-
Kwa Nini Uwakabidhi Wengine Kazi—Unaweza Kufanya Hivyo Jinsi Gani?Mnara wa Mlinzi—2009 | Juni 15
-
-
Jinsi ya Kuwakabidhi Wengine Kazi
Unapowakabidhi akina ndugu kazi, fikiria uwezo wa ndugu ambao unataka kuwakabidhi kazi. Kulipokuwa na uhitaji wa kushughulikia ugawaji wa kila siku wa chakula huko Yerusalemu, mitume waliwachagua ‘wanaume saba waliothibitishwa, wenye kujaa roho na hekima.’ (Mdo. 6:3) Ukimwomba mtu asiyetegemeka afanye kazi fulani, huenda akashindwa kuifanya. Kwa hiyo, mpe kazi ndogondogo kwanza. Mtu anapojithibitisha kuwa mwaminifu, anaweza kushughulikia madaraka zaidi.
Hata hivyo, mambo mengi yanahusika. Watu wana nyutu na uwezo tofauti-tofauti. Watu wana viwango mbalimbali vya uzoefu. Ndugu mwenye urafiki na mchangamfu anaweza kuwa mkaribishaji mzuri, naye ndugu anayefanya mambo kwa utaratibu na mpangilio mzuri anaweza kuwa msaidizi mzuri sana wa mwandishi wa kutaniko. Dada aliye na uwezo wa kurembesha vitu mbalimbali anaweza kukabidhiwa kazi ya kupanga maua wakati wa Ukumbusho.
Unapogawa kazi, eleza waziwazi jinsi kazi hiyo inavyopaswa kutimizwa. Kabla ya Yohana Mbatizaji kuwatuma wajumbe kwa Yesu, aliwaeleza mambo ambayo alitaka kujua na swali ambalo wangeuliza. (Luka 7:18-20) Kwa upande mwingine, Yesu alipowaagiza wanafunzi wake wakusanye masalio ya chakula kilichoandaliwa kimuujiza, aliwaambia mambo hususa ya kufanya. (Yoh. 6:12, 13) Kuwakabidhi wengine kazi kunategemea hasa kazi yenyewe na uwezo wa yule anayesaidia. Yule anayemkabidhi mwingine kazi na yule anayeombwa afanye kazi hiyo wanapaswa kuelewa jinsi kazi hiyo inavyopaswa kufanywa na ripoti kuhusu kazi hiyo zinapaswa kutolewa mara ngapi. Wote wawili wanapaswa kujua yule anayefanya kazi hiyo ana uhuru wa kutumia busara katika mambo gani. Ikiwa kazi hiyo inapaswa kukamilishwa kufikia tarehe fulani, itakuwa vizuri zaidi ikiwa watazungumzia tarehe ya kumaliza kazi hiyo na kukubaliana badala tu ya kuamuru kazi hiyo imalizwe tarehe fulani.
Mtu anayekabidhiwa kazi fulani anapaswa kupewa pesa, vifaa, na msaada anaohitaji. Huenda likawa jambo linalofaa kuwajulisha wengine mpango huo. Yesu alipomkabidhi Petro “funguo za ufalme wa mbinguni,” alimpa mbele ya wanafunzi wengine. (Mt. 16:13-19) Vivyo hivyo, katika hali fulani huenda ikawa vizuri kulitangazia kutaniko ni nani aliye na daraka la kufanya kazi fulani.
Ni vizuri pia kuwa mwangalifu. Ikiwa utaendelea kufanya kazi ambayo umemkabidhi mtu mwingine, ni kana kwamba unamwambia, “Sikuamini sana.” Ni kweli kwamba nyakati nyingine huenda kazi isifanywe kama ulivyotazamia. Hata hivyo, ikiwa ndugu ambaye amekabidhiwa daraka fulani anapewa kiasi fulani cha uhuru, inaelekea kwamba atapata ujasiri na uzoefu. Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba hupaswi kuangalia jinsi anavyofanya kazi uliyompa. Hata ingawa Yehova alimkabidhi Mwana wake daraka fulani katika kazi ya uumbaji, bado Yehova mwenyewe alishiriki katika kazi hiyo. Alimwambia hivi Stadi huyo wa Kazi: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu.” (Mwa. 1:26) Kwa hiyo, kwa maneno na matendo yako, unga mkono kazi inayofanywa na umpongeze mtu huyo kwa jitihada zake. Kuzungumza naye kwa ufupi kuhusu matokeo ya kazi anayofanya kunaweza kumsaidia. Ikiwa kazi hiyo haifanywi kwa njia inayofaa, usisite kutoa mashauri au msaada zaidi. Kumbuka kwamba unapomkabidhi mtu kazi wewe ndiye utakayetoa hesabu ya matokeo ya kazi hiyo.—Luka 12:48.
-
-
Kwa Nini Uwakabidhi Wengine Kazi—Unaweza Kufanya Hivyo Jinsi Gani?Mnara wa Mlinzi—2009 | Juni 15
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 30]
JINSI YA KUWAKABIDHI WENGINE KAZI
• Chagua watu ambao wanaweza kufanya kazi hiyo
• Eleza waziwazi kuhusu kazi hiyo/zungumza nao
• Fafanua jambo linalopaswa kutimizwa
• Wape vifaa wanavyohitaji
• Onyesha kwamba unapendezwa na kazi hiyo, na kwamba unawaamini
• Uwe tayari kutoa hesabu ya matokeo ya kazi hiyo
-