-
Yehova Alikuwa “Mwokoaji” Katika Nyakati za BibliaMnara wa Mlinzi—2008 | Septemba 15
-
-
Yehova Alikuwa “Mwokoaji” Katika Nyakati za Biblia
“Ee Mungu, uchukue hatua haraka kwa ajili yangu. Wewe ndiye msaada wangu na Mwokoaji wangu.”—ZAB. 70:5.
1, 2. (a) Waabudu wa Mungu wanamwomba msaada wakati gani? (b) Ni swali gani linalotokea, na tunaweza kupata jibu wapi?
WAKIWA katika likizo, wazazi wa mwanamke fulani aliyeolewa mwenye umri wa miaka 23 wanapata habari kwamba binti yao ametoweka katika hali ambazo hazieleweki. Wanafikiri kwamba kuna njama fulani. Bila kukawia, wanafunga virago na kurudi nyumbani, huku wakimsihi sana Yehova awasaidie. Shahidi mmoja mwenye umri wa miaka 20 anagunduliwa kuwa ana ugonjwa ambao utamwacha akiwa amepooza kabisa. Mara moja anasali kwa Yehova. Mama fulani asiye na mume anajaribu sana kutafuta kazi, hana pesa za kutosha kununua chakula kwa ajili yake na binti yake mwenye umri wa miaka 12. Anasali kwa Yehova kwa moyo wake wote. Ndiyo, waabudu wa Mungu wanapopata majaribu makali au matatizo wanamwomba msaada bila kukawia. Je, umewahi kumsihi Yehova akusaidie ukiwa na uhitaji mkubwa?
2 Swali hili la maana linatokea: Je, kweli tunaweza kumtazamia Yehova ajibu sala zetu za kuomba msaada? Zaburi ya 70 inatoa jibu lenye kuimarisha imani. Zaburi hiyo yenye kugusa moyo iliandikwa na Daudi, mwabudu mshikamanifu wa Yehova, ambaye alipata majaribu mengi makali na matatizo katika maisha yake. Mtunga-zaburi huyo aliyeongozwa na roho takatifu alichochewa kusema hivi kumhusu Yehova: “Ee Mungu, . . . wewe ndiye msaada wangu na Mwokoaji wangu.” (Zab. 70:5) Kuchunguza Zaburi ya 70 kutatusaidia kuona kwa nini sisi pia tunaweza kumwomba Yehova msaada wakati wa uhitaji na kuwa na hakika kabisa kwamba atakuwa “Mwokoaji” wetu.
“Wewe Ndiye . . . Mwokoaji”
3. (a) Zaburi ya 70 ina kilio gani cha kuomba msaada wa haraka? (b) Daudi anaonyesha uhakika gani katika Zaburi ya 70?
3 Zaburi ya 70 inaanza na kumalizia na kilio cha kumwomba Mungu msaada wa haraka. (Soma Zaburi 70:1-5.) Daudi anamsihi sana Yehova ‘afanye haraka’ na ‘achukue hatua ya haraka’ ya kumkomboa. Katika mstari wa pili mpaka wa nne, Daudi anasihi mara tano akitumia neno “na” au “nao” ili kuonyesha tamaa yake. Mara tatu za kwanza anasihi kwa ajili ya wale wanaojaribu kumuua. Daudi anamsihi sana Yehova awashinde maadui hao na kuwaaibisha kwa sababu ya uovu wao. Maombi yake mawili ya kusihi ambayo yanafuata, yaliyo katika mstari wa 4, ni kwa ajili ya watu wa Mungu. Daudi anasali kwamba wale wanaomtafuta Yehova wachochewe kumshangilia na kumtukuza Yehova. Daudi anamalizia zaburi hiyo kwa kumwambia Yehova hivi: “Wewe ndiye msaada wangu na Mwokoaji wangu.” Ona kwamba Daudi hasemi, “Na uthibitike kuwa,” kana kwamba anamsihi tena. Badala yake, anasema, “Wewe ndiye,” kuonyesha uhakika wake. Daudi anaamini kwamba Mungu atamsaidia.
4, 5. Tunajifunza nini kumhusu Daudi katika Zaburi ya 70, na tunaweza kuwa na uhakika gani?
4 Zaburi ya 70 inaonyesha nini kumhusu Daudi? Alipokabili maadui walioazimia kumuua, Daudi aliamua kutochukua mambo mikononi mwake. Badala yake, alikuwa na uhakika kwamba Yehova angewachukulia hatua wapinzani hao kwa wakati wake na kwa njia yake. (1 Sam. 26:10) Daudi aliendelea kusadiki kabisa kwamba Yehova anawasaidia na kuwakomboa wale wanaomtafuta. (Ebr. 11:6) Daudi aliamini kwamba waabudu hao wa kweli wana sababu nzuri sana za kushangilia na kumtukuza Yehova kwa kuwaambia wengine kuhusu ukuu wake.—Zab. 5:11; 35:27.
5 Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kama Daudi kwamba Yehova ni Msaidizi wetu na “Mwokoaji” wetu. Hivyo, tunapopata majaribu makali au kuhisi kwamba tunahitaji msaada wa haraka, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie haraka. (Zab. 71:12) Hata hivyo, Yehova anaweza kujibu jinsi gani sala zetu za kuomba msaada? Kabla ya kuzungumzia jinsi Yehova anavyoweza kutusaidia, acheni tuchunguze njia tatu ambazo alitumia kumwokoa Daudi, na kumsaidia alipohitaji msaada wa haraka.
Alikombolewa Kutoka kwa Wapinzani
6. Ni nini kilichomsaidia Daudi kujua kwamba Yehova anawaokoa waadilifu?
6 Kutokana na sehemu za Biblia ambazo alikuwa nazo, Daudi alijua kwamba waadilifu wanaweza kumtegemea Yehova awasaidie. Yehova alipoleta Gharika juu ya ulimwengu usiomwogopa, alimwokoa Noa na familia yake iliyomwogopa Mungu. (Mwa. 7:23) Yehova aliponyesha moto na kiberiti juu ya watu waovu walioishi Sodoma na Gomora, alimsaidia Loti aliyekuwa mwadilifu kuokoka kifo pamoja na mabinti wake wawili. (Mwa. 19:12-26) Yehova alipomharibu Farao mwenye kiburi pamoja na majeshi yake katika Bahari Nyekundu, Aliwalinda watu wake, na kuwasaidia kuepuka maangamizi. (Kut. 14:19-28) Basi, si ajabu kwamba Daudi katika zaburi nyingine alimsifu Yehova kuwa “Mungu wa matendo ya kuokoa.”—Zab. 68:20.
7-9. (a) Daudi alikuwa na sababu gani za kutegemea nguvu za Mungu za kuokoa? (b) Daudi alisema ni nani aliyemkomboa?
7 Daudi alikuwa pia na sababu yake binafsi ya kutegemea kabisa nguvu za Yehova za kuokoa. Daudi alikuwa amejionea mwenyewe kwamba “mikono ya milele” ya Yehova inaweza kuwaokoa wale Wanaomtumikia. (Kum. 33:27, Union Version) Katika pindi nyingi, Yehova alikuwa amemwokoa Daudi kutoka katika mikono ya ‘adui wenye hasira.’ (Zab. 18:17-19, 48) Fikiria mfano mmoja.
8 Wanawake wa Israeli walipoanza kumsifu Daudi kwa sababu ya ushujaa wake wa vita, Mfalme Sauli aliona wivu sana hivi kwamba pindi mbili alimtupia Daudi mkuki. (1 Sam. 18:6-9) Pindi zote mbili Daudi aliukwepa mkuki. Je, Daudi aliukwepa kwa sababu alikuwa mpiganaji mwepesi na mwenye uzoefu? Hapana. Biblia inasema kwamba “Yehova alikuwa pamoja naye.” (Soma 1 Samweli 18:11-14.) Baadaye, njama ya Sauli ya kumuua Daudi kwa mikono ya Wafilisti ilipokosa kufaulu, ‘Sauli aliona na kujua kwamba Yehova alikuwa pamoja na Daudi.’—1 Sam. 18:17-28.
9 Daudi alisema ni nani aliyemkomboa? Maneno ya utangulizi ya Zaburi ya 18 yanasema kwamba Daudi ‘alimwambia Yehova maneno ya wimbo huu siku ambayo Yehova alikuwa amemkomboa kutoka mkononi mwa Sauli.’ Daudi alionyesha jinsi alivyohisi alipoimba hivi: “Yehova ni mwamba wangu na ngome yangu na Mwokoaji wangu. Mungu wangu ni mwamba wangu. Nitamkimbilia.” (Zab. 18:2) Je, imani yetu haitiwi nguvu tunapojua kwamba Yehova anaweza kuwakomboa watu wake?—Zab. 35:10.
Alitegemezwa Katika Kitanda cha Ugonjwa
10, 11. Ni nini kinachotusaidia kujua wakati ambapo huenda Daudi alikuwa mgonjwa kama Zaburi ya 41 inavyosema?
10 Wakati fulani Mfalme Daudi alikuwa mgonjwa sana kama Zaburi ya 41 inavyosema. Kwa muda fulani, Daudi hangeweza kutoka kitandani kwa kuwa alikuwa mgonjwa sana hivi kwamba maadui fulani walifikiri kwamba “hatasimama tena.” (Mstari wa 7 na 8) Ni wakati gani ambapo Daudi alikuwa mgonjwa sana hivyo? Huenda hali zinazotajwa katika zaburi hiyo zinahusu kipindi chenye kufadhaisha sana katika maisha ya Daudi wakati Absalomu, mwana wake alipojaribu kunyakua ufalme wake.—2 Sam. 15:6, 13, 14.
11 Kwa mfano, Daudi anataja kwamba rafiki aliyemwamini, ambaye alikuwa akila mkate pamoja naye alimsaliti. (Mstari wa 9) Hilo linatukumbusha kisa kimoja katika maisha ya Daudi. Wakati Absalomu alipoasi, Ahithofeli, mshauri mwenye kutegemeka wa Daudi, alimsaliti na kujiunga na Absalomu katika kumwasi Mfalme Daudi. (2 Sam. 15:31; 16:15) Hebu wazia jinsi mfalme huyo aliyedhoofika na asiye na nguvu za kusimama alivyohisi akiwa kwenye kitanda chake cha ugonjwa, huku akijua kwamba amezungukwa na wasaliti waliotaka afe ili watekeleze mipango yao ya uovu.—Mstari wa 5.
12, 13. (a) Daudi alikuwa na uhakika gani? (b) Huenda Mungu alimtia nguvu Daudi jinsi gani?
12 Daudi alimtegemea yule “Mwokoaji” bila kuyumbayumba. Daudi alisema hivi kuhusu mtumishi mwadilifu wa Yehova, aliye mgonjwa: “Katika siku ya msiba Yehova atamwokoa. Yehova mwenyewe atamtegemeza katika kitanda cha ugonjwa; kitanda chake chote hakika utakibadilisha wakati wa ugonjwa wake.” (Zab. 41:1, 3) Katika andiko hilo, Daudi anaonyesha tena uhakika kwa kusema, “Yehova mwenyewe atamtegemeza.” Daudi alikuwa na uhakika kwamba Yehova angemwokoa. Jinsi gani?
13 Daudi hakutazamia Yehova amponye ugonjwa kimuujiza. Badala yake, Daudi alikuwa na uhakika kwamba Yehova ‘angemtegemeza,’ yaani, angemsaidia na kumtia nguvu akiwa amelala kwenye kitanda akiwa mgonjwa. Bila shaka, Daudi alihitaji msaada huo. Zaidi ya ugonjwa ambao ulimdhoofisha, alizungukwa na maadui ambao walikuwa wakisema mambo maovu kumhusu. (Mstari wa 5 na 6) Huenda Yehova alimtia nguvu Daudi kwa kumsaidia kukumbuka mambo yenye kufariji. Kwa mfano, Daudi alisema hivi: “Umenitegemeza kwa sababu ya utimilifu wangu.” (Mstari wa 12) Pia, huenda Daudi alipata nguvu alipotafakari uhakika wa kwamba Yehova alimwona kuwa mtu mtimilifu hata ingawa alikuwa amedhoofika na maadui wake walikuwa wakisema mambo mabaya kumhusu. Mwishowe, Daudi alipona ugonjwa wake. Je, haitii moyo kujua kwamba Yehova anaweza kuwategemeza wale ambao ni wagonjwa?—2 Kor. 1:3.
Alimpa Vitu Alivyohitaji
14, 15. Ni wakati gani ambapo Daudi na wanaume wake walihitaji sana chakula na kinywaji, nao walipata msaada gani?
14 Alipowekwa kuwa mfalme wa Israeli, Daudi alikuwa na vyakula na vinywaji bora na hata aliwaalika watu wengine wengi ili wale pamoja naye. (2 Sam. 9:10) Hata hivyo, Daudi alijua pia jinsi ya kuishi bila chakula cha kutosha. Wakati Absalomu, mwana wake, alipopanga uasi na kujaribu kunyakua ufalme, Daudi pamoja na watu fulani washikamanifu waliomuunga mkono walikimbia kutoka Yerusalemu. Walikimbilia nchi ya Gileadi, upande wa mashariki wa Mto Yordani. (2 Sam. 17:22, 24) Daudi na wanaume wake walilazimika kuishi kama wakimbizi, na muda si muda walihitaji sana chakula, kinywaji, na pia kupumzika. Hata hivyo, wangepata wapi vitu hivyo katika eneo hilo la nyikani?
15 Mwishowe, Daudi na wanaume wake walifika katika jiji la Mahanaimu. Huko walikutana na wanaume watatu hodari—Shobi, Makiri, na Barzilai. Walikuwa tayari kuhatarisha maisha yao ili kumsaidia mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu, kwa kuwa kama Absalomu angenyakua ufalme, bila shaka angemwadhibu vikali mtu yeyote aliyemuunga Daudi mkono. Raia hao watatu washikamanifu walipoona hali ngumu ya Daudi na wanaume wake, walileta vitu walivyohitaji sana, kutia ndani vitanda, ngano, shayiri, nafaka iliyochomwa, maharagwe mapana, dengu, asali, siagi, na kondoo. (Soma 2 Samweli 17:27-29.) Bila shaka, ushikamanifu na ukarimu wa pekee wa wanaume hao watatu uligusa sana moyo wa Daudi. Daudi hangesahau kamwe jinsi walivyomtendea.
16. Ni nani hasa aliyetimiza mahitaji ya Daudi na wanaume wake?
16 Hata hivyo, ni nani hasa aliyetimiza mahitaji ya Daudi na wanaume wake? Daudi alisadiki kwamba Yehova anawajali watu wake. Bila shaka, Yehova anaweza kuwachochea watumishi wake wengine, ili wamsaidie mwabudu mwenzao aliye na uhitaji. Alipotafakari kuhusu mambo yaliyotukia katika nchi ya Gileadi, hapana shaka kwamba Daudi aliona fadhili za wanaume hao watatu kuwa uthibitisho wa kwamba Yehova anajali na ni mwenye upendo. Alipokaribia mwisho wa maisha yake, Daudi aliandika hivi: “Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamwona mtu yeyote mwadilifu [kutia ndani yeye] akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate.” (Zab. 37:25) Je, haifariji kujua kwamba mkono wa Yehova si mfupi kamwe?—Met. 10:3.
“Yehova Anajua Jinsi ya Kuwakomboa Watu”
17. Yehova amethibitisha nini tena na tena?
17 Daudi ni mmoja tu kati ya waabudu wengi ambao Yehova aliokoa katika nyakati za Biblia. Tangu siku za Daudi, Mungu amethibitisha tena na tena ukweli wa maneno haya ya mtume Petro: “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.” (2 Pet. 2:9) Fikiria mifano mingine miwili.
18. Yehova aliwakomboa jinsi gani watumishi wake katika siku za Hezekia?
18 Jeshi lenye nguvu la Ashuru lilipovamia Yuda na kutisha Yerusalemu katika karne ya nane K.W.K., Mfalme Hezekia alisali hivi: “Ee Yehova Mungu wetu, utuokoe . . . ili falme zote za dunia zijue kwamba wewe, Ee Yehova, ndiye Mungu peke yako.” (Isa. 37:20) Hezekia alihangaikia hasa jina la Mungu na sifa yake. Yehova alijibu sala hiyo ya kutoka moyoni. Katika usiku mmoja tu, malaika mmoja aliwapiga na kuwaua Waashuru 185,000, naye akawakomboa watumishi waaminifu wa Yehova.—Isa. 37:32, 36.
19. Wakristo wa karne ya kwanza waliokoka msiba kwa kutii onyo gani?
19 Siku chache tu kabla ya kifo chake, Yesu alitoa onyo la kinabii ambalo lingewasaidia wanafunzi wake huko Yudea. (Soma Luka 21:20-22.) Miaka mingi ilipita, lakini katika mwaka wa 66 W.K., majeshi ya Roma yalikuja Yerusalemu kwa sababu ya uasi wa Wayahudi. Vikosi vya kijeshi vilivyoongozwa na Sesho Galo viliharibu sehemu ya ukuta wa hekalu; kisha vikaondoka ghafula. Wakristo waaminifu walitambua kwamba hiyo ilikuwa nafasi ya kuokoka uharibifu ambao Yesu alikuwa ametabiri, wakakimbilia milimani. Majeshi ya Roma yalirudi mwaka wa 70 W.K. Wakati huu hayakuondoka, yaliharibu Yerusalemu kabisa. Wakristo waliotii onyo la Yesu waliokoka msiba huo mbaya.—Luka 19:41-44.
20. Kwa nini tunaweza kumtegemea Yehova akiwa “Mwokoaji” wetu?
20 Imani yetu inatiwa nguvu tunapochunguza ushuhuda unaoonyesha kwamba Yehova anawasaidia watu wake. Mambo aliyofanya zamani yanatusaidia kuwa na uhakika. Hata tukipata matatizo gani sasa au wakati ujao, sisi pia tunaweza kumtegemea kabisa Yehova akiwa “Mwokoaji” wetu. Hata hivyo, Yehova anaweza kutuokoa kwa njia gani? Na namna gani watu wanaotajwa mwanzoni mwa habari hii? Walipata msaada gani mwishowe? Acheni tuone katika habari inayofuata.
-
-
Yehova Ni “Mwokoaji” WetuMnara wa Mlinzi—2008 | Septemba 15
-
-
Yehova Ni “Mwokoaji” Wetu
“Yehova atawasaidia na kuwaokoa.”—ZAB. 37:40.
1, 2. Ni ukweli gani wa msingi kumhusu Yehova ambao unatufariji na kututia nguvu?
KIVULI hakibaki palepale. Kadiri dunia inavyozunguka, vivuli vinavyosababishwa na jua vinasonga na kubadilika. Hata hivyo, Muumba wa dunia na jua, habadiliki. (Mal. 3:6) Biblia inasema, “naye habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.” (Yak. 1:17) Bila shaka, ukweli huo wa msingi kumhusu Yehova unatufariji na kututia nguvu, hasa tunapopatwa na majaribu na matatizo mazito. Kwa nini?
2 Kama tulivyoona katika habari iliyotangulia, Yehova alithibitika kuwa “Mwokoaji” katika nyakati za Biblia. (Zab. 70:5) Yehova habadiliki na sikuzote anatimiza ahadi zake; hivyo, waabudu wake leo wanaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba “atawasaidia na kuwaokoa.” (Zab. 37:40) Yehova amewaokoa jinsi gani watumishi wake leo? Anaweza kutuokoa jinsi gani sisi binafsi?
Kukombolewa Kutoka kwa Wapinzani
3. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba wapinzani hawataweza kuwazuia watu wa Yehova wasihubiri habari njema?
3 Hata Shetani akileta upinzani wa aina gani hawezi kamwe kuwazuia Mashahidi wa Yehova wasimwabudu Yehova kwa moyo wote kama anavyostahili kuabudiwa. Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu.” (Isa. 54:17) Wapinzani wamejaribu kuwazuia watu wa Mungu wasihubiri lakini wameshindwa. Fikiria mifano miwili.
4, 5. Watu wa Yehova walipata upinzani gani mwaka wa 1918, na matokeo yalikuwa nini?
4 Mwaka wa 1918, watu wa Yehova walipata mateso mengi yaliyochochewa na makasisi ambao walitaka kuikomesha kazi ya kuhubiri. Mnamo Mei (Mwezi wa 5) 7, serikali ilitoa hati ya kumkamata J. F. Rutherford, ambaye alikuwa akisimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote wakati huo, na hati za kuwakamata ndugu wengine wa makao makuu. Kwa muda usiozidi miezi miwili, Ndugu Rutherford na washiriki wenzake walishtakiwa isivyo haki kwamba walipanga njama, kisha wakahukumiwa vifungo virefu vya gereza. Je, wapinzani walikuwa wamefanikiwa kutumia mahakama kukomesha kabisa kazi ya kuhubiri? Bila shaka hapana!
5 Kumbuka ahadi ya Yehova: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa.” Mambo yalibadilika ghafula Machi 26, 1919 (26/3/1919)—miezi tisa baada ya Ndugu Rutherford na washiriki wenzake kuhukumiwa—wakati ambapo ndugu hao waliachiliwa kwa dhamana. Mwaka uliofuata, Mei 5, 1920 (5/5/1920), mashtaka yaliyoletwa juu yao yalifutiliwa mbali. Ndugu hao walitumia uhuru wao kuendelea na kazi ya Ufalme. Matokeo yamekuwa nini? Tangu wakati huo kumekuwa na ongezeko kubwa sana! Yule “Mwokoaji” ndiye anayestahili kusifiwa kwa ajili ya ongezeko hilo.—1 Kor. 3:7.
6, 7. (a) Ni kampeni gani ya kuwaangamiza Mashahidi wa Yehova iliyoanzishwa katika Ujerumani ya Wanazi, na matokeo yalikuwa nini? (b) Historia ya watu wa Yehova leo inathibitisha jambo gani la hakika?
6 Sasa fikiria mfano wa pili. Mwaka wa 1934, Hitler aliapa kuwaangamiza kabisa Mashahidi wa Yehova huko Ujerumani. Halikuwa tishio tu, aliazimia kufanya hivyo. Mashahidi wengi walikamatwa na kufungwa gerezani. Maelfu ya Mashahidi waliteswa; mamia waliuawa katika kambi za mateso. Je, Hitler alifaulu katika kampeni yake ya kuwaangamiza Mashahidi? Je, alikomesha kabisa kazi ya kuhubiri habari njema huko Ujerumani? Alishindwa kabisa! Wakati wa mateso hayo, ndugu zetu waliendelea kuhubiri kisirisiri. Baada ya kuanguka kwa utawala wa Wanazi, walitumia uhuru wao kuendelea kuhubiri. Leo, kuna wahubiri wa Ufalme zaidi ya 165,000 nchini Ujerumani. Kwa mara nyingine tena, yule “Mwokoaji” ametimiza ahadi yake: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa.”
7 Historia ya Mashahidi wa Yehova leo inathibitisha kwamba Yehova hataruhusu kamwe watu wake waangamizwe wakiwa kikundi. (Zab. 116:15) Namna gani tukiwa mtu mmoja-mmoja? Yehova anatuokoa sisi binafsi jinsi gani?
Namna Gani Kuhusu Kulindwa Kimwili?
8, 9. (a) Tunajua jinsi gani kwamba Yehova hajaahidi kumlinda kila mmoja wetu kimwili kwa sasa? (b) Ni jambo la akili kukubali nini?
8 Tunajua kwamba Yehova hajaahidi kumlinda kila mmoja wetu kimwili kwa sasa. Msimamo wetu ni kama wa wale Waebrania watatu waaminifu ambao walikataa kuiinamia sanamu ya dhahabu ya Mfalme Nebukadneza. Vijana hao waliomwogopa Mungu hawakumtazamia Yehova awaokoe kimuujiza wasipate madhara ya kimwili. (Soma Danieli 3:17, 18.) Ingawa hivyo, Yehova aliwaokoa kutokana na miale ya moto wa tanuru. (Dan. 3:21-27) Lakini, hata katika nyakati za Biblia, ni watu wachache sana waliookolewa kimuujiza. Wapinzani waliwaua watumishi wengi waaminifu wa Yehova.—Ebr. 11:35-37.
9 Namna gani leo? Akiwa “Mwokoaji,” bila shaka Yehova anaweza kumwokoa mtu mmoja-mmoja kutoka katika hatari. Je, tunaweza kusema kwa uhakika kwamba Yehova amewaokoa au hakuwaokoa watu fulani? Hapana. Hata hivyo, mtu ambaye ameokoka hali ya hatari anaweza kuhisi kwamba Yehova alimsaidia. Lingekuwa jambo la kimbelembele kwa wengine kukataa maoni yake. Hata hivyo, ni jambo la akili kukubali pia kwamba Wakristo wengi waaminifu wamekufa kwa sababu ya kuteswa, kama ilivyokuwa wakati wa Wanazi. Wengine wamekufa katika misiba. (Mhu. 9:11) Tunaweza kuuliza hivi: ‘Je, Yehova alishindwa kuwa “Mwokoaji” wa watu waaminifu ambao waliuawa au kufa katika msiba?’ Hilo si kweli.
10, 11. Kwa nini wanadamu hawana uwezo wa kuzuia kifo, lakini Yehova anaweza kufanya nini kuelekea kifo?
10 Fikiria jambo hili: Mwanadamu hana uwezo wa kuzuia kifo, kwa kuwa hakuna mwanadamu anayeweza “kuiokoa nafsi yake katika mkono wa Kaburi.” (Zab. 89:48) Namna gani Yehova? Dada mmoja aliyeokoka nyakati zenye hatari za Wanazi anakumbuka maneno haya aliyoambiwa na mama yake Shahidi aliyekuwa akimfariji baada ya wapendwa wao kuuawa katika kambi za mateso: “Kama wanadamu wangekuwa watumwa wa kifo milele, basi kifo kingekuwa na nguvu kuliko Mungu, sivyo?” Ni wazi kwamba kifo hakina nguvu kuliko Mungu mwenye nguvu zote ambaye ndiye Chanzo cha uhai! (Zab. 36:9) Watu wote walio katika Kaburi, wako katika kumbukumbu ya Yehova, na atamwokoa kila mmoja wao.—Luka 20:37, 38; Ufu. 20:11-14.
11 Kwa sasa, Yehova anahusika moja kwa moja katika maisha ya waabudu wake waaminifu leo. Acheni sasa tuchunguze njia tatu ambazo zinaonyesha wazi kwamba yeye ni “Mwokoaji” wetu.
Tunalindwa Kiroho
12, 13. Kwa nini ulinzi wa kiroho ndio wa maana zaidi, na Yehova anatulinda kiroho jinsi gani?
12 Yehova anatupa ulinzi wa kiroho ambao ndio wa maana zaidi. Tukiwa Wakristo wa kweli, tunajua kwamba kuna kitu ambacho ni chenye thamani zaidi kuliko uhai wetu wa sasa. Uhusiano wetu mzuri pamoja na Yehova ndicho kitu chenye thamani zaidi tulicho nacho. (Zab. 25:14; 63:3) Kama hatungekuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova, uhai wetu wa sasa haungekuwa na maana yoyote na hatungekuwa na tumaini lolote la wakati ujao.
13 Tunathamini kwamba Yehova anatupa msaada wowote tunaohitaji ili kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Neno lake, roho yake takatifu, na kutaniko lake la ulimwenguni pote linatusaidia. Tunaweza kufanya nini ili tufaidike kabisa kutokana na maandalizi hayo? Tukijifunza Neno lake kwa bidii na kwa ukawaida, tutaitia nguvu imani yetu na tumaini letu. (Rom. 15:4) Tukisali kutoka moyoni ili tupate roho yake, atatusaidia kushinda kishawishi cha kujiendesha kwa njia isiyofaa. (Luka 11:13) Tukifuata mwongozo ambao jamii ya mtumwa mwaminifu inatoa kupitia vichapo vinavyotegemea Biblia, mikutano, na makusanyiko, tutalishwa ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.’ (Mt. 24:45) Maandalizi kama hayo yanatulinda kiroho na kutusaidia kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.—Yak. 4:8.
14. Simulia kisa kinachoonyesha jinsi Yehova anavyotulinda kiroho.
14 Ili kuonyesha jinsi Yehova anavyotulinda kiroho, kumbuka wale wazazi waliotajwa mwanzoni mwa habari iliyotangulia. Siku chache baada ya binti yao, Theresa, kuripotiwa kwamba amepotea, walipata habari zenye kuhuzunisha sana: Alikuwa ameuawa.a Baba yake anakumbuka hivi: “Nilimwomba Yehova amlinde. Alipopatikana akiwa ameuawa, nakubali kwamba mwanzoni nilijiuliza kwa nini sala zangu hazikujibiwa. Bila shaka, ninajua kwamba Yehova hajaahidi kuwalinda kimuujiza watu wake mmoja-mmoja kwa sasa. Niliendelea kusali ili nielewe jambo hilo. Nimefarijiwa kujua kwamba Yehova anawalinda watu wake kiroho—yaani, yeye anaandaa tunachohitaji ili kulinda uhusiano wetu pamoja naye. Ulinzi huo ndio wa maana zaidi, kwa kuwa wakati wetu ujao wa milele unategemea ulinzi huo. Katika maana hiyo, Yehova alimlinda Theresa; alimtumikia kwa uaminifu mpaka alipokufa. Nimepata amani kwa kujua kwamba matarajio yake ya kuishi wakati ujao yako mikononi mwa Yehova mwenye upendo.”
Kutegemezwa Tunapokuwa Wagonjwa
15. Yehova anaweza kutusaidia katika njia gani mbalimbali tunapolemewa na ugonjwa?
15 Yehova anaweza kututegemeza “katika kitanda cha ugonjwa,” kama alivyomtegemeza Daudi. (Zab. 41:3) Ingawa Yehova hatuponyi kimuujiza leo, anatusaidia. Jinsi gani? Kanuni zilizo katika Neno lake zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima kuhusu matibabu na mambo mengine. (Met. 2:6) Tunaweza kupata mapendekezo mazuri sana na yenye faida katika habari zinazochapishwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zinazozungumza kuhusu ugonjwa wetu. Kupitia roho yake, Yehova anaweza kutupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili tukabiliane na hali yetu na kudumisha utimilifu wetu katika hali zozote zile. (2 Kor. 4:7) Kwa msaada wake, tunaweza kuepuka kukazia fikira sana ugonjwa wetu na kupuuza mambo ya kiroho.
16. Ndugu mmoja amekabiliana jinsi gani na ugonjwa?
16 Mfikirie ndugu kijana aliyetajwa mwanzoni mwa habari iliyotangulia. Katika mwaka wa 1998, iligunduliwa kwamba ana ugonjwa wa mishipa ya fahamu (amyotrophic lateral sclerosis) ambao mwishowe ulimfanya apooze kabisa.b Amekabiliana jinsi gani na ugonjwa huo? Anaeleza hivi: “Mara kwa mara nimehisi uchungu na kuvunjika moyo na kuhisi kwamba kifo ndiyo njia pekee ya kupata kitulizo. Ninapojihisi kwamba nimelemewa, ninasali kwa Yehova na kumwomba vitu vitatu: moyo mtulivu, subira, na uvumilivu. Ninahisi kwamba Yehova amejibu sala zangu. Kuwa na moyo mtulivu kunaniwezesha kutafakari kuhusu mambo yenye kufariji, kama vile maisha katika ulimwengu mpya wakati ambapo nitaweza kutembea, kufurahia chakula kitamu, na kuzungumza na familia yangu tena. Subira inanisaidia kuvumilia hali ngumu na matatizo ya kupooza. Uvumilivu unaniwezesha kuendelea kuwa mwaminifu na kutopoteza usawaziko wangu wa kiroho. Kwa kweli ninaweza kusema kama mtunga-zaburi Daudi, kwa kuwa ninahisi kwamba Yehova amenitegemeza katika kitanda cha ugonjwa.”—Isa. 35:5, 6.
Tunaandaliwa Mahitaji ya Lazima
17. Yehova ameahidi atatufanyia nini, na ahadi hiyo inamaanisha nini?
17 Yehova anaahidi kwamba atatutunza kimwili. (Soma Mathayo 6:33, 34 na Waebrania 13:5, 6.) Hilo halimaanishi kwamba mahitaji yetu yatatoshelezwa kimuujiza au kwamba hatupaswi kufanya kazi. (2 The. 3:10) Ahadi hiyo inamaanisha hivi: Tukitafuta Ufalme wa Mungu kwanza katika maisha yetu na kuwa tayari kufanya kazi ili tupate riziki, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatusaidia kupata mahitaji ya lazima ya maisha. (1 The. 4:11, 12; 1 Tim. 5:8) Anaweza kutuandalia vitu tunavyohitaji kwa njia ambazo hatutazamii, labda anaweza kumtumia mwabudu mwenzetu kutusaidia au kutupa kazi ya kimwili.
18. Simulia jambo halisi linaloonyesha kwamba tunaweza kutunzwa tunapokuwa na uhitaji.
18 Mkumbuke yule mama asiye na mwenzi aliyetajwa mwanzoni mwa habari iliyotangulia. Wakati yeye na binti yake mdogo walipohamia eneo lingine, haikuwa rahisi kwake kupata kazi. Anaeleza hivi: “Nilienda kwenye utumishi wa shambani asubuhi, na kutafuta kazi kila siku wakati wa mchana. Ninakumbuka siku moja nilienda dukani kununua maziwa. Nilisimama na kuangalia mboga zilizokuwa dukani, lakini sikuwa na pesa za kutosha kununua mboga zozote. Sijawahi kamwe kushuka moyo hivyo katika maisha yangu. Niliporudi kutoka dukani siku hiyo, nilipata mifuko mingi yenye mboga za kila aina ikiwa imewekwa nyuma ya nyumba yangu. Tulipata chakula cha kututosha kwa miezi mingi. Nililia na kumshukuru Yehova.” Baadaye, dada huyo alipata habari kwamba mifuko hiyo ililetwa na ndugu mmoja wa kutaniko lao ambaye alipanda mboga katika shamba lake. Dada huyo alimwandikia hivi baadaye: “Hata ingawa nilikushukuru sana siku hiyo, nilimshukuru Yehova pia kwa sababu alitumia fadhili zako kunikumbusha kwamba ananipenda.”—Met. 19:17.
19. Watumishi wa Yehova watakuwa na uhakika gani wakati wa dhiki kuu, na tunapaswa kuazimia kufanya nini sasa?
19 Ni wazi kwamba yale ambayo Yehova alifanya katika nyakati za Biblia na pia katika siku zetu yanatufanya tumtegemee akiwa Msaidizi wetu. Hivi karibuni, wakati dhiki kuu itakapokuja juu ya ulimwengu wa Shetani, tutahitaji msaada wa Yehova kuliko wakati mwingine wowote. Hata hivyo, watumishi wa Yehova watamtegemea wakiwa na uhakika kamili. Watainua vichwa vyao na kushangilia, wakijua kwamba ukombozi wao unakaribia. (Luka 21:28) Hata tukipata majaribu gani sasa, acheni tuazimie kumtegemea Yehova, tukiwa na uhakika kabisa kwamba Mungu wetu asiyebadilika, kwa kweli, ni “Mwokoaji” wetu.
[Maelezo ya Chini]
-