watu fulani wamefikia mkataa gani?
7 Ikitegemea muundo wa maumbile ya miili yetu, mamlaka yenye kuheshimika juu ya hali ya kuzeeka ilisema hivi: “Haiko wazi kwa nini kuzeeka kwapaswa kutokea.” Kwa kweli yaonekana kwamba twapaswa kuishi milele. Na hiyo ndiyo sababu watu wanajaribu kufikia lengo hilo kupitia tekinolojia zao. Muda mfupi uliopita, Dakt. Alvin Silverstein aliandika akiwa na uhakika katika kitabu chake Conquest of Death: “Tutavumbua mambo yanayotatanisha juu ya uhai. Tutafahamu . . . jinsi mtu anavyozeeka.” Kukiwa na matokeo gani? Alitabiri hivi: “Hakutakuwa tena na watu ‘wazee’ kwa kuwa ujuzi utakaoruhusu kushindwa kwa kifo utaleta pia ujana usio na mwisho.” Kwa kufikiria uchunguzi wa kisasa wa kisayansi kuhusu maumbile ya mwanadamu, je, wazo la uhai udumuo milele lasikika kuwa lisiloaminika? Kuna sababu nyingine yenye nguvu hata zaidi ya kuamini kwamba uhai udumuo milele wawezekana.
Tamaa ya Kuishi Milele
8, 9. Ni tamaa gani ya asili ambayo watu wamewaza juu yake katika historia yote?
8 Je, umewahi kutambua kwamba kuishi milele ni tamaa ya asili ya mwanadamu? Daktari mmoja aliandika hivi katika jarida la Ujerumani: “Ile tamaa kubwa ya uhai udumuo milele labda ni ya zamani kama mwanadamu mwenyewe.” Kikieleza itikadi fulani za Wanaulaya wa kale, kichapo The New Encyclopædia Britannica hutaarifu hivi: “Watu wanaostahili wataishi milele katika jumba lenye kung’aa lililoezekwa kwa dhahabu.” Na, lo! jinsi ambavyo watu wamejitahidi sana kutosheleza tamaa hiyo ya msingi ya uhai udumuo milele!
9 Kichapo The Encyclopedia Americana chasema kwamba zaidi ya miaka 2,000 iliyopita huko China, “wamaliki na watu wengine wa [kawaida] pia, chini ya uongozi wa makuhani wa Kitao, walipuuza kazi ngumu ili kutafuta madawa ya kurefusha maisha”—yanayoitwa eti chemchemi ya ujana. Kwa kweli, katika historia yote, watu wameamini kwamba kwa kutumia michanganyo mbalimbali au hata kunywa maji fulani, wangeweza kubaki wakiwa vijana.
10. Ni jaribio gani la kisasa ambalo limefanywa ili kufikia uhai uliorefushwa?
10 Jitihada za kisasa za kujaribu kutosheleza tamaa ya asili ya kuishi milele ni zenye kutokeza vilevile. Mfano unaojulikana na wengi ni zoea la kugandisha mtu aliyekufa kutokana na ugonjwa. Hilo limefanywa kwa matumaini ya kumrudishia mtu huyo uhai wakati fulani ujao, wakati tiba ya ugonjwa huo itakapokuwa imepatikana. Mtetezi wa zoea hili linaloitwa cryonics, aliandika hivi: “Ikiwa matumaini yetu chanya yatathibitika, na kujifunza jinsi ya kutibu na kurekebisha madhara yote—kutia ndani udhaifu wa umri wa uzee—ndipo wale ‘wafao’ leo watakapopata maisha yaliyoendelezwa kwa kipindi kisichojulikana kwa wakati ujao.”
11. Kwa nini watu hutamani kuishi milele?
11 Huenda ukauliza, kwa nini hii tamaa ya uhai udumuo milele imekazwa sana ndani ya akili zetu? Je, ni kwa sababu “[Mungu] ameweka milele akilini mwa mwanadamu”? (Mhubiri 3:11, Revised Standard Version) Hilo ni jambo linalohitaji kufikiriwa kwa uzito! Hebu fikiria: Kwa nini tutamani kuishi milele ikiwa lisingalikuwa kusudi la Muumba wetu kwamba tamaa hiyo itoshelezwe? Na, je, lingekuwa jambo la upendo kwa Mungu kutuumba tukiwa na tamaa ya uhai udumuo milele kisha atukatishe tamaa kwa kutuzuia tusitimize kamwe tamaa hiyo?—Zaburi 145:16.
-
-
Je, Kweli Uhai Udumuo Milele Wawezekana?Mnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 15
-
-
Je, Kweli Ni Kusudi la Mungu?
15. Ni nini kionyeshacho kwamba ni kusudi la Mungu tuishi milele?
15 Lakini, huenda ukauliza, Je, kweli ni kusudi la Yehova kwamba tufurahie uhai udumuo milele? Ndiyo, bila shaka! Neno lake laahidi uhai udumuo milele mara nyingi. “Zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele,” Biblia yatuhakikishia. Yohana mtumishi wa Mungu aliandika hivi: “Hili ndilo jambo lililoahidiwa ambalo [Mungu] mwenyewe alituahidi, uhai udumuo milele.” Haishangazi kwamba mwanamume kijana alimwuliza Yesu hivi: “Mwalimu, ni lazima nifanye wema gani kusudi nipate uhai udumuo milele?” (Waroma 6:23; 1 Yohana 2:25; Mathayo 19:16) Kwa hakika, mtume Paulo aliandika juu ya “tumaini la uhai udumuo milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi kabla ya nyakati zinazodumu muda mrefu.”—Tito 1:2.
16. Huenda Mungu aliuahidi uhai udumuo milele “kabla ya nyakati zinazodumu muda mrefu” katika maana gani?
16 Yamaanisha nini kwamba Mungu aliuahidi uhai udumuo milele “kabla ya nyakati zinazodumu muda mrefu”? Wengine hufikiria kwamba mtume Paulo alimaanisha kwamba kabla ya kuumbwa kwa wenzi wa kwanza, Adamu na Hawa, Mungu alikusudia kwamba wanadamu wapaswa kuishi milele. Hata hivyo, ikiwa Paulo alikuwa akirejezea wakati fulani baada ya wanadamu kuumbwa na wakati Yehova alipotaarifu kusudi lake, bado ni wazi kwamba mapenzi ya Mungu yatia ndani uhai udumuo milele kwa wanadamu.
17. Kwa nini Adamu na Hawa waliondolewa katika bustani ya Edeni, na kwa nini makerubi waliwekwa langoni?
17 Biblia yasema kwamba katika bustani ya Edeni, “BWANA Mungu akachipusha katika ardhi . . . mti wa uzima.” Sababu iliyotolewa ya kumwondoa Adamu nje ya bustani ni ili “asije akanyosha mkono wake akatwaa matunda ya mti wa uzima, akala, akaishi”—naam, milele! Baada ya kuwafukuza Adamu na Hawa kutoka bustani ya Edeni, Yehova akaweka “Makerubi . . . na upanga wa moto uliogeuka huko na huko, kuilinda njia ya mti wa uzima.”—Mwanzo 2:9; 3:22-24.
18. (a) Kula kutoka kwa mti wa uzima kungemaanisha nini kwa Adamu na Hawa? (b) Kula kutoka kwa mti huo kuliwakilisha nini?
18 Iwapo Adamu na Hawa wangeruhusiwa kula kutokana na mti wa uhai, hilo lingemaanisha nini kwao? Naam, pendeleo la kuishi milele katika Paradiso! Msomi mmoja wa Biblia alikisia hivi: “Mti wa uzima ni lazima uwe ulikuwa na uwezo fulani ambao kupitia huo, mwanadamu hangedhoofishwa na umri, wala kuoza kunakomalizikia katika kifo.” Hata alidai kwamba “kulikuwa na mitishamba katika paradiso, yenye uwezo wa kukabiliana na athari” za kuzeeka. Hata hivyo, Biblia haisemi kwamba mti wa uzima wenyewe ulikuwa na ubora wenye kutoa uhai. Badala yake, mti huo uliwakilisha uhakikisho kamili wa Mungu wa uhai udumuo milele kwa yeyote yule ambaye angeruhusiwa kula matunda yake.—Ufunuo 2:7.
Kusudi la Mungu Halikubadilika
19. Kwa nini Adamu alikufa, na kwa nini sisi, uzao wake, tunakufa pia?
19 Adamu alipokosea, alipoteza haki ya uhai udumuo milele kwa ajili yake na wazao wake wote ambao hawakuwa wamezaliwa. (Mwanzo 2:17) Alipopata kuwa mtenda-dhambi kwa sababu ya kutotii kwake, akawa mwenye kasoro, asiye mkamilifu. Tokea wakati huo na kuendelea, kwa kweli mwili wa Adamu ukapangiwa kufa. Kama isemavyo Biblia, “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Isitoshe, uzao usio mkamilifu wa Adamu nao pia ukapangiwa kufa, wala si kuishi milele. Biblia yaeleza hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.
20. Ni nini kionyeshacho kwamba wanadamu walikusudiwa waishi milele duniani?
20 Lakini vipi kama Adamu hangefanya dhambi? Vipi kama asingalikosa kumtii Mungu na awe ameruhusiwa kula kutokana na mti wa uzima? Angefurahia zawadi ya Mungu ya uhai udumuo milele akiwa wapi? Mbinguni? La! Mungu hakusema lolote kuhusu kupelekwa kwa Adamu mbinguni. Yeye alipewa kazi ya kufanya duniani. Biblia yaeleza kwamba “BWANA Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa,” nayo yasema: “BWANA Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.” (Mwanzo 2:9, 15) Baada ya Hawa kuumbwa awe mwenzi wa Adamu, wote wawili walipewa mgawo wa ziada wa kazi hapa duniani. Mungu aliwaambia hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”—Mwanzo 1:28.
21. Ni matazamio gani ya ajabu yaliyofurahiwa na wanadamu wa kwanza?
21 Wazia mataraja ya ajabu ya kidunia ambayo maagizo hayo kutoka kwa Mungu yalifungulia Adamu na Hawa! Walipaswa kulea wana na binti wenye afya kamili katika Paradiso ya kidunia. Kadiri watoto wao wapendwa walivyokua, wangeshiriki pamoja nao katika kuzaa na kufanya kazi ya kufurahisha kwenye bustani, ili kuidumisha Paradiso. Na wanyama wote wakijitiisha chini yao, maisha yao yangekuwa yenye kuridhisha sana. Fikiria ile shangwe ya kupanua mipaka ya bustani ya Edeni hivi kwamba dunia yote hatimaye ingekuwa paradiso! Je, ungefurahia maisha pamoja na watoto katika makao mazuri kama hayo bila kuhangaikia uzee na kifo? Acha moyo wako ujibu swali hilo.
-